Riwaya: Nitakupata tu

Riwaya: Nitakupata tu

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 074

Ilikuwa hivyo na ikawa hivyo. Ndimi zao zikakutana huku chini ya sakafu damu ikichuruzika. Harufu ya damu ilikuwa imetawala eneo hilo, harufu ambayo waliipenda na hata kuwavutia. Hawakuogopa damu wala hawakuziogopa maiti. Bado walikumbatiana wakiburudika na kuburudika. Lakini haikuchukua muda wakaachiana. Walikumbuka kuwa wapo kazini. Wapo katika kazi hii ya kifo. Kazi ambayo ilikuwa ikitembea na vifo vyao mikononi. Naam! Huu ulikuwa muda wa kumfuata mtu huyu, muda wa kumfuata mtu yule ambaye muda mfupi uliopitwa alikuwa akishurutishwa aujue na kuusema ukweli. Nilazima wajue kwa nini Askofu alimtaka Teddy afike pale. Ilikuwa ni lazima wamjue na kutambua hilo. Kila mmoja akapiga hatua kuelekea chumba kile, chumba ambacho sauti ya mtu ulikuwa akisikika. Kuingia hapo wakapokelewa na Dimbwi la damu. Juu yake alikuwa amelala mtu, alilala mtu ambaye kwa kumuangalia tu, ungejua huyu atakuwa ni marehemu. Hatua za umakini zikafuatia, hatua za kuelekea ulipolala mwili. Wakaufikia mwili wa mtu yule ambaye alikuwa uchi wa mnyama. Wakatizamana tena huku kila mmoja akiwa makini. Huku kila mmoja akiwa tayari kwa kuifyatua Risasi. Wakaugeuza mwili wa mtu huyu waweze kuufahamu. Wakafanikiwa kuugeuza, kila mmoja macho yakamtoka baada ya kuiona sura ya huyu Marehemu. Hakuna aliyekiamini kile alichokuwa akikiangalia. Macho yao yalikuwa yakitizama sura ya Sheikh mkuu wa mkoa. Hata huyu kisu kikubwa kilikuwa kimesimama tumboni. Kila mmoja akainua macho. Wakaangaliana kwa muda. Baba Askofu, na sasa alikuwa ameuawa Sheikh Mkuu Wa Mkoa. Kuna nini hapa? Ni swali ambalo lilipenya kichwani kwa Teddy. Swali ambalo lilimfanya amuangalie Masimba kwa Mara nyingine. Akimuangalia akihitaji kupata majibu. Majibu ya kile ambacho kimejificha nyuma ya Vifo vya watu hawa. Alitaka kujua kwa nini aliagizwa na Masimba kwenda kumuondoa mtu nyumbani pale kwa Baba Askofu. Hata Masimba akamuangalia kwa Umakini. "Haya ndiyo malipo ya Tamaa. Kilichofanyika kwa watu hawa ni kuzibwa midomo yao ili wasikutane nasi." Aliongea Masimba akiwa bado anamuangalia yule marehemu. Jibu la masimba lilionekana kumshangaza Teddy. Lilimshangaza kwa kuwa hakuwahi kuwaona watu hawa katika biashara kipindi yupo huku. Sasa hii tamaa anayosema Masimba ni Ipi? Lilikuwa swali lililofanya amtizame tena Masimba. "Najua hujawahi kuwaona watu hawa ndio maana unashangaa, lakini Mengi utayaona kwenye Hiyo bahasha uliopewa. Tunatakiwa kuondoka hapa. Huu mchezo nadhani kuna mtu ndani ya Ikulu anaucheza. Lazima tuwe makini na lazima Tuondoke hapa. Aliongea Masimba huku akiuvuta mkono wa Teddy ili kuondoka hapo. Teddy akafuata kama kondoo. Akili yake ilikuwa imesimama kwa muda kutokana na maneno haya kutoka kwa Masimba, maneno kwamba watu hawa ni wa moja katika biashara hii. Kwamba watu hawa nao walikuwa kundi moja na Jimmy na hata Waziri? Kwamba Baba Askofu alikuwa Mmoja wa wana kikundi? Kwamba Sheikh Mkuu wa mkoa alikuwa ni mmoja katika hili? Akaitamani ndoto. Ndoto ya kumtoa katika hili. Aliiona Dunia Jinsi ilivyokuwa ikiwapoteza watu. Akiwaaangamiza katika Matendo mabaya. Kwa mara nyingine akataka kumuuliza Masimba. Kumuuliza kuhusu ukweli huu. Kuhusu hili linalotokea. Lakini macho ya Masimba yakauziba mdomo wake. Macho ya Masimba yalikuwa yakimzindua kutoka katika hili. Kutoka katika lindi la mawazo alionayo. Alitakiwa katika utimamu wa kimwili na hata kiakili. Alitakiwa katika umakini wake wa siku zote. " Alitakiwa kurudi kuwa Teddy kama Teddy. Ilikuwa hivyo na akawa hivyo.

********
Walikuwa wawili ndani ya chumba kimoja, walikuwa wamejiinamia kila mmoja akiwaza kile ambacho kiliutawala ubongo wake kwa wakati huo. Wakati Teddy akiwaza mkanganyiko na mambo yanavyozidi kumshangaza. Masimba alikuwa akiwaza kile kilichopo ndani ya Ile Bahasha. Bahasha ambayo Teddy alipewa na Askofu Ibrahim Lexandre Rengima. Ingawa hakuwa ameifungua kwa kipindi kile lakini aliuhisi usiri mzito kuwepo ndani ya bahasha hili. Kama sheikh mkuu wa mkoa na Baba askofu walikuwa washiriki katika biashara ile, alihisi kuwepo kwa watu wengine wazito kupindukia. Kuiona Gari yenye nembo ya Ikulu sehemu zote mbeli, kisha kuwakuta wahusika wameuawa hii ilitoa picha kuwa hata ndani ya Ikulu kuna watu ambao wapo nyuma ya Biashara hii. Kitendo cha Idara ya Ujasusi kubadilika na kutotaka kuwaunga mkono katika hili ilimaanisha kwamba kuna kitu kizito ambacho hatakiweza Peke yake. Alitambua wanaweza kuuawa muda wowote na kushindwa kuimaliza kazi hii. Kama ikulu inatumika katika hili hii ilionyesha kuwa ilikuwa Hatari kubwa sana kwa upande wao. Hilo likamfanya amkumbuke rafiki yake, Rafiki ambaye walikuwa wote katika purukushani za kuchunguza kifo cha mke wa Rais. Mkasa ambao hautakaa usahaurike maishani kwake hasa baada ya kuigundua njama ya kutaka kumpindua Rais alieko madarakani kwa Wakati. Alikuwa amemkumbuka mwanaharamu, alikuwa amemkumbuka Nemisis The Bastard. Mwanausalama mwenzake Raia Wa Africa ya Kusini. Alimkumbuka katika aina fulani ya kuuhitaji msaada zaidi. Msaada wa kiuchunguzi na hata kuwasafirisha watu kuzimu. Hilo akalipitisha kichwani kwake. Lakini kabla hajamwambia alitaka kukijua kile ambacho kilikuwemo ndani ya Bahasha kutoka kwa baba Askofu. Kwa mara ya kwanza Masimba akainua uso wake, macho yake yakamtizama mwandani wake aliyekuwa pembeni yake akionekana kusafiri umbali mrefu kimawazo. Hakuwa hapo na hakuonekana kuwepo Hapo. Teddy alikuwa amesafiri umbali mrefu kimawazo. Akamsogelea na kumkumbatia kwa mapenzi yote. Kwa upendo wote na hata mahaba yote. Taratibu macho yao yakatizamana. Yakaangaliana na kuangsliana. Macho ya Teddy yaliijenga hofu, macho ya Teddy yalionyesha kuhofu kitu. Hilo lilikuwa jipya moyoni kwa masimba na Hata machoni. Teddy alikuwa akiogopa na Teddy alikuwa akihofia. Teddy alikuwa katika hofu, mduao na hata Bumbuwazi. Teddy anaogopa? Teddy ana hofu? Ameianza lini hii? Akajiswali mwenyewe pasipo majibu ya aina yoyote. "Teddy umeanza kuogopa? Umeanza lini kuwa muoga?. Aliuliza Masimba huku akimuangalia kwa umakini. Teddy hakujibu bali aliinua macho zaidi na kumuangalia masimba. Midomo yake ilikuwa ikicheza kutaka kuongea kitu lakini haikuwa hivyo. Hakuongea wala hakufumbua mdomo. Hata hili lilimshangaza Masimba, hata hili hakulitegemea. Teddy kushindwa kuongea? Hapana hawezi kuwa Teddy. Alijisemea mwenyewe huku akimtizama Zaidi. "Dady Nahisi Ikulu inahusika katika mapambano haya. Nahisi kuna kitu ikulu ama watu wanaoishi ikulu wapo nyuma ya hii biashara. Na kama ni kweli huioni hatari mbele yetu? Nadhani umeiona gari yenye nembo ya ikulu ikielekea pale nyumbani kwa Sheikh mkuu, na pia nadhani umewaona wana usalama ambao walikuwepo eneo lile tena kwa siri kubwa sana. Hii inaonyesha nini kwetu?" Aliongea Teddy huku akishindwa kuificha hofu. Hofu ambayo ilichukua nafasi kubwa usoni. "Ni kweli nimeona kila kitu, na hata hii gari yenye nembo ya Ikulu ulipishana nayo kidogo tu pale nyumbani kwa Baba Askofu. Hii inaonyesha watu hawa waliouawa ilitakiwa kuwa hivyo kabla hawajaingia mikononi mwetu. Kwahiyo kilichopo sasa hivi ni kutafuta na kujua ni nani ambaye alikuja na ile gari. Na tukishalifahamy hilo tutamtafuta mhusika." Aliongea masimba huku akikilaza kichwa cha Teddy kifuani. "Kwa nini Ulinituma nikamuue Baba Askofu?. Akauliza Teddy kwa mara nyingine huku akiuvaa uso wa kazi. "Nilikutuma kwa kuwa Alikuwa mmoja kati ya wahusika wakuu katika Biashara hii." Akajibu Masimba kwa Utulivu. "Ulijuaje hilo?" Akauliza tena. Ni swali hilo lililoubadirisha uso wa masimba. Sasa alikuwa akimtizama Teddy kwa macho ya sio na utani. Swali lake lilikuwa la kitoto kwa mtu mwenye uzoefu wa kiusalama kama yeye. "Swali gani la kitoto hilo unaloniuliza? Kwa hiyo mimi naweza kubuni tu kuwa mtu fulani anafanya biashara hii? Unajua kwa nini amekupa hiyo bahasha na kukwambia uilete kwangu?" Aliongea masimba kwa kufoka huku akimuangalia teddy. "Sio kwamba ni swali la kitoto, nimeuliza kwa kuwa kuwa kuwa kwangu kule sikuwahi kuwaona hata siku moja katika mikutano yetu." Akajibu Teddy kwa upole huku akikichezea kifua cha Masimba. "Naomba bahasha hiyo tuifungue, lakini tambua hii vita sasa tunapigana Na taasisi ya Urais. Kama gari za Ikulu zinatumika katika haya huku tunakoelekea ni kubaya. Usiikubali hofu ichukue sehemu kubwa katika Maisha yako. Hii ni vita ambayo inaweza kutupoteza na kutufuta katika Dunia hii. Licha ya kutufuta kwenye uso huu, lakini pia hatutokuwa na chochote cha kutukumbuka. Unatakiwa uitoe hofu na kuitokomeza. Ujuzi tulio nao utusaidie kutufikisha katika mwisho wa hii safari." Aliongea masimba kwa kirefu. Maneno yake yakamuingia Teddy na kumsisimua. Ulikuwa wakati wa kupambana, ulikuwa wakati wa kutumia ujuzi wao wote kuhakikisha hili linafika mwisho. Kwa nini awe na Hofu? Kwa nini aogope? Tokea lini yeye akaogopa Risasi? Tokea lini yeye akakiogopa kifo? Akazidi kujilaza kifuani kwa Masimba. "Nipo tayari Kupambana Dady? Nipo tayari kufanya kila kitu kwa sababu yako na sababu ya nchi yangu." Aliongea Teddy katika namna ambayo ilimsisimua. Muda wote huo hakuwa ameitoa Bahasha, hakuwa ameitoa kwa kuwa hakuambiwa afanye hivi. Akapeleka mkono mahali ambapo aliihifadhi Bahasha. Akaitoa na kumkabidhi masimba. Wakati masimba akitaka kuifungua Bahasha, simu yake ya Mkononi ikaita. Akatulia kwanza akimuangalia teddy machoni. Teddy naye akamkazia macho huku wivu ukionekana Shahiri machoni mwake. Alikuwa akihisi labda mpigaji ni Mwanamke. Masimba akaitoa Simu Mfukoni kwake, kabla ya kuipokea akatizama jina la mpigaji.. Major General Chomboko. Haraka akaipokea simu. "Utahitajiwa Ikulu Muda huu, lakini Make sure kabla hujaondoka hapo ulipo unaweka vizuri hiyo Bahasha. Ikipotea Hiyo basi Hata wewe Hutakuwa na Njia ya Kujinasua." Aliongea Major General Chomboko. Kisha pasipo kusubiri chochote. SIMU IKAKATWA.

MASIMBA AKAMTIZAMA TEDDY NA HATA TEDDY AKAMTIZAMA MASIMBA.

BADO KAZI YAO ILIKUWA NGUMU
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 075

"Nahitajika Ikulu Teddy. Lakini nimeambiwa nihakikishe bahasha na itunza na kuiweka vizuri. Kwani tukiipoteza nami nitafutwa kwenye uso huu wa dunia." Aliongea masimba baada ya kukatwa kwa Simu. "Nani amekupigia na kwa nini iwe hivyo?" Akauliza Teddy. "Teddy naomba ushtue ubongo wako ufanye kazi kama ulivyokuwa unafanya kule Syria. Maswali unayouliza hayapaswi kuulizwa na Afisa usalama wa kiwango cha Juu kama wewe. Kifupi ni kwamba nahitajiwa ikulu, lakini naamini hakutakuwa na usalama. Simu niliopigiwa na Meja jenerali Louis Chomboko ni simu inayonifanya niamini kuwa maisha yetu yapo hatarini hasa mimi hapa." Alijibu Masimba akionyesha kuipoteza furaha na hata tabasamu. "Dady unaniweka kwenye wakati mgumu, umeuweka moyo wangu katika sintofahamu. Tafadhali tuliache hili suala. Sitaki kukupoteza Masimba wangu. Aliongea Teddy kwa sauti ya Hisia. Alikuwa akimuangalia mpenzi wake usoni. Akashindwa kulizuia chozi lake lishuke mashavuni. Teddy alikuwa akilia, tena alikuwa na hofu ya kumpoteza masimba. Lakini hilo halikumfanya masimba abatilishe uamuzi wa Kwenda Ikulu. "Teddy siwezi kuliacha hili hata kama litanigharimy maisha yangu. Nipo tayari kufa kwa sababu ya nchi hii. Kama Rais ataona nastahili kufa basi nipo tayari. Nimempoteza mama na Dee Plus. Tumempoteza Vicky juzi tu hapa. Kuna roho za watu wengi wamekufa kutokana na hili. Nani anaweza kuirudisha roho ya Mama yangu Mzazi? Nani atairudisha Roho ya Vicky au Dee plus? Nipo tayari kufa. Kama wataweza kuwarudisha vijana walionyongwa na kuharibiwa na madawa?. Sikiliza Teddy naondoka nakuachia bshasha hii, hii bahasha ndio uzima na uhai wangu. Ukipoteza hiyo Bahasha utakuwa umenipoteza mimi. Itunze kama unavyotunza mapenzi yetu. Najua nikiondoka hapa kuna watu watakuja hapa. Kuna watu watakufuatilia ili kuichukua hiyo bahasha. Naomba upigane kama ulivyopigana tulipokuwa urusi na hata Syria. Pigana kwa Ajili yangu na Pigana sababu ya Nchi hii. Hata kama wataniua, naomba uje uwaambie wanangu mkasa huu. Acha niende mpenzi." Aliongea masimba na kumkumbatia Teddy kwa nguvu. Naye alishindwa kuvumila. Chozi la uchungu lilikuwa likishuka. Hakumsubiri Teddy atamke lolote. Akamuacha Teddy akiangua kilio chumbani wakati yeye alikuwa akiufungua mlango tayari kwa safari. Akili yake ilikuwa imevurugika katika kiwango kikubwa sana. Alihisi viongozi wa nchi yake hawakumpenda na hata kuthamini kile ambacho amekifanya. Leo hii alikuwa amegeukwa na Idara zote za usalama isipokuwa watu wachache tu ndani ya Idara hizo. Akatembea taratibu akielekea nje kabisa. Wakati akitembea akahisi uwepo wa mtu nyuma yake. Mtu ambaye alikuwa akilia. Akageuka taratibu, akageuka kumuangalia mtu huyo anayelia. Alipogeuka macho yake yakamuona Teddy akitembea Huku akilia. Akasimama kwa kupigwa na Butwaa. Akimuangalia Teddy alipokuwa akitembea. Hata walipokutana wote wakakumbatiana. "Teddy wewe ni shujaa, usiuruhusu udhaifu huu uondoe ule moyo wa kijasusi ulionao. Moyo wa kupambana katika aina yoyote. Siendi kufa nitarudi mama." Aliendelea kuongea masimba akimbembeleza Teddy. Hatimaye Teddy akatulia na kumuangalia tena masimba. Macho yake ambayo hayakuuonyesha utani tena. "Nenda Dady, naamini hawana uwezo wa kufanya chochote. Nakuamini na nina aamini kuhusu hili. Vita hii ni kubwa, vita hii ni vita dhibi ya utawala usiofuata Sheria." Aliongea Teddy akirudi katika uteddy wake ule ule. Tabasamu la uchungu likajitokeza Usoni. Masimba hakusubiri Tena, hakusubiri hilo liendelee. Akajitoa kwenye mwili wa Teddy na kuanza kuipiga hatua kuufuata mlango wa kutokea. Mwanga wa jua umlikaribisha Masimba katika aina ya kuburudika kabisa. Macho yake yalikuwa kwenye miwani maalum ya kiusalama huku hatua zake moja moja zikiikanyaga Ardhi kana kwamba alikuwa akiiogopa. Mwendo wake pekee usingeweza kukuvuta na kuhisi labda huyu alikuwa fulani. Bali kama ungemuona kwa wakati huo ungejua huyu lazima ni chekibobu fulani hivi mtoto wa mjini. Lakini licha ya mwendo huo bado macho yake yalikuwa yakitizama kwa hila pembezoni mwa barabara na maeneo yote yanayoizunguka Hoteli aliyomuacha Teddy. Sura nyingi alizoziona hapo hazikumpa mashaka kwa kuwa hazikuwa sura za kazi. Hata macho ya watu aliowaona pale hayakumtia wasiwasi kabisa kwa kuwa hayakuonyesha kama yalikuwa yakimtizama kwa hila. Akaongeza mwendo tena mara hii akibadili muelekeo ili kuona kama anafuatiliwa. Lakini haikuwa hivyo. Alikuwa peke yake katika njia hiyo. Hata moyo wake ukapata faraja baada ya kujua kuwa Teddy hatakuwa matatizoni. Lakini wakati anaumaliza mtaa fulani kabla ya kutokea barabara kuu, akapitwa na Magari mawili, magari ambayo yalimfanya asite kwanza kutembea. Akasimama pembezoni mwa barabara akiyatizama Magari yale mpaka yalipokwenda kusimama umbali mfupi kutoka pale Hotelini alipo Teddy. Hilo likamfanya ajipapase mifukoni kuitafuta simu yake. Lakini licha ya kujipapasa huko hakuiona. Akakumbuka kuwa simu yake aliiacha kitandani katika chumba kile alichomuacha Teddy. Hapo akaona kuna ulazima wa kurudi. Kwa kuwa gari zilisimama kwa upande wa mbele, Masimba akaona apitie mlango wa nyuma.

******

Teddy alikuwa amejiinamia kitandani akiitafakari kazi iliyombele yao. Kazi ambayo ilikuwa hatari na ngumu sana. Kazi ambayo ingeweza kuwapoteza na kuwafuta katika ulimwengu huu. Akainua uso wake juu kutizama darini. Akaiweka mikono yake pamoja kisha kupiga alama ya Msalaba. Kwa mara nyingine alikuwa amemkumbuka Mwokozi wake. Baada ya kufanya Ishara hiyo akainuka na kuiendea ile bahasha, akaichukua na kuishika mikononi mwake. Aliitizama ile bahasha kwa muda mrefu pasipo kufanya kitu chochote. Wakati akielekea kitandani ili kufungua ili kuangalia kilichopo ndani. Akausikia mlango wa chumba alichomo ukigongwa. Akasita kwanza kufungua, mlango ukagongwa mara ya pili, Teddy akatulia. Wakati huo huo wazo la kwamba watu hawa sio wakawaida likamjia kichwani. Alichofanya ni kuikunja ile bahasha na kuitumbukiza ndani ya nguo yake ya Ndani. Baada ya kumaliza kufanya hivyo, akaufuata mlango kisha kufungua. Mdomo wa bastola ndio kitu cha kwanza kukutana nacho. Kitu cha pili akasukumwa kurudishwa ndani. Watu watano wenye miili ya kutisha wakaingia ndani. Ni watu ambao Jenipher aliwatambua, ni watu ambao aliwajua na anawajua. Wote wakatizamana kwa muda bila kuongea kitu. Hawa kuzungumza kwa mdomo bali macho yao yalionyesha kule ambacho walikihitaji, kukitaka na hata kukichukua. "Tunaomba mzigo ambao mlipewa na Baba Askofu." Ilikuwa sauti ya mmoja kati ya watu wale akionyesha kutokuwa na masihara.

"Mzigo gani unausemea? Na mnamsemea Askofu yupi? Akajibu Teddy naye akionyesha kutokujua chochote. "Teddy hatukuja hapa kupoteza muda, bila shaka unatambua ukipewa oda unatakiwa kufanya sio kuuliza." Bado aliongea yule mtu huku akimuangalia Teddy usoni. "Oda ninayo tekeleza ni oda kutoka kwa Waziri mkuu, Raisi, Makamu na DG pekee. Nyie ni nani na mnatoa oda kama nani? Aliuliza Teddy huku akijiandaa na chochote ambacho kingeweza kutokea. "Teddy usitulazimishe kufanya kitu ambacho utakijutia.". Alionya mtu yule. "Dereck Usijifanye hujui kanuni za kiusalama. Nijibu hapa umetumwa na nani kati ya watu hao niliokutajia? Kwa nini uzungukezunguke tu. Pia nashanga.... kabla hajamalizia kauli yake. Ngumi nzito ikatua tumboni na kumfanya apepesuke huku maumivu makali yakisikika. "Tumekwambia usitulazimishe tukuumize tukashindwa kuangaliana. Tunachotaka ni bahasha tu." Alizidi kuunguruma mtu huyu.

"Fanyeni mnachotaka kufanya, sina bahasha wala simjui huyo Askofu. Mnashindwa vipi kujibu maswali yangu?. Aliongea Teddy kwa kufoka. "Carlos fanya kazi yako. " baada ya dereck kusema hivyo, Kijana huyo akamsogelea teddy kisha kumkamata. Wakaifunga mikono yake kwenye kitanda. Baada ya hapo wakaanza kumtandika ngumi mfululizo. Zilikuwa ngumi zilizompa maumivu makali sana. Alijaribu kuvumilia kwa muda mrefu sana. Lakini baadae alisalimu amri. "Subiri ni ni.. nitasema." Aliongea Teddy huku damu zikimvuja. "Carlos muache kwanza atueleze..." aliongea derick huku akimuangalia Teddy kwa macho makali. Wakati wakisubiri Teddy aseme, wakausikia mngurumo wa kitu. Mngurumo ambao kila mmoja aligeuka bastola mkononi kuangalia kule unapotokea mngurumo. Macho yao yakakutana na simu, simu ambayo ilikuwa ikiita. Hata Teddy hakuwa ameiona simu ya masimba. Kitendo cha kugundua Masimba ameisahau simu yake kulimpa nguvu kuwa masimba atarudi hapo. Akauvuta muda na kuuvuta tena.

******

Baada ya kugundua simu yake ameisahau pia kuyaona magari ya kisimama na watu wa aina fulani wakishuka, masimba akapanga kurudi. Lakini safari hii hakurudi kwa njia aliyotokea. Bali alikuwa amerudi kwa Njia tofauti ya kuingilia Nyuma ya Hoteli Hiyo. Alitembea akihakikisha haingii kwenye macho ya watu hawa. Akafanikiwa kufika nyuma ya hoteli hiyo.. akapenya uani na kufanikiwa kuingia ndani ya hotel pasipokuonekana. Kwa kuwa alikuwa amehesabu namba ya chumba chake wakati anaingia na hata kutoka. Ilikuwa ni rahisi kujua chumba chake kilikuwa sehemu gani. Akafikiri kidogo akaona nilazima apitie juu ya silling board ili kuepusha kuonekana. Chumba cha kwanza akakutana na miguno, hapo akajua watu walikuwa kstika shughuli yao. Chumba cha pili kilikuwa kimya. Akachungulia kwenye Tundu la Ufunguo, akakuta kwa ndani hapakuwa na mtu. Akachomoa Funguo zake malaya na kuitumbukiza kwenye tundu la kitasa. Sekunde iliyofuata masimba alikuwa ndani ya chumba kilichoonyesha kutandikwa vizuri. Akaaangalia juu akaiona sehemu maalum ya kupita. Akachukua kiti na kukiweka juu ya kitanda. Kisha akakanyaga na kupata urahisi wa kuutoa ule mfuniko. Baada ya hapo akajivuta kwa juu. Akafanikiwa kuingia pasipo wasiwasi. Baada ya kuhakikisha ameingia akaurudishia mfuniko, kisha kuanza kusota na tumbo kuelekea kwenye chumba alichomuacha Teddy. Ulikuwa ni mbuluziko mithiri ya nyoka, mbuluziko ambao haukutoa kishindo wala sauti. Akafanikiwa kufika usawa wa chumba chake. Kilio cha Teddy ndicho kilichomshtua, kilichomwambia kuwa Teddy alikuwa matatani. Masimba hakuchelewa.. Tayari Bastola mkononi na sekunde hii alikuwa akielekea pale ulipomfuniko wa kutokea.
 
Ibrah kama ungemalizia kipande hicho maana x kwa utamu huo
 
Masimba Katika Ubora Wake, Atatoka Na Teddy Wake Ataziacha Maiti Ndani Watatokea Kwenye Njia Ya Mfuniko Atakayotumia Masimba
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 076

Alikuwa akitambaa akiuendea mfuniko tayari kwa kutoka nje. Kelele za Teddy bado zilikuwa zikipenya masikioni na hata moyoni. Chuki na hasira zikapanda kwa pamoja. Hata alipoufikia mfuniko na kuufungua, hakuna hata mmoja ambaye alimuona. Hata alipotua katikati ya watu hawa. Kila mmoja akainekana kuduwaa. Kila mmoja hakulitegemea na hata kutarajia. Masimba akauwahi mlango na kuufunga kwa ndani. Kisha akageuka na kumtizama Teddy wake pale kitandani alipofungwa mikono yake kwa nyuma. Macho yake yakapokewa na damu iliyokuwa ikivuja kutoka kwenye mwili wa huyu malaika wake. Damu iliyokuwa ikishuka kutoka kwenye kinywa cha huyu mrembo. Kinywa cha mwanamke wa maisha yake. Kinywa cha mpenzi wake. Baada ya hilo akageuza macho kwa watu hawa ambao Bunduki bado zilikuwa mikononi. Bado hawakuweza kuzitumia. Bado hawakuruhusu mikono yao kufanya hivyo. Waliganda mfano wa barafu, waliganda mfano wa masanamu. Carlos hakuwa Carlos na Hata Derick alikuwa kimya. Kimya kama hakuwa yule. Aligwaya na pia alikuwa ameelemewa na mduwaa. Hakuuona umuhimu wa bunduki zaidi ya kumuangalia Masimba. Macho yake yakakutana na macho ya Masimba yaliokuwa yakiwaka. "Carlos mfungue huyo mwanamke hapo. Kisha hayo maswali mliokuwa mnahitaji huyu ajibu, mtaniuliza mimi na nitawajibu mimi." Aliongea masimba kwa sauti ya utulivu. Bado macho yake yalikuwa kwa Kipenzi Chake. Carlos akasogea kitandani na kufanya kama kile alichotakiwa kukitenda. Akaifungua kamba mikononi kwa Teddy. Baada ya kufunguliwa kamba kikatokea ambacho hakuna aliyekitarajia. Hata masimba hakutegemea kitu kile kutokea pale tena kutendwa na Teddy. Lakini wasichokitegemea ndicho kilitendeka. Carlos alikuwa chini kichwa kikiwa kimepasuka. Risasi kutoka kwenye Semi Automatic pistol zilitosha kukipasua kichwa cha Carlos. Derick akapagawa huku wengine wakichachawa. Sasa mdomo wa Semi automatic ulikuwa ukikitizama kichwa cha Derick, kichwa ambacho hakikuimaliza hata Sekunde moja. Tayari ubongo na damu ulikuwa hewani ukisambaratika na kutapakaa ndani ya chumba kile. Harufu ya Damu na Mauti ikasikika kwenye pua za watu wake. Huyu hakuwa Teddy wa muda mfupi uliopita, huyu hakuwa Teddy wa kipindi chote. Alikuwa teddy mtamu na mwenye kuvutia katika medani hiyo. Alikuwa mtamu na mwenye kuleta hamu. Bado bastola mkononi na Bado macho yakiwatizama watu hawa waliobaki. Watu hawa walioshtushwa na kilichotokea. Hapakuwa na utani wala masihara. Hapakuwa na utani katika macho na hata uso. Macho yalikuwa yakieleza kifo. Ni wakati wakiendelea kushangaa wakauona mlango ukisukumwa. Licha ya kusukumwa haukufunguka. Haukufunguka kwa kuwa Masimba aliufunga kwa ndani. Bado hawakujali kusukumwa kwa mlang0, lakini haikuchukua hata nusu dakika. Kitasa kilikuwa kikishambuliwa kwa Risasi kisha mlango kusukumwa huku watu wengine watatu wenye silaha mikononi wakiingia. Hawakujua kilichokuwa ndani, hawakujua kile ambacho kimewapata wenzao. Wakaingia wakiamini wanaweza. Waliingia wakiamini wanauwezo wa kupambana. Lakini kitendo cha kuingia ndani ya chumba kile. Wakapokewa na Risasi kutoka kwenye Bastola iliyoshikilia na Teddy aliyekuwa Akivuja Damu. Wote wakaanguka chini wakirusha miguu huku na huko. Teddy alikuwa kama amechanganyikiwa, teddy alikuwa kama mwenda wazimu. Chumba kilitapakaa damu huku harufu ya kifo akitamalaki chumba chote. Maiti za watu nane zilikuwa chini. Watu ambao walikuwa wana Usalama waliotumwa Bahasha. Bahasha ambayo ilikuwa na vitu vingi ndani yake. "Jifute damu hiyo tuondoke upesi, hii sehemu sio salama." Aliongea Masimba huku akichukua kitambaa ili kumsaidia Teddy kuifuta damu. Wakati anakichukua kitambaa simu yake ikaita tena. Macho yake yakaenda moja kwa moja kwenye kioo cha Simu. "Chief" ndio maneno yaliyosomeka Juu ya kioo. Masimba hakuipokea kwa muda ule. Akaiacha iendelee kuita mpaka ilipokata yenyewe. Alikuwa na maana yake kutokuipokea Simu ya Chief. Alitaka kujua kama watu hawa wametumwa na Idara au la. Kutokupokea simu kungemuwezesha Chief kujua kile ambacho kimetokea. Baada ya simu kukata, haikupita Hata Dakika moja, simu ya mmoja kati ya maiti zilizotambarajika Chini ikaita. Teddy na Masimba wakaangaliana. Kabla hajasema chochote Masimba akaichukua simu kutoka Mfukoni kwa maiti yule. "General Chomboko" ndio Jina lililosomeka juu ya kioo cha simu ile. "Mmh" masimba aliguna, aliguna kwa mshangao mkubwa. Kuliona Jina la Jenerali Chomboko kwenye simu ya mkora yule kulimshangaza. Kulimshangaza kwa kuwa ni huyu huyu mzee aliyepiga simu muda mfupi na kumwambia kuhusu kuitwa kwake Ikulu. Lakini muda huu jina lake lilikuwa likionekana Juu ya simu ya watu waliotumwa kuja kuichukua Bahasha. Akanyamaza na kutulia, hakuongea zaidi ya kuushika mkono wa Teddy na kuanzA kupiga hatua wakitoka ndani ya Hotel.

*******

Simu yake ya mezani ilikuwa ikiita katika usiku huo. Ilikuwa sio kawaida kupigiwa simu usiku mwingi kama ilivyoleo. Alijiinua Taaratibu na kuunyoosha mkono wake mpaka iliposimu. Akaisogeza karibu kisha moja kwa moja akaipeleka sikioni. "Hellow General Chomboko.!! Ilikuwa ni sauti kutoka upande wa pili. Sauti ambayo ilikuwa ikitoka kwa mkurugenzi wa Usalama wa Taifa. "Kimaro mbona usiku, kuna tatizo?" Aliuliza General Chomboko bila hata kusalimia. "Chomboko Hutakiwi kuruhusu uzee uchukue uwezo wako wa kiugunduzi. Chomboko yule wa kipindi kile asingeniuliza hili bali kutaka ufumbuzi." Akajibu Mr kimaro.

"Nimezeeka kwa sasa, nimewaachia nyie ambao bado mnadai. Tuyaache hayo, mpaka kunipigia simu usiku huu nahisi kuna jambo ambalo halikajakaa sawa." Akajibu jenerali Chomboko. Chief akatulia kwa Muda. Ukimya ukachukua mahala pake. "Kuna Bahasha imepotea mikononi mwa Askofu Ibrahim Lexandre Rengima. Bahasha hiyo inasemekana ipo mikononi mwa Masimba na Mwandani wake. Inasemekana Bahasha hiyo ina mambo mengi ya Siri na ya Hatari sana kwa Nchi. Sasa Mheshimiwa Rais Ameagiza kesho Masimba aitwe Ikulu apeleke bahasha hiyo walioichukua mikononi mwa Baba Askofu Rengima. Sasa nimekupigia kukuomba ushauri katika suala hili. Nimejaribu kuongea na Teddy lakini majibu aliyonipa ndio yaliyonifanya niinue mkonga wa simu nikupigie." Akaeleza Chief kwa kirefu. Jenerali chomboko akatulia kwa muda huku akitafakari maelezo hayo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya ujasusi. Baada ya kutafakari sana, akauliza. "Teddy amekujibu nini?"....

"Teddy amesema kama tuna uwezo wa kurudisha Roho ya Mdogo wake, roho ya Dee plus na Roho ya mama mzazi wa masimba, wataisalimisha Bahasha Hiyo. Lakini kama hatuna uwezo huo, basi hawataisalimisha Bahasha hiyo." Akajibu Chief.

"Kwa nini Mheshimiwa Rais Anaitaka Hiyo Bahasha? Akauliza generali Chomboko.

"Hata mimi bado sijajua kile kinachosababisha yeye kuihitaji hiyo bahasha na ni vipi ameijua kwamba ipo kwa askafu. Na kingine kinachonishangaza ni kuonekana kwa gari yenye Nembo ya Ikulu, ikitoka sehemu zote ambazo waliuawa Viongozi wa dini ambao wote wana Uhusiano na Hiyo Bahasha. Hapa ndipo ambapo pana nishangaza na kunipa wasiwasi." Akajibu Chief. Jibu la chief likaibua ukimya mwingine kutoka kwa General Chomboko. Kichwa chake kilikuwa kikifikiria mengi katika hili linaloendelea. Hili suala kukingiwa kifua na mheshimiwa Rais ni kuonyesha uhalisia kuwa kuna kitu anakijua na hata kukifahamu. Ameijuaje bahasha iliyochukuliwa nyumbani kwa Askofu. Ni nani aliyekwenda huko na gari ambayo ilikuwa na Nembo ya ikulu? Hayo yalikuwa maswali machache kati ya mengi aliokuwa nayo. Ilishaanza kuiona hatari, alishaanza kuuona msuguano katika idara. Idara ya usalama wa nchi. Lakini haya yote ni kwa sababu gani na zipi? Baada ya kujiuliza Maswali hayo yasio na majibu, akakumbuka kuwa bado Mkurugenzi wa Idara ya Usalama Yupo Kwenye laini. "Mr Kimaro vijana wako wapo nyuma ya suala hili. Ikiwa wewe mkuu wao hujui gari ile ilikwenda kufanya nini huko, ina maana kuna vitu vinafanyika pasipo wewe kushirikishwa. Sasa swali la kujiuliza Je Hili lililoibuka kwa sasa lina baraka ya kiti cha rais?" Akamaliza jenerali kwa kuuliza swali. "Nahisi lina baraka ndio maana anaihitaji hiyo bahasha. Unachotakiwa kufanya naomba umuarifu masimba kuhusu hili na pia hakikisha hiyo bahasha haifiki mikononi kwa rais wala Haipotei. Hiyo bahasha kuwepo kwake ndio uhai wa vijana hawa. Ikipotea ama kufika mikononi kwa Rais, basi tutakuwa tumepoteza watu sahihi." Aliongea Chomboko akionyesha kukijua kitu fulani. "Sawa nimekuelewa na nimekupata. Nakupongeza mwenzangu kwa kupata mwanga katika hili." Alijibu Jenerali. "Nadhani Asubuhi nitaongea na Masimba mimi mwenye ili kumpa Tahadhali katika hili." Akajibu kisha simu zikakatwa.

*****
Alimshika Teddy mkono na kuongozana naye kutoka katika viunga vya hoteli ile. Muda wote wakati wakitembea walikuwa wakihakikisha hawaingii mikononi kwa macho ya maadui zao.kichwani kwa masimba kulipishana mambo mengi sana. Vitu ambayo vilizidi kuisumbua akili ba hata kukivuruga kichwa chake. Kwa nini anahitajika Ikulu? Kwa nini Rais anaitaka Bahasha walioichukua kwa Baba askofu? Kwanza Rais amejuaje kuhusu hili? Kwa nini General chomboko awapigie simu watu hawa, wakati jana na hata Leo alinitahadhalisha? Ina maana hii vita iliyoanza kama utani leo hii imekuwa kubwa mpaka kumgusa Rais? Ni maswali hayo yaliomfanya amgeukie teddy. Akamwangalia kwa macho yake yenye kutia moyo. Kisha kwa Sauti ya utulivu akasema. "Teddy mke wangu, wakati huu lilipofikia hili ni wakati hatari kuliko huko tulipotoka. Naanza kuhisi kitukutoka ndani ya Taasisi kubwa hapa nchini. Naanza kuhisi kuwa tumegusa maslahi ya wahisani katika biashara hii. Niwakati wetu wa kusimama katika kupambana na hili. Meja jenerali chomboko ana kitu anachokijua kuhusu hili kinachoendelea. Teddy Nakupenda na sitaki kukupoteza katika hili. Wakati huu mimi nikielekea Ikulu, nakuomba wewe uwe ndani ya gari binafsi ukielekea Tanga kupanga mikakati ukiwa na hiyo bahasha. Bahasha ambayo imeonyesha kuleta sintofahamu kwa Nchi yangu. Natambua ni kiasi gani Chief Anasumbuliwa kwa sababu yetu. Nakuomba nenda Tanga ukajifiche huko hata kama huku wataniua utajua wapi pakuanzia." Alioongea masimba kwa mara ya kwnza machozi yakichungulia machoni. Hata Teddy alikuwa akilia sana. "Hapana Dady, siwezi kukuacha katika hili, siwezi kukuacha katika mapambano haya. Ufe mbele yangu au Nife mbele Yako." Aliongea Teddy akimaanisha kile anachokisema. "Fanya nilichokwambia Teddy, bahasha tulionayo hatupaswi kuwa nayo mikononi mwetu. Ondoka hapa jijini Upesi." Baada ya kuongea hilo akisubiri Teddy ajibu simu yake ikaita. Kuitizama namba ya mpangaji akagundua ilikuwa ni Namba ya Ikulu. Akamuonyesha Teddy kisha akaipoke.. "Tuna kusubiri wewe." Ilikuwa ni sauti iliyotoka upande wa pili, kisha simu ikakatwa. Masimba akaduwaa kwa muda akimuangalia Teddy. 'Kwaheri Teddy... fanya nilichokwambia." Akaaga masimba huku akiondoka akimuacha Teddy AMEDUWAA
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 077

Alibaki ameduwaa akimtizama Masimba akiondoka katika upeo wa macho yake. Akamtizama kana kwamba asingemuona tena. Kana kwamba asingemuona kwa miaka yote. Akatamani kumuita, akatamani japo amfuate, akatamani hata kuongea naye. Lakini kila kitu kilikuwa kigumu. Kilikuwa kigumu kwa kuwa masimba alikuwa akipotelea katika upeo wa macho yake. Akatambua kuwa alikuwa amemaliza dakika moja pale kitu ambacho kingekuwa ni Hatari kwake endapo angetokea mtu au watu wakumfuatilia. Muda mfupi baadae alikuwa ndani ya bajaj akielekea katikati ya jiji. Ulikuwa uamuzi ambao aliuchukua kutoka moyoni mwake. Hakupenda kumuacha nasimba. Moyo wake ulikuwa mzito kuliko chochote. Masimba kwake alikuwa anathamani kuliko bahasha ambayo alikuwa ameishika mkononi. Bahasha ambayo ilikuwa na maslahi kwa nchi. Hakujua ama alisahau kipaumbele cha usalama wa Taifa ni kuwa mzalendo kwa nchi yake. Kutoka moyoni kwake alimuona Masimba ni Bora kuliko nchi yake. Alitaka kuuona mwisho wa Masimba. Akaipa utulivu akili yake. Akaipa muda wa kutafakari kile ambacho alitaka kukifanya. Hakujua Bahasha ilikuwa na mambo gani mambo yake. Wakati bahaj akifika kwenye mataa ya faya, moyo wake ukamlipuka baada ya kuyaona magari mawili nyuma ya bajaj. Yalikuwa magari ambayo aliyatambua. Magari ambayo moja kwa moja alijua yalikuwa yakimfuatilia yeye. Wakati akilishangaa Hilo, akashtuka baada ya kumuona mtu akiingia kwenye bajaj na kutulia. Mtu huyu hakumzungumzisha Teddy bali aliingea na Dereva Akimtaka Ageuze bajaj na kuirudisha atokapo. Bado Teddy aliduwazwa na hilo, bado Teddy hakupata wasaa wa kuliuliza hilo. Akili yake ilikuwa imehama mbali na parefu sana. Akili yake haikuwa kwa mtu yule bali akili yake ilimuwaza sana Masimba. Alihisi hata muona Tena Masimba, alihisi hataweza kumpata tena mtu. Kuingiliwa na mtu ndani ya bajaji na kumtaka dereva wa Bajaj ageuze alikotoka, hilo hakulijali kutokana na uingiaji wa mtu huyu. Uingiaji ambao haukuonyesha labsha na hata chochote kile. Uingiaji wa mtu huyu ulijaa urafiki na haukuwa katika kile kinachoitwa kazi. Aliingia kanakwamba alipewa ama kupewa Lifti. Hakuonyesha bsstola wala silaha youote. Licha ya kufanya hivyo lakini sura ya mtu huyu iliongea naye vitu vingi sana. Kwanza haikuwa na tabasamu, pia sura hii haikuonyesha kama iliwahi kutabasamu. Dereva akataka kuhoji lakini jicho lililomtizama kutoka kwa mgeni wao huyu lilimfanya aigeuze Bajaj kama alivyoambiwa na mtu huyu. Muda wote huo bado Teddy hakuzinduka katika bumbuwazi. Bado alikuwa mbali sana. Sauti kutoka kwa mgeni Huyu ndio iliyomzindua na kumrudisha katika uhai. Uhai wa kutambua huyu ni nani na alikuwa nani. Alitambua alikuwa hapo kwa sababu ipi. "Teddy kwa nini unakuwa mkaidi kutii unachoambiwa? Upo tayari kumpoteza Masimba?. Mtu huyu akazidi kumuuliza, akamuuliza akimuacha akiyatafakari maneno yake. Maneno yaliyoanza kuirudisha Akili yake. akatambua hawa walikuwa watu waliotumwa na Chief ama Meja jenerali Chomboko. Akatambua kuwa ni kweli bahasha hii ilibeba maisha yao. Hakutakiwa kubaki hapa mjini. Alitakiwa aondoke. Lakini ataondokaje ikiwa hajui kile kinachoendelea juu ya Masimba? Ni swali ambalo halikupata majibu. Halikupata majibu kwa kuwa Tayari alipewa Ishara ya kushuka. Ishara ya macho pasipo sauti. Ishara ambayo aliitii kwa kushuka. Aliposhuka tu akashangaa kuiona gari moja aina ya Toyota Land cruiser ikisimama miguuni na wakati huo huo mlango ukafunguliwa na yeye kuingizwa ndani ya gari. Ni kitu kilichofanyika ndani ya dakika moja tu. Dakika ambayo iliacha mshangao kwa dereva yule wa bajaj. Hakuwaona watu walivyoshuka na hata walipompotea kwenye upeo wa macho yake. Wakati amepigwa na butwaa asijue hili. Akamuona mtu mwingine tena mwanamke mrembo. Mwanamke huyu hakuongea chochote isipokuwa kuunyoosha mkono wake ulioshika noti mbili za elfu kumikumi. Akionyesha kuikabidhi mikononi mwa kijana huyu. Hata pale alipoipokea bado mwanamke yule hakusimama. Bali alipotea katika aina ile ile. Aina ya penzi kupotea kipindi cha uchumba. Hakumuona na hapakuwa na mtu. Wote walipotea. Akatabasamu, tabasamu la kukata tamaaa, kisha muda ule ule akaiondoa bajaj kuelekea kijiweni kwake.

******

Muonekano wa ikulu ulimlaki masimba kwa hali ambayo ilikuwa tofauti sana. Watu maalum walikuwa pembeni wakifanya shughuli zao. Shughuli ambazo zilikuwa ni geresha. Hilo aliligundua baada ya kushuka wizara ya Elimu na kuanza kutembea Taratibu kuelekea Geti kubwa la kuingilia ikulu. Watu waliokuwa wakionyesha kufanya Shughuli sasa walikuwa wakimuangalia masimba kila alipokuwa akipiga hatua. Alikuwa akitembea kwa umakini akiufikiria wito wa kuitwa na Rais wa nchi. Moyo wake ulikuwa tayari kwa kitu chochote ambacho kingemtokea. Alijua hata kama akifa atakuwa ameipigania Tanzania kwa kiwango cha hali ya juu. Akalifikia geti na kukaribishwa na Wana Usalama wa Ikulu. Akaongozwa kuelekea sehemu husika akiwa sambamba na wana Usalama wasiopungua sita. Walitembea naye kila hatua ya mguu wake, wakaangalia wote upande pale ilipotokea masimba kufanya hivyo. Mbele ya lango la kuingilia ndani Akapokewa na wakuu wa Idara waandamizi. Alipokewa na watu ambao kwa kuwaona tu alijua kile ambacho kingeenda kutokea ndani. CDF Sambamba Na IGP Wote walikuwepo nje ya lango kumpokea Masimba. Muda wote walikuwa wakimtizama kijana wao, wakimtizama katika sura za bashasha. Muda wote alikuwa akichungwa na kutizamwa katika namna ambayo hata mwenyewe aliitilia shaka. Akasalimia kwa Utii na Heshima. Baada ya hapo akaongozwa moja kwa moja mpaka sehemu ambayo alitakiwa kufika. Sehemu ambayo ulitakiwa kufanyika huo mkutano. Kila alipokatiza ndani ya majengo ya Ikulu Ulinzi ulikuwa wa kutisha. Aliongozwa mpaka ndani ya chumba maalum. Chumba ambacho hakikuwa na mtu yoyote. Hapa Masimba akaambiwa akae ili apewe maelekezo mengine. Wakati anasubiri kile alichoambiwa Asubiri akawaona watu wawili wakiingia hapa chumbani. Watu hawa haikuwa ngumu kuwagundua. Hiki kilikuwa kikosi maalum cha kumlinda Rais. Wote waliingia, kisha kusimama mlangoni. Hawakumuangalia Tena Masimba. Wote walikuwa wakitizama Nje walikotoka. Haukupita Muda mrefu Rais naye akaingia pale akiwa sambamba na Mpambe wake sambamba na Walinzi wengine. Baada ya Rais kuingia Masimba Akasimama kwa Heshima zote. Rais akasogea akielekea alipokaa Masimba. Akaunyoosha mkono kumsalimia mwana usalama huyu ambaye hakuonyesha wasiwasi wowote. Wakati rais akitabasamu na kucheka. Usoni kwa masimba hapakuwa na Tabasamu. Alikuwa akimuangalia Rais kwa macho yasiotizama pembeni. Katika macho ambayo yalitaka kusoma kile ambacho kilikuwa ndani ya Rais Wa Nchi. Baada Ya salaam Masimba akapewa Ishara Ya Kukaa. Baada ya wote kukaaa mlango ukafungwa na walinzi wote kutakiwa kutoka Nje. Ndani akabaki mheshimiwa Rais na Masimba Wakitizamana.

*******

Kitendo cha Rais wa nchi kuitaka bahasha yenye Siri kubwa ya nchi kuliwashangaza wakuu wa Idara zote za Usalama Wa Nchi. Simu Zilitembea katika usiku ule kwa Lugha ambayo haikuwa Rahisi kueleweka machoni kwa Watu. Mawasiliano kati ya CDF, IGP, Chief na Hata Major General Chomboko yalimalizika Saa moja Asubuhi wote wakiwa na Azimio Moja. Azimio la kumtaka Masimba kutokuiwasilisha bahasha ile mikononi Mwa Rais. Baada ya kufikia muafaka wa kile kilichozungumzwa, ndipo walipotumwa Watu binafsi kumfuatilia Masimba na Teddy ili kuhakikisha Bahasha haingii mikononi mwa Rais. Hata pale Teddy alipochukua bajaj watu hawa walikuwa nyuma yake wakihakikisha hafiki kule anapotaka kwenda. Amri iliyotolewa ilikuwa ni lazima Teddy Aondoke ndani ya jiji hili. Nilazima apotee na asionekane. Ilitakiwa hivyo kwa kuwa Kuna kila dalili ya Masimba Kushurutishwa kutoa Bahasha kwa Njia Yoyote ile
 
[06-08, 14:36] Ibrahim Masimba: NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 078

Alikuwa akitizamana na kiongozi mkuu wa nchi. Alikuwa akitizamana naye katika namna ya kumsoma. Katika namna ya kumuangalia kwa umakini. Alikuwa tayari kufanya chochote pasipo kuhofia kitu. Rais alikuwa akimuangalia Masimba pasipo kupepesa jicho lake pembeni. Alikuwa na nia ya kumtia hofu, alikuwa na shida ya kumfanya masimba amuigope. Lakini hakumjua huyu masimba alikuwa nani, hakujua masimba alikuwa mtu wa kutokuogopa kitu. Muda ukazidi kuyoyoma huku wakitizamana. Bado Rais hakufumbua kinywa chake kuongea kile alichotaka kukiongea. Hata masimba naye aliiweka heshima mbele, nidhamu ya uzalendo na hata heshima ya kikazi. Akazidi kukaa kimya akisubiri kuambiwa kile alichoitiwa. "Nauomba ule mzigo mliouchukua nyumbani kwa Askofu Rengima. Nitakupa kiasi chochote cha pesa uitakayo." Kwa mara ya kwanza kiongozi wa nchi alizungumza. Maneno yake yakamfanya Masimba ainue macho yake na kumtizama Rais. Alimuangalia kwa umakini huku akilazimisha Rais amuangalie na kumsoma kupitia Macho yake. "Sikuwahi kufika nyumbani kwa Askofu na wala sijawahi kuonana naye, na kwahivyo hakuna mzigo niliopewa na Mtu huyo Mheshimiwa Rais." Akajibu Masimba akiendelea kumtizama Rais usoni mwake. Jibu lake likaonyesha kumfanya rais kuukunja uso wake. Licha ya muda mfupi kuukunjua lakini tayari masimba alikuwa amehisi kitu. Kitu ambacho alipanga kutoondoka ikulu mpaka akijue. "Masimba Mwanangu hii ni fursa ya kutengeneza maisha yako. Hili suala unaloendelea nalo halitafika popote. Bora upewe pesa yako uishi vizuri na familia yako. Na uachane na hili. Nakueleza haya kwa kuwa Nakupenda na Tanzania Haitaki kukupoteza. Hembu fikiria hilo kwanza. Aliongea mheshimiwa safari hii akiongea kwa upole sana. Jibu hilo lilionyesha kumkera Masimba, jibu hilo lilimfanya Masimba amtizame kwanza Rais. "Unajua hili suala limepoteza watu wangapi? Unajua hili suala limeharibu maisha ya vijana wangapi? Leo hii unapata wapi nguvu ya kulisema hili? Mama yangu amelala Kaburini kwa sababu ya suala hili, leo unaniambia hilo? Kama unaweza kuwarudisha wote waliokufa kwa suala hili nitakubaliana na wewe. Otherwise risasi yangu itamuua kila mmoja hata kama ni wewe." Akajibu Masimba akiendelea kumuangalia Rais pasipo hofu yoyote. Macho yake yalikuwa yakisomeka vingine Kabisa. Jibu la Masimba likaonyesha kumtingisha Rais, kitendo cha kusema atamuua hata yeye kilikuwa kitu kibaya sana kwake. Akamuangalia Masimba kwa muda mrefu sana bila kuongea chochote. "Unadhani ni kitu Rahisi hicho unachokisema? Unadhani nikiamua unaweza kutoka hapa? Akauliza Rais naye akionyesha kuhamanika. "Kama nimeweza kutoka Ikulu ya Rais Vladimir Putin Wa Russia basi hapa hakuna ambacho kitanisumbua. Na ungekuwa na uwezo wa kunifuta basi usingeniita hapa. Umeniita hapa kwa kuwa unajua na kutambua kuwa mimi ni nani. Kwa ajili ya Tanzania Nipo Tayari Uniue ama kunipoteza." Alijibu Masimba akimaanisha kile ambacho anakitoa moyoni. "Usijidanganye Masimba kumbuka Nchi ndio imekusomesha mpaka kufika hapo ulipo. Kumbuka Gharama ya kukusomesha wewe ingeweza kutengeneza maisha kwa watu wengine. Tambua hilo kijana. Pia kukuita hapa sikukuogopa bali tunakupenda. Tukikutaka Hutusumbui kabisa." Akajibu Rais.

"Kwahiyo kama Umenisomesha ndio unitumie katika kuwaua wa Tanzania wenzangu? Ndio unitumie kufanikisha Madhambi yako? Ndio unitumie kukubali nje yangu iharibiwe? Nimeapa kuwa mzalendo kwa Tanzania. Ukiona Hii kazi ndio inakufanya uniambie hayo basi kuanzia leo Mimi sio Mwana Usalama katika nchi hii. Aliongea Masimba huku akichomoa kitambulisho chake na kukiweka juu ya meza. Ni muda ule ule mlango ukafunguliwa na wana usalama. Kila mmoja alikuwa Tayari kwa chochote. Lakini tofauti na walivyotegemea, wakakutana na Tabasamu la Masimba. Tabasamu lililokificha kitu moyoni mwake. Muda ule ule akainuka, aliamua kuinuka kuelekea nje ya chumba kile akikiacha kitambulisho juu ya meza. Kilikuwa kitendo ambacho hakikutegemewa na Rais. Bado alikuwa katika mzubao wa kutoamini. Kutoamini kule kunakofanywa na kijana huyu. Akatamani aamuru akamatwe lakini moyo wake uliijenga hofu. Hofu ambayo hata yeye hakuijua. Akamsindikiza Masimba kwa macho, akamsindikiza alivyokuwa akitembea. "Ni mtoto sana huyu hawezi kunishinda." Alijisemea akikiangalia kile kitambulisho. Kitanburisho ambacho kiliachwa Juu ya meza. Maafisa wa ikulu sambamba na wakuu wa idara zote za usalama waliokuwa wamekaa sehemu ya siri wakilitizama tukio lile kila mmoja alitoka baada ya kumuona masimba akitoka huku kitambulisho chake akikiacha mikononi mwa kiongozi wa Nchi.
[06-08, 14:36] Ibrahim Masimba: Alitoka akiwa ni mwenye Hasira. Aliamua kuiacha kazi aliyoipenda. Kazi aliyoitendea haki tokea mwanzo kabisa wa maisha yake. Hakuuona umuhimu wa kuendelea kuwa katika Idara hiyo. Idara inayosahau misingi ya kuanzishwa kwake. Idara ambayo imekuwa ikishiriki siasa za nchi hii. Mama yake, dee plus, vicky na watu wengine ni Roho ambazo zimeondolewa kwa sababu ya hili linaloendelea. Kwa nini Rais ameamua kulikingia kifua hili suala. Ni nani ambaye yupo nyuma mpaka kusababisha msimamo huu dhaifu kwa kiongozi huyu wa nchi. Akaamua Rasmi kuiacha kazi yake. Kazi hii ambayo ilikuwa ni hatari katika maisha yake. Akairuhusu miguu yake itembee katika namna ya kuliwahi lolote lile. Hakujali taharuki aliyoiacha huko ndani. Hakuwa tena mwana usalama, hakuwa tena Yule Masimba Tegemezi katika nchi hii na Idara ambayo aliitumikia na kunusurika kuuawa katika mission mbalimbali alizotumwa kuipigania nchi. Akalifikia geti kubwa la kutokae nje. Alikuwa akitembea kana kwamba hakuna chochote ambacho kimetokea. Hata macho ya watu waliokuwa wakimtizama kwa hila, hakujali na hata kuwafuatilia. Akatembea na kutembea akikipita Chuo cha Usimamizi wa Fedha Ifm. Hatua kumi mbele alikuwa akifika makao makuu ya Jeshi la magereza. Akili yake bado haikuwa imetulia. Akili yake bado ilikuwa akifikiria Sauti na kauli za rais wa Nchi. Kuna wakati alikuwa akijisonya na hata kuongea peke yake. Aliipenda Tanzania kwa Moyo wake Wote. Kuiwaza Tanzania kukafanya akili yake imkumbuke Teddy wake. Teddy ambaye alimuacha katika Gesti waliolala usiku uliopita. Teddy ambaye alimuacha hapo kituuoni akiduwaa na kushangaa. Hapo akauona Ulazima wa kumtafuta. Ulazima wa kumuona mtu huyu, mtu ambaye alikuwa ni Muhimu kwake. Wakati akifikiria kuichomoa simu yake ili amtafute Teddy, macho yake yakamuona mtu ambaye uliyafanya mapigo yake ya Moyo kwenda kasi. Umbali wa hatua hamsini kutoka alipo akamuona Jimmy. Jimmy Lambert yule ambaye alikuwa akimtafuta kwa Udi na Uvumba. Hicho nikitu ambacho kilimshangaza, kilimshangaza kwa hiki ambacho alikuwa akikiona mbele yake. Jimmy aliyekuwa amemtafuta kwa muda mrefu bila kumuona, leo alikuwa hatua hamsini mbele yake. Akatabasamu akicheka kimoyo moyo. Kisha akajiuliza. Inakuwaje Jimmy ajitokeze Muda mfupi baada ya yeye kuiacha kazi Hii? Hilo likamfanya acheke kwa mara ya pili. Akaiona vita ambayo imeanza kupiganwa na taasisi kubwa nchini. Alitambua kutokea kwa Jimmy mbele yake ulikuwa ni mpango uliosukwa. Ulikuwa ni mtego ambao alitegewa ili umnase. Hilo aliligundua mapema. Hivyo akaamua kumpita Jimmy pasipokumuangalia. Pasipokuonyesha kama amemuona. Akatembea mbele zaidi mpaka lilipo jengo la Freemason. Akatulia hapo kwa muda akitizama viatu kutoka kwa wachuuzi waliokuwa wakiuza. Hakuwa na Shida ya viatu, lakini alikuwa hapo kwa kuwa alitaka kujua kama Alikuwa akifuatiliwa au la!. Wakati ameinama hapo akawaona wadada watatu nao wakisogea hapo. Hawa walikuwa wadada warembo kuwahi kutokea machoni Mwake. Walikuwa wazuri hasa. Kila mmoja alikuwa na mkoba mkononi kuonyesha kuwa Alikuwa Nwanafunzi katika chuo cha Usimamizi wa fedha, ama mfanyakazi wa Benki Kuu ya Tanzania. Utembeaji wa wasichana hawa ukampa hamu ya kusimama vizuri, akageuka na kutizama nyuma. Cha kushangaza akapokewa na matabasamu Kutoka kwa watoto hawa. Kengele za Hatari zikalia kichwani mwake. Ni kengele hizo zilizomuamsha na kumuweka kwenye majibu kuwa Alikuwa anaandamwa tokea alipoondoka pale Ikulu. Alijua kuwa alikuwa anatafutiwa sababu ya kufutwa hapa Duniani. Akajiapiza kuwa mtulivu katika kipindi hiki. Utulivu ambao haukutakiwa kufanya chochote kile. Akawangalia Wasichana wale kwa muda mfupi kisha akaamua kuondoka Zake.

******

Kwani Masimba ni nani? Kwani Masimba anafaida gani kwangu? Kwani nikiipeleka hii Bahasha kwa mheshimiwa Rais na nikapewa kile Rais alichoniahidi atanionea wapi? Yalikuwa maswali kutoka kwa Teddy akijiuliza mwenyewe baada ya kuachwa katika nyumba moja ya Siri. Roho ya usaliti na tamaa ya pesa vilishamuingia. Sasa alikuwa akitamani tena kumsaliti, alikuwa akiitamani sana Pesa. Taarifa aliyopewa muda mfupi kuwa Masimba amekataa kutaja kiasi chochote cha pesa anachotaka kilimsikitisha sana. Aliitamani pesa na kuipenda sana. Pesa kwake ilikuwa na thamani kuliko penzi na hata utu wa Masimba. Hakujua masimba alikuwa akihangaika kwa sababu ya Tanzania. Hakujua Masimba aliwapoteza Ndugu zake sababu ya Kazi hii. Kwa mara ya kwanza akatamani sana kutoka ndani ya jengo lile la siri. Kwa kuwa bahasha alikuwa nayo ndani ya nguo zake akaona kuondoka hapo ndio ingekuwa njia Bora. Kile kilio na kiapo cha muda mfupi kilianza kuyeyuka taratibu. Hapakuwa na kiapo wala kilio tena. Tamaa ya pesa tayari ilimchukua Teddy. Muda mfupi alikuwa akiinuka pale akiyatoa mavazi yake na moja kwa Moja akielekea bafuni. Alikuwa kwenye mkakati wa kuianza safari ya kuondoka katika Jumba hilo. Muda mfupi baadae akatoka chumbani akiwa kama Alivyozaliwa. Akauendea mlango kisha kubonyeza kengele ya hapo mlangoni. Punde mlinzi wa Jumba lile akafika na kuufungua Mlango. Macho yakamtoka baada kukutana na tukio la Teddy kuwa uchi kama Alivyozaliwa. Mlinzi akaupoteza umakini huku akilishangaa umbo la mtoto huyu. Teddy alikuwa akikipenda kitu hicho sana, akaanza kupiga Hatua kumfuata mlinzi yule aliyekuwa ameduwaa. Hatua ya kwanza, hatua ya pili na hata ya tatu, zikamkuta mlinzi yule akiwa chini akivuja Damu. Baada ya kuhakikisha mlinzi amepoteza uhai, teddy akamvuta kwa ndani, kisha kumpapasa na kuchukua vitu mbalimbali. Baada ya Hapo akayaendea mavazi yake, akavaaa kisha akaondoka Hapo Ndani Bastola Ikiwa Mkononi. Wakati anaukaribia mlango walioingilia,akauona Mlango ukifunguliwa kisha mwanaume wa makamu Akaingia hapo. Macho yake yalipotua Usoni kwa Teddy akagundua Teddy alikuwa Amesaliti na kutaka kutoroka na bahasha ile. Meja Jenerali Louis Chomboko akaupeleka mkono wake sehemu alipoihifadhi Bastola yake. Lakini mkono wake Haukufika popote. Risasi Mbili zikatua kifuani kwake na kumtupa chini. Teddy alikuwa ameamua kuasi tena. Baada ya Mzee Chomboko kupigwa Risasi na kuanguka chini, Teddy akatoka mle ndani na kuanza kusimamisha magari. Wakati Teddy akisimamisha Magari tayari kwa kuondoka, Masimba ndio alikuwa Akifika hapo tayari kwa kuonana na Meja Jenerali Chomboko.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom