Riwaya ya Kijasusi; Mtoto wa Rais

Riwaya ya Kijasusi; Mtoto wa Rais

Nina shida ktk simu yangu aina ya Samsung Galaxy tab A model number sm_T285 ni kwamba ni kwa nini haitaki kubadilishiwa line nina maana inasoma line moja tu naomba msaada nimejaribu mi mwenyewe nimeshindwa nimewashirikisha baadhi ya wadau nao wameshindwa msaada waungwana akhsanteni
 
Nina shida ktk simu yangu aina ya Samsung Galaxy tab A model number sm_T285 ni kwamba ni kwa nini haitaki kubadilishiwa line nina maana inasoma line moja tu naomba msaada nimejaribu mi mwenyewe nimeshindwa nimewashirikisha baadhi ya wadau nao wameshindwa msaada waungwana akhsanteni
Ulinunua tigo shop au duka lolote la mojawapo za laini?
 
Hii aimu niliinunua Lebanon ila hiyo line ikaja kusajiliwa hapa tz ni ya halotel
Daah apo chief inahitajika mtaalamu wa simu, ingekuwa izi zetu za kariakoo ningekushauri u flash
 
RIWAYA; MTOTO WA RAIS
HALFANI SUDY
SIMU 0652 212391

Sehemu ya Ishirini na Tisa

Hakuna aliyemjibu, kwani hakukuwa na aliyekuwa na jibu sahihi la kujibu.

***

Wakati huo, Daniel Mwaseba alikuwepo ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya taifa ya Muhimbili. Ndani ya chumba, alikuwepo yeye na maiti moja iliyokuwa imehifadhiwa katika sanduku. Bila shaka yoyote ilikuwa ni maiti ya Aneth.

Daniel alikuwa bado amelazwa katika machela karibu na ukuta. Alikuwa amefunikwa shuka nyeupe iliyoloa damu kidogo maeneo ya kifua. Hayo yote yalipangwa na Dokta Viran. Mwili wa Daniel Mwaseba haukufanywa kitu chochote kile, hayo pia yalikuwa ni maagizo kutoka kwa Dokta Viran kwenda kwa mhudumu wa chumba kile.

Daniel alifunua shuka upande wa usoni. Akaangaza huku na kule. Aliliona sanduku lenye mwili wa Aneth likiwa mita kama mbili karibu na mlango wa kutokea nje. Sanduku likiwa limepambwa vizuri kwa maua na mataji mazuri, ishara kwamba taratibu zote za kuuandaa zilikuwa zimekamilika. Kikichosubiriwa ni ndugu wa marehemu kuja kuuchukua mwili wa mpendwa wao.

Daniel aliiweka pembeni ile shuka aliyokuwa amefunikwa. Sasa alikuwa uchi wa mnyama. Taratibu alinyanyuka na kuelekea mahali lilipokuwa sanduku. Alihakikisha hatoi sauti yoyote ile wakati akipiga hatua zake. Na hii ilikuwa ni moja ya kazi rahisi kwake. Alifundishwa. Alielewa. Alihitimu. Alifaulu. Alitumia sekunde saba kulifikia sanduku lenye mwili wa Aneth.

Baada ya kuhangaika kwa sekunde kadhaa kulifungua sanduku, lilifunguka...

Alichokutana nacho sasa...

Dakika zipatazo tano zilipita, Daniel alikuwa ameshika kiuno chake kwa kuishiwa nguvu. Kwa mara ya kwanza tangu azaliwe, hakuyaamini macho yake. Macho yake mwenyewe lakini alihisi yanamdanganya, kwa maana alikuwa analitizama sanduku tupu, tupu kabisa. Amini, usiamini, ndani ya sanduku hakukuwa na mwili wowote ule.

Daniel alichanganyikiwa sana. Taarifa zilikuwa kwamba, maiti ya Aneth iliokotwa pwani ya Coco na kuletwa katika hospitali ya Muhimbili. Maiti ilikuwa imehifadhiwa katika chumba alichomo, katika sanduku analolitizama.
Sasa kwanini maiti isiwemo? Imeenda wapi?

Akiwa kasimama wima alisikia mlango ukifunguliwa. Kwa kasi aliruka kama samaki mkizi na kuelekea mahali alipolazwa awali. Alijifunika gubigubi kwa shuka mithili ya maiti.

Mlango ulifunguliwa. Waliingia watu kumi wakiwa na Mhudumu wa Monchwari. Daniel alisikia wakati wakifanya utaratibu wote wa kuondoka na maiti ya Aneth iliyopo kwenye sanduku. Baada ya kama robo saa jamaa walitoka nje na sanduku lenye maiti ya Aneth. Sanduku ambalo macho ya Daniel yalimwambia kwamba halikuwa na mwili wa Aneth.

Mlango ukafungwa.

Kukawa kimya tena.

***

Ilipita takribani nusu saa baada ya wakina Kizito kuondoka nyumbani kwa Daniel Mwaseba, ndipo gari ya jeshi la Polisi ilifika baada ya kupigiwa simu na Msamaria mwema.

Askari Polisi walilichunguza eneo lote kuzunguka nyumba ya Daniel Mwaseba. Walichobahatika kupata ni maiti nne, na majeruhi mmoja. Majeruhi akakimbizwa katika hospitali ya taifa ya Muhimbili. Walipoingia ndani ya kuta ya nyumba ya Daniel, pia bahati ilikuwa upande wao, walikuta maiti mbili. Lakini walipoingia ndani kabisa ya nyumba bahati haikuwa upande wao, kwa maana hawakukuta mtu yeyote yule. Tegemeo pekee likawa ni katika utambuzi wa zile maiti na yule majeruhi. Kesi hii ngumu ya mauaji ikawekwa katikati ya mikono ya askari wa kike, Inspekta Jasmin, kama tukiamua kumtambua kwa cheo sambamba na jina lake.

***

Inspekta Adrian alikuwa hajapiga hatua yoyote ile tangu apewe kazi ya kuwasaka watu waliomteka Aneth. Na baadae kesi hii kubadilika na kuwa kazi ya kuwasaka wauaji wa Aneth.
Vikwazo mbalimbali alivyokuwa anavipata katika kazi hii vilimkatisha tamaa kabisa. Alipewa kazi ya kuchunguza kesi ambayo hakutakiwa kupewa hata ripoti ya kifo cha marehemu. Kesi ambayo hakuruhusiwa kuiona hata maiti ya Aneth. Sasa kwa namna gani angefanikiwa kumpata muuaji?

Siku hii, Adrian alikuwa amekaa ofisini kwake. Mafaili kadhaa ya kesi yalikuwa yamelala hovyo mezani kwake. Mwenyewe, akiwa katika mavazi ya kiaskari alikuwa katika tafakari nzito. Kiganja cha mkono wa kushoto ukilala katika shavu lake la upande wa kushoto. Mkono wa kulia ukigongagonga katika meza kwa kutumia peni yake.

Ndipo, simu yake ilipata uhai.

Aliiacha peni mezani na kuiokota simu iliyokuwa juu ya meza. Baada ya kutupia jicho katika kioo chake.

Ilikuwa namba ngeni.

Aliipokea hivyohivyo.

"Bila shaka naongea na Inspekta Adrian." Sauti nzito ya kiume ilisema simuni.

"Ndio," Adrian alijibu kwa kifupi.

"Kama wewe ni Inspekta Adrian basi nimepiga sehemu sahihi,"
"Naongea na nani?" Inspekta Adrian alimkatisha.

"Askari gani mwenye papara namna hiyo. Sikiliza kwanza unataka kuambiwa nini?"

Adrian akavuta pumzi.

"Achana na kesi ya Mtoto wa Rais. Hili ni onyo. Onyo la kwanza na la mwisho. Achana na hiyo kesi utakufa bure kijana!"

Na simu ikakatwa.

Mwili wote wa Inspekta Adrian ulisisimka. Nywele zilimsimama. Kama mpigaji alidhamiria kumtetemesha Inspekta Adrian, basi alikosea sana. Ari ya Adrian kumsaka muuaji wa Aneth ilianza kupanda taratibu baada ya simu ile kukatwa. Simu hii ilikuwa ni kama kupandisha moto wa kipelelezi. Mara zote tangu aanze kuichunguza kesi hii hakuwa na pa kuanzia. Wauaji walifanya mauaji kiustadi sana. Wakiziba mianya yote ya kupatikana kwa muuaji. Lakini sasa, walimpa pakuanzia. Kuichunguza simu hii.
Simu ya onyo!

Itaendelea..
 
RIWAYA; MTOTO WA RAIS
IMEANDIKWA NA HALFANI SUDY
SIMU 0652212391

Sehemu ya Thelathini

Mwili wote wa Inspekta Adrian ulisisimka. Nywele zilimsimama. Kama mpigaji alidhamiria kumtetemesha Inspekta Adrian, basi alikosea sana. Ari ya Adrian kumsaka muuaji wa Aneth ilianza kupanda taratibu baada ya simu ile kukatwa. Simu hii ilikuwa ni kama kupandisha moto wa kipelelezi. Mara zote tangu aanze kuichunguza kesi hii hakuwa na pa kuanzia. Wauaji walifanya mauaji kiustadi sana. Wakiziba mianya yote ya kupatikana kwa muuaji. Lakini sasa, walimpa pakuanzia. Kuichunguza simu hii.
Simu ya onyo!

Moja kwa moja Adrian alimpigia simu afande Simon. Alikuwa ni askari katika kitengo cha TEHAMA. Simon alimhakikishia kwamba yupo ofisini.

"Nakuomba njoo ofisini kwangu mara moja." Inspekta Adrian alisema simuni.

"Nipo njiani afande." Simon aliitikia wito.

Dakika nne zilitosha kumfikisha afande Simon ofisini kwa Inspekta Adrian.

"Karibu sana Simon," Adrian alisema huku akimuonesha kiti Simon.

"Ahsante sana." Simon alisema huku akikaa kwenye kiti.

"Simon, nimekuita hapa kama ndugu yangu. Tunayoongea hapa naomba yabaki kuwa yetu tu, kama ndugu."

"Sawa Adrian. Amini upo na mtu sahihi wa kumwambia lolote lile." Simon alisema, macho yake yakiwa kwa Adrian.

"Simon, najua unafahamu nimepewa kazi ya kuchunguza kifo cha Aneth. Ukweli ni kwamba kesi hii imekuwa ngumu sana kuipeleleza kuliko kesi yoyote ile niliyowahi kupewa kabla. Hadi muda huu tunapoongea sijapiga hatua yoyote ile. Kila ninapojaribu kusonga mbele lakini kuna vikwazo vingi vinatokea. Ninajikuta ninazunguka katika duara lisilo na mwisho. Sasa leo nikiwa hapa nimepigiwa simu kutoka kwa mtu nisiyemfahamu. Mpigaji wa simu kaongea maneno machache sana, yenye dhamira ya kunipa onyo."

"Onyo gani?" Simon alidakia.

"Nisiendelee na kazi hii. Kama ninapenda kuishi basi nisichunguze kifo cha Aneth." Adrian alisema.

"Kabisa amethubutu kumwambia maneno hayo askari Polisi?"

"Ni dakika tano tu zilizopita hayo yametokea. Lakini simu ya onyo imenipa ari zaidi ya kupambana. Kujua chanzo cha kifo cha Aneth. Na kuwatia hatiani watu wote waliohusika katika mauaji ya Aneth. Sasa, kuna kitu nataka unisaidie, lakini iwe nje ya kazi. Unisaidie kama kaka yako, unisaidie kama ndugu yako." Adrian alisema.

"Usihofu Inspekta Adrian, nitakusaidia chochote kile ili kuhakikisha unawapeleka katika vyombo vya sheria wote waliohusika katika mauaji ya Aneth."

"Nashukuru sana Simon. Ninachohitaji kutoka kwako ni msaada wa kiteknolojia. Kitu cha kwanza ninachotaka kutoka kwako ni kuichunguza simu hii niliyopigiwa. Tujue ni simu ya nani? Na imepigwa kutoka wapi? Lakini iwe kazi yetu isiingie katika rekodi ya ofisi yenu. Iwe kazi yetu mimi na wewe." Adrian alisema.

Simon alifikiria kidogo, kisha akasema, " Daah mwanzoni nilikubali kukusaidia. Lakini hilo jambo nahisi litakuwa gumu kidogo. Kutumia tarakilishi za ofisi yetu bila kuweka rekodi sio utaratibu wa ofisi. Afande Bosco anahitaji kujua kila tulifanyalo."

"Simon, najua hayo yote mdogo wangu. Na hiyo ni sababu ya kukuita hapa wewe na kutokuja ofisini kwenu. Lengo ni tuongee sisi wawili, kutokana na utata wa kifo cha Aneth na jinsi mambo yaliyozunguka kifo hiki sitaki kuwajumuisha watu wengi. Nakuomba tufanye jambo hili kwa siri, matokeo yake ndio tutawashirikisha wengine."

"Sawa, nimekuelewa Adrian. Naomba hiyo namba iliyokupigia nitajua kwa namna gani nitafanikisha hilo."

"Ahsante sana kwa kukubali kuifanya kazi hii Simon. Nitakutumia namba ya huyo jamaa."

Wakaongea kidogo na Adrian kisha Simon akaondoka.

Simon alipofika tu ofisini alipokea ujumbe kutoka kwa wafanyakazi wenzake. Alikuwa anahitajika katika ofisi ya Bosco.

Taarifa ya kuitwa ghafla katika ofisi ya afande Bosco ilimstua sana Simon. Bosco alikuwa ndiye mkuu katika kitengo cha TEHAMA katika kituo kikuu cha Polisi.

Bosco alikuwa ni askari mmoja mrefu, mweusi mwenye mwili mkakamavu. Kwa bahati mbaya sifa zake kuu zilikuwa ni roho mbaya, ujivuni na unyanyasaji. Askari yeyote yule katika kitengo cha TEHAMA kuitwa katika ofisi ya Bosco halikuwa jambo jema hata kidogo. Watu walikuwa wanamuogopa Bosco kuliko askari yeyote yule pale kituoni, hata mkuu wa kituo mwenyewe alikuwa anaongea kwa namna ya pekee pindi aongeapo na Bosco. Alikuwa anaongea kwa heshima na taadhima. Na sababu kuu ya yeye kumheshimu Bosco ilikuwa ni moja tu, ukaribu wa Bosco na watu wakubwawakubwa kivyeo.

Simon alielekea ofisini kwa Bosco akiwa na mashaka tele ndani ya moyo wake. Lakini ungejaribu kumuuliza sababu ya mashaka hayo, pengine asingekuwa na majibu sahihi ya kukupa. Alifika nje ya mlango wa ofisi ya Bosco. Juu ya mlango kulikuwa na kibao kidogo cha rangi ya kahawia kilichoandikwa kwa maandishi ya rangi nyeusi.

'Mkuu wa kitengo cha Tehama.'

Taratibu, Simon alishika kitasa na kukizungusha kuelekea upande wa kulia. kwa macho yake aliushuhudia mkono wake mwenyewe ulivyokuwa unatetemeka uliposhika kitasa. Ilikuwa ni hali mbaya sana kwake. Alikuwa mithili ya ng'ombe anayepelekwa machinjioni.
Akagairi kushika kile kitasa.
Aligonga hodi.

"Ingia.." Sauti nzito ya Bosco ilisikika ndani. Sasa ndipo Simon alielekeza tena mkono wake kwenye kitasa. Akakizungusha na kusukuma mlango. Mlango haukumsaliti, ulifunguka taratibu. Akapiga jicho ndani, moja kwa moja akakutana na sura ya Bosco. Akajitutumua na kuingia ndani. Alipofika katikati ya ofisi alijikaza hasa. Akapiga saluti ambayo wala haikupokelewa na Bosco. Yeye, alikuwa bize akiongea na simu yake. Kwa mkono wake wa kushoto akamuonesha kiti. Akajua anaambiwa akae.
Simon akakaa, akimsubiri Bosco amalize kuongea na simu. Iwe zamu yake kuongea na yeye. Na zaidi asikie ni kitu gani alichoitiwa na Bosco?

Sidhani kama Simon alilisikia neno lolote kutoka kwa Bosco wakati akiongea na simu. Ilikuwa ni simu ya upande mmoja. Mara chache Bosco aliitikia ama kuguna. Maneno matatu tu yakapita katika akili ya Simon.

'Simu ya maagizo.'

Dakika saba za simu ya upande mmoja ziliisha. Sasa zikaanza dakika zingine mpya, dakika za yeye na Bosco, bosi wake katika kitengo cha TEHAMA.

"Karibu sana Simon," Bosco alisema huku akijiweka vizuri kitini.

"Ahsante sana." Simon alijibu, huku kwa mbali sauti yake ikimsaliti kwa uwoga.

"Simon, nimekuita hapa kama ndugu yangu. Tunayoongea hapa naomba yabaki kuwa yetu tu, kama ndugu." Bosco alisema akimkazia macho Simon.

Kauli hii ilimstua sana Simon. Pengine alipaswa astuke tangu mwanzo. Kwa maana hata ule ukaribisho ulikuwa na mfanano fulani na maneno haya. Kwa maana maneno haya yaliongelewa na Inspekta Adrian dakika chache zilizopita alipoenda ofisini kwake.

Simon hakujibu, ila mshangao wake ndio uliojibu.

"Naijua sababu ya mshangao wako. Najua umepewa kazi na Inspekta Adrian. Sasa kama mimi ni ndugu yako naomba achana na hiyo kazi. Najua una familia, kufuata maelekezo hayo ni sawa na kuipeleka familia yako katika matatizo." Bosco alisema huku akimkazia macho Simon, ambapo yeye alishindwa kumwangalia usoni.

Alibaki kimya.

"Onyo! Usimwambie chochote Inspekta Adrian juu ya ujumbe huu. Unachotakiwa kufanya ni kumwambia Inspekta Adrian kwamba kazi yake imeshindikana kufanyika.
Nukta!"
Bosco alisema huku akiipiga meza.

"La mwisho, kuanzia sasa unatembea na malaika wa kifo. Kuwa makini sana Simon.Wewe ni kijana mdogo, napenda kuona ukizifikia ndoto zako bila kuyaingilia maisha ya watu. Unaweza kwenda." Bosco alisema huku akimwonesha Simon mlango wa kutokea.

Akiwa amefadhaika, Simon alinyanyuka kitini. Akatoka nje huku akiwa katika mawazo makuu. Ni swali moja lenye maneno kumi ndilo liliomjia kichwani.

"Ina maana Bosco anahusika na mauaji ya mtoto wa Rais?.

Simon alienda hadi ofisini kwao. Mtu yeyote yule angeweza kugundua kwamba Simon alikuwa na mawazo. Lakini hakuna aliyeshangaa kwa wafanyakazi watatu wa ofisi ile ya TEHAMA. Wote walijua kwamba Simon aliitwa na Bosco, na mawazo ni kitu pekee unachorudi nacho ukitoka katika ofisi ya Bosco.

Kwa Regina, askari Polisi pekee wa kike katika idara hii mawazo haya ya Simon kwake yalikuwa nafuu. Yeye siku alipotoka katika ofisi ya Bosco alitoka na mawazo yaliyoambatana na kilio.

Ilikuwa ni siku ya tatu baada ya kuhamishiwa katika idara ya Tehama kutoka katika majukumu yake ya awali. Ndipo alipogundua kwamba bosi wake alikuwa anampenda kimapenzi, hapana, neno sahihi kulitumia ni bosi wake alikuwa anamtamani kimwili.

Regina, mhitimu wa shahada ya kwanza katika chuo kikuu cha Dar es salaam. Kwa bahati nzuri sana, Regina alikuwa kinara katika kitivo cha teknolojia ya mawasiliano na habari kwa mwaka aliomaliza. Lakini bahati mbaya ikafata, Regina akaja kuwa wa mwisho katika soko la ajira. Siyo kwamba hakuajirika. Hapana, aliajirika, lakini hakuajiriwa.

Mwaka wa kwanza ulipita, wa pili ukafuata, watatu ukaingia lakini Regina hakupata ajira pamoja na kuitwa katika sahili kibao, zote aliangukia pua. Mwaka wa nne ndipo alipoamua kurusha kete yake katika nafasi za ajira katika jeshi la Polisi. Huko alipata zari, aliajiriwa.

Ukazuka mgogoro mpya baada ya kupata ajira ndani ya jeshi la Polisi. Mgogoro wenyewe ulitokana na mpenzi wake, Boniface au Bonny kama mwenyewe alivyopenda kumwita. Bonny hakutaka mpenzi wake awe askari Polisi.

Mvutano ulikuwa mkubwa sana ndani ya mahusiano haya. Bonny alikuwa anamkataza Regina asifanye kazi bila sababu. Regina alitaka kufanya kazi kwa sababu.

Mgogoro ulikuwa siku baada ya siku.

Kitu kizuri ni kwamba, mgogoro huo haukuvunja mahusiano yao, ingawa yalitetereka kwa kiasi fulani.

Pamoja na kuwa na mgogoro lakini Regina alianza kazi kama Polisi wa kawaida, na baadaye kuhamishiwa katika kitengo cha TEHAMA katika kituo kikuu cha Polisi, huko ndipo akakutana na bosi mpya, Bosco.

Mwanzoni, Regina alihisi Bosco alikuwa anamtamani. Jinsi akivyomtazama, jinsi akivyomsemesha ilikuwa ni sawa na mwanaume yeyote yule anamyemtamani mwanamke kwa mara ya kwanza.

Regina alijiweka bize na kazi, akimkwepa Bosco mara kwa mara.

Lakini ikatokea siku aliyoitwa ofisini na Bosco.

Hakurudi salama.

Ni dakika mbili tu za kumkataa Bosco zilimfanya arudi na mawazo yaliyoambatana na kilio. Kwani bado hujaelewa Bosco alimfanya nini Regina?

Alimbaka!

Kitendo hiko kilimfanya Regina ajisikie mnyonge sana. Sio tu kilimuondolea hamu ya kufanya kazi, bali pia hata hamu ya kuishi. Kwake, kilikuwa ni kitendo cha udhalilishaji mkubwa sana. Kilimdhalilisha yeye na mchumbaye, Boniface.

Hapakuwa na pakwenda kushtaki. Mkuu wa kituo mwenyewe alikuwa anamwogopa Bosco, sasa angeenda wapi?
Hakumsimulia hata Boniphace maana alijua ungekuwa mwisho wa wa penzi lao, na Bonny angejiona nabii kwa kumkataza mapema kufanya kazi hii.

Regina aliamua kukaa kimya huku akiugulia ndani kwa ndani. Lakini siku zote akiomba kwa Mungu amfanye kitu Bosco. Ikapita miezi Mungu hakumfanya kitu Bosco, hadi leo hii Simon anaporudi akiwa na mawazo tele.

Simon akiwa katikati ya mawazo, akapokea ujumbe kutoka kwa inspekta Adrian.

'0710896977, namba ya kimeo hiyo.'

Simon akawa katika mtihani. Pengine unaweza kuwa mtihani mkubwa zaidi katika maisha yake. Kama alikuwa anaupenda uhai wake na familia yake, basi inampasa aache kazi ya kuipekua ile namba kama alivyoonywa na Bosco.

Mtihani.

Itaendelea..
 
RIWAYA; MTOTO WA RAIS
Imeandikwa na Halfani Sudy
Simu: 0 652 212391

Sehemu ya Thelathini na Moja

Simon akiwa katikati ya mawazo, akapokea ujumbe kutoka kwa inspekta Adrian.

'0710896977, namba ya kimeo hiyo.'

Simon akawa katika mtihani. Pengine unaweza kuwa mtihani mkubwa zaidi katika maisha yake. Kama alikuwa anaupenda uhai wake na familia yake, basi inampasa aache kazi ya kuipekua ile namba kama alivyoonywa na Bosco.
Mtihani.

Baada ya dakika sita za kufikiria, akakata shauri.

"Nitafanya, kwani ananiona?"

Aliamua lakini kitu ambacho alikuwa hakijui, tarakilishi zote za mle ndani zilikuwa zinapeleka taarifa katika tarakilishi ya bosi, ambaye Bosco.



***

Ni majira ya saa mbili usiku. Usiku ulioambatana na giza nene sana ndani ya jiji la Dar es salaam.

Dokta Viran alifanya mpango wa kumtoa Daniel Mwaseba katika chumba cha kuhifadhia maiti. Moja kwa moja walienda ofisini kwake.

"Daniel, nimetekeleza ombi lako kama ulivyohitaji. Ukweli ni kwamba lilikuwa ni ombi gumu sana kwangu, lakini kwa ajiri ya urafiki wangu kwako niliamua kukusaidia. Unachopaswa kujua, nimehatarisha kazi yangu kwa ajili yako Daniel, na zaidi nimehatarisha uhai wangu kwa kuheshimu urafiki wetu.
Daniel, ili urafiki wetu uendelee kudumu, naomba hii iwe kazi yangu ya mwisho kufanya mimi na wewe."

"Dokta Viran," Daniel alimkatisha, " Usinambie na wewe wamekuonya na kukutisha juu ya kusaidiana na mimi. Siamini na wewe ni mwoga kwa kiasi hicho.
Dokta Viran, nikuombe kitu kitu kimoja, usifanye hii kazi ya kunisaidia mimi kama marafiki. Fanya hii kazi kwa ajili ya uzalendo wa nchi yako. Kwa ajili ya usalama wa nchi hii ya asali na maziwa tuliyorithishwa na mababu zetu."

"Daniel, huwezi kunibadilisha, tayari nimeshafanya maamuzi. Maneno yako hayawezi kubadili kitu chochote kile. Nakufahamu jinsi ulivyo na nguvu ya ushawishi. Unachotakiwa kuelewa ni kwamba, huu ni mwisho wa kufanya kazi na wewe. Na ni maamuzi yangu mwenyewe. Sijatishwa wala kuonywa na mtu yeyote yule." Dokta Viran alisema kwa kusisitiza.

"Viran, nakufahamu wewe mwaka wa nne huu sasa. Nakufahamu tangu tulipokutana kwa mara ya kwanza nchini India. Sitaki kukumbusha kwa namna gani niliyatoa rehani maisha yangu na kukuokoa ulipotaka kuuwawa na Ragin. Najua misimamo yako. Kwakuwa nakujua kwa namna hiyo basi jua pia najua kama umetishwa ukae mbali na suala hili. Lakini pamoja na hayo yote nakubalina na maamuzi yako. Lakini baada ya kunisaidia kitu kimoja cha mwisho, na hiyo itakuwa ni fadhila kwa niliyokufanyia."

"Daniel,"

"Naomba nisikilize Dokta Viran, una nafasi ya kunikatalia baada ya kunisikiliza ninachotaka kukwambia, kwa sababu hili ni ombi. Ombi kutoka kwa muuaji wa adui yako, Ragin."

Dokta Viran alikaa kimya. Akimsikiliza Daniel Mwaseba.

"Ni hivi, naomba unisaidie kitu cha mwisho. Kuna mtoto yupo mikononi mwangu. Uhai wake unanitegemea mimi kwa asilimia mia moja.
Anaitwa Aisha
Mtoto pekee wa Salum Taiwan.

Mtoto Aisha ana ugonjwa wa ajabu sana. Ninahisi anahitaji msaada wa kidaktari. Ombi langu la mwisho kwako ninahitaji ukamuone. Na umsaidie kitabibu.
Ninakuahidi hii itakuwa kazi yangu ya mwisho kukutuma wewe." Daniel alisema.

Naomba iwe kazi ya mwisho kweli." Dokta Viran alisema baada ya kufikiria kidogo.

"Ninakuahidi." Daniel alisema.

Daniel Mwaseba na Dokta Viran walitoka nje ya ofisi. Wakaingia katika gari ya Dokta Viran na kuondoka.

Njiani, Daniel alijaribu kumpigia simu Martin lakini simu yake ilikuwa hapatikani.
Akampigia simu Hannan, naye simu yake ilikuwa hapatikani. Akashangaa.
Martin na Hannan hawapatikani?

"Kuna kitu hakipo sawa." Daniel aliwaza mwenyewe.

Safari yao iliwafikisha karibu na nyumba ya Daniel.

"Dokta Viran, tusifike hadi nyumbani kabisa, naomba tupaki hapahapa kwanza." Daniel alisema.

"Kwanini tusifike nyumbani kabisa? Nyumbani kwako si ndipo alipo huyo mtoto mgonjwa?" Dokta Viran aliuliza.

"Ni kweli, lakini ninahisi nyumbani kuna tatizo. Wale marafiki zangu wote hawapatikani kwenye simu zao. Hii sio hali ya kawaida. " Daniel alisema.

Wakashuka.

Kwa mwendo wa taratibu wakaanza kuelekea katika nyumba ya Daniel Mwaseba. Daniel akiwa makini sana. Milango yake yote ya fahamu ikiwa wazi.
Tayari kwa lolote.
Tayari kwa chochote.

Walipokaribia katika nyumba ya Daniel, ingawa kulikuwa na giza kidogo, lakini macho yao yaliona. Nyumba ya Daniel ilikuwa imezungushiwa utepe wa njano. Ulikuwa ni utepe wa jeshi la Polisi, kutahadharisha kwamba eneo lile lipo chini ya ulinzi wa jeshi la Polisi.

"Kimetokea nini hapa?" Daniel alijiuliza kwa sauti ndogo.

Daniel akataka kuuvuka utepe.

"Mpo chini ya ulinzi!" Sauti nzito ilisikika kutoka gizani.

Daniel akasita.

Bila kufikiria akanyoosha mikono yake yote miwili juu kama alivyoamriwa na sauti kutoka gizani.

"Ni nyumba yangu hii," Daniel alisema huku akiwa amenyoosha mikono yake juu.

"Mnajua kimetokea nini hapa katika nyumba hii?" Sauti ya mtu ikasema ikitokea gizani. Alikuwa ni kijana mmoja mrefu, akiwa katika mavazi ya jeshi la Polisi.

"Hatufahamu. Hii ni nyumba yangu. Nilikuwa safarini, nimerudi nimekuta kumezungushiwa huu utepe wa Polisi." Daniel alijitetea.

"Umefanya kosa kubwa sana. Hukupaswa kuvuka utepe huu. Hiyo ni sawa na kupingana na mamlaka halali. Nyumba hii ipo katika ulinzi maalum wa jeshi la Polisi." Yule askari alisema kikakamavu.

"Naomba nisamehe kwa hilo." Daniel aliomba msamaha.

"Sawa, ngoja nimpigie askari aliyepewa kazi hii. Mimi kazi yangu ilikuwa ni kulinda tu hapa." Yule askari alisema. Akachukua simu yake na kumpigia askari aliyepewa jukumu la uchunguzi wa mauaji ya watu wanne yaliyotokea katika nyumba ya Daniel Mwaseba.

Alikuwa Inspekta Jasmin..

Ilichukua takriban nusu saa, kwa Inspekta Jasmin kufika pale baada ya kupigiwa simu. Alikuja na pikipiki kubwa ya jeshi la Polisi.

"Afande, mmiliki wa nyumba ni huyu hapa." Yule askari alisema baada ya kupiga saluti.

Inspekta Jasmin akamsogelea mtu aliyeoneshwa aliyekuwa gizani. Akatoa tochi na kummulika.

"Daniel Mwaseba!" Inspekta Jasmin alisema kwa mshangao mkubwa.

"Ndiye, Inspekta Jasmin, nini kimetokea hapa nyumbani kwangu?" Daniel aliuliza.

"Kumbe hapa ni nyumbani kwako, kumetokea mauaji hapa. Zimekutwa maiti za watu nne. Mbili nje ya ukuta na mbili ndani ya ukuta wa nyumba hii. Majeruhi amepatikana mmoja, amepelekwa hospitali ya taifa ya Muhimbili. Nimepewa mimi jukumu la kuchunguza sababu ya mauaji hayo. Lakini hadi sasa sijapiga hatua yoyote ile." Inspekta Jasmin alisema harakaharaka.

"Hii ni nyumba yangu. Na kulikuwa na watu wangu humu ndani. Je umepata majina ya maiti na majeruhi?" Daniel aliuliza, sauti yake ikiambatana na uwoga.

"Waliofariki sijapata majina yao. Ila majeruhi anaitwa Martin, Martin Hisia."

Angalau Daniel akapumua kusikia Martin yupo hai, "Vipi katika hizo mauti kuna maiti ya kike?" Daniel aliuliza.

"Hapana. Wote ni wanaume." Inspekta Jasmin alisema.

Daniel alishukuru tena kugundua kwamba Hannan hayumo kati ya watu hao waliouwawa. Swali pekee lililotamalaki katika kichwa chake ni "Yu wapi Hannan?"

Wakiongozwa na Inspekta Jasmin waliingia ndani ya nyumba.

"Ni muda mrefu sana hatujaonana. Mpaka nimesahau kazi ya mwisho kufanya na wewe ilikuwa lini na ni kazi gani?" Inspekta Jasmin alisema.

"Nafikiri katika kazi ya kule Iringa. Ambayo kuna mwandishi ameitungia kitabu na kukiita Elizabeth Neville." Daniel alisema.

"Ni kweli nimekumbuka. Sikujua kabisa kama hii ni nyumba yako. Nilipata taarifa ya kulipuriwa kwa bomu nyumba yako ya kule Mikocheni." Inspekta Jasmin alisema.

"Ndio. Nilikuwa na nyumba hii kabla hata ya kule haijaripuliwa kwa bomu. Na kwa bahati nzuri kazi zangu nilikuwa nimezihamishia hapa." Daniel alisema.

Waliikagua tena nyumba yote, hawakupata kitu. Na hakukuwa na mtu.

"Kwani kulikuwa na watu wangapi humu ndani?" Inspekta Jasmin aliuliza.

"Kulikuwa na watu tisa. Itabidi nikaangalie hizo maiti nne kama ni watu wangu. Aah nimekumbuka," Daniel alikumbuka kitu wakati akiongea.

"Umekumbuka nini Daniel?" Inspekta Jasmin aliuliza.

"Kuna chumba cha siri katika chumba cha mateso. Ngoja tukaangalie labda waliamua kujificha huko baada ya kuona kuna matatizo."

Moja kwa moja walienda katika chumba cha mateso. Daniel akagundua kabati lilisogezwa. Akaziamini hisia zake. Akatoa simu yake mfukoni. Aliibonyaza akiwa kaielekeza ukutani.

Ukuta ulifunguka..

Hisia za Daniel zilikuwa sahihi. Salum Taiwan, mtoto Aisha, Candy na Cindy walikuwa humo. Lakini hao walikuwa ni wachache sana. Kuna watu hawakuwemo katika chumba cha siri, lakini kichwani mwa Daniel lilitamalaki jina moja tu, Hannan!

Yupo wapi Hannan?

Salum Taiwan ndiye aliyechukua nafasi ya kuelezea kila kitu. Jinsi Hannan alivyowakusanya na kwenda kuwaficha katika chumba cha siri. Kila mmoja alibaki mdomo wazi.

"Hannan alijua kama watavamiwa ndio maana akawaficha hawa. Sasa kwanini na yeye hakujificha pamoja nao?" Daniel alijiuliza.

"Hilo swali wa kulijibu ni Hannan mwenyewe. Pengine na Martin Hisia anaweza kulijibu swali hilo." Dokta Viran alijibu.

"Oosh Dokta. Hilo swali nilikuwa najiuliza mwenyewe. Nimesahau hata dhima ya wewe kuwa hapa. Huyu ndo mtoto Aisha niliyekwambia. Na huyu ni baba yake, anaitwa Salum Taiwan. Naomba uende nao hawa kama tulivyoongea. Gharama zote za matibabu zitakuwa juu yangu." Daniel alimwangalia Salum "Suala la kupata dawa kwa wale jamaa limekuwa gumu kidogo. Kama unavyoona wenzetu hatujui wako wapi. Mimi peke yangu itakuwa ngumu kidogo kutafuta mahali zilipo dawa na kuwasaka wenzangu. Tatizo la Aisha nimemkabidhi Dokta Viran, mtaenda kuishi nyumbani kwake hadi hali ya mtoto itakapokuwa sawa. Nitagharamia kila kitu."

"Sijui nikushukuru vipi Daniel. Wewe ni kiumbe wa ajabu kuwahi kukutana nae. Sijawahi kukutana na mtu mwenye moyo safi kama wako. Siku zote za maisha yangu nitazikumbuka siku hizi chache tulizoishi hapa pamoja." Salum alianza kulia..

"Salum, ni jukumu langu. Jukumu langu kama kaka, kama binadamu mwenzangu. Huna haja ya kumaliza maneno. Mnaweza kwenda." Daniel alisema.

Dokta Viran, Salum na mtoto Aisha wakaondoka.

"Candy na Cindy, ninyi ni ndugu zangu. Nafahamu mnanichukia kwasababu niliwateka. Pengine mimi ni mbaya kwenu. Lakini lengo langu halikuwa kuwapora uhuru wenu. Niliwaweka ninyi kama chambo ili kumnasa baba yenu ambaye ana mipango mibaya kwa nchi. Ninyi ni ndugu zangu, naomba msinichukie kwakuwa mtaendelea kubaki na mimi hadi muda ambao nitaona unafaa kuwaachia."

Candy na Cindy walimwangalia Daniel. Chuki dhahiri zilijionesha usoni kwao, lakini Daniel wala hakujari.

"Eeh Daniel, kipi kifuatacho?." Inspekta Jasmin aliuliza.

"Tutahama hapa. Washagundua kwamba hapa ni nyumbani kwangu. Ingekuwa ile nyumba yangu ya Mikocheni ipo tungehamia kule. Sasa haipo, nakusikiliza wewe wapi pa kwenda?" Daniel alisema akimwangalia Jasmin.

"Sehemu salama kwa sasa ni nyumbani kwangu. Tutapanga mashambulizi kutokea Vikindu, nyumbani kwangu. Uzuri wa Vikindu ni nje ya mji, itakuwa rahisi kwetu kupanga mipango yetu." Inspekta Jasmin alisema.

"Haina shida, hilo limepita."

Daniel, Jasmin wakisaidiwa na kina Candy walikusanya vitu walivyoona vinafaa. Wakahama kambi, walihamia Vikindu nyumbani kwa Inspekta Jasmin. Hadi wanafika Vikindu, ilikuwa ni saa saba usiku. Inspekta Jasmin aliandaa chakula harakaharaka, wakala kisha kila mmoja akaenda kupumzika katika chumba chake. Hawakulala pamoja.

Itaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom