NITAKUPATA TU
SEHEMU YA 008
Usiogope nakupenda sana mpenzi. Ilikuwa sauti ya masimba, sauti ambayo ilitokea nyuma yake.hakuwa amejiandaa na hilo, hakuwa amelitegemea lile la masimba kuwepo pale ndani. Hili likamnyong'onyeza. Akatamani kuongea kitu lakini maneno hayakutoka. Hakujua muda ambao masimba alifika nyumbani, hakutegemea uwepo wake hapo, na hata pale alipokumbuka kitendo alichokifanya, alichoka kwa kuwa alitambua kuwa masimba alikuwa amekishuhudia kitendo kile. Akaiona akili yake ikishindwa kumsaidia katika kulitatua hili ambalo lilikuwa mwisho wake. Hata pale mikono ya masimba ilipokuwa akipapasa kiuno chake, bado Teddy hakuweza kumjibu. Bado bastola yake ilikuwa mkononi, bado hasira zilionekana usoni, na hata dhamira ya mauaji ilijengeka kupitia macho yake. Hakuweza tena kumuangalia masimba, hakuweza tena kuuinua uso wake kumtizama. Alitazama pembeni na alikuwa ameinamia chini. Mwili ulikuwa unatetemeka, alijikuta kwenye wakati mgumu kupambana na moyo wake. Moyo uliojaa mapenZi juu ya masimba, moyo ambao haukuwahi kumpenda mwingine zaidi ya huyu mwanaume. Mwanaume ambaye alichukua asilimia mia moja katika moyo wake? Ni vipi ataweza kuitumia bastola kumlenga huyu mwanaume? Ni vipi angeweza kukiruhusu kidole chake kutekenya kitufe kuruhusu risasi imuue Masimba? Ni vipi pale atakapoiona Risasi ikimtupa masimba chini huku damu zikisambaa? Hapo akauona ugumu, ugumu wa kufanya kile ambacho alitaka kukifanya, lakini vilevile aliyafikiria mabilioni ya shilingi. Kwa mara nyingine akakiona kichwa chake kikitaka kupasuka. Lakini mpapaso wa mikono ya masimba ukamfanya teddy aachie mguno. Mpapaso ambao ulipanda mpaka kwenye kifua chake kilichobeba viazi vidogo. Mikono hiyo ikatulia hapo kwa muda ikitomasa na kuchezea kwa ustadi mkubwa. Hilo likaanza kumlegeza teddy, likamuacha teddy akisinzia na kulegea. Masimba akamgeuza na kufanya wote watazamane. Watazamane katika namna ya kuhitajiana. Jicho lilikuwa usingizini na hata midomo ikawa tayari kupokea zawadi. Wakatizamana zaidi, muda huu nguo zilikuwa zikitupwa chini baada ya kuvuliwa. Bastola ilianguka pasipo hata teddy kugundua. Alikuwa akihema kama mwizi, alikuwa akihema kama ametoka kukimbia mbio ndefu. Hakuwa teddy yule aliekuwa ameapa kumpoteza masimba. Hakuwa teddy yule mwenye uwezo wa kunyoosha mkono kumuua masimba. Huyu alikuwa kondoo, kondoo anayetii mamlaka ya bwana. Akasogezwa kitandani, hata yeye mwenyewe akasogea, akakalishwa kitandani, hata mwenyewe akakaa, na hata kulala, akalala huku macho yake yakiwa yamefumbwa na kufumbika. Midomo bado ilihitaji kupokea kitu, kitu ambacho kingeianzisha safari nyingine. Ilikuwa hivyo.
*****
Alishtuliwa na mlio wa simu yake, akaupeleka mkono pembeni yake ambapo alikuwa amelala masimba. Lakini akashangaa kutokuwepo kwake. Bado simu yake iliita, lakini aliendelea kuipuuza. Sasa alikuwa akiinuka kutoka pale kitandani na kuelekea kule sebuleni. Akalifunua pazia akidhani atakutana na masimba hapo, lakini hapakuwa na mtu. Hilo likamshangaza tena na tena. Haikuwa kawaida ya masimba kumuacha kitandani. Wakati akiendelea kuumizwa na hilo bado simu chumbani iliendelea kuita. Safari hii mpigaji alikuwa akipiga kwa mara ya tatu. Akakata shauri kurudi chumbani kwenda kuipokea simu hiyo. Akazivuta hatua zake taratibu akiwa mtupu kama alivyozaliwa.akasogea na kuingia chumbani huku mawazo yakiwa ni wapi alipoelekea masimba. Akaifikia simu na kuichukua, macho yakatua juu ya kioo.. akakutana na jina la mtu alieufanya moyo wake upige kwa haraka. Jimmy Lambert ndiye aliekuwa akiipiga simu. Akakipeleka kidole chake na kupokea simu.
"Jimmy." Aliita tedy kwa sauti ndogo yenye kuonyesha uchovu.
"Vipi umelala au?" Lilikuwa swali kutoka kwa Jimmy.
"Yeah! Nilikuwa nimelala, kuna lolote? Alijibu kisha kuuliza.
"Naomba Uje Tegeta muda mfupi ujao, kuna mtu nataka mkutane, mfahamiane na mtambuane. Tumeona tukutafutie mtu wa kusaidiana naye." Alijibu Jimmy kisha akakata simu bila kusubiri jibu kutoka kwa Teddy. Hilo la kutafutwa kwa mtu likaupa mashaka moyo wake. Ni kweli pesa alizitaka na kuzihitaji. Ni kweli anampenda masimba kuliko maelezo. Lakini hata kama atamuua masimba, wapo wanaume wengine ambao watamuoa. Kinachotakiwa ni kupanga njia ipi sahihi ya kumuua. Kwa mara nyingine roho yake, akili yake ilikuwa tayari tena kumuua masimba. Alikuwa amedhamilia na alikuwa ameamua kumpoteza. Alichokifanya ni kujiandaa kwa safari ya kuelekea huko tegeta huku akiwa na nguvu na maamuzi sahihi.
Wakati yeye akitoka na kulifunga geti, masimba alikuwa nyumba ya tatu kutoka pale. Alikuwa amesimama hapo kwa muda mrefu akitizama kila kitu ambacho kiliendelea pale. Muda mfupi akamuona mpenzi wake akilifunga geti na baada ya hapo akamuona akiondoka pale kwa kutembea kwa miguu. Bado alitulia akiendelea kuangalia kila kitu ambacho kilikuwa kikitendeka pale. Bado mpenzi wake aliendelea kutembea akielekea kituo cha daladala. Hilo pia lilimpa nafasi ya kumfuatilia pasipokuonekana. Simu ilikuwa sikioni akiwasiliana na vijana wake, alikuwa akiwaeleza kila kitu cha kufanya. Aliwaaachia wao kazi ya kumfuatilia Teddy. Alichokuwa akipokea ni maelezo ya nini kinaendelea katika hilo.
******
Teddy alitembea mpaka kituo cha daladala, alipofika hapo akatulia akiangaza macho yake huku na huko. Alikuwa ametulia kwa muda akitizama kila mienendo ya watu. Alikuwa na hisia za kufuatiliwa, lakini kila alipopitisha macho yake sehemu zote, hakuweza kumuona mtu ambaye labda angepata mashaka naye. Baada ya kuhakikisha hilo, akaingia kwenye daladala na muda mfupi gari likaondoka likielekea Tegeta. Ilikuwa safari ambayo kwake ilikuwa muhimu sana. Walikuwa na mzigo wa mamilioni ya shilingi lakini bado haikuwezekana kuuza kutokana na matukio haya yanayoendelea kutokea hakuwa tayari kuiacha pesa ile kwa sababu ya mwanaume. Moyoni alijisemea kwamba labda angekuwa mama yake ndipo angefanya hivyo. Wakati akiwaza hakujua kwamba kuna watu walikuwa siti ya nyuma yake wakimtizama. Walikuwa vijana wawili wadogo kiumri, vijana ambao kwa kuwaona ungedhani labda ni wanafunzi wa sekondary. Lakini haikuwa hivyo, hawa walikuwa vijana kutoka kitengo nyeti katika nchi hii. Walikuwa wakiendelea kuzungumza hili na lile, huku mara moja moja wakimtupia jicho mwanadada huyu. Kilikuwa kitu kizuri sana kumfuatilia mtu ambaye hajui kuwa anafuatiliwa. Gari ilipofika tegeta kwa ndevu vijana wale wakasimama tayari kwa kushuka. Hata teddy naye alikuwa akishuka hapo. Alitangulia yeye kushuka, kisha wakafuatia wao kushuka. Baada yakushuka vijana wale wakangoza kuelekea barabara fulani. Hata teddy alikuwa nyuma yao akifuata barabara ile. Hakujua kuwa waliombele yake hawakuwa mabishoo kama alivyodhania, bali walikuwa makachero wakifuatilia kila hatua yake na kila kitu anachokifanya.
ITAENDELEA