Tumzomee Mkapa
Charles Mullinda
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
NINA kila sababu ya kutofautiana na mawazo na misimamo ya watawala wetu, nikiamini kuwa tofauti zetu zitaisadia Tanzania kufika pale ilikokusudia. Nisipotofautiana nao, mimi na wengine kadhaa naamini kwamba watawala wetu hawatatekeleza ahadi yao ya kutupatia maisha bora Watanzania wote.
Wanaweza kutudharau kwa sababu sote tutakuwa tumekubali kufuata kile wanachokitaka wao - hata kama kinadhalilisha utu wetu.
Wa kwanza ninayetofautiana naye ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyetukataza tusimzomee Benjamin Mkapa, kiongozi wetu mstaafu wa serikali ya awamu ya tatu, anayetuhumiwa kwa mambo lukuki.
Kisa, eti ana heshima yake katika jamii yetu na kwamba utu wake lazima ulindwe hata kama yeye mwenyewe (Mkapa) hataki kuheshimiwa na jamii wala heshima yake hataki ilindwe.
Sikubaliani na Pinda katika hili na kama atachukia, sitasikitika kwa sababu nadhani nitakuwa sifanyi kosa. Hataki tuendelee kumzomea Mkapa, lakini mimi nadhani tuendelee kumzomea kwa sababu anaonekana anapenda kuzomewa.
Na kama Pinda atazidi kutulazimisha kuacha kumzomea mzee wetu huyu, tugeuze kibao, tumzomee yeye. Najua akizomewa atakasirika (na yeye anajua kuwa hasira hasara), tumwache akasirike kwa sababu hasira hizo zitamfundisha kitu.
Lakini tusifike huko kwenye kumzomea Pinda – ni mapema mno – lakini hapo ni bila kusahau ule msemo anaoujua kaka Pinda kwamba ‘mwenzake mtu fulani akinyolewa, yule anayesubiri kando yake lazima atie maji kichwani ili asije akaja akalalama kuwa wembe unamuumiza'. Tumwache kwanza Pinda hadi atakapoanza kutukorofisha kwa kutuzuia kuonyesha hisia zetu kwa viongozi wetu akiwamo yeye.
Kwa wakati huu sisi tuendelee kumzomea Mkapa hadi siku atakapotueleza ukweli kuhusu madai ya yeye kujitajirisha wakati akiwa ndani ya nyumba yetu takatifu - Ikulu.
Na Mkapa asidhani kwamba tunavyomzomea hatumuheshimu au tunamuonea, la hasha. Tunamzomea kwa sababu sisi tunadhani yeye ndiyo asiyetuheshimu. (Kuna kosa gani baba akiwaheshimu watoto wake! Si kuwaheshimu tu…baba anaweza hata kutaniana na watoto wake; cha ajabu nini? Si anatudharau na hao aliowapisha kuishi katika nyumba yetu takatifu, wanampa kiburi kwamba pamoja na madudu anayodaiwa kuyafanya katika kipindi chake cha uongozi, hakuna atakayemgusa.
Hakuna Mtanzania anayemchukia Mkapa, hivyo ndivyo ninavyoamini, wanachokichukia ni matendo yake yaliyochangia kuwafikisha katika wakati mgumu walio nao sasa.
Watanzania wanachukia wanapomuona Mkapa akionyesha ‘kiburi' cha wazi kwa kutojibu maswali anayopaswa kuyajibu kama kiongozi mstaafu na Mtanzania wa kawaida, anapotakiwa kufanya hivyo.
Wanachukia wanapowasikia watawala wa sasa wakisema Mkapa anapaswa aachwe apumzike, hawataki achunguzwe au ahojiwe kuhusu tuhuma zinazoelekezwa kwake.
Kwa sababu hawawezi kumfikia na kumlazimisha awaeleze kile wanachotaka kusikia kutoka kwake, kwa vile ana ulinzi usiopitika kirahisi, ndiyo maana wanamzomea ili akasirike, avunje ukimya wake, azungumze japo kidogo kuhusu utajiri anaodaiwa kuwa nao.
Kumzomea mtu ni njia mojawapo ya kumfanya azungumze, hivyo tusipomzomea Mkapa ataendelea na tabia yake ya kukimbilia kijijini kwao Lupaso kule wilayani Masasi, na kutoa kauli zisizoridhisha. Lakini kwa sababu anaowaambia ni jamaa zake na anakuwa amewapelekea ‘vijiwazadi' wanakubaliana naye na kumshangilia.
Sote tunakumbuka aliyoyasema hivi karibuni wakati akiwa huko kwao. Kwamba wanaomtuhumu wanafanya hivyo kwa vile aliwanyima vyeo wakati alipokuwa madarakani kwa kipindi cha miaka 10, na kwamba watu wote wanaomuita fisadi ni wa kupuuzwa kwa kuwa wana chuki binafsi naye.
Inawezekana ni kweli. Lakini Watanzania hawakuuliza kama alikuwa akifanya upendeleo kwa baadhi ya watu wakati akiwa Ikulu au la. Watanzania wanachohoji ni, je, Mkapa huyu aliyekingiwa kifua na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kuwa ni msafi na mkweli alifanya biashara wakati akiwa Ikulu? Hilo ndilo analopaswa kulitolea maelezo kinagaubaga kama hataki aendelee kuzomewa.
Na Pinda anapaswa kufahamu kuwa Mkapa anazomewa kwa mengi likiwamo la kumuaibisha Mwalimu Nyerere aliyetembea nchi nzima akimnadi Mkapa kama mtu safi, anayepaswa kuwa kiongozi wa Watanzania, lakini amekuwa kiongozi wa kwanza wa taifa hili kutajwa hadharani kama mtu aliyeichafua sifa ya Ikulu.
Ilielezwa na Mwalimu Nyerere kama Ikulu ni sehemu takatifu. Lakini yeye anadaiwa kuigeuza kuwa pango la walanguzi. Hapa anazomewa kwa kumwangusha Mwalimu.
Wanaomtuhumu Mkapa wanaeleza wazi ushahidi wa yeye kufanya biashara akiwa Ikulu kuwa upo Mamlaka ya Usajili wa Leseni na Biashara (BRELA), Tanesco na katika taasisi nyingine zinazohusika na mambo ya biashara.
Kikubwa anachopaswa kukitolea maelezo kwa Watanzania wote na si kijijini kwake tu ni iwapo yeye na rafiki yake, Daniel Yona, Desemba 2004 walipokuwa wanaitumikia Tanzania kwa nafasi za Rais na Waziri wa Nishati na Madini, walisajili kampuni ya Tanpower Resources, wakiwahusisha pia watoto, wake, wakwe na ndugu zao wengine wa karibu.
Awaeleze Watanzania kuhusu ukweli wa tuhuma hizi, wala asidharau kwa sababu anaweza kusababisha hata mke wake, Anna Mkapa, mtoto wake Nicholaus Mkapa, na baba mkwe wa mtoto wake anayetajwa kwa jina la Evans Mapunda, nao waanze kuzomewa kwa sababu ya kuficha ukweli.
Mkapa ambaye ametoa jibu la jumla kwamba si tajiri kama inavyoelezwa na anaodai kuwa wana kinyongo naye kwa sababu hakuwapendelea alipokuwa Ikulu, anapaswa awaeleze Watanzania kama kweli kampuni na washirika wake walitumia nyadhifa, majina au umaarufu wao kupata leseni ya kuchimba mkaa wa mawe, ili kufua umeme wa kuuza, transmita na vifaa vya kusambaza nishati na usimamizi wa miradi na ushauri wa miradi pia.
(Mimi nashindwa kuelewa mzee mstaafu anaposema hakuwapendelea viongozi fulani alipokuwa Ikulu - anataka ieleweke kuwa alipokuwa akitoa vyeo kwa mawaziri alikuwa anafanya hivyo kama mtu anavyogawa karanga, tena kwa watoto, bila kujali wana uwezo gani - wao bora warushe karanga tu mdomoni?) Tunajua viongozi wote waliopewa vyeo walikuwa watu makini waliostahili kuwa katika nafasi walizokuwa nazo.
Hapana bwana! Mzee wangu toa maelezo kuhusu tuhuma mbaya kabisa za kutumia wadhifa wako wa urais kubinafsisha mradi wa Kiwira Coal Mine na mwaka 2005 miezi michache baada ya kusajiliwa Tanpower Resouces, ikaingia ubia na serikali kununua asilimia 70 za hisa za Kiwira na baadaye kampuni hiyo ikaongeza hisa zake hadi kufikia asilimia 85, huku ikiiachia serikali asilimia 15 tu.
Pia Mkapa asiache kuzungumzia kampuni nyingine anayodaiwa kumiliki yeye na mkewe Anna ya ANBEN. Na bila kusahau atoe maelezo kuhusu madai kwamba waliokuwa wafanyakazi wa mgodi wa Kiwira hawakutendewa haki katika malipo ya mafao yao.
Akishamaliza kuzungumzia hayo, ageukie kwenye sakata la rada anakodaiwa kukataa ushauri wa wataalamu kuhusu ununuzi wa rada iliyogharimu mabilioni ya shilingi za walipa kodi, na ilipofikishwa nchini ikabainika kuwa haikuwa katika kiwango kinachotakiwa cha kufanya kazi.
Aeleze kama ni kweli au si kweli alishauriwa na viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani, viongozi wa taasisi mbalimbali na hata wale wa mataifa ya nje, kuwa Tanzania haikupaswa kununua rada hiyo kwa fedha nyingi kiasi hicho, lakini hakusikia.
Kwa makusudi au kwa sababu anazozijua akakubali kununuliwa rada hiyo na sasa imeibua kashfa kuanzia kwake hadi kwa wasaidizi wake, akiwamo Chenge. Wananchi mnajua kuwa mzee wetu Chenge naye anachunguzwa? Basi habari ndiyo hiyo.
Tuhuma hizo ni nzito kwa sababu ya maisha na ustawi wa Watanzania. Kama Mkapa alikosa aibu akaamua kufanya anayodaiwa kuyafanya, sidhani kama kuna kosa kwa Watanzania nao kukosa aibu na kumzomea, sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kumlazimisha aeleze ukweli anaoujua ili ahukumiwe kulingana na matendo yake.
Na akiwa mjanja, anaweza kuepukana na adha anazokumbana nazo sasa za kuzomewa na kulamizika kutoa maelezo yasiyolingana na upeo wake wa kuelewa mambo.
Aje Dar es Salaam ambako ndiko chimbuko la tuhuma zake, asema alivyohusika, kama hakufanya kabisa au alishawishiwa kufanya hivyo au ‘ibilisi alimpitia' kama binadamu wengine akajikuta anasahau kwamba yeye ni Rais, akafanya biashara akiwa Ikulu.
Na kisha akikubali kuhusika na kashfa hizo kwa namna yoyote ile, aombe radhi kwa matendo yake hayo na kurudisha mali zote alizochuma isivyo halali, wakati wa kipindi chake miaka kumi ya urais.
Akifanya hivyo atakuwa ameokoka kwa sababu Watanzania badala ya kumzomeoa wanaweza kumcheka na wengine kumshangaa kwa kutenda kinyume na walivyotarajia.
Wakishaona amerudisha kilicho chao, watamsamehe kwa sababu hiyo ndiyo jadi yao na ili awe na uhakika na hili aangalie jinsi mafisadi wa mabilioni ya fedha katika Akaunti ya Malipo ya Nje (EPA) wanavyorudisha fedha (kisirisiri) walizoiba kisha wanaendelea kudunda mitaani kama kawaida.
Vinginevyo ajue kuwa ‘kutosikia' kwake na kudharau kila ushauri anaopewa anazidi kujiharibia.
Na kama ataendeleza utamaduni ambao nadhani ameuiga kwa Andrew Chenge na Edward Lowassa wa kukimbilia katika vijiji walikotoka kujitetea, basi Watanzania wasiotoka kijijini kwake wataendelea kumzomea.