YEYE ASEMA ''SIJAACHA KAZI CLOUDS FM ILA........'' MASOUD KIPANYA
Hakuna ubishi kwamba kipindi cha PowerBreakfast kinachorushwa na radio ya Clouds FM ni mojawapo ya vipindi vya radio vyenye wapenzi na wasikilizaji wengi nchini Tanzania.
Hivyo basi haishangazi kwamba hivi karibuni watangazaji wawili wa kipindi hicho waliokuwa wamezoeleka,Masoud Kipanya(KP) na Fina Mango, walipopotea hewani maswali mengi yaliibuka.Wako wapi KP na Fina?Maoni na e-mails zikarushwa kwetu tukiombwa kuwatafuta na kujua nini kimetokea na kama wapo likizo tu au inakuwaje?
Wakati tukifanya juhudi za kujua nini kimetokea,blog maarufu ya Michuzi ikaandika habari iliyokuwa na kichwa cha habari Fina Mango na Masudi Kipanya niaje?Mjadala ukazuka.Kwa bahati nzuri,nasi tukawa tumebahatika kumpata mhusika mmojawapo yaani Masoud Kipanya(KP) ambaye hakusita kutupa yake machache kuhusu nini kimetokea au kilitokea,yuko wapi,anafanya nini nk.Anasisitiza kwamba nia yake ni kutoa ufafanuzi(kwa upande wake) ili watu wasiendelee kujenga picha ambazo pengine hazitakiwi kujengwa wala hazipo.
Je PowerBreakfast ya Masoud na Fina ndio imefikia kikomo? Je ni kweli kwamba masuala ya mshahara ndio yamesababisha wapotee hewani?Fuatana nasi katika mahojiano haya mafupi;
BC: KP,kwa muda wa wiki kadhaa sasa kumekuwepo na tetesi,minongono,udaku nk kuhusu kuwepo au kutokuwepo kwenu katika kipindi chenu maarufu cha PowerBreakfast kupitia CloudsFM.Hivi leo,blog ya Michuzi(bila shaka umesoma kilichoandikwa) iliweka kidogo kuhusiana na kilichokuwa kinazungumzwa mitaani. Je ukweli uko wapi? Upo au haupo tena katika PowerBreakfast?Nini kimetokea?
KP: Nimepata bahati ya kusoma blog ya Michuzi muda mfupi uliopita na nimeona taarifa pamoja na maoni mbalimbali ya wadau. Pengine bila ya kutoa ufafanuzi, watu wataendelea kuongea mambo ambayo hayapo kabisa. Ukweli ni huu ufuatao; Nitajizungumzia zaidi mimi kwa vile ishu yetu na Fina ni moja ila maamuzi yanatofautiana kidogo na yanatofautiana si kwa sababu ya upendeleo, la hasha, nataka kuamini ni kwa sababu ya aina ya mikataba tuliyokuwa nayo.Wa kwangu ulikwisha February 28 mwaka huu ingawa nilishaanza kuutumikia mkataba mpya wa miaka miwili, wa Fina unakwisha nadhani mwishoni mwa mwaka huu(sina uhakika)
Mimi sikuacha kazi Clouds Fm kama inavyosemekana, mimi nimepewa barua ambayo inazungumzia ku-revoke (kutengua,kuahirisha) mkataba wangu na Clouds.Nitazungumzia sababu za kupewa barua hiyo, ila kabla sijaingia ndani zaidi, mwisho wa barua ile niliyopewa imesema, nainukuu, we wish you all the best in your future endeavors mwisho wa kuinuukuu barua niliyopewa na HR Manager wa Clouds Media Group. kwa lugha rahisi ikimaanaisha tunakutakia kila la heri katika mahangaiko yako ya mbeleni.
Kwa mantiki hiyo labda wasomaji waniambie sijaielewa maana ya barua ile, lakini kwa kifupi nilichoelewa ni kwamba, kutokana na makosa niliyoyafanya, Clouds imeonelea kuwa sina sifa za kuendelea kuwa sehemu ya timu ya Clouds Fm. Sasa basi, hebu tuangalie makosa niliyoyafanya mimi pamoja na Fina.
Tarehe 29th May 2008, kwa pamoja, mimi na Fina tuliamua tusiingie kwenye kipindi kuonyesha kutoridhishwa na utendaji wa baadhi ya wenzetu. Kama kuna waliosikia, siku moja kabla yaani tarehe 28th May tulifanya mahojiano na Balozi wa Marekani nchini Tanzania.Bahati mbaya (kwa sababu ambazo zilikuwa ndani ya uwezo wa Technical Department) mahojiano yale hayakusikika vizuri, yalisikika vibaya mno!!! Na hata vifaa pia havikuwa timilifu, mfano mmoja mdogo tu ni kwamba tulikuwa tunatumia mic moja.Yaani watangazaji watatu na balozi, kwangu ilinipa wakati mgumu sana hasa ikizingatiwa taarifa za interview zilipatikana karibu wiki nzima.Nilitegemea wenzetu wangejiandaa kwa kila kitu. Kwa kifupi watu wa technical walikuwa na uwezo wa kusema kwamba interview isingewezekana kutokana na ufinyu wa signal na vifaa, TUNGEAHIRISHA.Makosa kama haya yamekuwa yakijirudiarudia mara kwa mara na ndio maana nasi tukaamua kuweka msisitizo kwa njia ile ya kugoma.
Najua kuna watakaojiuliza, hapa Gerald anaingia wapi, kwa sababu alisikika wakati wa mahojiano na balozi, akayapata madhira lakini hakugoma. Hilo sitolitolea maelezo nikiamini yeye mwenyewe ndiye mwenye nafasi nzuri ya kufafanua atakapotakiwa kufanya hivyo ingawa halazimiki. Ila ieleweke kwamba, kwenye mpango wa kugoma, ALIHUSISHWA NA AKAUKUBALI.
Kilichofuatia ni kutakiwa tujielezee kwa nini hatukwenda kwenye kipindi, tukajielezea, na hatimaye mimi nikapewa barua niliyoielezea hapo juu na tetesi za uhakika nilizo nazo ni kwamba mtu wa technical kapewa barua ya warning.
Kwa hiyo basi, kuondolewa kwangu hakuhusiani kabisa na suala la masilahi yaani mishahara. Kosa ni hilo hapo juu na tulilifanya kwa nia njema ya kujaribu kujenga zaidi kwa vile tunaamini Clouds inazidi kukua siku hadi siku.
Ni juu ya atakayesoma waraka huu kupima uzito wa kosa na uzito wa adhabu.Kwangu naona sawa kwa sababu si kila kinachotokea lazima kiwe na sababu za msingi. Bado mwenye mali ana mamlaka ya kuamua nani awe kwenye timu na nani asiwemo.Na ninaamini kila anayekosea lazima aadhibiwe,nami nimeadhibiwa na nimeheshimu. Maisha yanaendelea.
Namshukuru mungu na nawahakikishia wachache waliokuwa wakitusikiliza kwamba kamwe hatukuwahi kulewa sifa kwa sababu kama ni kulewa sifa tungeshagoma siku nyingi zilizopita kama suala lingekuwa ni mshahara. Kwa wenye kumbukumbu, Power Breakfast ilianza kama wake up show, enzi hizo kipindi kilikuwa kinaanza saa 11 alfajiri, maana yake ni kwamba mimi na Fina tulikuwa tunaamka saa 10 alfajiri, kwa mshahara wa kawaida kabisa na bado tuliweza kulibeba jahazi.
BC: Unawaambia nini wapenzi wasikilizaji wenu na wasikilizaji wa CloudsFm kwa ujumla?
KP: Nawaambia wasikilizaji wa Clouds na wasomaji wa Bongo Celebrity kwamba tuwe wepesi wa kukubali matokeo kama vile tunavyoweza kukikubali kifo kinapotutenganisha na wapendwa na tunaowachukia.Pia tuweze kukubali kwamba kila kitu kinajengwa taratibu. Hata waliobaki powerbreakfast wana vipaji na uwezo wa kukipeleka juu zaidi, kikubwa kinachohitajika ni subira yenu mnaowasikiliza, msijaribu kuwalinganisha wala kutafutia makosa. Mwisho wa siku mtazoea na mtafurahia.
Kwa upande wangu, napumzika kidogo, naelekeza nguvu zaidi kwenye katuni na kabiashara kangu kadogo. Pengine wakati umefika wa kuwekeza zaidi kwenye haka kabiashara.
Mwisho kabisa nawaomba radhi wale ntakaokuwa nimewakwaza kwa kuyaanika haya, ila kwangu ni kwa faida zaidi kwani ninapochora katuni nategemea wasomaji zaidi ambao ni watu, na ninapokuwa mmachinga wa nguo nategemea watu pia.Hivyo basi bila UFAFANUZI ni rahisi kwa watu hao ambao ni wasomaji wa katuni na wanunuzi wa nguo zangu kunishusha thamani kwa kudhani tumeacha Clouds kutokana na kudhani tumeshakuwa wakubwa hivyo basi tumeanza kuringa. LA HASHA!!!SIKUACHA CLOUDS, NIMETIMULIWA (nahofia kuuzungumzia mkataba wa Fina kwa kuwa una mambo yake haswa upande wa kisheria) NA SIJAPATA KAZI,ILA NINATAFUTA KAZI ILI WANANGU WAENDELEE KWENDA CHOONI. WALA SIJACHUKULIWA NA TBC, KWANZA UTUKUFU WALIONAO ZE COMEDY HATA ROBO SIJAUFIKIA.
Laiti nisingekuta mjadala kwenye blog ya Michuzi wenye kulaumu, kuponda kutoa pole na kutia moyo, kamwe nisingeyasema haya.Naomba kuwasilisha.
Note: BC inafanya juhudi kuwasiliana na uongozi wa Clouds FM kuhusu upande wao wa shilingi kuhusu suala hili.Tukifanikiwa tutawaleteeni mahojiano na mhusika/wahusika.
source;
http://bongocelebrity.com/2008/06/18/sijaacha-kazi-clouds-fm-ila-masoud-kipanya/#more-1530