OLE GUNNAR NA WOODWARD WAGEUKA MJADALA MZITO MAN UTD.
MANCHESTER, ENGLAND . HII Manchester United itawatoa watu roho. Juzi Jumapili, waliteseka sana uwanjani Anfield, wakapigwa 2-0 na Liverpool na baada ya hapo kila mtu anasema lake kwamba huyu hafai, yule hafai.
Beki na nahodha wa zamani wa miamba hiyo ya Old Trafford, Gary Neville kwa kauli moja amemshushia jumba bovu Makamu Mwenyekiti Mtendaji wa klabu hiyo, Ed Woodward kuwa hafai, anapaswa kuondoka haraka.
Neville alisema anashangaa kuona wamiliki wa Man United, familia ya Glazer wanaendelea kubaki na Ed Woodward mtu ambaye anaifanya timu hiyo kuwa ya kawaida kutokana na kufeli kwenye dili zake nyingi za usajili.
Neville alisema Woodward amekuwa akifanya dili za hovyo tu kwenye klabu hiyo kwa kushindwa kusajili wachezaji wa maana na matokeo yake Man United inakuwa na kikosi kichekesho ndani ya uwanja.
Baadhi ya wachezaji waliosajiliwa na Ed Woodward ni Angel Di Maria, Radamel Falcao Bastian Schweinsteiger, wakati wenzao kama Liverpool imewekeza kwa mastaa kama Mohamed Salah, Sadio Mane, Virgil van Dijk.
“Siuelewi kabisa huu uwekezaji wake anaofanya kwenye kikosi kwa kipindi cha miaka mitano, sita au saba sasa iliyopita,” alisema Neville.
“Niliona takwimu fulani wiki iliyopita zinasema kwamba Man United ni timu ya pili inayoongoza kulipa mishahara duniani. Sasa hiyo mishahara wanakilipa kikosi gani? Kwa kweli huyu mtu hapaswi kabisa kusamehewa. Hakika.
“Siwezi kubadili umiliki wa Manchester United, hakuna anayeweza kufanya hivyo. Lakini, nashindwa kuwaelewa hawa wamiliki wanafanyaje kazi na kiungo huyo anayeshindwa kujenga timu ya ubingwa tangu Sir Alex Ferguson alipoondoka. Ona kama hujapoteza kazi kwa kushindwa kufanya uwekezaji wa maana kwenye timu, basi kigezo tu cha kulipa mishahara mikubwa wachezaji wa hovyo ndani ya uwanja hilo linatosha kukuondoa kwenye kiti unachokaria. Lazima niseme, kuna kitu hakipo sawa.”
Wakati Neville akitaka Woodward aondoke, wenzake Roy Keane na Jamie Carragher walikuwa kwenye mjadala wa kuhusu Kocha Ole Gunnar Solskjaer kama anastahili kuendelea kukalia kiti hicho cha ukocha huko Old Trafford. Iliulizwa sana kama kweli Solskjaer ni sahihi kuendelea kubaki Old Trafford na hapo ndipo ulipoanza mjadala mzito, huku Patrice Evra na Graham Souness walibaki kuwa wasikilizaji tu wawili hao wakibishana.Keane alimuuliza Carragher: “Vipi kuhusu makocha waliopita, unasema kwamba nao walikuwa wahovyo?”
Carragher akajibu: “Klabuni Manchester United? Unadhani kwamba walifanya kazi nzuri? Mlimkosoa Mourinho wakati akiwa anainoa timu.”
Keane akajibu: “Lakini, Ole anahitaji muda zaidi.”
Carragher akauliza zaidi: “Anahitaji muda zaidi? Mlimpa muda zaidi Mourinho? Kwa kiwango cha timu yake ilichokionyesha Anfield mwaka juzi?” “Mechi ni kama hii tu. Tuhoji kama kama Ole kwenye ana CV za kuendelea kuwa kocha na zile sababu za wengine zilizowafanya aondoke,” Keane alijibu.
Carragher akamjibu: “Hiyo CV ya Ole ndicho kitu kinachotia wasiwasi.”
Sent using
Jamii Forums mobile app