Makala ya Mzee Mtei....
CHADEMA NI NINI NA NI NANI
Nikiwa Muasisi na Mwenyekiti (Taifa) Mstaafu wa Kwanza wa CHADEMA naona ninawajibika kujibu makala ilioandikwa na H. Nesario iliyokuwa na kichwa cha habari kama hapo juu, na kuchapishwa katika Toleo la Mtanzania Jumapili tarehe 4 Desemba, 2005.
Kuanzishwa kwa Chadema
Ni kweli kwamba wastaafu kadhaa walikuwa miongoni mwa watu waliojiunga nasi kuanzisha Chama cha Demokrasia na Maendeleo mwaka wa 1992. Lakini kulikuwa na wananchi wa kila rika, taaluma na kazi. Kulikuwa na wanasiasa kama Mheshimiwa Edward Barongo ambaye aliungana na mimi hata kutia saini katika Fomu ya Maombi ya kusajiliwa kwa awali na Mama Mary Kabigi, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania, Mkoa wa Dar es Salaam. Wafanya biashara kama Bwana Medard Mutungi na Kanali Mstaafu Geofrey Marealle walituunga mkono. Wana-ushirika kama Brown Ngwilulupi walijiunga siku zile za mwanzo. Mameneja wa makampuni kama Victor Kimesera, Michael Shang'a na Alphonse Maskini. Vijana kama Freeman Mbowe pamoja na kundi kubwa la wanazuoni kama Lenny Kassoga walishiriki kubuni katiba ya awali. Wanasheria pia walikuwepo, mmoja wao akiwa Bob Makani ambaye alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa kwanza na Mwanaidi Majaar ambaye alikuwa mmoja wa wadhamini wa mwanzo. Wakulima na wafanyakazi, wake kwa waume, walituunga mkono mara tu ilipojulikana kwamba tulikuwa na mpango wa kuanzisha Chama kipya cha siasa sheria itakaporuhusu. Kwa hiyo si kweli kwamba CHADEMA kilianzishwa tu na wastaafu.
Asili ya Misimamo ya Chama
Ni sahihi pia kwamba mimi binafsi nilibahatika kushika nyadhifa za kiserikali kuanzia wakati tulipopata Uhuru, zikiwepo Chief Establishment Officer, mwaka wa 1962, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha 1964, Gavana mwanzilishi wa Benki Kuu, 1966, Katibu Mkuu wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, 1974 na mwishowe, Waziri wa Fedha na Mipango. Wadhifa wa uwaziri niliushika mara baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki 1977, nikaendelea hadi wakati wa vita dhidi nduli Idi Amin wa Uganda.
Baada ya vita nilikuwa na msimamo tofauti na ule wa bosi wangu, Rais Mwalimu Julius Nyerere. Tofauti hizi zilihusiana na mikakati ya kufufua uchumi ambao uliathirika sana wakati wa (na hasa kutokana na) harakati za kumfukuza adui kutoka nchi yetu. Uchumi ulidorora pia kutokana na miradi na mashirika mengi ya umma kuanzishwa kisiasa bila uchambuzi yakinifu na kuendeshwa kwa hasara na kutegemea ruzuku kutoka Hazina. Kwa maoni yangu haya yote yalihitaji kurekebishwa kimuundo na kimenejimenti.
Kutokana na mlipuko mkubwa wa bei uliosababishwa na sera zetu za kuendesha serikali na mashirika ya umma, na uzalishaji duni wa bidhaa, thamani ya sarafu ya Tanzania ilikuwa imeshuka sana. Nilikubaliana na ushauri wa I.M.F. na Benki ya Dunia wakati huo kuwa tulihitaji kurekebisha thamani hiyo, pamoja na kutathmini uendeshaji wa miradi na mashirika kadhaa ya umma. Rais Nyerere alikataa kata kata kwamba hawezi kukubali ushauri huo na hata akaamuru ujumbe wa I.M.F. uliokuwa nchini ufukuzwe. Kwa vile niliona msimamo wa bosi wangu ulitokana na watu waliokuwa wanapotosha mambo na haungesaidia kutatua matatizo yaliyokuwa yanakabili taifa letu, nilimwandikia kumuomba ateuwe Mtanzania mwingine ambaye angeweza kuendesha naye uchumi wa nchi yetu. Rais alikubali kujiuzulu kwangu na ndipo nikaacha uwaziri, nikahamia Arusha kuwa mkulima kuanzia 1980.
Kwa hiyo ni hisia za Bwana H. Nesario tu kwamba eti mimi nilikuwa natetea au kusimamia haki za wenye mitaji, ambapo Mwalimu alikuwa anatetea haki za Watanzania masikini. Najiuliza kuendelea kuyapa ruzuku kutoka Hazina mashirika muflisi ni kutetea haki za Watanzania masikini? Huko ni kutoelewa menejimenti fanisi au uchumi! Nesario anahitaji kufunzwa uchumi na menejimenti yenye tija, licha ya kwamba alifanya kazi serikalini mpaka akastaafu. Alikuwa na cheo gani alipostaafu?
Historia ya nchi yetu kuanzia wakati nilipojiuzulu, mwisho wa 1979 imedhihirisha kwamba kama ushauri wangu ungekubaliwa, mambo yangeendelea kwa unafuu zaidi. Nimkumbushe Nesario na wengine wanaoonekana kusahau, kwamba kuanzia mwanzo wa 1980 bidhaa muhimu kwa matumizi ya wananchi wa kawaida zilikuwa adimu sana na Watanzania hasa wa kipato cha kawaida na cha chini, waliteseka sana. Ni wale wakubwa tu waliosafiri nje ya nchi ndiyo walioweza kuleta na kukidhi mahitaji yao.
Sijui Bwana Nesario alikuwa anaishi wapi wakati huu, lakini sabuni, sukari, mafuta ya kupikia, nguo, viatu, karatasi, unga wa sembe na wa ngano, mchele, mafuta ya taa na karibu kila aina ya bidhaa ilikuwa inauzwa kwa kibali au kwa bei ya juu sana. Hata baadhi ya wananchi mashambani walilazimika kuvaa mifuko mitupu ya saruji au ya mbolea! Ilifikia mtu akitoka nyumbani akaona foleni ya watu mbele ya duka alikuwa anajiunga nayo akitarajia mwisho wake angeweza kununua chochote kilichokuwa kinauzwa. Wenye magari hawakuwa wanaruhusiwa kuendesha Jumapili jioni, na petroli ilikuwa inauzwa kwa kibali na kwa bei ya kuruka. Nahisi Nesario alikuwa nje ya Tanzania ndiyo maana anajizungumzia tu bila kuona adha au taabu tuliokuwa tunapata.
Fursa ya kuunda chama mbadala kwa Chama cha Mapinduzi ilitulazimisha tubuni filosofia na sera ambazo zingeepusha taifa kurudia makosa ya zama za ujamaa zenye sera zisizo na tija na uendeshaji wa kiimla. Wananchi ni lazima waweze kuamua mambo yahusuyo maendeleo ya taifa lao kwa uhuru kamilifu, ujasiri na bila ya woga na kuepuka utawala wa kiimla. Rasilimali za nchi ni lazima zitumike kunufaisha wananchi. Serikali ina wajibu wa kuweka mazingira yanayowezesha mitaji kuingia nchini. Uhuru wa soko ndiyo njia endelevu ya kuvutia mitaji ili raslimali za nchi ziweze kutumika kikamilifu, lakini papo hapo lazima umma wote ufaidike na mazingira yawekwe kuhakikisha wananchi wanajituma kwa kadri iwezekanavyo kupata kipato chao wenyewe. Wasiojiweza na ambao hawakupata ajira watadhaminiwa na umma. Miundombinu ya kiuchumi na ya kijamii itamilikiwa na umma na kuendeshwa kisayansi, kuhakikisha ni endelevu na ina tija. Miradi ya umma itabuniwa na kuendeshwa bila pupa za kisiasa. Misimamo kama hii ni ya social democrats na ilitangazwa mapema na CHADEMA. Kama Bwana Nesario aliisoma au kuisikia hangeweza kusema eti kwamba chama hiki kinasimamia mabepari na wenye mitaji. Najisikia mshindi kwamba licha ya CCM kujidai eti ni chama cha ujamaa, wameiga sana misimamo ya CHADEMA kama tulivyoitangaza hapo awali.
Itakumbukwa kwamba licha ya matamshi ya Mwalimu Nyerere wakati wa kukataa ushauri wangu (na wa I.M.F) kwamba hatageuka kutazama nyuma kwani angekuwa "jiwe la chumvi kama mke wa Loti", sisi CHADEMA tulimpelekea kijitabu cha Sera na Misimamo yetu mwanzoni mwa mwaka 1994. Mwalimu alizisoma na baadaye alitamka hadharani alipokuwa huko Mbeya kwamba sera zetu zilikuwa safi na zingeweza kuwaondolea Watanzania kero zao. Maneno ya Mwalimu yalikuwa "Heri Mtei, Bwana"! Hizo ndizo sera za CHADEMA kimsingi.