Rais Kikwete na safari za nje

Rais Kikwete na safari za nje

Mheshimiwa Rais atafunga mwaka 2008 kwa ziara ya kikazi huko America ya kusini. Ziara ambayo itajumuisha Nchi za Brazil,Venezuela na Cuba,ziara hiyo itafanyika katikati ya Mwezi wa Novemba.Atakapokuwa anarejea Nyumbani atapitia USA kwa ziara ya siku mbili.Jana asubuhi 27/09/08 (Jumamosi) Rais amerejea New York akitokea Washington DC,baada ya kumaliza Ziara ya kikazi,Anatarajiwa kuondoka USA Jumapili jioni.
 
Anatarajiwa kuondoka USA Jumapili jioni.

Jana aliniambia kua ni lazima awahi idd nyumbani, hawezi mambo ya kula sikukuu kubwa kama hii majuu, I mean almost a King! Maana safari ilitakiwa awepo mpaka Jumatano!
 
Ziara ya JK USA

Na Mwandishi Maalum, New York, Marekani

Tanzania itatokomeza kabisa ugonjwa wa malaria katika miaka saba ijayo, yaani ifikapo mwaka 2015, kwa kutumia njia tatu zilizothibitishwa kimataifa kuwa zinamaliza ugonjwa huo, Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema leo (Jumapili, Septemba 28, 2008) mjini New York, Marekani.

Vile vile, amesema kuwa ziara yake kwenye Umoja wa Mataifa (UN) mjini New York imekuwa ya manufaa makubwa kwa sababu Afrika imefanikiwa kuwasilisha sauti yake katika masuala muhimu anayohusu Bara hili. Rais Kikwete anaondoka leo kurejea nyumbani.

Akizungumza na waandishi wa habari wa Tanzania walioandamana naye katika ziara hiyo kuhusu mafanikio ya ziara hiyo, Rais Kikwete amesema kuwa moja ya mafanikio ya ziara yake ni kwamba Tanzania imepata uhakikisho kuwa itaweza kutokomeza malaria ifikapo mwaka 2015.

Amesema kuwa ahadi mpya za kupambana na matatizo ya Afrika, ukiwemo mwelekeo mpya wa kupambana na magonjwa, na hasa malaria, inayoua watu wengi zaidi katika Afrika, ni moja ya mafanikio ya ziara yake kwenye UN.

“Katika Tanzania, tunapambana na malaria kwa njia tatu zinazokubalika duniani- kuhakikisha kuwa wananchi wetu wanatumia vyandarua vyenye dawa, tunanyunyizia dawa za kuuwa mbu katika madimbwi ya maji, na pia kuhakikisha kuwa wagonjwa wanapata dawa,” amesema Raia Kikwete katika mahojiano hayo kwenye Hoteli ya Intercontinental, mjini New York, Marekani.

Amesema kuwa njia zote tatu tayari zimeleta mafanikio makubwa Tanzania Visiwani ambako vifo kutokana na malaria vimeteremka mno, kutoka vifo 120,000 hadi 60,000 tu kwa mwaka.

“Na mafanikio hayo yanatokana na matumizi ya asilimia 40 tu ya vyandarua Tanzania Visiwani, lakini Zanzibar haiwezi kutomokeza malaria bila kuhakikisha kuwa Bara nayo inakuwa salama. Hii ni mara ya tatu, tunafikia hatua ya kutokomeza malaria Tanzania Visiwani na bado ugonjwa huo umerejea kwa sababu Bara haitiliwa maanani,” amesema Rais Kikwete.

Ameongoza kuwa Tanzania inahitaji kiasi cha vyandarua milioni 15 vyenye dawa, kwa kila Mtanzania kulala bila bugudha ya mbu, na kuwa vyanzo mbali mbali vya misaada vimekwishahakikisha kuwa vyandarua hivyo vitapatikana baada ya awamu ya kwanza ya vyandarua milioni 5.2 kuwa vimepatikana.

“Kama mlivyosikia, Waziri Mkuu wa Uingereza, Gordon Brown, pekee yake ameahidi kutoa kiasi cha vyandarua milioni 100 katika miaka michache ijayo. Tanzania itanufaika na sehemu na vyandarua hivyo. Pili, tunao msaada wa sekta binafsi ambayo pia itatoa vyandarua. Mpango ni kutokomeza malaria ifikapo mwaka 2015 ni dhahiri utafanikiwa,” amesisistiza Rais.

Rais Kikwete ambaye aliwasili mjini New York, Marekani Jumapili iliyopita, ameliwakilisha Bara la Afrika kwa maana ya kushiriki katika mikutano kadhaa muhimu ikiwa sehemu ya mikutano ya mwaka huu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Mikutano hiyo ni pamoja na ule iliojadili mahitaji ya maendeleo ya Afrika, Mkutano wa Mjadala wa Baraza Kuu la Mwaka huu, Mkutano kuhusu Malengo la Maendeleo ya Milenia (MDG’s) na yanavyotekelezwa katika Afrika, na mikutano kuhusu Afya ya Mama na Mtoto, pamoja na ule kuhusu malaria.

Rais Kikwete amesisitiza ujumbe wake katika mkutano wa mwaka huu wa Baraza Kuu kuwa sasa ni dhahiri kuwa Afrika siyo Bara lisilokuwa na matumaini, la ovyo, na lenye kukatisha tamaa.

“Nimewaeleza wenzangu kuwa Afrika siyo Bara la ovyo tena. Ni Bara linaloinuka. Demokrasia inapiga hatua, tunaendesha changuzi bora zaidi, hali ya kisiasa imeimarika zaidi, tuna amani ya kutosha, ni kweli bado tunayo matatizo pale Somalia, Darfur, na Mashariki mwa Congo, lakini kwingine hali ni rushwa,” amesema na kuongeza:

“Uchumi wa Afrika unakua kwa asilimia kati ya asilimia tano na sita. Lakini bado bara letu na watu wetu ni masikini. Huu ndio mpaka wa mwisho wa jitihada za binadamu kuleta maendeleo. Kati ya nchi 50 masikini dhalili katika Afrika, 34 ziko Afrika. Kazi bado ni kubwa na hivyo wakubwa hawa wanatakiwa kutelekeza ahadi zao za kusaidia Afrika ambazo wamezitoa katika mikutano mingi tu,” amesema Rais.

Amesema kuwa nchi tajiri duniani zinazo wajibu wa kihistoria na ulazima wa kiroho kuzisaidia nchi masikini, kwa sababu isitoshe ziliahidi zenyewe kutoa misaada hiyo. Hii ndiyo njia pekee ya kuisaidia Afrika kufikia malengo ya Milenia. Kikao cha hapa kilikuwa kinaangalia hili, yaani jinsi ya kuisaidia Afrika kuongeza kasi ya kuweza kufikia Malengo la Milenia.

“Wala siyo kwamba wakubwa hawa wana tatizo la kufanya hivyo. Wanazo pesa za kutosha kuisaidia Afrika kuweza kufikia Malengo haya. Miaka miwili iliyopita aliyekuwa Katibu Mkuu wa UN, Kofi Annan aliomba kiasi cha dola za Marekani bilioni 50 ambazo zingeiliwezesha Bara la Afrika kufikia malengo ya Milenia,”

Ameongeza: “Hiki ni kidogo sana. Fikiria wakubwa hawa wanatoa ruzuku ya kiasi cha dola bilioni 365, kiasi cha bilioni moja kila siku, kuwalipa wakulima wake wasilime chakula cha kutosha. Japan inatoa kiasi cha dola saba kila siku kwa ng’ombe mmoja. Pamba ya Mali haiwezi kuuzika duniani kwa sababu ya pamba ya Marekani inauzwa bei ya chee … hizi ndizo tunaita trade distorting subsidies …”

Rais amesema kuwa kinachoitajika ni utashi wa kisiasa wa kuisaidi Afrika, kwa sababu kiasi alichoomba Anan ni kidogo sana kulinganisha na ruzuku kwa nchi tajiri kwa watu wao.
 
KUbwajinga,
Hivi isingewezekana kutokomeza malaria bila rais kufanya ziara Marekani?
 
Mkuu Jasusi, umeuliza swali la msingi sana!!

Malaria itatokomwezwa kwenye sub sahara by 2015 na Bill & Melinda Gates foundation. Hiyo ni plan yao waliojiwekea foundation ya Gates na iko kwenye pipeline since 2006 baada ya Warren Buffett kucommit almost $26 billion++ kwenda Gates foundation.

Yeye Jk karukia tu vitu alivyosikia kina Gates wakiongea.

Ni sawasawa na UN Millenia goals za kutokomeza extreme poverty by 2015 (maybe 2025), yeye Jk akirukia na kusema tutatokomeza ni kuwa anadandia train ambayo hajui hata inaendeshwa vipi.

Huyu kazoea kusikia watu kama mfano wapenzi wa Man United wakisema tutawafunga Arsenal, haina maana wanajua itakuwa vipi bali ni mawazo yao tu ahahaha
 
kilaza JK mikakati yake ya kutokomeza malaria ni kupokea misaada ya Chandarua..kweli tuna Raisi!
 
Safari za Kikwete nje utata mtupu

Lula wa Ndali-Mwananzela Oktoba 1, 2008
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo

Tukiweka utani wote pembeni, kejeli zote pembeni, na dhihaka zote pembeni, bado tunakabiliwa na swali moja muhimu: Ni kwanini Rais Jakaya Kikwete hawezi kukaa Dar kwa angalau wiki tatu mfululizo bila kwenda nje ya nchi?

Hivi ni kweli kuwa bila Rais Kikwete kwenda safari za nje ya nchi Taifa haliwezi kuendelea na bila ya yeye mwenyewe kufunga safari hizo, basi, misaada ya kigeni na uwekezaji hautafanyika nchini kama alivyoashiria Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, mapema mwaka huu?

Ninatatizwa, ninakerwa na niseme wazi kuwa baadhi ya ziara hizi haziingii akilini, na kwa hakika zinanifanya nianze kuhisi ninaishi katika ulimwengu wa kufikirika ambamo mambo yote yanawezekana.

Jibu jepesi ambalo limekuwa likitolewa mara kwa mara kubariki ziara hizi ni kuwa Rais Kikwete analazimika kwenda nje kwa sababu kwa kufanya hivyo anakutana na viongozi mbalimbali, anapokea misaada na pia analitangaza jina la nchi yetu. Na wengine wamefikia mahali pa kutaka wananchi waamini kuwa bila ya Rais Kikwete kufanya ziara hizo, basi, Tanzania haitakumbukwa katika medani za kimataifa.

Kwa wenye kumbukumbu nzuri watakumbuka kuwa mwanzoni ilisemwa kuwa alikuwa anakwenda huko "majuu" kujitambulisha kuwa yeye sasa ndiye "Rais wa Tanzania" kana kwamba habari ya kuchaguliwa kwake ilikuwa siri.

Hebu tuangalie kama hoja zetu hizi ni za sisi waandishi tu au hata watu wengine wameanza kuziona? Taarifa ya ripoti ya Economic Intelligence ya Agosti mwaka huu inasema hivi kuhusu tathmini yake ya hali ya siasa za ndani "Rais Kikwete bado anatumia muda mrefu akisafiri nje ya nchi".

Kauli hiyo imetoka kwenye taasisi ya Economic Intelligence Unit ambayo iko chini ya Jarida maarufu la "The Economist". Ripoti yao hiyo inaelezea ni kwanini basi suala la Rais kuwa nje ya nchi mara kwa mara lina athari za aina fulani katika utendaji wa Serikali na ni kwanini sisi wengine tunahoji ulazima huu wa Rais Kikwete kuikimbia Dar es Salaam kila anapopata nafasi.

Jarida linasema hivi "baada ya Kikwete kukusanya madaraka makubwa kwake na kwa wasaidizi wake, basi, uwezo wa Serikali kufanya maamuzi muhimu wakati yeye hayupo unakuwa na kikomo".

Kwa maneno mengine ni kuwa kwa kadri Rais Kikwete anavyokuwa safarini nje ya nchi ndivyo hivyo hivyo baadhi ya maamuzi, hatua au maelekezo muhimu hayafanyiki hadi arudi.

Hapa tunaweza kupata mwanga kidogo wa kwa nini anapenda kusafiri nje ya nchi. Ni kwa sababu anakwepa kufanya maamuzi au hatua fulani yeye mwenyewe.

Kwa kadri Kikwete anavyokuwa nje ya nchi ndivyo vivyo hivyo maamuzi kadhaa yanaahirishwa kwa kisingizio cha "mpaka Rais arudi". Matokeo yake ni kuwa akirudi anakaa wiki chache halafu huyo anapaa tena!

Unaweza kuniuliza ni maamuzi gani hayo? Mengi tayari tunayafahamu, kuna suala la kufunguliwa mashtaka kwa baadhi ya viongozi wa juu wakati kesi dhidi yao ziko tayari na kinachosubiriwa (msiniulize ni kwanini) ni "go ahead".

Kuna suala la muafaka wa Zanzibar ambalo bila yeye kuingilia kati hilo haliendi; kuna masuala ya Dowans/Richmond, kuna suala la Rada, kuna masuala mengi tu ambayo tayari yanajulikana.

Kwa mujibu wa jarida hilo hilo inaonekana kuwa safari za Kikwete nje ya nje zinagusa masuala muhimu ya kiuchumi ya Taifa. Jarida hilo linazungumzia jinsi gani uamuzi wa Rais Kikwete kutuma vikosi vyetu kule Comoro vimempandisha chati kimataifa lakini wakati huo huo kusababisha madai kuwa kutokana na nafasi yake kama Mwenyekiti wa AU Rais Kikwete anaweka maslahi ya chati yake ya kimataifa mbele kuliko matatizo ya ndani ya Tanzania.

Hili linaweza kuwa na ukweli tukizingatia kuwa mara tatu sasa Rais Kikwete amefunga safari kwenda Kenya, Zimbabwe, na Sudan katika kujaribu kutatua migogoro ya nchi hizo. Wakati huo ameweza kukutana na viongozi waliogongana wa Kenya na wale wa Zimbabwe. Cha kushangaza hata hivyo ni kuwa hadi hivi sasa hajakutana na kusimamia mazungumzo ya Muafaka wa Zanzibar, hajatuma ujumbe wa nguvu kusuluhisha mapigano kule Tarime (isipokuwa kundi kubwa la waomba kura wa CCM wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti Pius Msekwa).

Kwa wale ambao tulipata nafasi ya kuisikiliza na kuisoma hotuba ya Rais Kikwete kwenye Umoja wa Mataifa, hotuba iliyochukua karibu dakika ishirini hivi, ilituacha tujiulize kama alikuwa anazungumza kama Mwenyekiti wa AU au Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tukiachana na hayo hatuna budi kujiuliza swali jingine; Je, ziara zake hizi zinaendena na hali ya kiuchumi na vipaumbele vya Taifa letu? Ninaamini kuwa endapo tutapata mchanganuo wa gharama za ziara hizi tunaweza kupigwa na mshangao. Licha ya kutokuwa na hesabu mkononi ninaamini tunatumia fedha nyingi kweli kugharimia ziara hizi.

Hebu fikiria msafara wa Rais kwenda New York na Washington DC ukitanguliwa na safari ya mke wake ambaye yuko kimatibabu huko. Yeye Rais tu anaposafiri anakuja "standard". Wasaidizi, walinzi, watendaji wa Serikali (mawaziri), na wadandiaji wengine (wakiwemo wabunge na wanafamilia yake).

Hivi karibuni aliposafiri vyanzo vya uhakika vinasema kuwa alikwenda na mwanae aliyetoka kufunga ndoa hivi karibuni (sijui kama Serikali ilimlipia fungate hilo au zilitoka mifukoni mwa familia ya Rais).

Ukijumlisha watu wote hao walioambatana na Rais, gharama ya kuwaleta na kuwaweka Marekani kwenye mojawapo ya hoteli zenye hadhi ya juu kabisa si utani. Sitaki kukisia lakini Mkaguzi Mkuu wa serikali akithubutu kujumlisha gharama ya safari, malazi, chakula na matumizi mengine ya ki-Rais, sitashangaa jumla itakuwa kwenye mamilioni.

Katika hayo tusisahau kupiga hesabu za posho za wasaidizi mbalimbali na watumishi wanaosafiri na Rais au mawaziri wengine waliokuwa kwenye msafara huo.

Je, hawa wasaidizi wanalipwaje wanapokwenda nje ya nchi kwa siku? Kuna mtu anajua mahesabu haya na natumaini siku moja wataweka wazi kiasi kinachotumika kwa Rais kusafiri nje ya nchi.

Jambo jingine linalosumbua katika ziara hizi ni kile ambacho naweza kukiita "duplication" ya safari. Kuna wakati ndani ya miezi michache utaona Makamu wa Rais ameenda nchi fulani na siku chache baadaye Rais Kikwete yuko nyuma. Hili limetokea kwenye safari ya Rais Kikwete kule India na nikikumbuka vizuri hata alipokwenda Uarabuni. Hapa najiuliza kama yawezekana Rais Kikwete hawaamini watu wa chini yake (makamu na mawaziri) kwenda nchi nyingine na kuwakilisha maslahi ya Taifa?


Sasa hivi habari za uchunguzi zinasema huenda Rais akafanya ziara ya Marekani ya Kusini hivi karibuni. Inatarajiwa kuwa atatembelea nchi kama Cuba, Venezuela na Brazil. Nchi hizi zote zimetembelewa na Makamu wa Rais miezi michache tu iliyopita. Bila ya shaka huko hawamjui Rais wa Tanzania na ni eneo pekee ambalo Rais Kikwete hajatembelea tangu aingie madarakani.

Lakini hatuna budi kujiuliza kama Makamu wa Rais alikuwa huko ni kitu gani hiki kinacholazimisha Rais naye kwenda huko huko? Ni kitu gani ambacho Makamu wa Rais alishindwa kukifanya hadi Rais apitie huko? Kuna tetesi pia yawezekana akitoka huko atapitia tena Marekani!

Kuna safari ambazo naamini ya kuwa zinamuhitaji Rais kwenda kama siku chache pale Umoja wa Mataifa. Lakini kuna safari nyingine zingeweza kufanywa na Makamu au Waziri Mkuu. Huu ulazima wa visafari hivi vyote kuwa aende yeye kunaonyesha tatizo kama lilivyoonyeshwa katika hiyo ripoti ya EIU.

Pamoja na hayo ni lazima tutafute njia nzuri ya kupima mafanikio ya ziara hizi tukilinganisha na gharama yake. Sijui ni kwa kiasi gani safari hizi ziko tayari kwenye bajeti na kwa kiasi gani bajeti inazingatiwa.

Hapa naamini kazi ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali itaonyesha umuhimu wake mkubwa sana. Mkaguzi Mkuu atalifanyia taifa hisani kubwa kama akiweza kuchanganua matumizi ya safari hizi za Rais na misafara ya watu anaoandamana nao ambao wanagharimiwa na fedha za walipa kodi wa Tanzania.

Ni lazima tuwe na utaratibu wa kujali fedha za wananchi kuliko kufikiria kuwa kwa vile zipo basi "tutumbue". Mnapokuwa na baba ndani ya nyumba au mama ambaye anasafiri mara kwa mara watoto hamna budi kujiuliza kama yote hayo ni mazuri kwa familia au la.

Kama kila wakati baba akirudi nyumbani watoto mkifurahia na kabla hamjaanza kumueleza yaliyowakuta shuleni au matatizo na majirani yeye anatimka kwenda kwingine mwisho kila mtoto ataanza kufanya mambo yake. Mwisho wake baba atashindwa kusimamia nidhamu ya watoto wake.

Ndugu zangu hilo ndilo linalotokea sasa hivi Tanzania kiasi kwamba watu wana shaka kama Rais Kikwete ana udhibiti wa Serikali na chama chake. Kwa kadiri mambo yanavyokwenda inaonekana kana kwamba Rais amefanya uchaguzi; uchaguzi wa kufuata safari zake na si maslahi ya wananchi na kuliongoza Taifa.

Tunapokabiliwa na changamoto za maamuzi magumu na hatua nzito Rais wetu anapokuwa hapatikani, kunatufanya tuamini kuwa aidha hatujali au hajali ule wajibu ambao tumempa.

Kama hadi hivi sasa ameshindwa kusimamia mazungumzo ya Muafaka wa Zanzibar huku Uchaguzi Mkuu ujao ukisogea karibu kabisa na matokeo ya kuingia katika uchaguzi huo bila Muafaka tukiwa tunayajua wote, kama hadi hivi sasa ameishia kuambia ulimwengu kuwa "tunapambana na rushwa" wakati ripoti ya Transparency International ya mwaka huu inaonyesha kuwa rushwa imeongezeka, basi, tuna matatizo.

Na bahati mbaya nyingine ni kwamba inaelekea hakuna watu wanaoweza kumwambia kwa yakini, kwamba kwa uzuri wote anaodhani anawafanyia Watanzania, wangependa wamwone akishughulikia matatizo ya ndani zaidi, isifike mahali umma ukamchoka wakati kimsingi yeye ni bora kuliko viongozi wengi waliopo kwa maana ya uadilifu.

Rais Kikwete anahitaji kuliongoza Taifa katika mambo haya magumu yanayolikabili Taifa na kufanya maamuzi magumu ambayo yataonyesha kuwa yeye kweli ana udhibiti wa Serikali yake. Kama anaona hili ni gumu na "kuruka" kila baada ya wiki ndiyo uongozi wenyewe, basi, Bunge letu liamue kupitisha sheria ya kujenga Ikulu ndogo Ulaya, Marekani na Asia ili Rais wetu awe anaishi huko huko majuu na arudi nyumbani kutusalimia akijisikia. Kwani hadi hivi sasa, mambo yanakwenda kama hayaendi bila yeye.

Unapomaliza kusoma makala hii Rais atakuwa amerudi nyumbani kwa Sikukuu ya Idd. Lakini sitashangaaa ndani ya wiki moja ijayo au mbili tukasikia ameondoka tena kwenda mikoani au "kwa mjomba".

Vyovyote vile lazima tukubali kuwa kuna kitu kinamfanya Rais wetu asipende kukaa Dar es Salaam na kupenda kukimbilia mikoani au kwenda nje ya nchi. Bado natafakari ni kitu gani hicho kinachomfanya apaone Dar es Salaam pachungu.

Vyovyote vile, sitoshangaa kuwa kina Marco Polo na Vasco Da Gama wanaweza kuwa wanasikia wivu. Angalau wao walikuwa ni wafanyabiashara na wavumbuzi; wa kwetu ndiye Rais mwenyewe.
 
Safari hizi nadhani zina manufaa kwake kama mtu binafsi na si kwa ajili ya Taifa. Inanishangaza sana kwa mtu kwenda nje ya nchi na kuomba msaada wa kuchimbiwa choo. Yaani kula ule halafu mtu mwingine ndaje akuchimbie choo!

SAFARI YA MPUMBAVU INA MWISHO
 
Maswali magumu haya hata Ikulu hawawezi kujibu kabisa
 
Lula wa Ndali-Mwananzela, asante sana kwa makala nzuri, shukurani Bubu Msemaji kwa kutubandikia hili...niliisha sema uwezo huyu Mkwere Raisi wetu JK ni mdogo sana, hata washauri wake nao ni matatizo...nafasi ya waziri wa mambo ya nje nadhani ilimuthiri sana hajajua yeye ni raisi...kuna watu wanahisi muungwana huwa anakwenda kukarabati afya yake ina mushkeri

Ushi
 
Kuna Mmomonyoka mkubwa wa maadili ya Uongozi,na hii yote inaongozwa na Mkuu wa Nchi,Hawa wakuu wamekuwa sio waoga kwa matumizi mabaya na makubwa ya pesa za walipa kodi.....Ni kazi ya wananchi kuiuliza serikali yao matumizi ya Ofisi ya huyu Muungwana,inawezekana kabisa akimaliza utawala wake akaiacha Hazina tupu ilhali yeye na wapambe wake wakiwa na mali Lukuki kama ilivyokuwa kwa Mtangulizi wake.

Safari aliyoifanya Muungwana mwezi wa Tisa aliongozana na watu wengi akiwemo mwanae (Ridhiwani),watu wa Embassy waliulizwa ujio wa Bwana mdogo huyo lakini majibu yalikuwa "Ni ziara binafsi",na walio karibu na huyo jamaa walidai alikuja kwenye biashara na shopping ya Harusi yake...Ridhiwani aliwasiliana na baadhi ya watu waliopo Canada kwa madai kwamba anatafuta Bulldozers kwa ajili ya mradi wa Ujenzi wa barabara ya Mbeya - Rukwa ambao nae ana kipande cha Ujenzi wa Barabara hiyo....Nafahamu kuwa Ridhiwani ni Mwanasheria,lakini kwetu pia anaweza kupewa Tender ya Ujenzi wa Barabara (Kumbukeni kuna fungu la 700mil huko kutoka Millenium Programme).

Mwaka jana Rais alipokuwa anakuja kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa,Mmoja wa wasaidizi wake alizuiwa Airport,na sababu ya kumzuia alikuwa amebeba kiwango kikubwa cha pesa.....Msaidizi huyo ambaye alikuwa ndege moja na Rais alitakiwa atoe maelezo ya wapi zinakwenda pesa hizo......Ilijulikana baadaye kuwa pesa hizo zilikuwa za matumizi ya msafara wa Rais....walipata Clearance ya pesa hizo baada ya Ubalozi kuzungumza na watu wa State Department.Haya hayakusemwa nyumbani lakini baadhi ya Wabunge walioambatana na Mkuu walionekana kushangaa.

Kwa mtazamo wangu nafikiri "Hesabu za Ofisi ya Rais" inatakiwa ziwe wazi,na sio kusingizia kila kitu kuwa siri kwa mambo ya usalama...Suala la Usalama kwetu ndio limekuwa kificho cha matumizi ya pesa.....
 
Kama wataamua kukaa kimya baada ya makala hii; wasubiri wiki ijayo.... huu wizi wa mchana lazima ukome!
 
rizwani ameanza lini kuchukua kandarasi za ujenzi wa barabara ....kiasi cha kupewa tenda mbeya ..aua mbeya wameona ndio wanastahili barabara mbovu...!!!

ujasiriamali mwingine.......hawa wanataka tuwafurushe....
 
rizwani ameanza lini kuchukua kandarasi za ujenzi wa barabara ....kiasi cha kupewa tenda mbeya ..aua mbeya wameona ndio wanastahili barabara mbovu...!!!

Ujasiriamali mwingine.......hawa wanataka tuwafurushe....

au nimepitwa na wakati nini? Maana kila kitu ni kipya kwangu, ina maana wamempa tenda ya kujenga barabara mbeya. Anaanza kufisadi bado mtoto
 
Mimi ni miongoni mwa waliojaribu kutaka kuona kuwa kuna vitu "positive" katika hizo ziara, na kutetea kuwa anayofanya ni sehemu ya majukumu ya rais, lakini nimeanza kuona (quite late, sorry folks) kwamba kumbe nilikuwa nachemka vibaya sana! Kuna muungwana mmoja ameorodhesha kwenye blog ratiba ya JK (on a day-to-day basis) ya mwezi wa nane na wa tisa, nikachoka kabisa! Katika hiyo miezi miwili kuna mmojawapo alipatikana ofisini ikulu kwa siku 3 (tatu) tu!
 
rizwani ameanza lini kuchukua kandarasi za ujenzi wa barabara ....kiasi cha kupewa tenda mbeya ..aua mbeya wameona ndio wanastahili barabara mbovu...!!!

ujasiriamali mwingine.......hawa wanataka tuwafurushe....

Inasemekena alikuwa Marekani kutafuta matrekta toka Caterpillar ili akayakodishe kwenye kampuni iliyopewa mkataba wa kujenga barabara ya Mbeya si ajabu hata mkataba kapewa yeye.
 
Inasemekena alikuwa Marekani kutafuta matrekta toka Caterpillar ili akayakodishe kwenye kampuni iliyopewa mkataba wa kujenga barabara ya Mbeya si ajabu hata mkataba kapewa yeye.

Acha kabisa hiyo, Rizwan gani anaongelewa hapa? Jamani msije mkawa mnajadili vitu bila ya kuwa na ushahidi? Napenda JF iendelee kuwa Kioo na sio Jukwaa la kuropoka.
 
Back
Top Bottom