Ubalozi wa Tanzania katika Jamhuri ya Afrika Kusini unawashukuru kwa dhati watu wote waliotusaidia kuwapata ndugu wa Bw.Karim, Mtanzania mwenzetu mwenye matatizo ya akili hivi sasa, ambaye aliondoka nchini Tanzania mwaka 1998 kwa ajili kuja Afrika Kusini (Bondeni), kutafuta fursa za Kimaisha.
Aidha, Ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini umempeleka Hospitali Bw. Karim, kwa ajili ya kumcheki afya yake ya mwili na akili, ili pia kupata Cheti cha Daktari kitakachoonesha kuwa anaweza kusafirishwa kwa Ndege kurudi nchini Tanzania bila ya yeye kuwa hatari kwake mwenyewe na kwa abiria wengine. Kupatikana kwa Cheti hicho, kutauwezesha Ubalozi kumrejesha nyumbani Tanzania ili aungane na familia yake.
Bw. Karim akiwa hospitali jana mchana sambamba na Maafisa wa Ubalozi waliofika kumjulia hali na kupata taarifa ya maendeleo yake. Pichani, Bw. Karim akizingumza na Mama yake Mzazi kwa mara ya kwanza baada ya miaka 26 ya familia kutofahamu iwapo angali hai au alikwishafariki.