Wanaotajwa kumiliki Dowans ni usanii mtupu
· Kwa nini Karamagi alishinikiza TANESCO iingie mkataba na Dowans?
LILIKUWA ni shinikizo la aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wa wakati ule Bw. Nazir Karamagi lililosababisha TANESCO kukubali kuhamisha mkataba wake na Richmond kwenda Dowans Holdings SA.
Bw. Nazir Karamagi alikuwa ana uhusiano wa kibiashara na kampuni ya Portek Systems and Instruments ya Singapore ambayo ilishiriki kuleta mawinchi kwa ajili ya kampuni ya TICTS ambayo wakati ule Bw. Karamagi alikuwa ni mbia mkuu.
Ni kampuni hiyo Portek Systems and Instruments inayotajwa katika nyaraka za BRELA kuwa na asilimia 39 ya hisa kwenye kampuni ya Dowans Tanzania Limited. Bila uchunguzi huru haijulikani ni kwa nini Bw. Karamagi alishinikiza Shirika la Umeme la Tanzania ((TANESCO) kubadili mkataba wake na kuupeleka kwa Dowans Holdings ya Costa Rica.
Kuhusika kwa Karamagi kunatajwa mara ya kwanza kwa kina kwenye ripoti ya Kamati Teule ya Bunge iliyoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe. Sehemu ya ripoti hiyo ilijaribu kuelezea kuhusishwa kwa Wizara ya Nishati na Madini katika kuingilia watendaji wa TANESCO.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, wakati TANESCO wamewaandikia kampuni ya Richmond kutaka maelezo juu ya ucheleweshaji wa kuingiza majenereta na uhalali wa kampuni hiyo huko Marekani au uwezo wake wa kifedha, ilikuwa ni Wizara ndiyo iliyoingilia kati kuikingia kifua kampuni hiyo ya Richmond.
TANESCO wakaamua kuiandikia kampuni ya Richmond taarifa ya tahadhari (default notice) kuwa inaonekana walikuwa wanaelekea kushindwa kutekeleza mkataba. Ripoti hiyo inaongeza na kusema kuwa: "Wizara ya Nishati na Madini haikufurahishwa na mwelekeo huo wa TANESCO wa kuvunja Mkataba huo licha ya kwamba hali ya maji nchini ilizidi kuwa nzuri na kampuni hiyo ya Marekani ilikuwa haionyeshi dalili ya kuweza kutekeleza mradi huo kinyume na makubaliano."
Alikuwa ni Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Karamagi akipitia Kamishna wa Nishati Bw. Bashir Mrindoko, aliyetaka maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa TANESCO ya kwa nini shirika hilo liliandika taarifa hiyo ya tahadhari kana kwamba kuashiria kuelekea kuvunjwa mkataba.
Ripoti inasema: "Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO akajieleza kwa barua aliyomwandikia Waziri moja kwa moja yenye Kumb. Na. MD/ 003 ya tarehe 23 Novemba, 2006" . Ilikuwa ni siku tano baada ya barua hii, kwa mujibu wa Ripoti ya Mwakyembe, Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Balozi Fulgence Kazaura alimwandikia barua Mkurugenzi wa TANESCO na kumueleza kuwa amepokea mawasiliano ya simu toka kwa Waziri
Karamagi akiwa nchini Canada "akimuarifu kwamba Richmond Development Company LLC walikuwa wanataka kuhamisha majukumu yao yaliyobaki katika mkataba wa uletaji mitambo na uzalishaji umeme wa dharura kwa kampuni nyingine."
Jambo hili ni muhimu kulizingatia kidogo. Wawili waliotajwa na Waziri Ngeleja, hivi karibuni, kuwa ni sehemu ya wakurugenzi wa kampuni ya Dowans Tanzania Limited ni Wacanada. Hawa ni Bw. Guy Arthur Picard na Bw. Andrew Jamess Tice. Hilo peke yake haliwezi kutushtua sana isipokuwa wasifu wa mmoja wao unatufanya tudadisi kidogo.
Bw. Andrew James Tice anatajwa kuwa ni mtaalamu wa mambo ya kibenki. Wasifu wake ulioko kwenye mitandao mbalimbali unatudokeza juu ya utaalamu wake uliobobea katika kulinda maslahi ya wateja wake ambao wanaaminisha fedha na majina yao kwake.
Kwa maelezo yake mwenyewe amefanya kazi hii ijulikanayo kama fiduciary kwa wateja wake wa Mashariki ya Kati na Afrika huku akiwakilisha maslahi yao katika nchi za Mauritius, Guernsey, Singapore na Cayman. Nchi zote hizo pamoja na Costa Rica ni miongoni mwa nchi ambazo zina usiri sana katika masuala ya makampuni.
Kutokana na nafasi yake hiyo, Bw. Tice ni mtaalamu anayejua jinsi ya kufungua makampuni hewa au yale ya kificho ambayo wamiliki wake halisi hawataki kujulikana. Hii ni sehemu ya kazi yake.
Ndipo hapa suala la Karamagi kuwepo Canada na kutoa maelekezo kwa TANESCO kuwa mkataba wa Richmond upelekwe kwa kampuni nyingine linapoonekana kwa mwanga zaidi. Je yawezekana kuwa ni wakati ule ndipo Bw. Karamagi alipewa taarifa na "vigogo" wahusika waliotaka huduma ya Bw. Tice kuwafungulia kampuni huko Costa Rica ambayo itarithi mkataba wa Richmond?
Naomba nipendekeze kuwa hivyo ndivyo ilivyo kwani msisitizo uliofuatia hapo hauwezi kuelezewa isipokuwa kulikuwa na nguvu kubwa nyuma ya Karamagi iliyotaka kampuni pekee ambayo ingerithi mkataba huo iwe ni Dowans.
Kitu cha kwanza ambacho ripoti ya Mwakyembe inasema Bw. Karamagi alifanya ni kuhoji (ninaamini alikuwa anajua) kama mkataba wa Richmond/TANESCO "unaruhusu" kukabidhi majukumu kampuni nyingine.
Jibu la Mkurugenzi wa TANESCO kama inavyoelezwa na Kamati hiyo kwenye ripoti ni kuwa "uongozi wa TANESCO ulimshauri Mwenyekiti wa Bodi amtaarifu Mhe. Waziri kwamba Kifungu cha 15.12 cha mkataba huo hakiruhusu kukabidhi majukumu ya mkataba kwa kampuni nyingine isipokuwa kwa maafikiano ya pande mbili za mkataba".
Pamoja na ukweli huo, Richmond wakaiandikia TANESCO barua tarehe 4 Disemba, 2006. Ikapokea barua kutoka kwa Richmond Development Company LLC ikielezea makusudio ya Richmond kuhamisha majukumu yake yote ndani ya mkataba huo kwenda kwa Dowans Holdings, S.A"
TANESCO, katika ujasiri wa kupingana na Wizara yake mama, ikaandika barua siku hiyo hiyo kupinga mpango huo. Ripoti ya Mwakyembe inatudokeza kuwa TANESCO walitoa sababu tatu za kwa nini jambo hilo haliwezekani. Sababu hizo ni kuwa "(i) Kifungu 15.12 cha mkataba kinataka kuwepo kwa makubaliano ya pamoja ya kimaandishi (written mutual agreement) kutoka kwa wahusika wote wa mkataba (parties) kabla ya kufikiwa uamuzi wa kuhamisha mkataba. (ii) Richmond Development Company LLC haijatoa sababu zozote za msingi kwa pendekezo hilo la kuhamisha Mkataba. (iii) TANESCO haifahamu historia, uzoefu wala uwezo wa kifedha wa hao wanaopendekezwa kuhamishiwa mkataba."
Lakini wizara haikujali hoja za TANESCO na badala yake tarehe 21 Disemba 2006 ikaandika barua kuilazimisha TANESCO kuhamisha mkataba huo kwenda Dowans wakati dharura yenyewe ilishakwisha.
Dk. Mwakyembe alitutaarifu kuwa: "Uamuzi huo wa kuruhusu uhaulishwaji wa mkataba kipindi ambacho nchi ilikuwa imeondokana na hali ya dharura, tena kwa masharti yaleyale ya kulaliwa yanayoweza kukubalika pale tu ambapo nchi imebanwa kweli kweli na tatizo, ulimfedhehesha hata Mkurugenzi Mwendeshaji wa Dowans Holdings S.A, Bw. Guy Piccard, raia wa Canada, alipohojiwa na Kamati Teule tarehe 27 Disemba, 2007."
Kwa maneno mengine, maelezo kuwa TANESCO ndiyo italipa gharama ya kesi iliyopoteza kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Biashara inashangaza sana. TANESCO walikataa kuhamisha mkataba, na walitoa sababu ambazo hazikujibiwa.
Kwamba Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Nishati na Madini chini ya Karamagi, ndio waliilazimisha TANESCO kuhamisha mkataba kwenda Dowans badala ya kuuvunja kama walivyotaka na wao ndio walipe bilioni 94, ni jambo linalotakiwa kumuudhi na kumkera kila Mtanzania.
Hasara hii ambayo ukijumlisha na fedha nyingine ambazo zimeshalipwa kwenye suala hili hadi sasa ambayo zinakaribia zaidi ya bilioni 50 (nina uhakika Ngeleja na wenzake wanataka tuamini kuwa bilioni 94 ndio malipo pekee), ni lazima iende na vichwa vya watu!
Vyama vya siasa vikatae, kina mama wakatae malipo haya haramu, na vijana wa Tanzania wayakatae. Viongozi wa dini watoe tamko na kukataa malipo haya ya kidhalimu; kwani kuyaendekeza ni kuendekeza kunyonywa na kutawaliwa kimabavu.
Lakini vile vile kuna watu wanatakiwa watoe maelezo kwa taifa miongoni mwao ni Bw. Nazir Karamagi na kundi zima la wanasiasa waliohusika na kuliiingiza taifa katika aibu hii. Na binafsi ninaamini Rais Kikwete mwenyewe ni lazima atoe msimamo kwani toka mwanzo alikuwa anajua kilichokuwa kinafanywa na marafiki zake wa karibu. Kwa nini ameridhia serikali ibebeshwe mzigo huu? Kwa nini Watanzania walipe gharama ya uzembe wa viongozi ambao yeye amewateua? Rais Kikwete ana uwezo ndani yake wa kuliepusha taifa na aibu hii. Akitaka.
SOURCE: Gazeti la Raia Mwema, January 12 - 16, 2011