Posted Date::6/2/2008
Wanaomtetea Benjamin Mkapa waanza kushambuliwa
*Wabunge, wanasiasa wataka yeye ajibu
*Wasema tuhuma za nyaraka zijibiwe kwa nyaraka
*Wahoji Kiwira walikuwa wapi siku zote hizo
Na Muhibu Said
BAADHI ya wabunge na wanasiasa, wameiijia juu Kampuni ya Kiwira Coal and Power Limited (KCP) kwa kukanusha kuwa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, ni miongoni mwa wamiliki wa mgodi huo, wakiitaka kampuni hiyo imwache ajibu tuhuma hizo yeye mwenyewe.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba alisema jana kuwa kitendo kilichofanywa na KCP, ni cha kuwapiga chenga wananchi kwa vile Mkapa ndiye aliyepaswa kujibu mwenyewe tuhuma za kujimilikisha mgodi huo alipokuwa madarakani.
Hata hivyo, Profesa Lipumba alisema majibu ya KCP, bado yana utata kwani sheria ya maadili ya viongozi, bado inamtaka aeleze mali alizonazo baada ya kuwa madarakani.
"Mbunge Aloyce Kimaro alipotoa tuhuma hizo bungeni, hakuwa akieleza kitu ambacho si sahihi. Mkapa anatakiwa atoe taarifa kamili mbele ya waandishi wa habari. Aeleze mali alizokuwa nazo wakati anamaliza kipindi chake cha uongozi na si kusubiri dakika za mwisho wamsafishe," alisema Profesa Lipumba.
Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willibrod Slaa alisema kama ambavyo wao walitumia nyaraka kumtuhumu Mkapa hadharani kwamba, kinachotakiwa kufanywa naye, ni kujibu kwa nyaraka na si kutegemea watu wengine wamjibie.
"Kama tulivyomtuhumu kwa documents (nyaraka), tunataka na yeye atujibu kwa documents, lakini siyo masuala ya kujibiwa. Sisi hatusemi hivi hivi, tuna akaunti za Mkapa," alisema Dk Slaa ambaye pia ni Mbunge wa Karatu (Chadema) na kuongeza:
"Inashangaza kuona hata Sumaye alipotuhumiwa ana ng'ombe, Mkapa ndiye aliyemjibia kuwa ni mfugaji. Ni utaratibu ule ule wa kujibiana".
Dk Slaa alisema hata kama Mkapa alijiondoa wakati wa kununua Kiwira bado ukweli unabaki kwamba, kampuni yake ilishiriki kwa namna moja mchakato wa kuinunua. "Walikuwa wapi muda wote hadi leo watoe tamko hilo, hapa kuna walakini mkubwa," alisema Slaa.
Naye Wakili wa Mahakama Kuu, Juvenalius Ngowi aliiambia Mwananchi kwamba Kiwira walipaswa kuonyesha nyaraka na vielelezo badala ya maneno matupu.
"Ni muhimu wakatoa nyaraka, haya maneno matupu hayaingii akilini," alisema.
Alisema Kiwira pia wanapaswa kuwaambia wananchi kama Mkapa akiwa mwanahisa naye alishirikia katika maandalizi na je hisa zake alimuuzia nani?
"Ni lazima watuambie kwamba hizo hisa zake alimuuzia nani na kwa bei gani, kwa sababu anaweza akawa ameuza kwa bei kubwa kwa kujua kuna faida huko mbele," alisema.
Naye Mbunge wa Vunjo (CCM), Aloyce Kimaro alisema alichokisema bungeni ni sahihi na kwamba, mtu mwenye shaka na ukweli huo, aende kwenye Kitengo cha Usajili wa Makampuni (BRELA) Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko.
"Waulizeni Wizara ya Nishati na Madini na BRELA. Lengo langu lilikuwa wengine wasirudie tatizo hilo," alisema Kimaro.
Jana, baadhi ya vyombo vya habari viliikariri KCP ikikanusha tuhuma kuwa Mkapa ni miongoni mwa wamiliki wa mgodi huo.
Badala yake, KCP ambayo inamiliki mgodi huo, ilisema Kampuni ya ANBEN inayomilikiwa na Mkapa na mkewe, Anna, ambayo awali ilikuwa sehemu ya Kampuni ya Tanpower, ilijitoa baada ya baadhi ya wanahisa wenzake kuwa na mpango wa kununua mgodi huo.
Mtendaji Mkuu wa KCP, Francis Tabaro alisema ingawa katika hati za umiliki (Articles of Association) inaonyesha kuwa Mkapa ni sehemu ya Tanpower, lakini baadaye alijitoa.
Aprili 25, mwaka huu, Kimaro, alimtuhumu bungeni Mkapa pamoja na aliyekuwa Waziri wa Fedha, Daniel Yona, kwamba walinunua Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira (KCML), ulioko Wilaya ya Rungwe, mkoani Mbeya kwa kificho.
Kimaro alisema mwaka 2004, Mkapa kwa kushirikiana na mkewe, Anna pamoja na Yona walianzisha Kampuni ya TanPower Resources Ltd na mwaka mmoja baadaye wakauziwa mgodi huo kimya kimya.
Kimaro alisema hayo alipokuwa akichangia bungeni Muswada wa Sheria ya Umeme wa Mwaka 2007, uliowasilishwa bungeni mwezi Aprili.