*Wamsaka wakala wakidai aliwapunja mgawo
*Washangaa kusikia zilikuwa ni sh. bilioni 12
SAKATA la rushwa katika ununuzi wa rada iliyonunuliwa na Tanzania mwaka 2002 kutoka kampuni ya British Aerospace (BAE Systems) ya Uingereza, limeingia katika sura nyingine baada ya kudaiwa kuwa baadhi ya vigogo waliohusika katika 'dili' hilo sasa wanahaha kumsaka wakala huyo, akidaiwa kuwatapeli.
Mshituko huo umekuja baada ya vigogo hao kusoma kwenye vyombo vya habari kuwa 'kamisheni' waliyopewa wakati wa kufanikisha ununuzi wa rada hiyo, hailingani na kiwango cha sh. bilioni 12, ambacho wakala aliyekuwa akiwaunganisha alikaririwa kukiri kuzipokea kutoka BAE Systems.
Wakala huyo, aliyeelezwa kuwa karibu na wanasiasa wengi wa Tanzania, alikiri alipohojiwa na wachunguzi kutoka Kitengo Maalumu cha Makosa ya Ulaghai (SFO) cha Uingereza na kula kiapo mbele ya Hakimu wa Tanzania, akithibitisha kupokea fedha hizo ambazo ziliwekwa kwenye akaunti yake binafsi Uswisi.
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha kuaminika, imedaiwa kuwa wakala huyo tangu alipohojiwa na SFO, amekuwa akisakwa na vigogo hao wakitaka kujua undani halisi wa 'kamisheni' hiyo ya sh. bilioni 12 ya BAE.
Chanzo hicho kimeiambia Majira, kuwa hata hivyo, wakala huyo hayupo nchini kwa sasa.
"Inaelezwa kuwa hata ofisi yake imefungwa, kila watu wanapomuulizia kwa jamaa zake, wanaambiwa amekwenda India," kilisema chanzo chetu na kueleza kuwa ndiyo maana hata ile habari ya gazeti la The Guardian la Uingereza, iliandikwa kwa kuhojiwa rafiki yake, ambaye naye alikubali kuongea huenda kwa sababu wamekorofishana kibiashara.
"Wanahaha kumsaka, inaelekea walichoambulia wakati wa kuchagiza ununuzi si kile wanachokisoma sasa kwenye vyombo vya habari," kilisisitiza chanzo chetu ambacho kinafahamu kwa kina zaidi kuhusu sakata hilo la rada.
Akizungumzia vigogo hao, mpasha habari huyo aliiambia Majira kuwa sakata la rada lilihusisha viongozi wengi na kwa nyakati mbalimbali, kuanzia mawaziri, makatibu wakuu wa wizara na hata naibu mawaziri, wengi wao wakiwa wastaafu kwa sasa.
"Hawa, hasa huyu ...(anamtaja Waziri mwandamizi katika Serikali ya Awamu ya Tatu), ndiye aliyeshughulikia sana suala la rada na anajua mchakato wote.
"Yeye ndiye hasa aliyeratibu zile hatua muhimu. Sijui kama anaweza kupatikana. Najua hili ni suala nyeti, kila mmoja atakwepa na kukataa kuzungumza," kilisema chanzo hicho.
Kikizungumzia zaidi kuhusu uchunguzi wa SFO, kilisema kuna mambo mengi ambayo mawakala hao wameyaeleza na kukiri mbele ya wachunguzi hao.
Hata hivyo kiliwaasa wadau wote wa maendeleo nchini kuhakikisha kuwa suala la watu kutuhumiwa kuhusika katika rushwa na ubadhirifu wa fedha za umma, linapatiwa majibu sawia.
"Tujue, kwamba wale jamaa kutoka SFO wanachunguza kashfa ya rushwa si kwa faida ya Watanzania. Hata gazeti la The Guardian linaifuatilia sana habari ya rushwa katika rada kwa maslahi ya Waingereza wenyewe.
"Sisi tujiulize, tunachukua hatua gani kusaka ukweli wa viongozi wetu kudaiwa kuhusika katika sakata hilo? Nawaomba tuelekeze nguvu zetu katika hilo kwa sasa," kilisisitiza chanzo hicho.
Jana gazeti hili lilimkariri Mwanasheria Mkuu wa Uingereza, akisisitiza kuwa uchunguzi wa suala hilo nchini Tanzania utaendelea kufanyika kwa nguvu zote.
Rais Jakaya Kikwete ambaye Serikali yake imedhamiria kupambana na vitendo vya rushwa na ubadhirifu unaokwaza maendeleo ya nchi hii, alisisitiza akiwa London, Uingereza hivi karibuni, kuwa Serikali yake inafuatilia kwa karibu uchunguzi dhidi ya sakata hilo na hautaliingilia.
Kuhusishwa kwa viongozi waandamizi katika Serikali ya Tanzania katika mgawo wa 'kamisheni' ya sh. bilioni 12, ni suala ambalo sasa linazidi kuibua mjadala nchini na maoni ya wengi, wakiwamo viongozi wa vyama vya upinzani, ni kuwa Serikali ya Tanzania nayo inahitaji kujisafisha katika hilo, kwa kuunda tume huru.
http://www.majira.co.tz/kurasa.php?soma=tanzania&habariNamba=2183