Riwaya: Nitakupata tu

Riwaya: Nitakupata tu

Dah pumzika kwa aman bro hii story nilikuwa sijaanza kuisoma niltaka iishe kwanza Mungu akuondelee adhabu ya kabri mkuu
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 004

Aliondoka kwa kupitia mlango wa nyumba ile. Kichwa chake kilishavurugwa kama sio kuvurugikiwa. Hakuamini kama tukio la kuuawa kwa mwanamke yule lingeyavumbua mambo makubwa kama yale tena kwa muda mfupi. Lakini ni nani waliomuua Rafiki huyu wa Teddy? Kwa nini wamuue? Au waliniona nikiondoka nyumbani wakaamua kunifuatilia? Kama walinifuatilia kwa nyuma ni vipi damu ilikuwa imeganda kuonyesha mauaji yalifanyika muda mrefu kidogo? Maswali hayo yakampa hamu ya kumchunguza mkewe, sio mkewe tu bali hata na Jimmy. Kwani aliondoka nyumbani akiwa peke yake, hakuona kitu chochote kilichompa wasiwasi kama alikuwa akifuatiliwa, sasa ilikuwaje kufika tu nyumbani kwa mtu aliekuwa akimuhitaji amkute ameuawa? Hilo likampa kile ambacho hakuwahi kukiwaza, tukio la coco beach lilibeba tukio zima la kuuawa kwa mwanamke huyu. Akatambua kuwa alitakiwa kuwa makini, alitambua kama atakwenda ndivyo sivyo basi anaweza asiimalize kazi hii. Alijua kama mkewe ni mshirika wa Jimmy na kama ni kweli ni yule aliemuona coco beach, basi alijua kuwa lazima atakuwa akitembea na macho ya watu kila mahali. Akairudia gari yake kwa kutokea uelekeo tofauti, baada ya kuikuta gari yake akawasha kitufe fulani cha kucheki usalama, aliporidhika muda mfupi alikuwa barabarani akielekea nyumbani kwake huku akiubeba utulivu wa Hali ya Juu. Hakutaka kumpa mashaka mpenzi wake, alitaka kumchunguza chini kwa chini. Muda mfupi alikuwa akiingiza gari ndani ya geti la nyumba yake. Akashuka na kurudi getini tena, baada ya kulifunga akaongoza kuingia ndani. Ile anaufungua mlango akapokewa na macho ya Teddy yakimtizama katika namna ya kuvutia. Yalikuwa macho malegevu, macho yanayohitaji kitu fulani. Masimba alilijua hilo, lakini hakutaka litendeke. Akapiga hatua mbili tatu mpaka aliposimama mwandani wake. Akamkumbatia kwa upendo wa hali ya juu. Walibaki wamesimama katika kumbatio lile, kumbatio ambalo lilidumu kwa muda wa dakika mbili. Kila mmoja akiliwaza lake. Punde walikuwa wakiachiana lakini huku wakiwa wanatizama.. kila mmoja alikuwa akimuangalia mwenzake kwa upendo. Lakini upendo ambao haukubeba maana nzima ya kutizamana kwao. Kwa mbali Masimba alikigundua kile ambacho kilifichika katika mtizamano ule. Kulikuwa na wasiwasi Machoni kwa mpenzi wake. Hakusubiri zaidi kumuangalia, aliushika mkono wake na kuelekea naye chumbani, hapo wakapokewa na kitanda, kitanda ambacho leo hili kilichelewa kuupumzisha mwili wa Masimba. Akaendelea kupiga hatua kuelekea pale kitandani. Alipofika alimlaza teddy kisha naye akayatoa mavazi yake kisha kujilaza kando ya Teddy. Wakauvuta usingizi kwa muda, usingizi ambao haukua rahisi kwa masimba. Sauti ya mwanamke alieuawa usiku wa juzi bado iliendelea kusikika masikioni mwake, bado hakujua kwa nini ilikuwa vile, bado hakujua wauaji walikuwa na lengo gani. Akapanga siku inayofuata kuelekea nyumbani kwa marehemu. Alitaka kwenda kupeleleza na kujua nini ambacho kipo nyuma. Alitaka kuujua ukweli juu ya kifo cha Asteria, alitaka kujua kuna uhusiano gani na Jimmy. Akaivuta shuka usoni, kisha kuutafuta usingizi.

*******

"Lazima Tumuue." Ilisikika sauti kutoka ndani ya chumba fulani. "Hawezi kucheza na sisi, hata hao waliomtuma tutawamaliza kabla ya jua la kesho kutwa." Aliendelea kuunguruma mwanaume yule. Alikuwa mwanaume wa makamo, mweusi na mwenyekitambi ambacho kilimfanya aonekane kama mkurugenzi au waziri katika wizara fulani. Ukimuondoa mwanaume huyo pembeni alikaa Jimmy na kushoto kwake alikaa mwanaume mwingine ambaye muda wote alikuwa kimya. Kilikuwa kikao ambacho hakikuwa rasmi. Kikaa ambacho kiliitishwa na watu watatu baada ya kupata taarifa ya kuuawa kwa vijana wao wawili. Hilo liliwapa mashaka makubwa sana, mashaka ambayo hapo mwanzo hawakuwa nayo. Ukweli waliujua na walimjua muuaji. Licha ya kumjua muuaji lakini hawakuwaza kama lingefika huko. Hawakujua kama Masimba angeanza kwa kuwatia Hasara, hawakujua kama wangewapoteza watu wao ambao walikuwa ni msaada mkubwa kwao, kwa mara ya kwanza wakajikuta wakikijutia kitendo cha kumuua Asteria Mbele ya Masimba. Walijua kitendo hicho ndicho kilichosababisha yote ambayo yalitokea usiku wa jana. Kila mmoja akatulia akihitaji kuipa utulivu akili yake ili kupata majibu sahihi juu ya kudili na mtu huyu ambaye ameonekana kuwa kikwazo kwao. Hakuna ambaye aliinua mdomo ama kuufumbua kuzungumza na mtu mwingine. Walinyamaza kumsubiri mtu ambaye ndie mtu wa mipango, walikuwa wakimsubiri Teddy Kupata majibu ya kipi ambacho kilitokea na kipi ambacho kifanyike. Kila mmoja NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 003

********

Namba ya Mwisho kumpigia marehemu ilikuwa namba ya Mpenzi wake. Hilo likamsisimua mwili wake, ile hisia kwamba mpenzi wake ndiye aliemuona kule coco beach sasa ilikuwa imeupata ushahidi wake. Lakini bado kichwa chake kilikuwa kizito kupindukia kuamini kwamba Teddy ni Mhusika katika tukio la kuuawa kwa mwanamke yule. Hilo halikumpa mashaka zaidi lakini alijiuliza ni vipi ameweza kufanya hilo wakati alikuwa naye ndani kwa kipindi chote. Ni katika kuyawaza hayo ndipo akaikumbuka siku iliopita pale alipoagwa na Teddy kuwa anakwenda kwao na hatarudi kwa siku hiyo. Kulikumbuka hilo kulizidi kuusisimua Mwili wake. Alitanbua kuna kila dalili za mpenzi wake kuhusika na kifo cha mwanamke yule. Lakini alijiuliza sababu za kumuua mwanamke mbele yake kulikuwa na maana gani kwake? Walikuwa wakimpa ujumbe gani kwake. Hapo akaipata hamu ya kuendelea kuichunguza simu ya marehemu Asteria. Jina la pili kukutana nalo ni la Mtu ambaye aliambiwa amchunguze. Lilikuwa jina la Jimmy Lambert. Alikuwa mmoja kati ya watu waliowasiliana na Asteria Muda Mfupi kabla ya kifo chake. Kila alichokuwa akikiona kilikuwa kama ndoto asioiamini. Kwa nini jina la Teddy kisha Jimmy? Teddy yupo wapi katika hili? Ana husika vipi katika kifo cha mwanamke huyu? Yalikuwa maswali mazito sana, maswali ambayo hayakuwa na majibu kwa wakati ule. Hakuwa na jibu kwa wakati ule lakini ilikuwa lazima kulitafuta jibu kabla hakujapambazuka. Aliinuka na kuvirudisha vitu vyake sehemu yake, alipohakikisha kila kitu kipo sawa akaanza kutembea kuelekea nje ya nyumba yake. Hakupata hamu ya kulala kwa wakati ule. Uhusiano wa kifo cha mwanamke yule na urafiki wa Jimmy na Teddy kilikuwa kitu kilichomtia shaka na kuvuruga kichwa chake. Safari hii hakutaka kutumia usafiri wa kukodi, aliamua kutumia gari yake mwenyewe. Alikuwa amekata shauri ya kuelekea magomeni Mikumi nyumbani kwa rafiki wa mpenzi wake. Alitambua huko anaweza akaupata Ukweli kuhusu mauaji ya Binti yule na Uhusiano uliokuwepo kati ya Jimmy na Teddy. Kwa kuwa barabara haikuwa na magari, hapakuwa na ugumu wowote. Aliendesha gari kwa mwendo wa kawaida huku akiwa makini kuangalia kama alikuwa akifuatiliwa. Lakini hapakuwa na kitu chochote kilichomtia wasiwasi. Baada ya muda alikuwa akiegesha gari umbali mfupi kutoka iliponyumba ananyoishi Rafiki wa mpenzi wake. Ilikuwa nyumba kubwa ya vyumba sita, sebule, choo sambamba na jiko. Hakuwa akiishi na mtu kutoka na mumewe kutokuwepo hapa nchini. Masimba alishuka na kuufunga mlango wa gari kisha akaongoza kuelekea getini kwa nyumba ile. Giza lilikuwa limechukua sehemu kubwa huku ukimya nao ukitawala kuonyesha kwamba watu wengi walikuwa wameshalala. Alitembea taratibu huku akiwa makini na kila kitu, alipolifikia geti akataka kuligonga lakini akagundua kuwa lilikuwa wazi. Hilo likamstaabisha, tokea amfahamu mwanamke huyu hakuwahi kumuona ama kukuta geti hili likiwa wazi. Kitendo cha leo kilimstaabisha sana. Akakata shauri aingie pasipokuligonga geti. Akalisukuma taratibu na kuzama ndani. Hapo pia akashangazwa kwa ukimya ambao aliukuta ndani. Taa zote zilikuwa zikiwaka, mlango wazi lakini hakukuwa na sauti yoyote kuashiria kama kulikuwa na mtu ama lah. Hilo likampa machale, akajivuta zaidi kuufuata mlango.. akaukuta ni kweli ulikuwa uko wazi. Akaingia na kusogea ndani, bado alipokewa na ukimya. Ukimya ambao hakuwahi kukutana nao katika jumba lile. Ukimya uliomfanya aichomoe bastola yake na kuishikilia mkononi. Akatembea kwa makini huku macho yake yakicheza pande zote. Bado hakuiona dalili ya kuwepo kwa mtu. Akaendelea kutembea huku umakini ukiongezeka. Akatokea sebuleni, kutokea sebuleni tu akahisi mwili ukisisimka.. sebule ilikuwa ilikuwa imevurugwa na vitu kutupwa huku na huko..

Akaikamata bastola yake vizuri kisha akaanza kusogea mbele zaidi na zaidi. Hatua saba mbele akaiona michirizi ya damu. Umakini ukaongezeka zaidi na Zaidi. Akatembea mdomo wa bastola ukitangulia. Alikuwa akitembea kuifuata michirizi ile ya damu. Alikuwa amejiweka tayari kwa kila kitu. Akaendelea kuifuatilia michirizi ile nyuma nyuma, mbele kidogo Akaiona ikiwa imeishia mlangoni mwa chumba fulani mle ndani. Hapo akasimama kwanza, baada ya hapo akausukuma mlango kisha kujitoma ndani. Hapo akajikuta akitizamana na Mwili wa Rafiki Wa Teddy Ukiwa umelala chini huku damu zikionekana kutuama. Akatembea mpaka pale ulipo mwili wa dada yule. Hakuonekana kuwa na uhai, hakuonekana kama alikuwa hai. Masimba akautazama mwili wa mwanadada yule kwa muda wa kama sekunde tano bila kufanya lolote. Kichwa chake kilikuwa kimevurugika, asteria, na sasa alikuwa ameuawa mwanamke huyu. Kipi kipo nyuma katika mauaji haya? Bado alitaka kujua kiundani zaidi, wakati akiwa bado ameduwaa asijue nini anatakiwa kufanya, akaisikia miguu ya watu ikitembea kisha minong'ono ikafuatia. Akatulia tuli huku mdomo wa bastola akiuelekeza mlangoni. Bado hatua za miguu na minong'ono ikaendelea kusikika, Sasa zilikuwa sasa hatua zile zilikuwa zikiukaribia mlango ule, punde akakiona kitasa kikitikiswa, wakati huo huo mlango ukasukumwa.. hakusubiri chochote kitokee, hakusubiri chochote kivuruge plani yake, mlio mdogo mfano wa chafya ukasikika, bastola ikakohoa mara mbili.. Hapakuwa na kelele. Ilikuwa miguno tu, miguno ilioambatana na kutambarajika kwa watu. Masimba akaurudia umakini wake, akatembea mpaka pale ilipolala ile miili ya watu wale wawili, akainama na kuigeuza miili. Zilikuwa sura ngeni machoni, hakuwahi kuwaona popote watu hawa. Alichokifanya nikuwapekua watu wale nakuchukua kila alichokiona kinafaa, kisha akatoweka eneo lile kwa kupitia mlango wa nyuma wa nyumba Ile. alikuwa akiitizama saa yake. Muda ulikuwa muda ulikuwa ukienda bila kumuona Teddy, kila mmoja akashangazwa na kitu kile, kila mmoja lishangazwa na kuchelewa kufika kwa Teddy, mmoja akaona aipige namba yake japo kumuuliza. Lakini kinyume chake namba haikuwa inapatikana. Hilo likawashangaza wote, liliwashangaza kwa kuwa taarifa alikuwa nayo na aliahidi kufika hapo katika muda husika. Lakini muda huu alikuwa hapatikani kabisa. Kila mmoja akasonya, akasonya huku akitukana matusi ya nguoni.

*****
Wakati akisubiriwa kule na watu wake, teddy alionekana akiingia katika maeneo ya nyumba ya rafiki yake. Ni ile nyumba ya rafiki yake alieuawa jana.aliukuta umati wa watu umezunguka eneo lote huku polisi wakiwa wamezungusha utepe kuonyesha kuwa hapakutakiwa mtu kupita hapo. Alipenya katikati ya watu mpaka karibu kabisa na waliposimama askari wa usalama. Akawasogelea kisha kuongea nao mawili matatu, wakaonekana askari wale wakimruhusu kupita kuingia ndani ya nyumba ya Rafiki yake. Alitembea bila kuonyesha wasiwasi wowote mpaka sebuleni ambapo aliwakuta wataalam wa picha wakiendelea kupiga picha mbali mbali, pia walikuwepo wanausalama kadhaa wakitizama hiki na kile, akawapita na kuelekea kule ambapo ilielekea michirizi ya damu. Akatembea akiangalia hiki na kile. Hatua tano akamuona mtu ameinama akiichunguza miili ya watu wawili ambao walikuwa wamelala katikati ya damu. Alimtambua mtu huyo na alimjua. Alikuwa mpenzi wake. Alikuwa masimba akiitizama miili ya wanaume wawili aliowauaa Jana. Akataka kusimama lakini alijikuta akiendelea kutembea baada ya masimba kugeuka na macho yao kukutana.

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 005

Alitaka kusimama asiendelee na safari yakuelekea pale alipochuchumaa Masimba. Kitendo cha kumkuta mpenzi wake kulimpa picha mbili tofauti. Picha ambazo hazikuonyesha kumfurahisha yeye. Hata masimba alipogeuka na macho yao kukutana, bado alitembea na bado alikuwa akimuangalia kwa mashaka. Hata masimba alikitambua kitendo kile, lakini hakutaka kumshtua, hakutaka kumuonyesha kama anajua kitu. Baada ya Teddy kusogea pale, kwa mara ya pili masimba akainua uso na macho yake kumtizama Teddy. Alimuangalia kwa muda kisha kurudisha macho yake kwenye mwili wa Marehemu, alimuona jinsi alivyolala uso wake ukiwa umekunjamana kutokana na maumivu ambayo aliyapata wakati anauawa. Kila alipokuwa akimuangalia marehemu ndipo hasira juu ya mpenzi wake ziliongezeka. Alitambua kuuawa kwa mwanamke huyu ilikuwa ni kuzibwa mdomo juu ya kitu fulani ambacho hata yeye alihisi kuwa labda utakuwa ule mzigo. Kwa mara nyingine akajiapiza kuyafikia makazi ya Jimmy Lambert. Matundu mawili ya risasi kifuani na mawili shingoni ikikuwa ni kithibisho kuwa marehemu huyu hakutakiwa kuachwa hai. Baada ya kuridhika na kile alichokifanya pale akainuka, akaongea mawili matatu na mpenzi wake, alipomuacha hapo akaongea na wana usalama kisha akaondoka maeneo yale kuelekea nyumbani kwa Marehemu Esteria. Kwa kuwa hapakuwa mbali na eneo ambalo alikuwepo, masimba hakuona tatizo kutembea kwa miguu.. alitembea huku sura ya wasiwasi ilionyesha mpenzi wake ikijirudia. Hakuwa na wasiwasi pale alipotembea hapa na kutokea pale. Hakuwa na mashaka kuwa anafuatiliwa kwa kuwa walikuwepo vijana ambao walikuwa wakimfuatilia kwa nyuma kuangalia nani ambaye alikuwa nyuma yake. Bado alitambua mkewe alikuwa nyuma ya matukio haya, alijua Teddy alikuwa katika hili. Hilo lilimpa matumaini ya kugundua kuhusu mzigo uliokamatwa, na hata kuugundua ukweli mwingine ambao umefichwa kwa njia moja ama nyingine. Akaifikia nyumba ya marehemu Asteria. Askari walikuwa wengi wakilinda eneo lote. Kila mmoja alikuwa makini kwa kila hatua. Masimba akawafikia na kuongea nao mawili matatu, punde alikuwa akipiga hatua kuelekea ndani ya nyumba ile iliojaa waombolezaji. Kila mtu alionekana ni mwenye uchungu sana. Kila mmoja alikuwa akilia kwa uchungu wa hali ya juu. Hilo likampa Masimba wakati mgumu. Wakati wakupata maelezo kutoka kwa ndugu wa marehemu Asteria. Alitembea macho yakitizama kila sura ya mtu aliekuwepo pale, siku zote alitambua kuwapo katika tukio lile na umati wa watu kiasi kile, ni njia moja wapo ya kuweza kumtambua ama kumshuku kwa macho, vile tu hisia zake zitakavyo. Kila sura ilionyesha majonzi, kila mmoja alionyesha kuumizwa na kifo cha Asteria. Hilo likamfanya masimba aikumbuke sauti ya msichana yule wakati alipokuwa akimuita. Hapo akahisi kitu kikimkaba kwenye koo. Kwa nini hakusimama kumsaidia binti huyu anayeonyesha kupendwa na watu? Alipewa kazi ya kuchunguza mzigo uliokamatwa, mzigo ambao haijulikani kama ni wote ambao umekamatwa. Lakini sasa alikuwa amebeba uchunguzi wa vifo vya watu wengine wawili. Vifo ambavyo vinaonyesha kuwepo na uhusiano wa kupotea kwa mzigo ambao alipewa kazi ya kuuchunguza. Alitembea kwa utulivu mpaka sehemu moja ambayo walikaa wakina mama wengi wakionyesha kumshika mama mmoja ambaye alionekana hajiwezi kwa kilio. Baada ya kufika hapo akaongea na dada mmoja ambaye alifanana sawia na marehemu Asteria.

"Wamemuua mdogo wangu, wamemuaa kwa sababu ya uaminifu wake kazini!" Alianza kuongea dada yule huku akiangua kilio.

"Najua una uchungu, najua unaumia, lakini hatuna lakufanya kwa kuwa limeshatokea. Naomba ufute machozi kwa kuwa niko hapa kwa kazi yakutaka kujua nani wapi nyuma ya kifo hiki. Futa machozi. Kisha nataka unijibu maswali kwa uchache. Aliongea masimba huku sasa akitoa kijitabu kidogo.

"Tunaweza kuanza mazungumzo.. nataka kujua kila kitu unachokijua wewe kuhusu marehemu.' Akaongea masimba huku akijiandaa.
Dada wa Asteria alimuangalia Masimba, kisha kwa sauti ya upole akaanza kumueleza.

"Asteria ni Mdogo wangu na mimi ndio msiri wake. Hakuwa akinificha chochote katika maisha yake. Wiki mbili zilizopita alinipigia simu akiniambia kwamba kuna kitu anataka kunieleza, lakini kitu chenyewe ni Cha hatari na hatuwezi kuzungumza kwenye simu. Baada ya kuniambia hivyo nilimshauri aje nyumbani anieleze kisha tuangalie hatua za kuchukua. Kweli Asteria alikuja siku ya pili yake usiku, tena akiwa katika mavazi ya ajabuajabu ambayo yalifunika mpaka uso wake. Ki ukweli aina ile ya mavazi na uingiaji wake ndani, ulinifanya nihisi kuwa kweli mdogo wangu alikuwa katika hatari. Basi sikutaka kumhoji kuhusu yale mavazi na hata uingiaji wake, nilimtaka aniambie tatizo lake. Ndipo hapo aliponieleza kuwa kuna watu matajiri wanataka wasaidiwe kuingiza madawa ya kulevya yenye thamani ya mamilioni ya shilingi. Lakini sasa wanataka wawasaidie kuingizwa na kama yakifanikiwa Basi kila mmoja katika kitengo chao angepewa shilingi milioni mia tano. Na wenzake wotw wamekubali na anayesubiriwa ni yeye. Baada ya maelezo hayo nikamwambia wewe unaamua nini? Akasema yeye hayupo tayari, na aliongeza kuwa alitaka kukutana na mpelelezi aitwaye masimba amueleze hicho kitu kwa kuwa kulikuwa na mtu wake wa karibu anashirikiana na mtu anayeitwa Jimmy pamoja na viongozi wa serikali. Siku ambayo aliondoka hapa kumfuata Huyo mpelelezi, mdogo wangu hakurudi Tena akiwa hai. Amerudi akiwa marehemu." Alimaliza kuongea yule dada wa marehemu huku akiangua tena kilio.

Mishipa ya hasira na uchungu ilikuwa usoni kwa masimba. Kumbe marehemu alikuwa akimtafuta yeye, kumbe marehemu alikufa akitaka kuikabidhi siri mikononi mwake. Kwa nini hakusimama kumsikiliza. Masimba akatulia akifikiria kwa uchungu. TEDDY mpenzi wake alikuwa akihusika katika kifo cha Asteria. Akainuka akitaka kuondoka lakini akashikwa bega. Alipoinua kichwa alikutana na sura ya mama mzaZi Wa Asterina, akimuangalia kwa macho makali, macho ambayo hayakuonyesha woga. Wakaangaliana tena na tena.. Mama akataka kuongea kitu lakini sauti haikutoka.

*********

Walikaa kwa muda mrefu wakiisubiri simu kutoka kwa Teddy. Lakini bado simu yake haikuwa ikipatikana. Kila mmoja alikuwa akichanganywa na Ukimya ule. Lakini wakati wakiendelea kusubiri wakauona mlango ukifunguliwa. Teddy alikuwa akiingia akionekana hana tabasamu lake. Kila mmoja akabaki ameduwaa akimuangalia mwanadada huyu usoni.

"Kuna watu wawili wanatakiwa kufa". Akaongea Tedy kisha ukimya na hamaniko kutoka kwa watu wale likionekana. Kila mmoja alikuwa amekanganywa na maneno ya Teddy. Huna ambaye aliinua kinywa chake kuongea chochote. Mshangao bado uliwazubaisha. Wakiwa bado katika hilo teddy akaingeza.

"Hili Suala lipo mikononi mwa Idara ya Usalama wa Taifa. Vijana wanafanyakazi kubwa sana kutokana na vifo hivi. Masimba amelishikia bango hili suala na muda sio mrefu tunaweza kuumbuka." Teddy akaeleza mienendo yote ya masimba, mazungumzo yake na ndugu wa asteria. Na kuhusu watu wao waliouawa usiku wa kuamkia leo na kutoweka kwa Simu zao. "Sasa ni lazima mama wa Asteria na dada yake wauawe katika njia yoyote. Tukiwaachia hapa kisha wakakutana tena Na masimba kamwe hatutaweza kupona. Ni lazima wafe na ikibidi Hata Masimba Naye atawafuata...

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 006

Lazima tuwaondoe duniani, na ikibidi hata masimba atawafuata huko huko kuzimu. Hili suala bado gumu sana. Kukutana kwa masimba na wenzetu kule coco beach, kutoweka simu ya Marehemu Asteria pamoja na simu za vijana wetu, ni moja kati ya vitu hatari sana. Ninachoamini mimi Dada wa marehemu Asteria kuna kitu atakuwa anakijua kuhusu kifo cha mdogo wake, nilazima asteria alimpa siri kuhusu sisi. Kwa hiyo ilikujiweka katika mazingira sahihi nilazima tuwaondoe hawa watu. Nina amini hata masimba kuna kitu amekigundua kwangu, nadhani hata pale coco beach aliniona ndio maana hawakukaa sana. Sasa ni wajibu wetu kufanya kile ambacho kitatuweka salama zaidi. Kwani hata watu wa Idara ya Usalama Wa Taifa wamecharuka katika hili, nahawa ndio wanaompa nguvu huyu mwanaume, kwahiyo kwangu mimi nimemaliza na hii ndio mipango yangu." Aliongea Teddy kwa kirefu huku akiwaangalia wanaume wale wa tatu kwa zamu.

Kila mmoja alionekana yupo mbali kimawazo, kila mmoja alionekana akitafakari kuhusu jambo hili. Ukimya ukachukua nafasi katika eneo la chumba chote. Ni kweli hakikuwa kitu kidogo, lakini licha ua ukubwa wa kitu hiki hauwezi kuzuia mapambano. Mapambano sababu ya kupigania mamilioni yao ya Shilingi. Walikuwa tayari kumuua mtu yoyote kwa sababu ya pesa. Kila mmoja alikuwa akiutafakari ujumbe ulioletwa pale. Walihitajika kuawa watu wawili, na ikibidi watu watatu. Watu ambao watawafanya wao waishi kwa usalama zaidi. Watu ambao watakifanya kitendawili cha mzigo wao kubaki katika usiri nzito. Lakini watamuuaje masimba? Nani atainua bastola na kulenga kichwa ama kifua cha masimba? Hayo yalikuwa maswali ambayo yalikuwa yakipita vichwani mwao. Bado ukimya ulitawala na bado hapakuwa ni mtu wa kuzungumza. Kama Idara ya usalama imecharuka nini hatima yao katika hili. Walijua hapakuwa panahitajika nguvu, wakajua kutumia nguvu nikutafuta kushindwa katika hili pambano. Kila mmoja alitaka kuwa huru katika hilo. Kama simu za vijana wale zimetoweka, na simu zenyewe zilikuwa na mawasiliano walioyafanya na vijana hawa, nini ambacho kingewaponyesha.. hapo ndio walipouona Umuhimu wa kumuondoa Masimba kwanza kabla ya dada na mama wa Asteria. Kwa mara ya kwanza Jimmy aliamua kusimama kuzungumza kuhusu hilo. Kila mmoja alikuwa akimtizama akisubiria kusikia kile alichotaka kukizungumza.

******
Baada ya kumaliza kuongea na mama wa Asteria sambamba na dada yake, masimba akaona ni muda wa kuelekea nyumbani kwake huku akifikiria ni kipi ambacho atakifanya kuhusu mpenzi wake. Hakutaka kukurupuka katika hilo lakini kule kuambiwa na dada wa asteria kuhusu ukaribu wake na mmoja ya watu wenye mzigo huo, kulizidi kuitoa picha kuwa bado Teddy ni mhusika katika matukio yote ya mauaji. Ukianzia kuikuta mamba yake kuwa namba ya mwisho kuwasiliana na marehemu Asteria, kumuona coco beach usiku ule, kuonyesha wasiwasi alipomkuta akikagua miili ya watu wale mawili ni matukio ambayo yalimuaminisha na kuzifanya hisia zake kuwa sahihi. Licha ya kutembea pasipo na tahadhali, lakini bado alitanbua kuwa alikuwa na vijana wake wakimuangalia kila hatua. Alitambua umuhimu wa vijana wake. Wakati anataka kutokea kituo cha magomeni Hospital, akavutiwa na kitu fulani ambacho alikiona upande wa pili wa barabara. Licha ya kitu hicho pia hata simu yake ilipokea ujumbe kutoka kwa vijana wake. "Kuna vichwa viwili Vimeunda Urafiki nawe" ulisomeka ujumbe huo. Haikuwa kazi ngumu kuijua maana halisi ya ujumbe ule. Hata macho yake yalipoangaza katika maeneo yale ni kweli yakakutana watu wawili ambao walikuwa katikati ya umati wa watu ambao walikuwa wakisubiri usafiri wa kuelekea makwao. Ingawa watu hawa walijichanganya na abiria, lakini bado muonekano wao ulikuwa ni wakipekee, bado hawakuonekana kutulia hasa machoni mwao. Kila wakati walikuwa wakimwangalia Masimba kwa namna fulani ya kipekee. Aina ambayo haiwezi kufichika machoni kwa watu wenye fani ya ujasusi. Watu wale wawili, wakike na kiume bado walisimama wakionekana wakisubiri kitu, hata pale magari yaliposimama bado hawakupanda, bado hawakuonyesha kama walihitaji kupanda. Masimba akatabasamu kisha kupiga hatua akielekea pale waliposimama. Alitembea sawa na watu wengine waliokuwa wakiivuka barabara. Hata walipofika kituoni, gari ya kwanza kusimama masimba akapanda akiwaacha watu hawa wakihamanika. Lakini bahati nzuri konda aliwaona na kumuomba dereva asimame. Ni wakati watu wale wakipanda ndipo masimba alipoisikia miluzi na mayowe kutoka nje, watu waliokuwa wakishangilia kitu walichokiona. Akaruhusu macho yake yaelekee huko. Hapo hata yeye akashikwa na butwaa la muda, butwaa huku macho yakivutika kwa kile kinachopita nje.

Alikuwa akitembea kama twiga nyikani, alikuwa akitembea kama anaiogopa ardhi. Miguu ilitua kwenye ardhi kanakwamba haitaki. Alitembea akijitupa huku na huko. Kivazi chake kifupi kilikuwa kikiwavuta na kuwakata shingo wanaume kwa wanawake. Hata alipokuja kuingia kwenye daladala bado masimba alikuwa akimtizama, bado alikuwa akimuangalia twiga huyu, twiga alietoroka mbugani na kuja mitaani. Binti alikuwa haonyeshi kujali, haonyeshi aibu na kingine hakuonyesha kwamba labda angemuonea yoyote aibu. Ndio kwanza alikuwa akijipinda na Kujigeuza. Alikuwa akijishika hapa na kujiachia hapa. Hata pale alipokuwa akimtizama alihisi alikuwa akitizamana na Heaven Sent, ama alikuwa akiitizama picha yake. Alikuwa mzuri, alikuwa ameumbwa na alikuwa akivutia hata kutizamwa. Ni hapo binti yule alipotupa macho yake usoni kwa Masimba. Hata masimba alipomtupia jicho na hata macho yao kukutana, Kuna kitu kilionekana machoni kwa mwanamke yule. Kitu ambacho hakikuwa kigeni wala kipya machoni kwa Masimba.

WAKATIZAMANA ZAIDI NA ZAIDI..

KESHO

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 007

Wakatizamana tena na tena. Masimba hakuwa mjinga katika kile ambacho kilikuwa kikitokea pale. Muda wote alimuangalia yule msichana akikitafuta kile ambacho kilifichwa upande wa pili. Alikitafuta kile ambacho kingempa picha huyu alikuwa nani. Macho pekee ya mwanadada yule hayakuweza kumpa jibu la kwamba huyu alikuwa nani. Jicho legevu kama mtu alieupoteza usingizi kwa muda mrefu halikuweza kumpa majibu alioyataka. Kwa jicho la mwanamke huyu hata jasusi ama mpelelezi wa kiwango cha aina yoyote asingeweza kuligundua hilo. Akakumbuka kuwa kulikuwa na watu wengine, watu ambao walikuwa wakimuandama kila hatua. Aliwatambua na kuwajua, alihitaji kuutafuta ukweli kutoka kwa hawa na yule mwanamke alievaa mavazi ya kutamanisha. Alitaka kujua kama kunakujuana, kutambuana na hata kufahamiana. Alitaka kuifanyakazi kwa kutumia akili zake. Macho yake yakatembea taratibu yakizibwa na gazeti. Muda wote alihitaji kupata ujumbe kutoka kwa wenzake wakimjulisha kuhusu huyu mwanamke. Lakini hilo halikuwezekana kwa wakati ule, si kuwezekana kwa kuwa hawawezi, la hasha! Hata vijana hawakuwa wamemjua huyu mwanamke. Akatulia na kutulia tena, punde konda akatangaza kituo kinachofuata. Akili yake ikachemka kwa haraka, kilikuwa kipimo sahihi cha kugundua kama yule mwanamke ni abiria ama alikuwa mmoja kati yao. Akainuka naye akijiandaa kushuka.. macho yake muda wote yalikuwa machoni kwa watu ambao waliambatana naye, kuambatana kwa maana ya kumfuatilia. Bado alikikosa kile ambacho alikuwa akikitafuta. Bado hakufanikiwa kugundua kama walikuwa wakifahamiana ama lah. Akatembea akisogea mlangoni. Alikuwa makini kwa kila hatua, mikono yake ilikuwa tayari kuifanya kazi kama ingebidi. Daladala ikasimama kituo cha kinondoni mkwajuni. Masimba akashuka akiwa pamoja na abiria wawili watatu. Baada ya kushuka hakutaka kuangalia nyuma. Alitembea akiingia hapq na kutokea pale. Safari yake Hiyo ikaishia Eneo la kinondoni studio. Licha ya kutambua kuwa alikuwa akifuatiliwa tokea pale magomeni, cha kushangaza hakuwaona tena watu wale. Alitumia mbinu zake zote lakini bado hakufanikiwa kugundua chochote. Akatembea sasa akiivuka barabara fulani katika mitaa ile ya kinondoni, wakati anakikaribia kituo fulani cha teksi, mara akaisikia sauti ya mtu ikimuita, sauti ambayo ilikuwa ngeni kwake. Akaipuuza kama hakuwa amesikia. Lakini kwa mara nyingine sauti ile ilikuwa ikimuita tena. Sasa alionekana mtu yule akimuita tena huku akimfuata kule alipokuwa akielekea. Ilikuwa sauti ya mwanamke, sauti ya mtu ambaye hakuwahi kumuona achilia mbali kuisikia sauti ile. Akajipa kazi ya kugeuka, ni kweli akageuka.. macho yake yakamuona mtu, mtu yule yule ambaye alipanda pale kwenye daladala, mtu yule yule ambaye alimuacha ndani ya daladala. Lakini sasa alikuwa akimuita tena kwa jina lake, jina ambalo halitumii sana. Hakuuficha mshangao, hakuuficha kwa mtu kama yeye kugundua. Amenijulia wapi? Kwa nini anifuate mpaka huku? Nini anakitaka kwangu? Alijiuliza maswali mengi huku akisimama kumsubiri mwanamke yule.

Mwanamke yule akatembea kwa mwendo ule ule wa kuogopa kuikanyaga ardhi. Bado masimba alikuwa akipata kukitafuta kile ambacho alikikosa kule alipotoka. Bado mwanamke yule hakuonyesha uhatari na vilevile hakuonyesha kama alikuwa ni mtu wa misukosuko. Wakakutana na kwa mara ya kwanza wakishikana mikono. Wakasalimiana wakiangaliana. Masimba alimuangalia machoni kwa muda mrefu akikitaka kile ambacho alikihisi. Lakini bado huyu hakuonyesha kama ni mmoja kati ya hao. Bado jicho lake legevu lilitengeneza urembo wa kumvutia mwanaume yoyote lijali. Akataka kusema kitu, lakini kabla hajafanya hivyo akausikia mlio wa simu yake. Akaichomoa kutoka mfukoni na kukutana na kiboksi cha Ujumbe mfupi wa maneno, kuonyesha kuna ujumbe umetumwa. Kidole kikashuka na kuruhusu ujumbe ule kufunguka.

"Ni mmoja wao kuwa makini." Ulisomeka ujumbe ule. Ujumbe uliomfanya atabasamu na kucheka. Kwa mara ya kwanza alikuwa amekutana na mtu ambaye amefanikiwa kuyarahai macho yake. "Ni Mmoja Kati yao" neno lile likajirudia kichwani. Akahamisha macho kwa mwanamke huyu. Bado akakutana na jicho legevu, jicho ambalo liliuficha uhalisia wa kikazi.

"Nadhani hatutaweza kuongea kwa sasa. Chukua mawasiliano yangu nitafute saa mbili usiku. Bila shaka unanifahamu sana hivyo na mimi nataka nikufahamu." Aliongea Masimba huku akitoa business card yake na kumkabidhi mwanamke yule, huku akiondoka katika eneo hilo.

*********

Alishuka na kuingia nyumbani kwake. Akili yake ilikuwa imevurugwa kutokana na mambo kuonekana kuharibika mapema sana. Kitendo cha kuingia kwa masimba katika sakata hili, hakikuwa kitu kizuri kwake na kwa wengine. Hakutakiwa masimba kuijua hii mipango. Lakini kuuawa kwa Asteria wakati akitaka kuonana na masimba kumeharibu kila kitu. Kifo cha Asteria ndicho kikichomuibua masimba. Kutoweka kwa simu ya marehemu na mazungumzo yale, alihisi masimba atakuwa amegundua kuwa yeye ni mshirika wa Mpango ule. Teddy alijikuta kichwa chake kikiwa kizito. Teddy alijikuta katika wakati ambao hakuwahi kuwa nao. Akaelekea chumbani kwao, akaongoza mpaka sehemu anapoweka bastola yake. Akafungua na kuichukua kisha kuishika mkononi. Aliitizama huku akiwaza. Alikuwa tayari kumuua Masimba iwapo atagundua kama anaijua siri yao. Alikuwa tayari kumuua mpenzi wake kwa sababu ya pesa. Akasimama akiiangalia bastola. Hapo akakumbuka penzi lao lilipoanzia. Alikumbuka mengi.. moyo ukakosa ujasiri. Muda ule ule akahisi mikono ikimshika kiunoni kisha sauti nzito ikasikika. "Usiogope Mpenzi Nakupenda Sana... ilikuwa sauti ya Masimba. Teddy hakutegemea, hata alipogeuka na macho yao kukutana.. Hakuweza tena kumuangalia MASIMBA..

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 008

Usiogope nakupenda sana mpenzi. Ilikuwa sauti ya masimba, sauti ambayo ilitokea nyuma yake.hakuwa amejiandaa na hilo, hakuwa amelitegemea lile la masimba kuwepo pale ndani. Hili likamnyong'onyeza. Akatamani kuongea kitu lakini maneno hayakutoka. Hakujua muda ambao masimba alifika nyumbani, hakutegemea uwepo wake hapo, na hata pale alipokumbuka kitendo alichokifanya, alichoka kwa kuwa alitambua kuwa masimba alikuwa amekishuhudia kitendo kile. Akaiona akili yake ikishindwa kumsaidia katika kulitatua hili ambalo lilikuwa mwisho wake. Hata pale mikono ya masimba ilipokuwa akipapasa kiuno chake, bado Teddy hakuweza kumjibu. Bado bastola yake ilikuwa mkononi, bado hasira zilionekana usoni, na hata dhamira ya mauaji ilijengeka kupitia macho yake. Hakuweza tena kumuangalia masimba, hakuweza tena kuuinua uso wake kumtizama. Alitazama pembeni na alikuwa ameinamia chini. Mwili ulikuwa unatetemeka, alijikuta kwenye wakati mgumu kupambana na moyo wake. Moyo uliojaa mapenZi juu ya masimba, moyo ambao haukuwahi kumpenda mwingine zaidi ya huyu mwanaume. Mwanaume ambaye alichukua asilimia mia moja katika moyo wake? Ni vipi ataweza kuitumia bastola kumlenga huyu mwanaume? Ni vipi angeweza kukiruhusu kidole chake kutekenya kitufe kuruhusu risasi imuue Masimba? Ni vipi pale atakapoiona Risasi ikimtupa masimba chini huku damu zikisambaa? Hapo akauona ugumu, ugumu wa kufanya kile ambacho alitaka kukifanya, lakini vilevile aliyafikiria mabilioni ya shilingi. Kwa mara nyingine akakiona kichwa chake kikitaka kupasuka. Lakini mpapaso wa mikono ya masimba ukamfanya teddy aachie mguno. Mpapaso ambao ulipanda mpaka kwenye kifua chake kilichobeba viazi vidogo. Mikono hiyo ikatulia hapo kwa muda ikitomasa na kuchezea kwa ustadi mkubwa. Hilo likaanza kumlegeza teddy, likamuacha teddy akisinzia na kulegea. Masimba akamgeuza na kufanya wote watazamane. Watazamane katika namna ya kuhitajiana. Jicho lilikuwa usingizini na hata midomo ikawa tayari kupokea zawadi. Wakatizamana zaidi, muda huu nguo zilikuwa zikitupwa chini baada ya kuvuliwa. Bastola ilianguka pasipo hata teddy kugundua. Alikuwa akihema kama mwizi, alikuwa akihema kama ametoka kukimbia mbio ndefu. Hakuwa teddy yule aliekuwa ameapa kumpoteza masimba. Hakuwa teddy yule mwenye uwezo wa kunyoosha mkono kumuua masimba. Huyu alikuwa kondoo, kondoo anayetii mamlaka ya bwana. Akasogezwa kitandani, hata yeye mwenyewe akasogea, akakalishwa kitandani, hata mwenyewe akakaa, na hata kulala, akalala huku macho yake yakiwa yamefumbwa na kufumbika. Midomo bado ilihitaji kupokea kitu, kitu ambacho kingeianzisha safari nyingine. Ilikuwa hivyo.

*****
Alishtuliwa na mlio wa simu yake, akaupeleka mkono pembeni yake ambapo alikuwa amelala masimba. Lakini akashangaa kutokuwepo kwake. Bado simu yake iliita, lakini aliendelea kuipuuza. Sasa alikuwa akiinuka kutoka pale kitandani na kuelekea kule sebuleni. Akalifunua pazia akidhani atakutana na masimba hapo, lakini hapakuwa na mtu. Hilo likamshangaza tena na tena. Haikuwa kawaida ya masimba kumuacha kitandani. Wakati akiendelea kuumizwa na hilo bado simu chumbani iliendelea kuita. Safari hii mpigaji alikuwa akipiga kwa mara ya tatu. Akakata shauri kurudi chumbani kwenda kuipokea simu hiyo. Akazivuta hatua zake taratibu akiwa mtupu kama alivyozaliwa.akasogea na kuingia chumbani huku mawazo yakiwa ni wapi alipoelekea masimba. Akaifikia simu na kuichukua, macho yakatua juu ya kioo.. akakutana na jina la mtu alieufanya moyo wake upige kwa haraka. Jimmy Lambert ndiye aliekuwa akiipiga simu. Akakipeleka kidole chake na kupokea simu.

"Jimmy." Aliita tedy kwa sauti ndogo yenye kuonyesha uchovu.

"Vipi umelala au?" Lilikuwa swali kutoka kwa Jimmy.

"Yeah! Nilikuwa nimelala, kuna lolote? Alijibu kisha kuuliza.

"Naomba Uje Tegeta muda mfupi ujao, kuna mtu nataka mkutane, mfahamiane na mtambuane. Tumeona tukutafutie mtu wa kusaidiana naye." Alijibu Jimmy kisha akakata simu bila kusubiri jibu kutoka kwa Teddy. Hilo la kutafutwa kwa mtu likaupa mashaka moyo wake. Ni kweli pesa alizitaka na kuzihitaji. Ni kweli anampenda masimba kuliko maelezo. Lakini hata kama atamuua masimba, wapo wanaume wengine ambao watamuoa. Kinachotakiwa ni kupanga njia ipi sahihi ya kumuua. Kwa mara nyingine roho yake, akili yake ilikuwa tayari tena kumuua masimba. Alikuwa amedhamilia na alikuwa ameamua kumpoteza. Alichokifanya ni kujiandaa kwa safari ya kuelekea huko tegeta huku akiwa na nguvu na maamuzi sahihi.

Wakati yeye akitoka na kulifunga geti, masimba alikuwa nyumba ya tatu kutoka pale. Alikuwa amesimama hapo kwa muda mrefu akitizama kila kitu ambacho kiliendelea pale. Muda mfupi akamuona mpenzi wake akilifunga geti na baada ya hapo akamuona akiondoka pale kwa kutembea kwa miguu. Bado alitulia akiendelea kuangalia kila kitu ambacho kilikuwa kikitendeka pale. Bado mpenzi wake aliendelea kutembea akielekea kituo cha daladala. Hilo pia lilimpa nafasi ya kumfuatilia pasipokuonekana. Simu ilikuwa sikioni akiwasiliana na vijana wake, alikuwa akiwaeleza kila kitu cha kufanya. Aliwaaachia wao kazi ya kumfuatilia Teddy. Alichokuwa akipokea ni maelezo ya nini kinaendelea katika hilo.

******
Teddy alitembea mpaka kituo cha daladala, alipofika hapo akatulia akiangaza macho yake huku na huko. Alikuwa ametulia kwa muda akitizama kila mienendo ya watu. Alikuwa na hisia za kufuatiliwa, lakini kila alipopitisha macho yake sehemu zote, hakuweza kumuona mtu ambaye labda angepata mashaka naye. Baada ya kuhakikisha hilo, akaingia kwenye daladala na muda mfupi gari likaondoka likielekea Tegeta. Ilikuwa safari ambayo kwake ilikuwa muhimu sana. Walikuwa na mzigo wa mamilioni ya shilingi lakini bado haikuwezekana kuuza kutokana na matukio haya yanayoendelea kutokea hakuwa tayari kuiacha pesa ile kwa sababu ya mwanaume. Moyoni alijisemea kwamba labda angekuwa mama yake ndipo angefanya hivyo. Wakati akiwaza hakujua kwamba kuna watu walikuwa siti ya nyuma yake wakimtizama. Walikuwa vijana wawili wadogo kiumri, vijana ambao kwa kuwaona ungedhani labda ni wanafunzi wa sekondary. Lakini haikuwa hivyo, hawa walikuwa vijana kutoka kitengo nyeti katika nchi hii. Walikuwa wakiendelea kuzungumza hili na lile, huku mara moja moja wakimtupia jicho mwanadada huyu. Kilikuwa kitu kizuri sana kumfuatilia mtu ambaye hajui kuwa anafuatiliwa. Gari ilipofika tegeta kwa ndevu vijana wale wakasimama tayari kwa kushuka. Hata teddy naye alikuwa akishuka hapo. Alitangulia yeye kushuka, kisha wakafuatia wao kushuka. Baada yakushuka vijana wale wakangoza kuelekea barabara fulani. Hata teddy alikuwa nyuma yao akifuata barabara ile. Hakujua kuwa waliombele yake hawakuwa mabishoo kama alivyodhania, bali walikuwa makachero wakifuatilia kila hatua yake na kila kitu anachokifanya.

ITAENDELEA

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 009

Hakujua kuwa alikuwa njia moja na wanausalama. Hakujua kuwa vijana waliombele yake walikuwa wanausalama, tena wakimfuatilia yeye. Bado aliongoza akitembea kwa umakini, akichungulia na kuangalia kila sehemu kwa chati. Alikuwa tayari kumuua mwanaume anayempenda kwa sababu ya pesa. Licha ya kuwa tayari lakini hakuujua mwisho wa mambo yale utakuwa nini. Kingine kilichomtatiza ni mtu ambaye ameambiwa kuwa ameongezwa katika kazi ile ya kumfuta masimba katika uso huu wa dunia. Kilikuwa kitu kigumu mwanzo lakini kila alipokumbuka kifo cha Asteria na Rafiku yake, alijikuta akinong'ona mwenyewe. Muda nfupi baadae alikuwa akiingia ndani ya Bar moja maeneo yale ya tegeta. Baada ya kuingia, akaongoza mpaka moja kwa moja katika vyumba vya eneo lile. Akauendea mlango wa chumba ambacho huwa wanakutaniana. Akaugonga mlango katika namna ambayo ilitambulika ama kuzoeleka miongoni mwao. Mlango ukafunguliwa kisha akaruhusiwa kupita. Alipoingia mlango ukafungwa tena. Macho yake yakatembea usoni kwa kila mmoja, shauku yake ilikuwa ni kumuona mtu ambaye aliambiwa atakuwa nao katika sakata lile. Kila mmoja ndani ya chumba kile alikuwa kimya, ukimya ambao uliyaruhusu macho yao kutizamana. Sura ya mwanamke mrembo ndio sura pekee ngeni ambayo ilimpa majibu kuwa huyu alikuwa ndie mtu alieletewa ili kusaidiana naye. Akasogea macho yake yakilazimisha kutizamana na mwanamke huyu. Alikuwa akifanya hivyo kutaka kujua kama huyu mwanamke atakuwa mmoja kati ya watu wa aina yake. Ni kweli walitizamana, ni kweli waliangaliana na kuangaliana tena na tena. Lakini hakufanikiwa kukiona kile alichokuwa akikitafuta. Macho ya mwanamke huyu hayakumuonyesha kile alichokuwa anakitafuta. Hayakumjulisha kama yeye alikuwa nani. Bado yalikuwa macho ya kulegea, macho ya kusinzia na kibaya zaidi hayakumuonyesha chochote kile. Hilo likaonyesha kumpa mashaka. Akatafuta mahala puzuri na kukaa. Bado macho yake hayakuacha kuonyesha mashaka. Bado hakumuamini mwanamke yule. Ndio alikuwa mrembo, ndio alikuwa mzuri na alivutia katika kutizamwa na hata kuwekwa ndani na wanaume. Lakini licha ya uzuri huo bado hakukiona kile ambacho kingempa picha, picha kwamba anaweza kuzimudu kashkash zote za wanausalama. Akauvuta muda huku akimtizama Jimmy na wengine waliokuwepo pale ndani. Alitaka kusikia kutoka kwake, alitaka kusikia kwamba huyu ni nani, na ni vipi atamudu kupambana na masimba. Jimmy ni kama aliyasoma mawazo ya Jenipher. Akasimama kutoka pale alipokaa kisha kupiga hatua kusogea mpaka pale alipokaa Jenipher. Akamuangalia kwa muda kisha akanena.

"Nimekuletea Shetani yule akusaidie kumuondoa masimba katika uso wa dunia hii.." yalikuwa maneno yaliozunguka kichwani kwa teddy. Hakuuamini ushetani wa mwanadada yule. Alimuona ni kama wadada wa mjini na asingeweza chochote.

"Jimmy unadhani ataiweza hii kazi? Tambua tunachokifanya ni kazi ya kifo. Na hii kazi tunaifanya kwa siri sana. Pia tambua watu tunaopambana nao hawana masihara. Una uhakika yule mrembo ni shetani kweli?" Aliongea Jenipher akionyesha kuwa na mashaka.

Tabasamu likachanua usoni kwa Jimmy, kisha likafuatiwa na kicheko, kicheko ambacho kilitumika kama jibu kwa maswali ya Teddy. Wote wakasimama kwa pamoja kisha kushikana mikono. Mkataba ukaingiwa na makubaliano kufikiwa. Kilichobaki ilikuwa kazi ya kumuondoa Masimba, kisha wabia wenzao, harafu kugawana mzigo wao.

********

Wakati Vijana Wake wakiwa tegeta, masimba ndio kwanza alikuwa akiiisimamisha gari mtaa wa pili kutoka nyumba anayoishi Jimmy. Baada ya kushuka akaufunga mlango. Baada ya kuufunga mlango akaangaza huku na huko, aliporidhika akatembea bila wasiwasi kuelekea ilipo nyumba ya Jimmy. Hakuwa na wasiwasi juu ya kuingia katika jumba hilo kwani vijana wake walikuwa wakimpa taarifa za kile kilichokuwa kikiendelea kule tegeta. Alijua ndani ya muda huo alikuwa na uwezo wa kuingia na kutoka pasipo wasiwasi wowote. Alitembea kama mwananchi wa kawaida akiangalia hiki na kangalia kile. Mtaa wote ulikuwa kimya, hapakuwa na watu ambao wangemsumbua ama kumtilia mashaka. Mzigo umekamatwa na kutangazwa katika vyombo vya habari. Lakini cha ajabu mzigo huu unaonyesha kutokukamatwa, unaonyesha kuna mchezo nyuma ya sakata hilo. Nani yupo nyuma ya jambo hili? Ndio kitu peke ambacho alijiuliza masimba pasipo kupata majibu. Akaendelea kutembea huku mazingira yakimpa uhuru wa kufanya kitu. Sasa alikuwa akiangaliana na jumba la Jimmy Lambert. Lilikuwa jumba la kifahari, likiwa limezungushiwa Uzio, uzio ambao ulikuwa mrefu kiasi chake. Ukiondoa hilo pia jumba hilo lilizungushiwa nyaya maalum za umeme ambazo zilisaisia kuongeza usalama wa jumba lile. Pia licha ya hivyo vitu, lakini pia hapakuwa na walinzi. Mlinzi alikuwa mmoja ambaye alikaa kwenye geti la mbele. Baada ya kuliangalia vyakutosha sasa aliamua kuingia ndani. Huyu aliamulia kuingia katika Geti la mbele. Akasogea akitembea kawaida sana. Mlinzi wa kampuni binafsi alikuwa mlangoni mkononi akiwa ameshikilia bunduki aina ya gobole. Masimba akasogea zaidi na zaidi mpaka karibu kabisa na mlinzi yule. Kabla hajazungumza naye chochote, Masimba akachomoa simu kisha kumpa mlinzi yule. Mlinzi akasita kwanza kuipokea. Akamwangalia mtu huyo usoni, mtu ambaye alikuwa akimpa simu pasipokuongea naye chochote. Macho yake yakakutana na tabasamu, tabasamu ambalo liliitoa hofu ya mlinzi yule.

"Ongea Na Jimmy Lambert ana maagizo anataka kukupa." Akaingea Masimba pasipo masihara. Mlinzi yule akalifanya kosa la kupiga hatua kumsogelea Masimba. Hakufanikiwa kusogea tena kwani pigo moja la karate likatua Shingoni. Mlinzi akatambarajika chini. Akamvuta na kumuweka kando ya maua ya jumba lile. Alipohakikisha hawezi kuonwa na watu, alilisukuma geti na kujitoma ndani. Alitembea kwa tahadhari kubwa mpaka uani mwa jumba lile. Akasimama hapo akiangalia zilipo camera za usalama za jumba la Jimmy. Baada ya kuhakikisha hamna chochote kile, akachomoa funguo zake malaya kisha kuichomeka sehemu, punde mlango ulikuwa ukifunguka na kumruhusu Masimba Kuingia. Baada ya kuhakikisha ameingia, masimba akaichomoa bastola yake na kuanza kuingia kila sehemu akipekua. Kwa kuwa alikuwa akipewa taarifa na vijana wake juu ya uwepo wa jimmy na washirika wake, hakuwa na wasiwasi katika kupekua. Alifungua vyuma karibia vyote kwa kutumia funguo malaya na kuvipekua. Hakuweza kupata kitu chochote. Wakati anaingia kwenye chumba anacholala jimmy, ndipo hapo alipouona mlango mdogo, mlango ambao alizani labda ni wachoo ama bafu.. lakini alipoutingisha ulikuwa mgumu na haukuwa unafunguka kwa Funguo Malaya.

MASIMBA AKATULIA

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 010

Mlango ulikuwa mgumu na haukuweza kufunguka hata kwa funguo malaya. Hilo likamfanya masimba atulie kwanza. Alitulia akiwaza ni kipi cha kufanya ili kuufungua mlango. Akawaza na kuwazua huku akijaribu mara kwa mara kuufungua mlango. Lakini bado mlango ulikuwa mgumu kufunguka. Akaachana na kimlango hicho kisha kuiendea droo ya kitanda. Hapo pia akatumia funguo malaya kufungua, safari hii alifanikiwa. Baada ya kuifungua droo ile, akayatupa macho yake kwa chati ndani yake. Cha kwanza kukiona zilikuwa funguo kama tano, funguo ambazo mara moja alitambua kuwa ni zile ambazo huwenda zinatumika kuufungua mlango ule. Akazitwaa kisha kurudi pale mlangoni. Zoezi la kufungua likaanza tena. Safari hii haikumchukua muda, kimlango kile kikafunguka.. macho yake yakapokewa na mabegi matano, mabegi ambayo aliyatambua kuwa ndio ule mzigo ambao ulitangazwa kukamatwa uwanja wa ndege. Kichwa chake kikachemka kwa haraka sana, alitakiwa kuondoka na mabegi yale katika muda ule. Alitaka kuliacha hili suala katika kutuhumiana wenyewe kwa wenyewe. Lakini kuna kitu kimoja kilikuwa kikimtatiza.. mzigo huu usingeweza kutoka pale airport kwa nguvu ya Jimmy pekee. Jimmy hakuwa na uwezo wa kuishawishi Idara ya Usalama pasipo kuwepo kwa msaada wa mtu mwingine hapa. Mtu huyo ni nani? Lilikuwa swali pekee lililosumbua kichwani mwake. Alitambua lazima kuna uwepo wa mtu tena mkubwa sana katika sakata lile. Kwa mara ya kwanza majukumu yakaendelea kuongezeka. Sasa alikuwa akimuhitaji huyu mtu wa tatu. Lakini pia alitambua ahadi ya kupigiwa simu na mwanamke yule mrembo. Baada ya kufikiria kwa muda mrefu pasipokupata majibu sahihi, akaona huu ulikuwa wakati wa kuondoka pale ndani, lakini akajiapiza kwamba ni lazima atoke pale akiwa na mzigo ule. Akavuta begi la kwanza kisha la pili, alipotaka kuvuta begi la tatu, masikio yake yakainasa michakato ya miguu ya mtu, ikionyesha kusogea pale mlangoni. Masimba akainuka haraka na kujisogeza pembeni kidogo ya mlango. Punde akauona mlango ukifunguliwa kisha mdomo wa bastola ukatangulia Mbele, bado akaendelea kutulia, hata mtu yule alipoingia bado hakujitoa pale. Alitaka kumfahamu huyu alikuwa nani.akamsubiri mtu yule aurudishie mlango ndipo amkabili. Hilo likafanyika, muda mfupi mtu yule alikuwa akitizamana na mdomo wa bastola huku macho yasio na mzaha yakimtizama. Mtu yule hakulitegemea hilo, akajikuta akiupoteza umakini, sasa alikuwa akitetemeka. Hakuonekana kama ni mjuzi katika misukosuko, bali huyu alionekana kuwa mgeni katika medani hii ya mapambano. Masimba akaendelea kumtizama huku bastola yake ikiwa imelengwa kwenye paji la uso la mwanaume yule. Mara tukio la ajabu likatokea, tukio ambalo lilimfanya masimba aamini kuwa huyu mtu alikuwa mbwa koko. Mkojo ulikuwa ukimtoka na kulowanisha mavazi yake. Hilo lilimfanya masimba apange kumtumia katika kuyaondoa mabegi katika chumba kile. Punde alikuwa akiishusha bastola na kuanza kumtizama mateka wake. Hakuongea naye chochote zaidi ya kumpa Ishara ya kufanya kile ambacho alitaka kukifanya. Muda mfupi walikuwa wakitoka nje huku wameongozana, mateka yule akiwa na mabegi mawili makubwa, hata masimba naye ilikuwa hivyo. Bastola ilikuwa mkononi akimuongoza mtu yule njia za kupita. Wakafanikiwa kutoka getini pasipo na ugumu wowote kwani bado mlinzi yule hakuwa amerudiwa na fahamu. Alimuongoza mateka wake mpaka mahali alipoiacha gari yake. Wakapakia mabegi yao na muda mfupi walikuwa wakiondoka hapo kwa pamoja huku bado bastola ikizigusa mbavu zake.

******

Ilikuwa yapata majira ya saa nne usiku wakati Teddy akiwa njiani kuelekea kimara nyumbani kwa dada wa Asteria tayari kwa kwenda kuifanyakazi. Wakati anayavuka mataa ya ubungo, simu yake ya kiganjani ikawa inaita. Akasonya huku akiitoa simu yake kutoka mfukoni. Jina la Jimmy likasomeka kwenye kioo cha simu yake. Haraka akapokea na kuipeleka simu sikioni.

"Rudi mikocheni Haraka." Baada ya maneno hayo simu ikakatwa, rudi mikocheni haraka kisha simu kukatwa ni kitu ambacho kilimchanganya akili yake. Atumwe akawaue ndugu wa Asteria, wakati bado hajakamilisha hilo aambiwe arudi mikocheni tena! Ulikuwa ujumbe ulioonyesha hapakuwa na usalama. Akaavunja sheria za barabarani kwa kugeuza gari sehemu ambayo haikuruhusiwa. Watu waliokuwa pembeni mwa barabara sambamba na askari wa usalama barabarani walikishuhudia kitendo kile kwa karibu sana. Hata walipomsogelea kutaka kumsimamisha, Teddy akawapelekea gari kwa kasi sana, askari wakaruka na kuangukia pembeni. Teddy akakanyaga mafuta gari ikawa inatembea kwa mwendo wa hatari. Kila mmoja alikuwa akiiangalia gari kwa mshangao. Wengine waliahangilia na hata kupiga miluzi, lakini wachache walilaani huku wakitukana matusi mazito. Teddy hakusikia ndio kwanza alikuwa akiipita Changanyikeni na sasa alikuwa akiitafuta mwenge. Kila mmoja aliekuwa akiitizama gari ile ilivyokuwa ikiendeshwa, alifumba macho akiogopa kutizama. Wakati anafika maeneo ya Mwenge mataa, mbele yake akakiona kile ambacho kilimfanya aupunguze mwendo. Mbele yake kurukuwa na diffender tano za palisi na Askari wasiopungua Ishirini, kila mmoja akiwa na Sub Machine Gun akiwa ameilekeza kule lilipo gari la TEddy. Amri ikatolewa akitakiwa kushuka akiwa amenyoosha mikono juuu.. Teddy akatii huku bastola akiiacha ndani ya gari. Aliposhuka chini tu huku akiwa amenyoosha mikono askari wengi walimtambua kuwa alikuwa ni mwenzao, lakini licha ya kumtambua huko hawakuacha kumuuliza hili na lile. Baada ya kama dakika tano walimuachia na kumtaka kuwa muangalifu.

********

Alisimamisha gari nje ya jumba la Jimmy, akashuka na kuingia ndani. Hapo akapokelewa na mwili ambao haukuonekana kama una Uhai. Mbele yake alisimama Jimmy sambamba na washirika wao kila mmoja akionekana kuchanganyikiwa. Tedy bado hakuwa amekielewa kile kilichokuwa kikiendelea humo ndani. Hata pale alipoambiwa aingie chumbani hakuwa bado anatambua kile ambacho kimetokea. Alipoingia chumbani kisha kutupa macho yake pale kwenye hazina yao, Teddy akaporomoka chini akiwa ameishiwa nguvu. Mzigo wao wao wa Mamilioni ya Shilingi ulikuwa umetoweka. Mzigo uliomfanya awe tayari kumuua Mpenzi wake haukuwepo tena. Mzigo uliomfanya amuue Asteria haukuwepo tena. Umeenda wapi? Nani amewazunguka? Masimba? Hapana!! Juma Kitumbe? Inawezekana!!! Yalikuwa mawazo yaliopishana kichwani mwake. Alipoinua kichwa kuwatizama Wenzake, alijikuta Akitizamana na Midomo Miwili Ya Bastola.

NGOMA NDIO KWANZA NI MBICHI

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 011

Alikuwa akitizamana na midomo miwili ya bastola. Washikaji wakiwa katika umakini wa hali ya juu. Teddy hakuamini kile alichokuwa akikitizama. Akataka kujaribu kumuuliza Jimmy kinachoendelea, lakini sauti haikutoka, akabaki akiitizama midomo ya bastola ambayo ilikuwa umbali mfupi kutoka usawa wa paji la uso wake. Akili yake ikaganda, ikashindwa kufanya kazi kwa wakati, mzigo umepotea, harafu tena anashikiwa bastola! Hilo likamchanganya kama sio kumshangaza. Akakitamani kitendo kile kiwe ndoto, lakini bado haikuwa hivyo. Mzigo haukuwepo na kibaya zaidi alikuwa akitizamana na midomo ya bastola. Akainamisha kichwa chini akijaribu kukiamini kile kinachoendea pale. Kwa mara nyingine akainua kichwa kutizama tena, lakini safari hii hakukiona kile ambacho alikiona mwanzo. Hakuwa akitizamana tena na midomo ya bastola, hapakuwepo na watu wawili waliokuwa wameshika bastola. Walipotea na kutokuonekana kabisa. Mbele ya macho yake alisimama Jimmy pekee. Hata Jimmy hakuwa yule wa tabasamu. Huyu alionekana kuchanganyikiwa na hata kukata tamaa. Uso ulikunjamana kwa hasira, sasa alikuwa akimtizama Teddy kwa macho yake makali. Uso wake ulikuwa ukiongea kifo, macho yake yalikuwa yakiitangaza shali. Kila alipokuwa akimuangalia Teddy mishipa ya hasira ilikuwa ikizidi kuharibu taswira yake. Alikuwa akihitaji kuongea na Teddy. Alitambua teddy hakuwa mhusika wa kilichotokea, alimjua tena na pia aliufahamu uaminifu na hata msimamo wake. Asingeweza kukifanya kile. Hilo likampa ugumu kuongea, kitendo cha watu wao kumnyooshea Bastola kilimpa wakati mgumu sana. Alimjua fika katika medani ya mapambano, alimjua fika katika medani ya mapigano, huyu alikuwa ni zaidi ya Jean Claude Van Damme na hata zaidi ya Don Yen na Hata Jet lee. Kitendo cha kumnyooshea bastola ni kumkosea sana. Hilo likamfanya Jimmy awe mnyenyekevu mbele ya mwanadada huyu. Lakini kile alichokitegemea hakikuwa hivyo.uso wa teddy haukuwa katika masihara tena, alimuangalia Jimmy kwa macho yenye maswali lukuki. Akatamani kuongea neno moja lakini hakuipata nafasi hiyo. Teddy alisimama na kupiga hatua bila hata kumuangalia Jimmy. Alitembea akitoka katika jumba lile akiwa ni mwenye hasira sana. Aliuhisi mchezo mzima kuchezwa na watu wake hao ili kumzunguka. Hilo hakuwa tayari kuliona likitokea. Alikuwa tayari kumuua yoyote katika hilo. Alishakubali kumuua masimba sababu ya mzigo ule, sasa kwa nini hawa wanataka kunizunguka?
Lilikuwa swali ambalo lilikivuruga na kukichanganya kichwa cha teddy. Bado Jimmy hakuweza kuongea kitu. Bado jmmy alikuwa akimkodolea macho. Teddy akakiinua kichwa chake kwa mara ya pili kisha kumuangalia tena jimmy. Macho yake yalikuwa yakiongea kitu kingine kabisa. Hakuwa teddy yule mrembo na mwenye tabasamu, huyu alikuwa teddy tofauti kabisa. Bado hakuyaondoa macho yake usoni kwa Jimmy. "Huu ndio Wema wangu? Haya ndio malipo ya kuwasaidia mzigo wenu? Umenisahau mimi ni nani? Umesahau kuwa ninauwezo wa kuwaua kwa muda mfupi tu? Sasa naomba uniambie ukweli, nataka kuujua mzigo uko wapi na nani ameuondoa hapa. Usipokuwa mkweli maiti yako itakutwa humu ndani. Aliongea teddy akimuangalia jimmy pasipo kupepesa macho bastola ikiwa mkononi. Jimmy alijikuta midomo ikimkauka, akajikuta mate yakishindwa kupita kooni. Alimtizama teddy machoni kwa muda mrefu akitamani kuongea kitu. Hakupata neno la kuongea, alijikuta akianza kutetemeka. Jimmy leo alikuwa akimuogopa teddy.

Akaona kukaa kimya kutasababisha makubwa. Kwa sauti ya uoga akaanza kuelezea kila kitu tokea waliporudi na kuikuta maiti ya mlinzi, akaeleza walivyoingia ndani wakishuhudia mzigo wao ukiwa haupo. Hakuficha chochote kile. Baada ya Jimmy kumaliza kuongea teddy hakuongea kitu. Alipiga hatua mpaka nje pale ulipolazwa mwili wa mlinzi yule. Akaufunua na kuuangalia kwa makini. Cha kwanza kukiona ni jeraha shingoni kwa marehemu yule.

"Masimba!" Lilikuwa neno pekee kutoka kwa teddy. Hili likamfanya jimmy aliekuwa amesimama nyuma kidogo ya teddy asogee na kuonyesha kushangazwa. "Masimba aliingia hapa na ndiye aliefanya hiki kitu. Na kama kweli ni yeye alieuchukua mzigo, itabidi uwasiliane na mwamvita muda huu, ili watakapo kutana ajue anatakiwa kufanya nini." Aliongea teddy akitoka pale akionyesha ni mwenye mawazo.

*********
Ulikuwa usiku wa saa mbili na nusu pale simu ya Masimba ilipotoa sauti kuonyesha kulikuwa na ujumbe mfupi wa maneno. "Upo wapi Masimba? Uliuliza ujumbe ule. Masimba akatulia kwanza kujipa muda wa kufikiria.

"Nipo nyumbani!" Alijibu nakutulia tena.

'Bila shaka utakuwa upo tayari kwa sasa kukutana na mimi?" Ujumbe mwingine ukaonyesha kuuliza.

"Yeah! Naomba tukutane Ngamia Pub kigamboni, nadhani panafaa kwa aina ya maongezi yetu.". Alituma ujumbe huo ambao ulipokewa kwa ukimya wa muda mrefu. Kwa mtu aina ya Masimba aliutambua ukimya ule. Aliutambua kwa maana moja. Mwanamke yule alikuwa akifanya mawasiliano na watu wengine, watu ambao alitambua lazima watakuwa wameshaanza kuelekea sehemu ya mkutano wao. Hakuwa na shaka kwa kuwa Charty John alikuwepo sehemu ya tukio akimuangalia kila aingiaye na kutoka. Hakuwa na shaka kuhusu hilo.

Muda mfupi alikuwa akiingia maliwatoni, akajimwagia maji, kisha kutoka na kuyaendea mavazi yake. Baada ya kuvaa na kujiangalia akachukua bastola zake mbili revolver colt na dernng up automatically na kuziweka sehemu yake. Baada ya kumaliza hapo akaweka vitu vyake sawa pale ndani. Muda mfupi alikuwa akiliacha jumba lake akielekea sehemu ya tukio akiwa katika tabasamu la aina yake. Siku zote alipenda kucheza na watu wa aina yake, alipenda kucheza na watu walioupenda mchezo ule. Alitaka kumalizana na hawa kisha kurudi kwa teddy. Alitaka kumfanya kuwa wa mwisho.

*****

Sehemu kubwa ya eneo hili la mjimwema lilikuwa limechangamka watu wakionyesha kuifurahia siku hii. Muziki ilikuwa ukisikika, muziki ambao ulikuwa ukiwa burudisha vijana kwa wazee. Sehemu yote ilikuwa katika hali ya kupendeza na hata kuvutia. Charty alikuwa pembeni kabisa macho yake yakiwa busy kutizama kila tukio linaloendelea hapo. Muda mfupi akaiona gari aina ya Toyata ikisimama eneo la maegesho. Macho yake yakavutiwa na watu walioshuka kwenye gari ile. Hayakuvutiwa kwa uzuri wa mavazi yao ama sura zao, bali alivutiwa kwa kuwa ndio wale aliowaona mchana wakimfuatilia masimba. Hilo likamuweka kwenye utayari. Muda mfupi akamuona mwanamke yule akiingia pale, alikuwa katika mavazi ya aina yake. Sketi fupi ilioishia juu ya magoti kwa juu kabisa. Sketi ya kubana na kusababisha mistari ya chupi aliovaa kuonekana kwa uwazi zaidi. Wateja wote wakageuka kutizama kule alipokuwa akitokea mwanamke yule. Miluzi ikasikika na shangwe kutamalaki. Wakati mwanamke yule akiendelea kuwahenyesha wanaume na kuzivunja shingo zao, masimba ndio kwanza alikuwa akiwasili eneo la tukio, bastola mbili zikiwa kiunoni, akitembea kuelekea pale pale.

Kesho

[20:20, 10/03/2017] Ibrahim Masimba: NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 012

Wakati masimba akishuka eneo la Ngamia Pub, macho yake yalikuwa yakiangaza huku na kule kuangalia nani na nini walikuwa wakimtiza. Kila aliemuona alikuwa kwenye mambo yake, hakuna ambaye alikuwa akimtizama. Hilo halikumfanya ajiamini kabisa, bado akatembea akiangalia huku na huko. Hata pale macho yake yalipomuona mwanamke mrembo alieketi pembeni, bado masimba hakuvutika kumtizama. Macho yake yalikuwa yakitizama upande mwingine kabisa. Hakutazama huko kwa makusudi, bali alikuwa akimtizama mtu ambaye alikuwa akimfananisha. Alifanana kabisa na mpenzi wake, alifanana kabisa na teddy. Akahitaji kufanya kitu ambacho kingemuaminisha kwamba mtu yule alikuwa mpenzi wake. Kengele ya tahadhali ikagonga kichwani pale alipowaona watu watatu wengine wakimtizama. Tabasamu mubashara likachomoka usoni kwake, halikuwa tabasamu la kufurahi wala kuwavutia wasichana waliojazana pembeni. Hili lilikuwa tabasamu la kukubali kile ambacho alikiwaza. Kile ambacho alijua lazima kitendwe na yule mwanamke. Alitambua baada ya kuwasiliana na kumwambia sehemu ambayo wangekutana, ni lazima naye angeisambaza taarifa ile. Hilo aliliamini na hapa alikuwa akilithibitisha. Vichwa vitano vilivyokaa sehemu tofauti vilikuwa vikimtizama yeye. Vikimuangalia na hata kumshuti basi wangefanya hivyo. Akaendelea kusogea akimuangalia yule mtu anayefanana na mpenzi wake. Ni kweli alikuwa teddy, ni kweli alikuwa yeye! Kwa nini yeye? Kwa nini hapa muda huu? Yupo kwenye hili? Hilo likamshangaza tena na tena. Lakini kwakuwa alikuwa na watu wake eneo lile, alijua kila kitu kingewekwa wazi, ingawa hakupewa taarifa ya uwepo wa Teddy, hilo halikumsumbua kwa kuwa alimjua teddy. Aliutambua uwezo wake wakijasusi, alitambua uwezo wake wakujibadilisha. Hilo halikumfanya Awalaumu vijana wake.

Akaifikia meza ambayo ilikaa mwanamke yule. Hakusubiri kukaribishwa, bali alivuta kiti na kukaa.

"Bila shaka sikatazwi kukaa hapa!" Aliongea huku akimtupia mwanamke yule jicho. Bado akakutana na jicho lile lile la ulaghai, jicho ambalo bado liliendelea kumdanganya Masimba. Jicho la usingizi, jicho la kuvutia na hata kubadilisha mtazamo wa watoto wakiume.

Kabla hajajibu, akaliachia tabasamu, tabasamu ambalo liliendelea kuufanya uso wake ung'are na uzuri kuongezeka.

"Sio hapa tu, hata nyumbani, tena chumbani kabisa ungekaribishwa." Akajibu mwanamke yule akiendelea kutabasamu.

"Kumbe hata chumbani nakaribishwa, kwanini tumekuja hapa? Akauliza masimba huku macho yake yakiendelea kutembea usoni kwa mwanamke huyu. Kuna kitu alikuwa akikitafuta, lakini usoni kwa mwanamke huyu bado hapakuonekana kile ambacho alikuwa akikitafuta. Sura ya mwanamke huyu ilipambwa na uzuri wa haja, uzuri wa kuvutia na kuwavutia wengi.

"Nimekuita hapa ili tufahamiane, pia kuna mawili matatu nahitaji tuongee!" Baada ya maneno hayo, mwanamke yule akaonekana kuwa tofauti, safari hii hapakuwa na tabasamu wala mbwembwe. Uso wake ulikuwa uso wa kazi. Hilo likamfanya Masimba naye abadilike. Lakini ubadilikaji wake haukuwa ubadilikaji ule. Huu ulikuwa ubadilikaji wa kuiteka akili ya mwanamke yule. Wakatizamana kwa muda kila mmoja akitafuta kilichopo ndani ya mwenzake.

"Naitwa Mwamvita Rajabu, ni ndugu wa binti alieuawa juzi usiku. Nimekuja hapa jijini leo asubuhi kufuatilia kile ambacho kimesababisha kifo cha ndugu yangu." Aliongea mwanamke yule huku akiendelea kuivaa sura ya Huzuni. Licha ya sura hiyo lakini kwa Masimba bado sura ile haikuwa katika huzuni hiyo, bali ilikuwa katika huzuni ya kulazimishwa.

'"Wewe ni Polisi, afisa usalama ama? Na kwa nini umeniona mimi pekee ndiye wakuongea nawe? Sasa aliuliza masimba safari hii ikiwa makini kumuangalia mwanamke yule usoni. Bado sura yake iliendelea kuwa na huzuni, lakini kitu kingine mwanamke yule alikuwa kimya akionyesha kupatwa na huzuni zaidi. Kwa jasusi aina ya masimba hakuwa mgeni wa mbinu zile, hakuwa mgeni kwa kuwa alijua mwanamke yule hakuwa na jibu kwa wakati ule. Ukimya wake haukusababishwa na huzuni bali swali aliloulizwa halikuwa na majibu. Safari hii mwanamke yule akainua uso wake na kumwangalia masimba. Hata macho yao yalipokutana, safari hii Masimba alikiona kile ambacho alikuwa akikitafuta. Macho yao yalikuwa yakielezana kwamba wote ni watu katika fani moja. Wote walikuwa majasusi wa kiwango cha hali ya juu.

"Nadhani umenitambua sasa, nadhani ulichokuwa unakitafuta umekiona." Akaongea mwanamke yule akiendelea kumuangalia masimba.

Tabasamu likachanua usoni, tabasamu ambalo lilifuatiwa na kicheko. Hakikuwa kicheko cha furaha, hiki kilikuwa kicheko cha ushindi. Ni rahisi kumuua adui unayemjua kuliko usiemjua. Kitendo cha mwanamke huyu kuongea kile alichokuwa anakitafuta kikampa kuamini kwamba hata huyu ni mmoja wao.

"Yeah! Nimekiona na nimepata majibu. Lakini bado hujaniambia wewe ni nani? Na umeniita hapa kutaka nikujue ama kuniambia ulichoniitia? Safari hii masimba aliongea kwa ukali huku macho yako ya kibadilika.

"Hupaswi kujua masimba, hupaswi kunijua. Lakini nakuomba uachane na hili ulilolianzisha. Hutafika popote masimba." Safari hii aliongea akichezesha midomo.

"Bahati mbaya aliekuelekeza kwangu amekosea. Kamwambia mimi huwa sitishwi na wala siogopagi. Sitaacha na sitarajii kuacha, lakini nadhani leo kuna kitu umesikia. Basi ile ni kazi yangu mimi." Alijibu masimba kwa kejeli. Alishajua adui zake washakuwa waoga, wameshaanza kumhofia. MASIMBA akasimama na kuanza kuondoka eneo lile. Alimuacha mwanamke yule akijisonya, akitamani kumlipua.. lakini haikuwa amri kwa siku hiyo.
[16:28, 13/03/2017] Ibrahim Masimba: NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 013

Akamuangalia masimba alipokuwa akiondoka katika eneo lile, akatamani kuichomoa bastola yake ili ikiwezekana airuhusu risasi, lakini hakutaka kufanya hivyo kwa kuamini kuwa masimba hawezi kuwa pale peke yake. Akashuhudia akitembea na kupotelea katika upeo wake. Kuondoka kwa masimba kukampa nguvu ya kuamini kuwa masimba hakuwa mtu wa kutishwa. Aliamini hilo baada ya maneno yake. Akatamani kusimama kuwapa ishara watu wake ambao walikuwa katika maeneo tofauti. Lakini bado alisita akiamini kuna macho yapo mahali yakimtizama kwa kila alichokuwa akikitenda. Akajipa uvumilivu huku akishusha kinywaji kinywani. Masimba baada ya kuachana na mwanamke yule alitembea akitoka eneo la pub ile. Macho yake bado yalikuwa yakiangaza kuhakikisha kama kwelu mwanamke aliyekaa pembeni kabisa mwa Pub ile alikuwa Mpenzi wake. Lakini safari hii macho yake hayakumuona Teddy, hayakumuona mwanamke ambaye alidhani ni Mpenzi wake, bali yalimuona mtu mwingine, tena mwanamke harafu alikuwa amevaa mavazi kama yale yale aliokuwa amevaa Teddy. Hilo likampa tafsiri kwamba ulikuwa mchezo, ulikuwa mchezo ambao ulichezwa kwa kipindi kile. Ni kweli mwanzo alimuona Teddy, nikweli alikuwa na uhakika huo, lakini cha ajabu safari hii alikuwa akimuona mwanamke mwingine, mwenye sura nyingine, lakini alievaa mavazi yanayofanana na yale aliovaa Mpenzi wake. Lakini huyu hakuwa teddy! Mshangao kilikuwa kitu cha kwanza kutokea usoni kwake. Akaona ni wakati wakuondoka hapo kwa kuwa alikuwa akihitaji kwenda kuongea na Mama wa Marehemu Asteria, sambamba na dada yake. Akatoka akaelekea sehemu ambayo aliipaki gari yake. Alitembea macho yake yakiangalia kila kitu, hatua kadhaa kabla ya kufika kwenye maegesho ya magari akakiona kivuli, kivuli kuonyesha uwepo wa mtu karibu na alipoipaki gari yake. Kengele za hatari zikagonga kichwani kwake, hakujua kwa nini lakini alijikuta akiushusha mkono wake pale alipohifadhi bastola yake. Hakutaka kukiamini kile alichokiona. Akaendelea kutembea akikiangalia kile kivuli.. lakini kabla hajagundua chochote akausikia mlipuko mkubwa, mlipuko ambao ulisababisha hata yeye kutupwa pembeni kabisa na kuanguka mfano wa furushi. Gari yake na magari mengine yalikuwa yakiwaka moto kuonyesha kuwa alitegewa bomu kwenye gari yake. Eneo lote la mjimwema likawa katika taharuki, watu walikuwa wakikimbia huku na huko kila mmoja akipigania kuiokoa nafsi yake. Sehemu yote ikageuka vilio, iligeuka somalia kwa muda mfupi. Pale alipoangukia masimba ndio kwanza alikuwa akirudiwa na akili zake, alikuwa akifumbua macho huku akijaribu kuvuta kumbukumbu. Kumbukumbu ambayo haikuwezekana kurudi kutokana na mkanganyiko na vilio vya watu. Akatambaa na tumbo mpaka pembeni kidogo. Muda mfupi alikuwa akisimama huku akishuhudia gari yake ikiteketea, gari ambayo alipewa kama zawadi na mwanamke mmoja hivi baada ya kumfanyia kazi yake ipaswavyo.

Bado hakuamini kama amesalimika... akaituliza akili yake, alitaka kuirudisha kumbukumbu kabla ya mlipuko ule. Kivuli cha mtu kilikuwa kitu pekee alichokiona. Kivuli ambacho hakufanikiwa kumuona mhusika halisi wa kivuli kile. Kwa mara ya kwanza akashukuru. Ilikuwa ni lazima aondoke pale, ilikuwa ni lazima apotee hapo, akaipima nguvu katika mwili wake. Alipoiona inatosha akaanza kupiga hatua huku hisia kuwa teddy alikuwa mmoja kati ya wapangaji washambulie lile. Akatembea akijichanganya na watu waliokuwa wakipita katika eneo hilo wakikimbia. Naye alikuwa akikimbia sambamba nao, ni wakati akikimbia ndipo alipomuona tena Teddy akitokea upande ule ambao alikiona kivuli kabla ya mlipuko.. Hata yeye alikuwa akikimbia, hata yeye alionyesha kufadhaika, Alionyesha kutafuta kitu, hakuwa teddy yule kiburi, hakuwa teddy yule gaidi na mwenye usiri. Huyu alikuwa teddy aliechanganyikiwa. Hili likamvutia Masimba kulitizima. Lakini wakati hilo halijafika popote akaishuhudia gari ikisimama pale alipokuwa amesimama teddy. Gari iliposimama milango ikafunguliwa, teddy akaingia kisha gari kuwashwa. Kilikuwa kitendo kilichofanyika kwa sekunde mbili, kitendo ambacho kilimfanya masimba aduwae. Kitendo ambacho kilimpa picha na kumuaminisha kuwa teddy hakuwa Teddy yule walioanzana akiwa ndio kwanya yupo kwenye mafunzo ya awali ya kijeshi. Hakuwa Teddy Yule wa Ifakara, hakuwa Teddy yule mwenye kutangaza mapenzi ya kweli. Huyu sio teddy yule anayetoka Idara ya usalama wa Taifa, hakuwa teddy yule alietoka urusi katika mafunzo ya juu ya Ujasusi. Huyu alikuwa Teddy Muuaji, teddy msaliti. "NITAKUPATA TU" Ndio kauli pekee aliotamka wakati gari ile ikimpita kwa mwendo wa kasi.

*********

Palikuwa na ukimya wa ajabu, ukimya ambao kwa mbali ulikuwa ukiondolewa na mbwa waliokuwa wakibweka. Alikuwa hapo kwa minajili ya kuongea na dada wa marehemu Asteria. Alitembea kama kama kawaida akielekea mlangoni mwa nyumba ile. Muda wote macho yake yaliozoea giza yalikuwa yakiangaza huku na huko. Akaufikia mlango, akasimama kwa muda kisha akaanza kuangalia eneo lote, alipoona hakuna mtu wa kumtilia mashaka, akaugonda mlango kwa mara ya kwanza, hakujibiwa, kwa mara ya pili hapakuwa na majibu tena.. alipogonga kwa mara ya tatu, akasikia nyayo za mtu zikisogea pale mlangoni, wakati akiusubiri mlango ufunguliwe akashangaa kumuona mtoto mdogo akilia kwa ndani. Hilo hakulitarajia, mkono wake ukashuka na kuichomoa bastola.. kabla hajaingia mlango ukafunguliwa kisha sura ya mtoto mdogo wa miaka kumi alietapakaa damu mwili mzima akatokea. Masimba hakutaka kuuliza, akamuweka mtoto pembeni kisha kuingia ndani, sebuleni akapokelewa na damu iliosambaa kila sehemu, huku miili ya watu wawili ikiwa imelala ikionyesha haina uhai. Masimba akaisogelea miili iliokuwa imelala katikati ya damu. Godfrey Maboba akiwa na mkewe Irene Charles walikuwa wamelala katikati ya dimbwi la damu wakiwa maiti. Walikuwa wamepigwa risasi vifuani mwao. Masimba akainama kwa uangalifu, akawaangalia marehemu. Bado walikuwa wa moto kuonyesha hawakuawa muda mfupi uliopita. Wakati ameinama hapi akakisikia kitu mfano wa chafya, kitu ambacho kilitokea dirishani. Aliujua mlio ule, aliujua haukuwa mlio mwingine bali wa bastola. Masimba akawahi kuchupa huku akisahau uwepo wa mtoto wa marehemu. Wakati anatua nyuma ya kiti pale sebuleni, akajikuta akitua sambamba na mwili wa Mtoto Yule ukiwa hauna Uhai....

MASIMBA AKAISHIWA NGUVU
 
NITAKUPATA TU


SEHEMU YA 094
Masimba akifuatana na Mwanaharamu walikuwa wamepakiza mwili wa Veronika kwenye gari waliyokuja nayo huku wakihakikisha wamemfunga Teddy vizuri na kumuweka kwenye buti kisha wakaondoka eneo hilo nakuelekea maeneo ya nje ya jiji la Dar es salaam.
***********
Wakati Vero akielekea kwenda kwa mzee Raymond hakujua kuwa tayari Teddy alikuwa amenusa na kufahamu wapi walipokuwa watoto wa masimba, akiwa na lengo moja tu la kuhakikisha kuwa anamuua Masimba, ndipo alipopigiwa simu na makao makuu ya ujasusi kutoka nchi ya marekani,kumtaarifu kuhusu ni wapi walipo watoto wa Masimba na kuhusu Mzee Raymond na uhusika Wake na kundi hatari la Mafia duniani na uhusika wake katika kuhakikisha kuwa wanaiyaribu mipango yote ya Marekani na kuhakikisha inapatikana betri kwa kila hali.
Teddy alipopata taarifa zote ndipo alipo wai kwenda kwa Mzee Raymond na kumchoma Sindano ya sumu maeneo ya shingo na Mzee kufariki hapo hapo. Kisha kwakutumia uzoefu alio upata nchini Syria na mafunzo ya kijajusi aliyopata Kwa hisani ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania alifanikiwa kuwahamisha watoto na kuwapeleka kwenye nyumba kubwa iliyopo maeneo ya Masaki karibu na Double tree hotel kisha yeye kurudi na kumsubiri Masimba hakujua kuwa Veronika ndiye angetokea
***********
Gari iliendeshwa taratibu huku kila mmoja akiwa mwenye hudhuni akifikiria kuhusu kifo cha Veronika, "Mwanaharamu"Masimba alimwita na kumstua na kumtoa katika dimbwi la Mawazo, Angalia kwenye saiti mila, hamadi gari nne zilikuwa zikija Kwa kasi kuwafuata wakina Masimba, ikabidi Masimba akanyage mafuta na kuongeza mwendo... Itaendelea
 
NITAKUPATA TU


SEHEMU YA 094
Masimba akifuatana na Mwanaharamu walikuwa wamepakiza mwili wa Veronika kwenye gari waliyokuja nayo huku wakihakikisha wamemfunga Teddy vizuri na kumuweka kwenye buti kisha wakaondoka eneo hilo nakuelekea maeneo ya nje ya jiji la Dar es salaam.
***********
Wakati Vero akielekea kwenda kwa mzee Raymond hakujua kuwa tayari Teddy alikuwa amenusa na kufahamu wapi walipokuwa watoto wa masimba, akiwa na lengo moja tu la kuhakikisha kuwa anamuua Masimba, ndipo alipopigiwa simu na makao makuu ya ujasusi kutoka nchi ya marekani,kumtaarifu kuhusu ni wapi walipo watoto wa Masimba na kuhusu Mzee Raymond na uhusika Wake na kundi hatari la Mafia duniani na uhusika wake katika kuhakikisha kuwa wanaiyaribu mipango yote ya Marekani na kuhakikisha inapatikana betri kwa kila hali.
Teddy alipopata taarifa zote ndipo alipo wai kwenda kwa Mzee Raymond na kumchoma Sindano ya sumu maeneo ya shingo na Mzee kufariki hapo hapo. Kisha kwakutumia uzoefu alio upata nchini Syria na mafunzo ya kijajusi aliyopata Kwa hisani ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania alifanikiwa kuwahamisha watoto na kuwapeleka kwenye nyumba kubwa iliyopo maeneo ya Masaki karibu na Double tree hotel kisha yeye kurudi na kumsubiri Masimba hakujua kuwa Veronika ndiye angetokea
***********
Gari iliendeshwa taratibu huku kila mmoja akiwa mwenye hudhuni akifikiria kuhusu kifo cha Veronika, "Mwanaharamu"Masimba alimwita na kumstua na kumtoa katika dimbwi la Mawazo, Angalia kwenye saiti mila, hamadi gari nne zilikuwa zikija Kwa kasi kuwafuata wakina Masimba, ikabidi Masimba akanyage mafuta na kuongeza mwendo... Itaendelea
hongera mkuu.. ila pengo la Ibra naona halizibiki
 
KWA NIABA YA FAMILIA YA MZEE Masimba WA HANDENI MKOANI TANGA, TUNAPENDA KUTOA SHUKRANI ZETU ZA DHATI KWENU WAPENDWA WETU AMBAO MLIKUWA NASI KTK KIPINDI IKI KIGUMU CHA MAJONZI YA KUONDOKEWA NA MTOTO WETU MPENDWA MAREHEMU Ibrahim Haji Islam ( MASIMBA ) ALIE FARIKI JUZI TAR.4/07/2017 SAA MBILI UCKU KTK HOSPITAL YA TEMEKE DAR-ES-SALAAM,NA KUZIKWA LEO TAR.6/07/2017 VIBAONI HANDENI MKOANI TANGA,SHUKRANI ZETU ZA DHATI ZIWAFIKIE MADAKTARI NA MANESI WA HOSPITAL YA TEMEKE WALIO AKIKISHA WANAPIGANIA UHAI WA Ibrahim LAKINI KWA UWEZO WAKE MUNGU IKASHINDIKANA,PIA TUNA WASHUKURU WATU WOTE WA KIGAMBONI ALIPO KUWA ANA ISHI MAREHEMU KWA MSAADA WAO WA HALI NA MALI KUAKISHA TUNA MALIZA HILI SWALA ZITO KWETU,PIA TUNA WASHUKURU MARAFIKI WOTE AMBAO WALIO KUWA WANAISHI NA MAREHEMU KWA KUJITOLEA KWA NAMNA MOJA AU NYENGINE,ASWA SHUKRANI ZETU ZIWAFIKIE WALE WOTE WALIO TUSAIDIA KTK UPANDE WA HELA HILI TUFANI KISHE PALE PALIPO NA MAPUNGUFU YA PESA,NA PIA TUNA WASHUKURU WALE WALIO PIGA SIMU NA KUTUPA POLE PAMOJA KUTOA MAWAZO YAO,KWANI TUNA THAMINI MAWAZO YENU NA KUTAMBUA UMUHIMU WENU KWA MTOTO WETU MASIMBA, KWA UFUPI ATUWEZI KUTAJA MTU MMOJA MMOJA ZAIDI YA KUWASHUKURU WOTE,HILA JUMAMOSI TUTA MALIZA TATU NA KUPITISHA KISOMO MOJA KWA MOJA, TUNA RUDIA TENA ASANTENI SAANA KWANI TUMEJIFUNZA KUWA MTOTO WETU ALIKUWA NANYI VIZURI KTK MAISHA YENU YA KILA SIKU,NDIO MAANA ASILIMIA YA WATU WENGI MLIGUSWA NA KIFO CHAKE MPAKA WENGINE WALIFIKIA KUTOAMINI KAMA MASIMBA AMEFARIKI KWELI? HILA TUNA PENDA KUSEMA KAZI YA MUNGU AINA MAKOSA,KIKUBWA NI KUMUOMBEA DUA HILI APUMZIKE KWA AMANI, ASANTENI SANA NA ATUNA CHA KUWALIPA HILA MUNGU NDIO ATAKAO WALIPA HAPA DUNIANI MPAKA HAELA.....by haji mvula
 
Mwenyezi mpumzishe kwa Amani mja wako na umsamehe dhambi zake,
Hakika kifo cha IBRA kimetugusa wengi na tunashindwa jinsi YA kuisapoti hata familia ya marehemu,
 
Nashauri km itawezekana kwa wale tuliokuwa tuna soma riwaya zake kuchangishana ili kuwasaidia hata wanae iwe mchango wetu kwake
Busara tupu hapa umeandika juzi kati niliandika kuhusu jambo hili kiasi kuonyesha thlimthamini akiwa hai na pia tunamuenzi japo kwa pesa kidogo ni jambo jema.
 
Nashauri km itawezekana kwa wale tuliokuwa tuna soma riwaya zake kuchangishana ili kuwasaidia hata wanae iwe mchango wetu kwake
ni jambo jema. nashauri liratibiwe vizuri kuepuka yale ya wala rambirambi wa Arusha
 
[06-08, 14:36] Ibrahim Masimba: NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 078

Alikuwa akitizamana na kiongozi mkuu wa nchi. Alikuwa akitizamana naye katika namna ya kumsoma. Katika namna ya kumuangalia kwa umakini. Alikuwa tayari kufanya chochote pasipo kuhofia kitu. Rais alikuwa akimuangalia Masimba pasipo kupepesa jicho lake pembeni. Alikuwa na nia ya kumtia hofu, alikuwa na shida ya kumfanya masimba amuigope. Lakini hakumjua huyu masimba alikuwa nani, hakujua masimba alikuwa mtu wa kutokuogopa kitu. Muda ukazidi kuyoyoma huku wakitizamana. Bado Rais hakufumbua kinywa chake kuongea kile alichotaka kukiongea. Hata masimba naye aliiweka heshima mbele, nidhamu ya uzalendo na hata heshima ya kikazi. Akazidi kukaa kimya akisubiri kuambiwa kile alichoitiwa. "Nauomba ule mzigo mliouchukua nyumbani kwa Askofu Rengima. Nitakupa kiasi chochote cha pesa uitakayo." Kwa mara ya kwanza kiongozi wa nchi alizungumza. Maneno yake yakamfanya Masimba ainue macho yake na kumtizama Rais. Alimuangalia kwa umakini huku akilazimisha Rais amuangalie na kumsoma kupitia Macho yake. "Sikuwahi kufika nyumbani kwa Askofu na wala sijawahi kuonana naye, na kwahivyo hakuna mzigo niliopewa na Mtu huyo Mheshimiwa Rais." Akajibu Masimba akiendelea kumtizama Rais usoni mwake. Jibu lake likaonyesha kumfanya rais kuukunja uso wake. Licha ya muda mfupi kuukunjua lakini tayari masimba alikuwa amehisi kitu. Kitu ambacho alipanga kutoondoka ikulu mpaka akijue. "Masimba Mwanangu hii ni fursa ya kutengeneza maisha yako. Hili suala unaloendelea nalo halitafika popote. Bora upewe pesa yako uishi vizuri na familia yako. Na uachane na hili. Nakueleza haya kwa kuwa Nakupenda na Tanzania Haitaki kukupoteza. Hembu fikiria hilo kwanza. Aliongea mheshimiwa safari hii akiongea kwa upole sana. Jibu hilo lilionyesha kumkera Masimba, jibu hilo lilimfanya Masimba amtizame kwanza Rais. "Unajua hili suala limepoteza watu wangapi? Unajua hili suala limeharibu maisha ya vijana wangapi? Leo hii unapata wapi nguvu ya kulisema hili? Mama yangu amelala Kaburini kwa sababu ya suala hili, leo unaniambia hilo? Kama unaweza kuwarudisha wote waliokufa kwa suala hili nitakubaliana na wewe. Otherwise risasi yangu itamuua kila mmoja hata kama ni wewe." Akajibu Masimba akiendelea kumuangalia Rais pasipo hofu yoyote. Macho yake yalikuwa yakisomeka vingine Kabisa. Jibu la Masimba likaonyesha kumtingisha Rais, kitendo cha kusema atamuua hata yeye kilikuwa kitu kibaya sana kwake. Akamuangalia Masimba kwa muda mrefu sana bila kuongea chochote. "Unadhani ni kitu Rahisi hicho unachokisema? Unadhani nikiamua unaweza kutoka hapa? Akauliza Rais naye akionyesha kuhamanika. "Kama nimeweza kutoka Ikulu ya Rais Vladimir Putin Wa Russia basi hapa hakuna ambacho kitanisumbua. Na ungekuwa na uwezo wa kunifuta basi usingeniita hapa. Umeniita hapa kwa kuwa unajua na kutambua kuwa mimi ni nani. Kwa ajili ya Tanzania Nipo Tayari Uniue ama kunipoteza." Alijibu Masimba akimaanisha kile ambacho anakitoa moyoni. "Usijidanganye Masimba kumbuka Nchi ndio imekusomesha mpaka kufika hapo ulipo. Kumbuka Gharama ya kukusomesha wewe ingeweza kutengeneza maisha kwa watu wengine. Tambua hilo kijana. Pia kukuita hapa sikukuogopa bali tunakupenda. Tukikutaka Hutusumbui kabisa." Akajibu Rais.

"Kwahiyo kama Umenisomesha ndio unitumie katika kuwaua wa Tanzania wenzangu? Ndio unitumie kufanikisha Madhambi yako? Ndio unitumie kukubali nje yangu iharibiwe? Nimeapa kuwa mzalendo kwa Tanzania. Ukiona Hii kazi ndio inakufanya uniambie hayo basi kuanzia leo Mimi sio Mwana Usalama katika nchi hii. Aliongea Masimba huku akichomoa kitambulisho chake na kukiweka juu ya meza. Ni muda ule ule mlango ukafunguliwa na wana usalama. Kila mmoja alikuwa Tayari kwa chochote. Lakini tofauti na walivyotegemea, wakakutana na Tabasamu la Masimba. Tabasamu lililokificha kitu moyoni mwake. Muda ule ule akainuka, aliamua kuinuka kuelekea nje ya chumba kile akikiacha kitambulisho juu ya meza. Kilikuwa kitendo ambacho hakikutegemewa na Rais. Bado alikuwa katika mzubao wa kutoamini. Kutoamini kule kunakofanywa na kijana huyu. Akatamani aamuru akamatwe lakini moyo wake uliijenga hofu. Hofu ambayo hata yeye hakuijua. Akamsindikiza Masimba kwa macho, akamsindikiza alivyokuwa akitembea. "Ni mtoto sana huyu hawezi kunishinda." Alijisemea akikiangalia kile kitambulisho. Kitanburisho ambacho kiliachwa Juu ya meza. Maafisa wa ikulu sambamba na wakuu wa idara zote za usalama waliokuwa wamekaa sehemu ya siri wakilitizama tukio lile kila mmoja alitoka baada ya kumuona masimba akitoka huku kitambulisho chake akikiacha mikononi mwa kiongozi wa Nchi.
[06-08, 14:36] Ibrahim Masimba: Alitoka akiwa ni mwenye Hasira. Aliamua kuiacha kazi aliyoipenda. Kazi aliyoitendea haki tokea mwanzo kabisa wa maisha yake. Hakuuona umuhimu wa kuendelea kuwa katika Idara hiyo. Idara inayosahau misingi ya kuanzishwa kwake. Idara ambayo imekuwa ikishiriki siasa za nchi hii. Mama yake, dee plus, vicky na watu wengine ni Roho ambazo zimeondolewa kwa sababu ya hili linaloendelea. Kwa nini Rais ameamua kulikingia kifua hili suala. Ni nani ambaye yupo nyuma mpaka kusababisha msimamo huu dhaifu kwa kiongozi huyu wa nchi. Akaamua Rasmi kuiacha kazi yake. Kazi hii ambayo ilikuwa ni hatari katika maisha yake. Akairuhusu miguu yake itembee katika namna ya kuliwahi lolote lile. Hakujali taharuki aliyoiacha huko ndani. Hakuwa tena mwana usalama, hakuwa tena Yule Masimba Tegemezi katika nchi hii na Idara ambayo aliitumikia na kunusurika kuuawa katika mission mbalimbali alizotumwa kuipigania nchi. Akalifikia geti kubwa la kutokae nje. Alikuwa akitembea kana kwamba hakuna chochote ambacho kimetokea. Hata macho ya watu waliokuwa wakimtizama kwa hila, hakujali na hata kuwafuatilia. Akatembea na kutembea akikipita Chuo cha Usimamizi wa Fedha Ifm. Hatua kumi mbele alikuwa akifika makao makuu ya Jeshi la magereza. Akili yake bado haikuwa imetulia. Akili yake bado ilikuwa akifikiria Sauti na kauli za rais wa Nchi. Kuna wakati alikuwa akijisonya na hata kuongea peke yake. Aliipenda Tanzania kwa Moyo wake Wote. Kuiwaza Tanzania kukafanya akili yake imkumbuke Teddy wake. Teddy ambaye alimuacha katika Gesti waliolala usiku uliopita. Teddy ambaye alimuacha hapo kituuoni akiduwaa na kushangaa. Hapo akauona Ulazima wa kumtafuta. Ulazima wa kumuona mtu huyu, mtu ambaye alikuwa ni Muhimu kwake. Wakati akifikiria kuichomoa simu yake ili amtafute Teddy, macho yake yakamuona mtu ambaye uliyafanya mapigo yake ya Moyo kwenda kasi. Umbali wa hatua hamsini kutoka alipo akamuona Jimmy. Jimmy Lambert yule ambaye alikuwa akimtafuta kwa Udi na Uvumba. Hicho nikitu ambacho kilimshangaza, kilimshangaza kwa hiki ambacho alikuwa akikiona mbele yake. Jimmy aliyekuwa amemtafuta kwa muda mrefu bila kumuona, leo alikuwa hatua hamsini mbele yake. Akatabasamu akicheka kimoyo moyo. Kisha akajiuliza. Inakuwaje Jimmy ajitokeze Muda mfupi baada ya yeye kuiacha kazi Hii? Hilo likamfanya acheke kwa mara ya pili. Akaiona vita ambayo imeanza kupiganwa na taasisi kubwa nchini. Alitambua kutokea kwa Jimmy mbele yake ulikuwa ni mpango uliosukwa. Ulikuwa ni mtego ambao alitegewa ili umnase. Hilo aliligundua mapema. Hivyo akaamua kumpita Jimmy pasipokumuangalia. Pasipokuonyesha kama amemuona. Akatembea mbele zaidi mpaka lilipo jengo la Freemason. Akatulia hapo kwa muda akitizama viatu kutoka kwa wachuuzi waliokuwa wakiuza. Hakuwa na Shida ya viatu, lakini alikuwa hapo kwa kuwa alitaka kujua kama Alikuwa akifuatiliwa au la!. Wakati ameinama hapo akawaona wadada watatu nao wakisogea hapo. Hawa walikuwa wadada warembo kuwahi kutokea machoni Mwake. Walikuwa wazuri hasa. Kila mmoja alikuwa na mkoba mkononi kuonyesha kuwa Alikuwa Nwanafunzi katika chuo cha Usimamizi wa fedha, ama mfanyakazi wa Benki Kuu ya Tanzania. Utembeaji wa wasichana hawa ukampa hamu ya kusimama vizuri, akageuka na kutizama nyuma. Cha kushangaza akapokewa na matabasamu Kutoka kwa watoto hawa. Kengele za Hatari zikalia kichwani mwake. Ni kengele hizo zilizomuamsha na kumuweka kwenye majibu kuwa Alikuwa anaandamwa tokea alipoondoka pale Ikulu. Alijua kuwa alikuwa anatafutiwa sababu ya kufutwa hapa Duniani. Akajiapiza kuwa mtulivu katika kipindi hiki. Utulivu ambao haukutakiwa kufanya chochote kile. Akawangalia Wasichana wale kwa muda mfupi kisha akaamua kuondoka Zake.

******

Kwani Masimba ni nani? Kwani Masimba anafaida gani kwangu? Kwani nikiipeleka hii Bahasha kwa mheshimiwa Rais na nikapewa kile Rais alichoniahidi atanionea wapi? Yalikuwa maswali kutoka kwa Teddy akijiuliza mwenyewe baada ya kuachwa katika nyumba moja ya Siri. Roho ya usaliti na tamaa ya pesa vilishamuingia. Sasa alikuwa akitamani tena kumsaliti, alikuwa akiitamani sana Pesa. Taarifa aliyopewa muda mfupi kuwa Masimba amekataa kutaja kiasi chochote cha pesa anachotaka kilimsikitisha sana. Aliitamani pesa na kuipenda sana. Pesa kwake ilikuwa na thamani kuliko penzi na hata utu wa Masimba. Hakujua masimba alikuwa akihangaika kwa sababu ya Tanzania. Hakujua Masimba aliwapoteza Ndugu zake sababu ya Kazi hii. Kwa mara ya kwanza akatamani sana kutoka ndani ya jengo lile la siri. Kwa kuwa bahasha alikuwa nayo ndani ya nguo zake akaona kuondoka hapo ndio ingekuwa njia Bora. Kile kilio na kiapo cha muda mfupi kilianza kuyeyuka taratibu. Hapakuwa na kiapo wala kilio tena. Tamaa ya pesa tayari ilimchukua Teddy. Muda mfupi alikuwa akiinuka pale akiyatoa mavazi yake na moja kwa Moja akielekea bafuni. Alikuwa kwenye mkakati wa kuianza safari ya kuondoka katika Jumba hilo. Muda mfupi baadae akatoka chumbani akiwa kama Alivyozaliwa. Akauendea mlango kisha kubonyeza kengele ya hapo mlangoni. Punde mlinzi wa Jumba lile akafika na kuufungua Mlango. Macho yakamtoka baada kukutana na tukio la Teddy kuwa uchi kama Alivyozaliwa. Mlinzi akaupoteza umakini huku akilishangaa umbo la mtoto huyu. Teddy alikuwa akikipenda kitu hicho sana, akaanza kupiga Hatua kumfuata mlinzi yule aliyekuwa ameduwaa. Hatua ya kwanza, hatua ya pili na hata ya tatu, zikamkuta mlinzi yule akiwa chini akivuja Damu. Baada ya kuhakikisha mlinzi amepoteza uhai, teddy akamvuta kwa ndani, kisha kumpapasa na kuchukua vitu mbalimbali. Baada ya Hapo akayaendea mavazi yake, akavaaa kisha akaondoka Hapo Ndani Bastola Ikiwa Mkononi. Wakati anaukaribia mlango walioingilia,akauona Mlango ukifunguliwa kisha mwanaume wa makamu Akaingia hapo. Macho yake yalipotua Usoni kwa Teddy akagundua Teddy alikuwa Amesaliti na kutaka kutoroka na bahasha ile. Meja Jenerali Louis Chomboko akaupeleka mkono wake sehemu alipoihifadhi Bastola yake. Lakini mkono wake Haukufika popote. Risasi Mbili zikatua kifuani kwake na kumtupa chini. Teddy alikuwa ameamua kuasi tena. Baada ya Mzee Chomboko kupigwa Risasi na kuanguka chini, Teddy akatoka mle ndani na kuanza kusimamisha magari. Wakati Teddy akisimamisha Magari tayari kwa kuondoka, Masimba ndio alikuwa Akifika hapo tayari kwa kuonana na Meja Jenerali Chomboko.
Hatareeee sanaaaa nzuriii
 
Nilianza kuisoma hii riwaya wiki hii nikijua itafika mwisho kumbe mwandishi wetu kipenzi anatutoka hivi hivi so sad IMENIUMA SANA! Ulazwe mahali pema peponi Ibrahim Masimba sisi tupo nyuma yako.
 
daaaaaa!!!!,inauma saaana aseee, Mungu mpunzishe kwa amani ndugu yetu
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom