Ni vipengele gani vya katiba vinahitajika kufanyiwa marekebisho kabla ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2009 na Uchaguzi Mkuu 2010? kwa manufaa ya nani?
Kwanza ieleweke wazi, kwa katiba yetu ilivyo na mapungufu mengi inahitajika katiba mpya- ambayo itaandaliwa pia kwa kuwashirikisha wananchi kikamilifu tofauti na katiba iliyoko sasa.
Lakini hata kama tunataka kufanya marekebisho tu kwa ajili ya kuboresha mfumo wa uchaguzi na kufanya chaguzi ziwe huru na haki. kwa maoni yangu yafuatayo yafanyike mwaka 2008.
1. Lazima uchaguzi wa serikali za mitaa uwe chini ya Tume ya uchaguzi badala ya hivi sasa ambapo uchaguzi huu upo chini ya serikali kuu! Haiwezekani serikali ya chama tawala ikajisimamia yenyewe katika uchaguzi. Rekebisho hili lazima lifanyike kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2009.
2. Tume ya uchaguzi iwe huru zaidi- watendaji wake lazima wawe na security of tenure, bajeti yake lazima iwe bajeti huru, na tume isitumie maofisa wa serikali kama wakurugenzi wa halmashauri na maafisa watendaji wa kata kusimamia uchaguzi katika ngazi za chini; tume itafute watendaji huru wa tume katika ngazi hizo.
3. Katiba iruhusu mfumo wa uwakilishi wa uwiano mpaka zaidi- badala ya kwa viti maalumu vya wanawake pekee.
4. Sheria ziwekwe bayana za kuthibiti kiasi cha matumizi katika kampeni na kulazimisha kutangaza wazi vyanzo na matumizi wakati wa kampeni za uchaguzi
5.Daftari la Kudumu la Wapiga Kura(DWKW) liboreshwe, kuanzia mfumo wake mpaka hatua zake za kuliboresha; kitovu cha daftari cha kwanza kabisa kiwe ni kituo cha kupigia kura, mtaa/kijiji na kuendelea ili daftari liweze kutumika hata kwenye chaguzi za mitaa. Bahati mbaya serikali imeshaanza tayari kuboresha daftari bila kuzingatia masuala haya. Kwa hiyo its another Garbage In Garbage Out(GIGO) na matumizi mabaya tu ya mabilioni ya walipa kodi! Pamoja na kuwa daftari limeanza kuboreshwa suala la wapiga kura walioko nje ya Tanzania halijazingatiwa hii inaonyesha kwamba mwaka 2010 walioko nje wanaweza wasiweze tena kupiga kura kama hawatarejea nyumbani na kujiandikisha.
6. Vituo vya kujiandikisha na kupigia kura viwe vya kudumu na vitangazwe rasmi kabisa kwa sheria ama gazette la serikali!
7. Chama tawala kitengenishwe na dola- Ma DC, Ma-RC kama watumishi wa umma wasiwe sehemu ya uongozi wa chama kinachotawala nk. Lazima sheria iwepo kuthibiti watumishi wa umma kama Rais, Mawaziri nk kutumia kofia zao za kiserikali na rasilimali za taifa kujenga vyama vyao. Najua sheria imegusia kidogo, lakini enforcement ni muhimu.
Haya ni baadhi ya mambo ya msingi lakini unaweza kupata mengi zaidi katika mada yangu ifuatayo kuhusu "Uzoefu katika uendeshaji wa uchaguzi Tanzania"- bonyeza hapa:
http://www.chadema.net/habari/misc/misc_10.html
Cha msingi si kujadili tu haya mambo, ni kuchukua hatua! Kwa wale waandishi wa habari na waandishi wa makala- ombi langu kwenu ni kufanya suala la mabadiliko ya katiba na marekebebisho ya sheria za uchaguzi kuwa ajenda zenu za kudumu kwa mwaka 2008. Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo mnaweza kusaidia mabadiliko Tanzania mwaka 2010. Hata kama uko serikali, mashirika ya hiyari na hata taasisi za kimataifa, angalia unawezaje kusukuma mbele haya masuala kwa maslahi ya taifa. Hatuwezi kuwa na uchaguzi ambao ni mnada wa gulio na kura la kaburi la ridhaa ya wananchi!
JJ