Riwaya: Nitakupata tu

ibra87

R I P
Jul 22, 2015
5,614
5,338
[14:58, 18/02/2017] Ibrahim Masimba: NITAKUPA TU

SEHEMU YA 001

Mwandishi Ibrahim Masimba

*********
Alihisi ilikuwa sauti ya mwanamke, sauti ambayo mwanzo alidhani haikuwa ya mwanamke kutoka na usiku ule kuwa vigumu. Lakini sauti ile bado ilikuwa ikisikika katika ngoma za masikio yake. Sauti ya mwanamke akilia na kuomba msaada, sauti ikipiga kelele za hali ya juu kuonyesha kwanba kunakitendo kiovu kinatendeka. Bado hakuijali sauti ile, alichukulia kwamba labda atakuwa ni malaya amekula pesa za watu sasa analazimishwa kulipa. Bado akapuuza akitembea kuelekea nyumbani kwake. Licha ya kupuuza lakini safari hii, sauti ikasikika tena kwa karibu. Sauti ambayo ilipita masikioni na kwenda kuweka kituo ndani ya kina cha moyo wake. Sauti nayo ikazidi kuhanikiza, lakini safari hii kwa aina ambayo ili msisimua. Aina ambayo ilifanya kengele za hatari kugonga kichwani. Binti anayefukuzwa kulitaja jina lake usiku ule kulimpa mashaka makubwa. Kwa mara ya kwanza mkono wake ukashuka mpaka alipoihifadhi bastola yake. Kitendo cha kuitwa jina katika mazingira yale kulimpa hisia kuwa kulikuwa na namna, namna ambayo ilitengenezwa kwa aina fulani ya kutaka kitu kutoka kwake. Wamejuaje niko hapa? Walijuaje nitapita njia hii tena katika muda huu? Yalikuwa maswali yaliokisumbua kichwa chake, yalikuwa maswali yaliomfanya aziamini hisia zake, hisia ambazo hazikuwahi kumuangusha. Sasa akatembea kwa umakini mkono ukiwa juu ya Bastola. Hakujali tena kelele za mwanadada yule. Licha ya kutokuwa na ulahai wowote katika sauti yake, lakini hakutaka kuliamini hilo, akaendelea kutembea.. lakini hakufika popote akausikia mlio wa bastola, mlio ambao uliambatana na yowe, yowe kutoka kwa mwanadada yule. Kwa mara ya kwanza akageuka nyuma, akageuka kukiangalia kilichotokea nyuma.. naam akamuona mwanadada amelala chini tena barabarani. Hakuonekana kama alikuwa hai. Mbele kidogo ya ulipoangukia mwili wa binti yule, aliwaona wanaume wawili waliovalia makoti meusi wamesimama. Walikuwa wanaume hasa kwa kuwaangalia. Hakutaka kuupoteza muda, hakutaka kuupoteza muda kuwepo eneo lile. Akatokomea akiwaacha wanaume wale wamesimama wakimuangalia. Alitembea akijiuliza maswali mengi sana. Kama lengo lilikuwa ni yeye kwa nini wamemuua yule msichana? Walitaka nishuhudie kitu gani na kwa madhumuni yapi? Haiwezekani watoke huko kisha waje wamuulie mtu mbele yangu harafu mimi wasinifanye kitu, kuna zaidi ya hili. Alijisemea peke yake akiufungua mlango wa nyumba yake, akaingia ndani moja kwa moja akaenda kujibweteka kwenye kiti. Sauti ya mwanamke yule bado ilikuwa ikijirudia kichwani mwake, bado aliisikia bado masikioni mwake. Akajaribu kuivuta kumbukumbu ya sauti ile kuona kama angeugundua ulahai katika sauti ya mwanamke yule, lakini hakukuwa na kitu chochote kilichoashiria kwamba mwanamke yule alikuwa akimrahai. Ilikuwa sauti iliokatika ukweli, haikuwa na hata shaka ndani yake. Lakini sasa kwa nini mazingira yake yalikuwa ya kutilia mashaka? Hilo likamfanya ainuke na kuelekea bafuni ambapo alijimwagia maji kisha akarudi chumbani kwake. Akachagua mavazi ya kimichezo akavaa na baada ya hapo akachukua bastola yake na kutoka pale kuelekea kule alipoangukia yule mwanamke. Muda wote aliutamani ukweli wa jambo lile. Haikuwahi kutokea mtu kuuawa mbele ya macho yake. Hii ilikuwa mara ya kwanza na ilimtia mashaka sana. Alitaka kwenda kumuona marehemu, alitaka kumuona kwa kuwa aliamini angekipata kile ambacho kingemsaidia katika kumfahamu marehemu. Akaurusisha mlango kisha akalifunga geti kwa ndani kisha yeye akauparamia ukuta na kuangukia upande wa nje. Hii ndio ilikuwa njia yake awapo katika shughuli ambayo alihisi ilikuwa na hatari mbele yake. Alipotua akachepuka na kutafuta njia mbadala tofauti na ile alioipita mwanzo. Alitembea usiku sambamba na vivuli vya miti, hata alipotokea sehemu ile bado palikuwa kimya na hata mwili wa mwanamke yule bado ulikuwepo ukionyesha kutokuwa na uhai. Macho yake yaliozoea giza yalikuwa yakizunguka maeneo yote, bado hakuiona dalili ya uwepo wa mtu katika eneo lile. Hakuiona dalili ya kufuatiliwa wala kuwekewa mtego. Mkono wake ulikuwa juu ya bastola akipiga hatua kuufuata mwili uliolala chini bila uhai. Damu ilikuwa imeunda dimbwi kubwa. Akaufikia mwili ule na kuanza kuuangalia kwa makini.

Kwa kuwa hakutaka kuupoteza ushahidi, alichokifanya ni kutoa gloves na kuzivaa mikononi. Akaushika mwili wa binti yule na kuugeuza. Cha kwanza kukiona ni matundu matatu ya Risasi kifuani. Lakini kilichomchanganya katika matundu yale ni jinsi matundu yale yalivyo. Mpigaji alionekana kusimama kwa mbele na sio nyuma kama alivyokuwa akidhani. Hilo likampa picha, picha ya kuwa yeye ndie alikuwa mlengwa. Alikuwa mlengwa kutokana na ukweli kwamba marehemu alionekana hakuwa akikimbia. Bali alikuwa ameshikwa na alikuwa akilazimishwa kukifanya kitu. Alikuwa akilazimishwa kumuita yeye. Hapo akapata picha nzima kuwa alikuwa akihitajika yeye na sio huyu msichana. Alichokifanya nikuupekua ule mwili, hapo akakutana na vitamburisho vitatu, pamoja na kadi moja kubwa ambayo hii iliikuta kwenye Mkoba, pamoja na Simu yake ya mkononi. Akavichukua vyote na kuvisunda mifukoni. Baada ya hapo akapata wasaa wa kuiangalia sura ya mwanadada huyu. Hapo akakutana na sura nzuri na yakuvutia.

"Watu wanaroho ngumu, ya nini kumuua mtoto mzuri kama huyu? Alinong'ona huku akiinuka tayari kwa kurudi kwake.

***********

Chumba chote kilikuwa kimya, kila mmoja alikuwa ametulia akitizama mbele kuliko na Tv kubwa. Walikuwa wakiangalia taarifa ya habari kutoka shirika la utangazaji nchini. Kila mmoja alikuwa akitarajia kutangazwa kwa habari fulani ambazo zingewafurahisha. Kila mmoja ndani ya chumba kile alikuwa akiisubiri taarifa hiyo kwa hamu. Alikuwa akisubiri kile ambacho kingewafanya wao wawe katika kiwango cha juu katika biashara zao. Lakini ilikuwa kinyume wa kile walichokitarajia. Taarifa ambayo walikuwa wakiisubiri kwa hamu haikuja kama vile walivyotarajia. Bali vijana wao wanne walikuwa wamekamatwa wakiwa na mzigo wa madawa ya kulevya. Walikamatwa na maafisa wa usalama uwanjani hapo. Kila mmoja akapagawa, kila mmoja akahisi labda yupo ndotoni. Mzigo wao wenye thamani ya bilioni ishirini na mbili za kitanzania ulikuwa umekamatwa. Wakawaona vijana wao wakisukumwa kuelekea katika chumba maalum kwa ajili ya mahojiano zaidi. Chumba kikazizima kwa taharuki. Mmoja akaiendea simu yake na kupiga namba fulani. Muda mfupi simu ya upande wa pili ilikuwa ikiita. Iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa. Hata aliporudia bado hali ilikuwa pale pale.. hilo likawafanya watu wale watizamane.

"Haiwezekani!! Mmoja akanguruma.

"Kuna mchezo, huyu mwingine aliongea huku akishindwa kuuhimili presha.

"Jimmy hawezi kutufanyia hivi!!!" Mwingine akaongeza.

Lakini bado haikuondoa ukweli kwamba Mzigo wao ulikuwa umekamatwa na kulikuwa na uwezekano hata wao wenyewe wakatajwa. Bado simu haikupokelewa, bado iliendelea kuita kwa muda mrefu. Wajumbe wote wakazidi kushangazwa na hali ile. Lakini kabla hawajakaa sawa wakaisikia simu ikiita. Safari hii ilikuwa ikipigwa.

"Jimmy!!" Aliita.

"Jackson!!" Naye akaita..

"Atafutwe Teddy Harryson!!" Aliongea Jimmy kisha bila kusubiri maelezo yoyote akakata simu. Wajumbe wote wakaangaliana, hakuna alieamini maneno ya Jimmy. Kila mmoja alikuwa akiwaza mzigo wao uliokamatwa. Kitendo cha kuambiwa wamtafute Teddy Harryson bila kupewa maelezo yoyote kuliwakera baadhi ya wajumbe. Lakini wakiwa bado kwenye Mshangao wa kutokumuelewa Jimmy, simu ikatoa mliokuonyesha kuna ujumbe umeingia.

"Mpigie Teddy Mwambie akailete Roho ya Binti mmoja ambaye alikuwa chanzo cha kukamatwa kwa mzigo wetu. Nataka nikikupigia simu kwa mara nyingine unipe taarifa ya Roho Ya huyo Binti kuwasili hapo." Ulisomeka Ujumbe Ule.

ITAENDELEA
[18:28, 18/02/2017] Ibrahim Masimba: NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 002

Mwandishi Ibrahim Masimba
*******

Ilihitajika Roho ya Binti aliesababisha kukamatwa kwa mzigo wao. Mzigo ambao ulikuwa wa mamilioni ya shilingi. Ilikuwa ni lazima wampigie simu Teddy kwa kuifanya kazi ya kuileta roho ya mwanamke huyo. Ilikuwa ni amri kutoka Kwa Jimmy, amri ambayo ilitakuwa kutekelezwa katika usiku ule. Hilo likafanyika na Roho ya mwanamke alietakiwa ikaletwa sehemu husika. Licha ya kumuua mwanamke yule lakini bado hawakuridhika kwa hilo kutokana na kutokuupata mzigo wao. Wajumbe wote waliokuwepo ndani ya Chumba, wakaufanya mkutano wa kujadili kipi cha kuufanya ili kuupata mzigo wao. Ni ndani ya mkutano huo likapitishwa Jina la Masimba. Alitakiwa kutafutwa kwa lazima, alitakiwa kutafutwa ndani ya muda ule. Kutafutwa kwa kazi maalum. Kazi ya kujua nani alikuwa nyuma ya ukamatwaji wa Mzigo wao wa madawa. Hawakuamini kuwa mwanamke yule pekee anaweza kuwa chanzo cha kupotea kwa mzigo wao. Walitambua kuna mchezo mchafu, mchezo ambao ulikuwa ukichezwa nyuma ya pazia. Muda mfupi kijana mmoja alitoa simu yake na kutafuta namba, alipoipata akabonyeza batani ya kijani, muda wa sekunde tano simu ikaanza kuita.

"Dogo!" Ilisikika sauti upande wa pili.

"Yeah Mkuu!!" Alijibu kijana Yule.

"Kuna nyekundu au kijani?" Lilikuwa swali kutoka kwa masimba. Alitambua simu nyingi za usiku kutoka kwa kijana huyo hazikuwa za usalama hata kidogo.

"Nyekundu Mkuu, kuna kitu tunahitaji ukifanyie kitu, lakini hatuwezi kuongea kwenye simu. Tukutane coco beach muda huu kama muda upo." Akajibu dogo.

"Nitakuwa hapo muda mfupi, mtanikuta pale kwenye mishkaki." Akajibu Masimba huku akikata simu. Hakutaka kupoteza muda, alichofanya ni kumuamsha Mpenzi wake, akamuaga kuwa anakwenda coco beach na asingechelewa kurudi. Akaruhusiwa huku akiombwa kutozidisha masaa mawili. Alitoka nyumbani kwake kinondoni manyanya, akaelekea kituo cha pikipiki, hapo akamueleza dereva wapi anaelekea. Muda mfupi alikuwa juu ya pikipiki akielekea coco beach kuitikia wito. Kuambia kuwa kuna nyekundu ni dalili ya kuwepo kwa kazi ya umwagaji damu. Alikuwa ni mtu wa kutumainiwa katika mipango mbalimbali. Alishapewa kazi nyingi na zote alizifanya katika weledi wa hali ya juu. Siku zote aliishi kutokana na kufanyakazi ambazo ni tofauti na kazi yake ya halali. Licha ya kuwa afisa usalama wa Taifa tena wa kutegemewa, lakini upande mwingine alikuwa akishiriki mipango mingi ya hatari. Baada ya Dakika tano walikuwa wamewasili eneo la coco beach. Akashuka kwenye pikipiki, akaingiza mkono mfukoni akatoa noti ya Elfu tano akampa dereva, kisha bila kusubiri chenji akapiga hatua kuelekea pale alipowaambia wakutane. Alitembea kama mtu wa kawaida, suruali ya Jeans, tshirt nyeupe na raba nyeupe miguuni zilimfanya abadirike na kuonekana kama kijana. Akaendelea kutembea macho yake yakitembea huku na huko. Mbele kidogo akaiona gari ambayo aliifahamu. Ilikuwa gari inayotumiwa na watu wake. Hii ilimaanisha kuwa wao walishafika kabla yake. Akaendelea kutembea akiipita gari ile kama hakuiona, alipoipita akainama na kuzuga kama anafunga viatu. Lakini muda huo huo macho yake yakitembezwa kwa ustadi mkubwa. Ni hapo alipokiona kitu ambacho kwanza kilimshangaza na pili kilimtia hofu. Wakati ameinama akifunga viatu, alimuona mtu kama Mpenzi wake. Alimuona mwanamke kama Teddy akitembea kwa kificho ndani ya fukwe za coco. Hilo lilimshangaza, halikuishia kwenye kumshangaza tu, bali lilimpa hisia tofauti. Hakuwa amemfananisha Na haitatokea amfananishe Teddy. Lakini amefuata nini hapa? Mbona kama alikuwa akinifuatilia? Yalikuwa maswali, maswali ambayo alihitaji kupata majibu katika wakati ule.

Akaendelea bila kugeuka nyuma, hakutaka kufanya hivyo kuogopa kumshtua Teddy. Hatua kama tano kabla hajawafikia watu wake, masimba akaitoa Ishara kwa watu ambao walikuwa wamekaa mbele yake. Ishara ambayo ilijibiwa haraka na watu wale, kilichofuatia ni kuingia ndani ya gari na muda ule gari likaondoshwa pale coco na kurudi katikati ya mji. Ulikuwa mchezo ambao hakuna ambaye aliuelewa mapema. Wote walijua kwamba lazima wangezungumza palepale ufukweni. Lakini haikuwa hivyo, kila mmoja alishangazwa na mabadiliko ya Masimba.

"Nipeni kazi nishukie hapa." Ilikuwa sauti kutoka kwa masimba. Wajumbe wote wakashangazwa na haraka ile. Mmoja akataka kuhoji lakini alipoangaliana na macho ya Masimba akafumba mdomo na hakukumbuka tena kutaka kuuliza.

"Tuokoeni muda, aliongea tena masimba, safari hii akitaka kuufungua mlango.. lakini akashikwa bega na kijana yule. "Nadhani umeisikia taarifa habari ya jana kuhusu kukamatwa kwa mzigo wa madawa ya kulevya? Akauliza huku akimuangalia masimba usoni.

"Yeah nimeona na nilikuwepo eneo hilo." Akajibu akiangalia nyuma.

"Basi ule mzigo ni wa kwetu na tunahisi kuna mmoja wetu atakuwa ameivujisha taarifa za kukamatwa kwa mzigo wetu kwa faida zake." Alieleza kijana yule kwa kirefu kisha akaongeza "Tuna mashaka na Jimmy Lambert, tuna mashaka kwa kuwa anaonyesha kutokuwa na uchungu na mabilioni yetu yaliopotea.


"Umesema mnamuhisi kuwa amewageuka? Akauliza masimba.

"Ndio, tunahisi kwa kuwa hana uchungu na Bilioni ishirini na mbili. Safari alijibu mtu mwingine tofauti na kijana. Masimba akakaa kimya kwanza akionekana kuwaza kitu. Alipokuja kuinua kichwa chake akatingisha kichwa kuonyesha kubaliana na kazi ile. "Tambueni hii kazi ni ngumu na ya hatari sana, ninakwenda kuifanya kwa kuwa pesa iliopotea ni nyingi. Lakini pia naenda kinyume na kazi yangu. Hivyo basi naomba nitakapoanza kuifanya kazi hii sitaki kusikia chochote kikizungumzwa. Pia pesa yangu nusu niingizieni kwenye account yangu.. kisha tukutane Mbagala rangi tatu baada ya sikutano nitakuwa na chochote cha kuwaeleza!!" Akaongea masimba akishuka ndani ya gari tayari kwa kuelekea kwake. Ule wasiwasi wa kumuona mkewe pale coco beach ndio kwanza ukaanza baada kushuka kwenye gari. Kila alipojaribu kutafuta sababu ya mkewe kumfuatilia nyuma nyuma hakuipata. Hakuwahi kumuhisi mkewe tofauti lakini kwa kitendo cha leo akahisi kuna kitu mpenzi wake amekihisi ama labda wivu ndio unamsumbua.

*******
Aliingia nyumbani akiwa hana wasiwasi, baada ya kuingia akaongoza chumbani ambapo alimkuta mkewe akiwa amelala. Akamuangalia kwa muda mrefu bila kufanya lolote. Alimuangalia mpenzi wake huyu kwa muda mrefu bila kufanya kitu chochote. Hakutaka kwenda pale kitandani, kuna kitu alitaka kukifanya kwa wakati ule.alivikumbuka vitamburisho na mkoba wa yule dada alieuawa usiku wa jana. Akatembea mpaka sehemu yake ya siri ambayo ndio huhifadhi mambo yake mengi. Akavichomoa vitu alivyovichukua kwa marehemu yule, akatoka nje kabisa na kuanza kuvitizama. Jina lake mwanamke yule lilisomeka kama Asteria Paul. Alikuwa mfanyakazi wa Uwanja wa ndege. Akahisi kitu kama kengele zikigonga kichwani mwake. Alihisi kuna kitu kipo nyuma ya mauaji yale. Akarudisha vitambulisho na kuiwasha simu ya binti yule. Baada ya muda akaenda kwenye majina ya watu waliompigia.. Hakuamini Macho yake Pale alipokutana na namba ya Mpenzi wake ikiwa ndio namba ya mwisho kumpigia marehemu..
 
Story yaonekana itakuwa nzuri .....pia ungeza episode nyingi kwa siku km tano hivi
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 003

********

Namba ya Mwisho kumpigia marehemu ilikuwa namba ya Mpenzi wake. Hilo likamsisimua mwili wake, ile hisia kwamba mpenzi wake ndiye aliemuona kule coco beach sasa ilikuwa imeupata ushahidi wake. Lakini bado kichwa chake kilikuwa kizito kupindukia kuamini kwamba Teddy ni Mhusika katika tukio la kuuawa kwa mwanamke yule. Hilo halikumpa mashaka zaidi lakini alijiuliza ni vipi ameweza kufanya hilo wakati alikuwa naye ndani kwa kipindi chote. Ni katika kuyawaza hayo ndipo akaikumbuka siku iliopita pale alipoagwa na Teddy kuwa anakwenda kwao na hatarudi kwa siku hiyo. Kulikumbuka hilo kulizidi kuusisimua Mwili wake. Alitanbua kuna kila dalili za mpenzi wake kuhusika na kifo cha mwanamke yule. Lakini alijiuliza sababu za kumuua mwanamke mbele yake kulikuwa na maana gani kwake? Walikuwa wakimpa ujumbe gani kwake. Hapo akaipata hamu ya kuendelea kuichunguza simu ya marehemu Asteria. Jina la pili kukutana nalo ni la Mtu ambaye aliambiwa amchunguze. Lilikuwa jina la Jimmy Lambert. Alikuwa mmoja kati ya watu waliowasiliana na Asteria Muda Mfupi kabla ya kifo chake. Kila alichokuwa akikiona kilikuwa kama ndoto asioiamini. Kwa nini jina la Teddy kisha Jimmy? Teddy yupo wapi katika hili? Ana husika vipi katika kifo cha mwanamke huyu? Yalikuwa maswali mazito sana, maswali ambayo hayakuwa na majibu kwa wakati ule. Hakuwa na jibu kwa wakati ule lakini ilikuwa lazima kulitafuta jibu kabla hakujapambazuka. Aliinuka na kuvirudisha vitu vyake sehemu yake, alipohakikisha kila kitu kipo sawa akaanza kutembea kuelekea nje ya nyumba yake. Hakupata hamu ya kulala kwa wakati ule. Uhusiano wa kifo cha mwanamke yule na urafiki wa Jimmy na Teddy kilikuwa kitu kilichomtia shaka na kuvuruga kichwa chake. Safari hii hakutaka kutumia usafiri wa kukodi, aliamua kutumia gari yake mwenyewe. Alikuwa amekata shauri ya kuelekea magomeni Mikumi nyumbani kwa rafiki wa mpenzi wake. Alitambua huko anaweza akaupata Ukweli kuhusu mauaji ya Binti yule na Uhusiano uliokuwepo kati ya Jimmy na Teddy. Kwa kuwa barabara haikuwa na magari, hapakuwa na ugumu wowote. Aliendesha gari kwa mwendo wa kawaida huku akiwa makini kuangalia kama alikuwa akifuatiliwa. Lakini hapakuwa na kitu chochote kilichomtia wasiwasi. Baada ya muda alikuwa akiegesha gari umbali mfupi kutoka iliponyumba ananyoishi Rafiki wa mpenzi wake. Ilikuwa nyumba kubwa ya vyumba sita, sebule, choo sambamba na jiko. Hakuwa akiishi na mtu kutoka na mumewe kutokuwepo hapa nchini. Masimba alishuka na kuufunga mlango wa gari kisha akaongoza kuelekea getini kwa nyumba ile. Giza lilikuwa limechukua sehemu kubwa huku ukimya nao ukitawala kuonyesha kwamba watu wengi walikuwa wameshalala. Alitembea taratibu huku akiwa makini na kila kitu, alipolifikia geti akataka kuligonga lakini akagundua kuwa lilikuwa wazi. Hilo likamstaabisha, tokea amfahamu mwanamke huyu hakuwahi kumuona ama kukuta geti hili likiwa wazi. Kitendo cha leo kilimstaabisha sana. Akakata shauri aingie pasipokuligonga geti. Akalisukuma taratibu na kuzama ndani. Hapo pia akashangazwa kwa ukimya ambao aliukuta ndani. Taa zote zilikuwa zikiwaka, mlango wazi lakini hakukuwa na sauti yoyote kuashiria kama kulikuwa na mtu ama lah. Hilo likampa machale, akajivuta zaidi kuufuata mlango.. akaukuta ni kweli ulikuwa uko wazi. Akaingia na kusogea ndani, bado alipokewa na ukimya. Ukimya ambao hakuwahi kukutana nao katika jumba lile. Ukimya uliomfanya aichomoe bastola yake na kuishikilia mkononi. Akatembea kwa makini huku macho yake yakicheza pande zote. Bado hakuiona dalili ya kuwepo kwa mtu. Akaendelea kutembea huku umakini ukiongezeka. Akatokea sebuleni, kutokea sebuleni tu akahisi mwili ukisisimka.. sebule ilikuwa ilikuwa imevurugwa na vitu kutupwa huku na huko..

Akaikamata bastola yake vizuri kisha akaanza kusogea mbele zaidi na zaidi. Hatua saba mbele akaiona michirizi ya damu. Umakini ukaongezeka zaidi na Zaidi. Akatembea mdomo wa bastola ukitangulia. Alikuwa akitembea kuifuata michirizi ile ya damu. Alikuwa amejiweka tayari kwa kila kitu. Akaendelea kuifuatilia michirizi ile nyuma nyuma, mbele kidogo Akaiona ikiwa imeishia mlangoni mwa chumba fulani mle ndani. Hapo akasimama kwanza, baada ya hapo akausukuma mlango kisha kujitoma ndani. Hapo akajikuta akitizamana na Mwili wa Rafiki Wa Teddy Ukiwa umelala chini huku damu zikionekana kutuama. Akatembea mpaka pale ulipo mwili wa dada yule. Hakuonekana kuwa na uhai, hakuonekana kama alikuwa hai. Masimba akautazama mwili wa mwanadada yule kwa muda wa kama sekunde tano bila kufanya lolote. Kichwa chake kilikuwa kimevurugika, asteria, na sasa alikuwa ameuawa mwanamke huyu. Kipi kipo nyuma katika mauaji haya? Bado alitaka kujua kiundani zaidi, wakati akiwa bado ameduwaa asijue nini anatakiwa kufanya, akaisikia miguu ya watu ikitembea kisha minong'ono ikafuatia. Akatulia tuli huku mdomo wa bastola akiuelekeza mlangoni. Bado hatua za miguu na minong'ono ikaendelea kusikika, Sasa zilikuwa sasa hatua zile zilikuwa zikiukaribia mlango ule, punde akakiona kitasa kikitikiswa, wakati huo huo mlango ukasukumwa.. hakusubiri chochote kitokee, hakusubiri chochote kivuruge plani yake, mlio mdogo mfano wa chafya ukasikika, bastola ikakohoa mara mbili.. Hapakuwa na kelele. Ilikuwa miguno tu, miguno ilioambatana na kutambarajika kwa watu. Masimba akaurudia umakini wake, akatembea mpaka pale ilipolala ile miili ya watu wale wawili, akainama na kuigeuza miili. Zilikuwa sura ngeni machoni, hakuwahi kuwaona popote watu hawa. Alichokifanya nikuwapekua watu wale nakuchukua kila alichokiona kinafaa, kisha akatoweka eneo lile kwa kupitia mlango wa nyuma wa nyumba Ile.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom