Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) amekanusha kumtaja Rais mstaafu Benjamin Mkapa katika ripoti yake ya Mashirika ya Umma kuwa alitumia vibaya mkopo wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF). Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Ludovick Utouh, alikanusha habari zilizoandikwa na gazeti la MwanaHalisi la Mei 13 mwaka huu, kwamba Mkapa achota NSSF mabilioni ya shilingi na ashindwa kuyarejesha.
Napenda kukanusha taarifa hii, kwani katika ripoti yangu ya mashirika ya umma kwa mwaka unaoishia tarehe 30 Juni 2008, hakuna mahali nilipomtaja Mheshimiwa Rais mstaafu Benjamin Mkapa.
Katika ripoti yangu hiyo, aya ya 3.2.4 (ukurasa wa 74 hadi 77), nilitaka wakopaji tisa ambao kwa pamoja wamekopa NSSF jumla ya Sh 58,757,794,802 na katika deni lililotajwa na gazeti la MwanaHalisi la Sh 8,127,000,000 linahusu kampuni ya Kiwira Coal & Power Company, alisema.
Aliongeza kuwa kutaja jina la Rais mstaafu Benjamin Mkapa kama mkopaji badala ya mkopaji halali ni kinyume na ripoti yake na huo ni upotoshaji ambao angependa kuukanusha kwa nguvu zote. Ninaomba vyombo vya habari viwe huru kutumia ripoti yangu kama ilivyo na si vinginevyo, kwani kwa kutoa taarifa kama hiyo, kunapotosha umma na kunaweza kuleta mfadhaiko na chuki kwa waliotajwa isivyo halali, alisema.
Alisema lengo la vyombo vya habari ni kutoa taarifa sahihi bila kuongeza maelezo ambayo yanaweza kusababisha taarifa husika ieleweke visivyo na ni imani yake kuwa umma utaendelea kuhabarishwa juu ya ripoti yake kwa usahihi. Pale patakapokuwa hapaeleweki, naomba mje ofisini kwangu kwa ufafanuzi, kabla ya kuchapisha taarifa zinazopotosha na ambazo hazielezi yaliyo kwenye ripoti zangu, alisema Utouh.