CCM wadai mtandao umewapa ushindi mnono Busanda
Frederick Katulanda na Elias Msuya, Busanda (mwananchi)
WAKATI Chadema ilipopeleka helikopta kwenye kampeni za uchaguzi mdogo wa kiti cha ubunge cha Busanda, makamu mwenyekiti wa zamani wa CCM, John Malecela aliipuuza na kusema kuwa chombo hicho kilikuwa kinatimua vumbi tu na kwamba askari wa ardhini ndio watakaofanya kazi.
Ndivyo ilivyodhihirika jana wakati msimamizi wa uchaguzi huo, Dani Mollel alipomtangaza Lolensia Bukwimba kuwa mshindi wa kiti hicho kwa tofauti ya zaidi ya kura 5,000 dhidi ya mgombea wa Chadema, ambayo ilikuwa ikikusanya mamia ya watu kwenye mikutano yake ya kampeni.
Bukwimba, ambaye kampeni zake za mwanzo zilitawaliwa na zomeazomea, aliibuka kidedea kwa kupata kura 29,242 na kufuatiwa na mgombea wa Chadema, Finias Magesa aliyepata kura 22,799 huku wagombea wa CUF Oscar Ndallawah na Beatrice Lubambe wa UDP wakigawana kura 1,248 zilizosalia.
"CCM ilijipanga vizuri kwa kuwa ina mtandao kuanzia ngazi ya shina, matawi, wilaya hadi mkoa," alisema mwanasiasa mkongwe na muasisi wa chama hicho alipozungumza na Mwananchi jijini Dar es salaam jana.
"Mara nyingi, vyama vya upinzani vimekuwa vikienda kwa pupa na hata kuonekana vinaungwa mkono na umati mkubwa wa watu, lakini havina kiungo cha kuwaunganisha watu hao kwenye ngazi za chini.
"Kampeni zao huwa zenye hamasa nyingi, lakini wakishaondoka wananchi hurudi kwenye maeneo yao na kujikuta wako kwenye mtandao wa CCM," alisema mkongwe huyo ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na ambaye amefanya kazi kwenye serikali za awamu zote nne.
Kingunge alisema kwa mtandao huo mzuri wa CCM, wana uhakika wa kuendelea kunyakua zaidi ya asilimia 80 ya viti vyote vya ubunge katika uchaguzi ujao wa mwaka 2010 kwa sababu wapinzani hawajajijenga.
Pamoja na ushindi huo mkubwa, kulikuwa na matukio mengi ya utata yaliyosababisha baadhi ya viongozi wa Chadema na mgombea wake kupinga matokeo hayo kwa madai kuwa msimamizi alishinikiza ayatangaze, huku mgombea wa Chadema akieleza kuwa atajaza fomu za kutokubali matokeo na kusubiri uamuzi wa chama chake kuhusu kufungua kesi.
Viongozi hao wa Chadema walifika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita na kumuomba msimamizi kuwapatia fursa ya kuwasikiliza na kuwasomea matokeo kabla ya kusaini, lakini wakajibiwa kuwa hawakuwepo wakati fursa hiyo ilipotolewa.
Matokeo hayo hayakutangazwa asubuhi kama ilivyopangwa awali kutokana na msimamizi wa uchaguzi kueleza kuwa alikuwa akiwangojea wawakilishi wa vyama kwa ajili ya kushuhudia ujumlishaji wa kura hizo kabla ya kuzitangaza.
Msimamizi huyo, Molleli alieleza alijaribu kuwatafuta kwa simu lakini hawakupatikana na ndipo alipowasiliana na mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi ambaye alimshauri kuwaandikia barua kuvikumbusha vyama kutuma wawakilishi hao.
Kiliwaandikia barua tarehe 23 mwezi huu kuwaeleza kuwa Mei 24 usiku wanatakiwa kuwa na mawakala katika kujumulisha kura. Mwakilishi wa Chadema alikuwa (Habibu) Mnyaa pekee hadi usiku alipoamua kuondoka," alisema Mollel.
"Nilipomuuliza alisema tuendelee. Asubuhi tena nikampigia Mnyaa aje akanijibu endeleeni, lakini tukaandika barua kwa vyama tena kuwaomba wawakilishi.?p>
Ilipofika saa 4: 45 mgombea wa Chadema, Magesa alifika akiwa ameambatana na kamanda wa uchaguzi wa chama chake, Benson Kigaila na baadaye akaingia mgombea wa CCM, Lolesia Bukwimba na viongozi wa chama chake.
Mara baada ya kuingia msimamizi wa uchaguzi aliwaeleza alikuwa akiwasubiria kwa ajili ya kutoa matokeo, lakini alikwama kutokana na kuwepo kwa mwakilishi wa CCM pekee na kwamba wakati huo angeweza kutangaza kwa sababu idadi imetimia.
Chadema walitaka kupatiwa fursa ya kupitia upya kura zote kabla ya kujumlisha kwa madai kuwa walikuwa na mashaka nayo, lakini msimamizi alipinga akieleza kuwa muda huo ulishapita na hivyo kuwaomba wananchi kusubiria nje kwa muda wa dk 45 ili akamilishe kujumlisha matokeo katika baadhi ya kata kabla ya kusoma matokeo yote lakini muda huo ulipitiliza hadi majira ya saa 9:35.
Wakati msimamizi akifanya majumuisho hayo, wafuasi wa CCM walikuwa wakipiga kelele nje kutaka kutangazwa kwa matokeo huku ndani ya ukumbi akizongwa na wafuasi wengine wa chama hicho tawala waliokuwa wakishinikiza kutangazwa kwa matokeo.
Kamanda wa polisi wilayani Geita, Shaaban Kimea alilazimika kuwaondoa nje baadhi ya wafuasi hao wa CCM na kubakia viongozi wachache wa chama hicho na Chadema.
Pamoja na Chadema kushinikiza matokeo hayo yasitangazwe, msimamizi wa uchaguzi alishikilia msimamo wake.
Hilo halina nafasi naomba wagombea waje kusaini matokeo?hatuna muda wa kuanza hayo tena,?alieleza Mollel akiwa amezungukwa na mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mwanza, Clement Mabina, Anthony Diallo na Esau Barnabas ambao walikuwa wakitaka matokeo yatangazwe.
Baada ya mgombea wa CCM kusaini, ndipo matokeo yalipotangazwa.
Mara baada ya kutangaza matokeo hayo, mgombea wa Chadema, Magessa aliongea na waandishi wa habari kueleza sababu za kukataa kuyatambua.
Tuliitaarifu tume ya uchaguzi kuwa CCM wanagawa chumvi, chupi, magodoro kwa mgongo wa kanisa na kutandaza nguzo za umeme na kujenga barabara wakati wa kampeni, lakini hawakuchukua hatua yoyote. Nitawezaje kuyakubali matokeo,?alihoji Magessa.
Magesa pia alilalamikia ukiukwaji wa taratibu siku ya kupiga kura,
siku ya kupiga kura tulimkamata mratibu wa elimu Kata ya Katoro akigawa posho za wasimamizi wakati wa kupiga kura kitu ambacho ni kosa kwa mujibu wa msimamizi wa uchaguzi wa wilaya. Lakini tunashangaa kumwona mratibu huyo akiendelea na kazi yake ya kuhesabu kura,?alisema.
Aidha Magessa pia alilalamikia kitendo cha Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha kutembelea vituo vya kupigia kura na hata kuwaruhusu askari polisi kuingia kwenye vyumba vya kupigia kura. Alidai Waziri Masha aliwatishia wanachama wa Chadema na kushindwa kuwakamata wafuasi wa CCM kila walipotuhumiwa kufanya makosa.
Naye Robert Kakwesi kutoka Uyui anaripoti kuwa CCM wilayani Uyui imeibuka mshindi katika uchaguzi mdogo wa kata ya Ibiri uliofanyika juzi Jumapili.
Kwa mujibu wa msimamizi wa uchaguzi huo, Dorothy Rwiza CCM iliibuka mshindi kwa kupata kura 1,059 dhidi ya mahasimu wao wakubwa, CUF ambayo ilipata kura 317. Kutokana na matokeo hayo, diwani mpya anakuwa Juma Athumani (CCM) aliyemshinda Mbaraka Kapulilo (CUF) katika uchaguzi ulioshirikisha vyama viwili.