Makapuku Forum

Makapuku Forum

SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA
SIMULIZI: ANTI EZEKIEL
MTUNZI: George Iron Mosenya

SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA

Akili ikanicheza upesi!! Kwa mbali kabisa nikaangaza sikufanikiwa kuiona sura ya Masawe wala dalili yoyote ya uwepo wake!! Upesi nikatoa simu yangu mfukoni, nikaitazama kana kwamba ilikuwa inaita nikapokea wakati si kweli kuwa ilikuwa inaita.
Nikajizungusha huku na kule kama ninayetafuta mtandao.
Nia yangu ikiwa kutazama kama naweza kuona chochote kitu kinachoendelea!!
Mlango wa duka ukafungwa!! Upesi nikaikumbuka kauli ya Masawe kuwa aliwahi kuchungulia ndani baada ya kutolewa nje! Nami nikajitia jeuri tena nisiyekuwa na hatia nikajisogeza mbele kwa kujiamini funguo zangu zikiruka hewani huku na kule.
Nikakifikia kile kibanda.
“Masaweee!!” nikaita kwa sauti ya chini!!
Kimya! Nikaita tena kwa sauti ya chini bado hapakuwa na jibu. Nikalisogelea lile gari niweze kuangaza kulikoni, nikajifanya natazama kama kuna mtu ndani yake niweze kumuulizia kulikoni mbona Masawe hajafungua duka.
Nilipolikaribia gari nikakutana na vioo vilivyovikwa utando mweusi ‘Tinted’ nikatamani kujua ni nini kinaendelea ndani!!
Nikachungulia!!
Lahaula!! Pua yangu ikagusa na kioo. Ving’ora vya dharula vikaanza kulia, hofu ikanitanda. Nikapagawa na kuamini kuwa wakati wa kuumbuka na kukamatwa ulikuwa umewadia, nikataka kukimbia lakini nikagundua kuwa ni upuuzi uliopitiliza. Sijaiba cha mtu, nimevaa kofia na miwani machoni, nikimbie nini.
Nikaamua kungoja atakayetoka niweze kumuuliza kulikoni!!!
Maajabu!!
Hakutoka mtu hadi king’ora cha dharula cha kwenye hiyo gari kilipokoma kulia.
Ina maana wapo mbali sana hao watu!! Ama ndo mambo ya ushirikina? Nilijiuliza mwenyewe huku nikisogea ule upande ambao Masawe aliutumia kuchungulia ndani siku ile aliyonisimulia!! Nilikuwa natetemeka sana lakini kitu ambacho sikutaka kufanya ni kupiga hatua nyuma!!
Kupiga hatua walau moja tu nyuma ningejidhihirishia ni kwa namna gani mimi ni muoga tena nisiyekuwa na uchungu na nafsi zilizopotea kimasihara!!!
Pia ningekuwa si mzalendo hata kidogo!! Kama Anitha alipotea akinipigania, mimi nikipotea kuna tatizo??
Nikajipa moyo na kupata nguvu mpya!!

Hakika! Hapakuwa na mtu ndani ya chumba kile, nikasogea karibu zaidi nikachungulia kwa ukaribu. Nikaangaza huku na kule bila mafanikio. Hapakuwa na mtu, wala dalili ya kitu chochote chenye uhai.
Wachawi hawa! Nikafikiria, kisha nikaanza kuondoka, nikajiweka mbali kabisa na eneo lile. Nilimwona Shanta kwa mbali alikuwa analalamika akitupa mikono huku na kule ma ajishike tumbo ma ra kichwa. Nikajua ni njaa zinamsumbua, nikachomoa pesa mfukoni na kumwonyeshea kuwa nitamwongezea nyingine akaendelea kulalamika huku akiniita kwa kutumia viganja vyote viwili vya mikono yake!! Kuna jambo alikuwa anamaanisha natakiwa kulifanya labda hasahasa nikiwa karibu yake lakini sikujali sana sikudhani kama lingeweza kuwa na umuhimu wowote ule kwangu kwa wakati ule ambao kila dakika ilikuwa na umuhimu wake.
Nikaenda upande mwingine ili nipate eneo zuri la kuweza kuona kila kona.
Nikalipata jumba bovu lisilotumika tena, baada ya aidha kubomoka ama ujenzi wake kuishia njiani.
Au ndo magofu ya Michigani haya!!! Nikajiuliza.
Nikajiweka pale na kuchungulia nini kinatokea kwa hao watu waliopotea kimaajabu ndani ya duka lile dogo kabisa la Masawe! Nilivuta subira bila kupepesa macho kona nyingine. Nilitaka kukata tamaa baada ya kungoja sana lakini nikakumbuka kitu!!
Subira yavuta heri!
Naam ile heri ikawadia hatimaye!! mlango wa kibanda cha Michigani ukafunguliwa!!
Wakatoka wanaume wawili, mmoja akiwa amevaa suti nyeusi, huyu alikuwa mweusi, na mwingine alikuwa……. Hakika alikuwa ni yeye, haikuwa mara ya kwanza kuonana naye.nisha kichwa chaka kama niliwahi kukiona mahali.
Hatimaye akageuka na hisia zangu hazikuwa potofu hata kidogo!!
Alikuwa yule mzungu, cheupe aliyehusika katika kumkamata mke wangu!!
Alikuwa ni cheupe dawa! Mtu ambaye niliamini kabisa kuwa anahusika katika kuniachia ujumbe wa ‘UTAMFUATA MWENYEWE’.. hakika alikuwa anajua, maana siku aliyomteka mke wangu ndo siku hiyo hiyo yule mtoto mtukutu Selemani alinambia kuna ujumbe upo ndani ya nyumba yangu. Na nilipomwagiza na yeye akakamatwa!!
Sijui walimpeleka wapi watu hawa wabaya!!!
Nilijihakikishia kuwa sijakosea, wakati nikiamini kuwa eneo lile wapo watu wawili, mara nikawaona wawili wale wakigeuka ghafla, na mimi nikageuka nao. Ana kwa ana na shanta wa ile gari. Alikuwa anaangaza huku na kule, bila shaka alikuwa katika harakati za kunifuata nilipokuwa!!
Cheupe dawa akamuita!! Shanta akababaika, lakini alivyoitwa na yule mwafrika akaenda huku dalili za uoga zikiwa bayana. Alifika nan kuzungumza nao kuna jambo walimuuliza lakini sikuweza kulisikia. Shanta akawa anaangaza huku na kule, bila shaka akinitafuta mimi. Sijui walimuuliza mimi nipo wapi ama?
Wakaongozana naye hadi jirani kabisa na gari yao.
Ghafla yule mzungu akamkwida, huku akitazama huku na kule, dereva akawa anarusha miguu huku na kule. Nilijisikia kutetemeka miguu, shanta aliyekuwa mkarimu kwangu alikuwa matatani sasa.
Nikataka kupiga mayowe lakini nikatambua kuwa nitakuza tatizo badala ya kulipunguza. Na ugumu zaidi ungekuja upande wangu!!!
Punde akamrusha ndani ya gari. Milango ikafungwa wote wakiwa ndani kisha ikatimua vumbi, kutoweka eneo lile ikiipita taksi yetu.
Nilibaki nimebung’aa nisijue nini cha kufanya.
Funguo mkononi!! Shanta katoweka, maskini labda walidhani kuwa alikuwa anawafuatilia!!
Kumbe na mimi wangenikuta ningeambulia kipigo na kukamatwa!!.....
Nusu saa baadaye nikiwa katika kuhakikisha kuwa wale watu wametoweka kabisa, na Masawe naye aliwasili, niliusikia mluzi wake kwa mbali kisha akatokea akiwa katika mwendo wake wa kusuasusa na hapo nikatambua kuwa alikuwa ana ulemavu mguu mmoja ulikuwa mfupi.
Kabla ya kufungua duka, alichukua kipande cha fagio na kuanza kusafisha eneo linalozunguka duka, huku akiendelea kupiga mluzi. Baada ya kuhakikisha kuwa Masawe hana walau muonekano wa kujua ama kutaka kujua kilichotokea humo ndani nikatokea mafichoni na kumkabili na asijue ni wapi nimetokea.
“Aisee nimekuja asubuhi sijakupata shehe wangu!!” nilimsemesha kwa lafudhi ya kichaga, akacheka kabla ya kunieleza kama nilivyoona. Kuwa bosi alikuwa na mambo yake!!
“Kwa sasa yupo wapi?” niliuliza ili nipate kujitoa mashaka na usalama wangu!!
“”Wameenda Mbeya huko, hapo safari maana huwa wanaondoka na ndege!!” alinijibu. Amani ikarejea kiasi lakini kuna mambo mawili yalikuwa ya msingi zaidi.
Kujali muda nilimalize hili tukio upesi na pili nitambue juu ya siri iliyopo katika kibanda kile.
“Kwa hiyo akiwa hayupo nani sasa anakusimamia hapa!!”
“Hata akiwepo hakuna wa kunisimamia” alinijibu bila wasiwasi.
“Maana mguu wangu hapa kwako nia yangu unisaidie kuingia mjini kunilangulia vifaa kadha wa kadha vya kazi. Si unajua mimi mgeni wasije kunipiga bei kali…” nilidanganya. Masawe akafurahi kuona kuwa ninamthamini, akazungumza mawili matatu kisha akaniuliza tunaongozana ama aondoke peke yake!!
Nikamwomba aondoke peke yake na mimi kama kuna uwezekano nijilaze kidogo, Masawe akaniruhusu kuingia katika kile kiduka ambacho thamani yake haikuwa ya kumwogopa mwizi.
Masawe akatoweka baada ya kumpa mahesabu ya uongo!
Aliponipa mgongo, nami nikaanza kufanya kilichonipeleka, nikatazama huku na kule bila mafanikio. Nikaituliza akili yangu na hatimaye nikaona kitu.
Tundu la funguo katikati ya makablasha ya kuwekea bidhaa, nikajaribu kuvuta pakawa pagumu kufunguka, nilijaribu tena na tena lakini bado hali ilikuwa ileile.
Nikachukua funguo zilizokuwa pale ndani lakini hazikufanania na tundu lile!!
Nguvu zikaniishia tena, nilitamani dakika za mwisho za uhai wangu ziishie ndani ya huo mlango ilimradi nijue tu ni kitu gani huwa kinaendelea katika maficho yale. Nilitaka kujua kitu kimoja tu, hiyo Michigani ni Michigani kweli? Na je inahusiana vipi na Anti Ezekiel??
Wakati nawaza juu ya ufunguo.. nikakumbuka kuwa kuna funguo nilipewa na Ezekiel Ubungo na kunisihi mambo kadha wa kadha. Nilipotazama kile kitasa hakika kiliendana na ule ufunguo!! Walau matumaini yakajengeka upya huku nikimshukuru Ezekiel kimoyomoyo!!
Lakini mara nikafadhaika!! Na ilikuwa lazima nifadhaike kutokana na kilichopita kwa kasi kichwani mwangu!!!
Nikakumbuka kuwa ufunguo ulipotea ukiwa ndani ya bahasha nyumbani kwa mama lao!!
Kazi ikawa ngumu zaidi!! Tena mpya!!

****

**TUNDU LIPO ufunguo hakuna……
**Kikwazo katika harakati!!!!
 
1469302210753.jpg
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI
SIMULIZI: ANTI EZEKIEL
MTUNZI: George Iron Mosenya

SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI

Aliponipa mgongo, nami nikaanza kufanya kilichonipeleka, nikatazama huku na kule bila mafanikio. Nikaituliza akili yangu na hatimaye nikaona kitu.
Tundu la funguo katikati ya makablasha ya kuwekea bidhaa, nikajaribu kuvuta pakawa pagumu kufunguka, nilijaribu tena na tena lakini bado hali ilikuwa ileile.
Nikachukua funguo zilizokuwa pale ndani lakini hazikufanania na tundu lile!!
Nguvu zikaniishia tena, nilitamani dakika za mwisho za uhai wangu ziishie ndani ya huo mlango ilimradi nijue tu ni kitu gani huwa kinaendelea katika maficho yale.
Wakati nawaza juu ya ufunguo.. nikakumbuka kuwa kuna funguo nilipewa na Ezekiel Ubungo na kunisihi mambo kadha wa kadha. Nilipotazama kile kitasa hakika kiliendana na ule ufunguo!!
Nikakumbuka kuwa ufunguo ulipotea ukiwa ndani ya bahasha!!
Kazi ikawa ngumu zaidi!!

****
Nilirejea kimaficho katika nyumba ya kulala wageni niliyokuwa nimefikia, lakini9 nikakumbuka kununua magazeti kadha wa kadha, nikatilia maanani gazeti la yule mzee Matata, mzee ambaye kwangu mimi alikuwa kama adui tayari.
“MZIMU WA SAM WAONEKANA DAR UKIZURURA”
Nilishikwa na hasira kuiona picha yangu tena katika kurasa za mbele za magazeti. Nikajikuta nakabiliana na donge la hasira kooni, nikakumbuka kuwa funguo nimepoteza tayariu ambazo zingenisogeza karibu na ukweli na sasa gazeti la kipuuzi la mzee Matata linaandika ujinga tena kuwa nimeonekana Dar.
Huyu mzee na shahada zake za kutosha bado anashikiliwa akili na wajinga wajinga hawa. Haoni uchungu mwanaye amepotea? Ama nd’o upendo uliopoa?
Ghafla nikavamiwa na wazo kuwa huenda Anitha alirejeshwa nyumbani kwao, na huu msala umebaki kuwa mzigo wangu mwenyewe!!
Wazo hili halikutaka kutoka kichwani mwangu hata kidogo!! Nikajiaminisha kuwa namuwaza mtu ambaye yu huru!!
Nd’o maana baba yake anaendelea kufanya upumbavu huu!!
Nilijihisi kutetemeka mwili mzima, huku lile gazeti mkononi mwangu nikiliona kuwa mzigo mzito sana tena mzigo wa miiba unaochoma kwa hasira.
Mwendo mfupi wa kuifikia ile nyumba ya kulala wageni niliona ni sawa na kilometa kumi. Nilitamani kukifikia chumba nikivamie kitanda na kujilaza. Sikuwa na la ziada.
Hatimaye nikafika chumbani, nikalifunua lile gazeti. Kama ilivyo kawaida ya wasiojiamini, akaandika kuwa habari ile imeandikwa na ‘MWANDISHI WETU’
Nikasonya kwa ghadhabu na kulichana vipande vipande gazeti lile, kisha nikalala! Bila hata kuvua viatu vyangu!!

HARAKATI ZA JOJINA DAR

Nilikuja kushtuka masaa kadhaa mbele, usiku ulikuwa umeingia tayari na sikuwa nimepata walau hamu ya kula, niliumiza sana kichwa nisijue ni wapi pa kuweza kuanzia tena ili niufungue mlango ule, nikajiuliza mara mbili zaidi na kukosa majibu. Nikaingia bafuni na kujimwagia maji huenda kuna jambo jipya limezibwa na uchovu wa mwili litajitokeza.
Hakuna kilichojitokeza. Nilishika hiki na kuacha kile labda nitapata ufumbuzi lakini sikuwa na ujanja wowote, nikafikiria juu ya kuchongesha funguo za bandia lakini ajabu hata ramani ya tundu lile sikuwanayo na haikuonekana kuwa kazi nyepesi kuchonga funguo zahali pale. Funguo za maajabu.
Simu yangu ya mkononi ambayo namba yake alikuwanayo Jojina pekee ilipatwa na uhai na kuanza kuimba! Nikaisogelea kwa hofu maana sikutarajia simu kutoka Dar es salaam niliamini Jojina alikuwa mwenye ghadhabu na labda hakutaka kusema nami lolote.
Naam hakuwa mwingine aliyepiga simu ile.
Alikuwa Jojina!
“Nambie Mama lao…” nilimuanza kiutani ili kama ana jazba azitulize kidogo
“Safi tu Sam vipi ulikuwa umelala tayari.” Alinijibu kwa uchangamfu, ile saauti yake ya kimahaba ikanituliza woga wangu.
“Hapana nilikuwa bafuni ….”

Nikajirusha kitandani na kujilaza simu sikioni niweze kusikia Jojina ana lipi jipya!!
Alinieleza mambo kadha wa kadha kuhusu uwepo wake jijini Dar na mimi nikamweleza juu ya hali ya hewa ya Iringa, kisha akachukua nafasi kuel;ezea nia ya kunipigia simu usiku ule pasi na matarajio.

JOJINA.

SAM, kwanza sahau kuhusu yaliyopita, nadhani tulipishana lugha tu, nilipokukosea nisamehe nami nishasamehe uliponikwaza. Sam ni siku kadhaa hatujazungumza na ni kama siku yangu ya nne ama ya tano huku Dar es salaam. Kubwa zaidi la kukupigia hii simu ni kwamba hatimaye nikafanikiwa kuonana na mzee Matata. Sam yaleyale ya mzee Madati kurukwa akili ndo huku pia lakini afadhali huyu hajawekewa madawa lakini kupotea kwa mtoto wake kumemchanganya sana. Nilipofika kule mara ya kwanza nilizuiliwa kuingia eti kwamba mzee hatakiwi kuonana na watu madaktari wamekataza.
Nikaondoka kapa siku hiyo! Lakini sikufa moyo.
Sikukata tamaa Sam. Mara ya pili nikajieleza kuwa shida yangu kuonana na mzee ni kuhusu mwanaye. Wacha wee! Hapo sasa nikaonekana lulu mchangani, kila mtu ananiuliza kulikoni. Nikagoma kusema lolote hadi niongee na mzee. Kama yeye atawaeleza ni juu yake! Lakini mimi simwelezi mtu tofauti na yeye, na kama sitaruhusiwa siku hiyo basi tena hawataniona mimi kukanyaga pale nyumbani kwao.
Sam niliyasema haya huku natetemeka, maana najua kuwa maaskari watakuwa wameshirikishwa juu ya jambo hili, hivyo wakisikia kuna mtu anajua wanaweza kumweka kizuizini ili asaidie upelelezi. Nikaamua kujitoa muhanga huku nikiamini kuwa Mungu anamshika mkono mwenye haki.
Ama kweli damu nzito kuliko maji!!
Mzee akaelezwa nikakubaliwa kuingia japo walinionya kuwa ana tatizo la kubadilika badilika yule. Sikujali kuhusu hilo nilichotaka kuonana naye kwanza.
Sam, yule mzee amekwisha na hapa sasa naamini alikuwa akimpenda sana mtoto wake, yaani amekuwa dhaifu sana. Akanikodolea macho nami nikajiweka sawa, tulikuwa wawili tu, nikaanza kumweleza kilichonileta hadi pale, nikamsimulia baadhi ya matukio hadi ujio wa Anitha Iringa, sikukutaja wewe hata kidogo kwanza, nikadanganya kuwa alikuwa amekuja kufanya biashara huko.
Nikamwelezea juu ya mikasa ya ajabu ya Anti Ezekiel mjini Iringa. Mikasa ambayo inasemekana kuwa ni ya kishirikina ama mauzauza mengine!
Hapo akakodoa macho yule mzee, na kwa mara ya kwanza akasema na mimi. Kumbe na yeye ni mtu wa Iringa ni Mbena yule mzee. Hapa tukabadili lugha tukahamia katika kabila, nikasema naye kibena. Ushirikiano ukawa mkubwa sana tukawa marafiki.
Nikamweleza kuwa nauhitaji sana msaada wake maana hata mimi nimepoteza mtoto na kuna mwenzangu familia yake yote inateketea. Kufikia hapa nikaona hakuna haja yoyote ya kuendelea kuficha siri hii ilhali mzee ameonyesha ushirikiano na nilichokisema hakikuwa katika maandishi ningeweza kukibadili muda wowote ule!!!
Nikamtajia jina lako, sikumpa nafasi ya kusema lolote bali nikamlaumu kwa kutotaka kukusikiliza nikamweleza juu ya tuhuma unazozushiwa na watu wabaya na nd’o haohao wamemchukua mtoto wake. Kufikia hapo nikamweleza kuwa Anitha alikuwa katika harakati za kukusaidia wewe na wao wakagundua nd’o wamemshikilia.
Macho yakamtoka mzee na akatoa ushirikiano!!
Akakiri kuwa kuna watu walikuwa wakileta taarifa zile ofisini, na hakujua kama ni watu wabaya. Nikamuonya asithubutu kumweleza mtu yeyote juu ya hili maana hao watu ni hatari, wakigundua umewajua tu wanaanza kukuonya kimatendo, mzee akakiri kuitambua skendo hiyo ya UKIMJUA UNAPOTEA. Akajionya!!! Aliwahi kuisikia Iringa miaka hiyo!!
Kumbe ni mchezo wa miaka mingi tu huu Sam!! Na bado umefumbiwa macho. Anti Ezekiel ni nani hadi alibabaishe taifa letu!! Yeye ni nani katika ardhi hii huru??

Baada ya mazungumzo marefu tukapanga mikakati kabambe! Mkakati wa kumvumbua huyo Anti Ezekiel.
Mzee alichangamka na hakuna hata ndugu mmoja aliyeweza kuamini kuwa yule alikuwa mzee wao.
Leo asubuhi mikakati hiyo imeanza kufanya kazi!
Gazeti la mzee Matata limeandika taarifa zako kuwa umeonekana maeneo ya Dar es salaam mjini ukizurura.
Nia yetu kubwa ni kuwavuta hawa watu waje huku ili tuweze kushughulika nao vyema. Baada ya taarifa hiyo ofisi ya mzee Matata ikapokea simu kutoka kwa watu wanaojiita wapelelezi kutoka Iringa, mmoja akazungumza Kiswahili na mwingine akasema kiingereza. Wakadai wanahitaji kuonana na huyo mtu aliyekuona wewe waweze kujua wapi pa kuanzia ili kuujua ukweli, walilalamika kuwa wao wanaamini umekufa hivyo uzushi kama huo unashusha thamani ya utendaji kazi wao.
Kufikia hapo mzee Matata ameniamini sana na kujua ni kweli kuna jambo linafichwa nyuma ya pazia..
Hao mabwana wakawasili kutoka Iringa na kukutana na watu wa mzee Matata, ni mzungu mmoja na muafrika na wamekuja na gari binafsi aina ya Nissan patrol! Kwa leo wametoa tu salamu, kesho watakuwa ofisini kwa mzee Matata, japo mzee hatakwenda amewaambia wakitoka huko wamtembelee nyumbani kwake.
Kwa hiyo Sam hapo nd’o tumefikia!!
JOJINA AKAMALIZA.,

Nilikuwa natetemeka sana, ilikuwa ni sababu ya baridi pamoja na uoga tele huku kihoro cha matumaini kikinipagawisha. Mwanzoni nilikuwa na hasira wakati namsikiliza mama lao kwa sababu nilihisi mzee Matata ni mnafiki na anamhadaa lakini kumbe ile habari gazetini imepikwa maksudi ili kuwaweka karibu maadui kuwa marafiki ili shambulizi likifanyika wawe katika taharuki bila matarajio wala maandalizi ya kujikinga!!
Watu waliotajwa nilikuwa nimewaona asubuhi hiyohiyo katika kijumba cha Michigan!!
Cheupe dawa na yule mwenzake wapo Dar tayari.
Nikamweleza Jojina juu ya mkasa wangu kwa ufupi sana, nikamwelezea juu ya watu hao na jinsi wanavyoishi kimaajabu katika kibanda cha Michigan. Nikamwelezea kila nilichofanya hadi kufikia hatua ya kukuta tundu la kufunguliwa na funguo. Sikusita kumhakikishia kuwa cheupe dawa huyo ndiye aliyemkamata mke wangu jijini Dar…
“Jojina, tumekaribia kulipata jibu lakini kuna kitu kimoja ambacho kinanipa utata na kuniumiza kichwa, sehemu ya kufungulia geti la kuingia katika maficho yao imeonekana tayari na ninaweza kujua namna ya kupaingia tena. Lakini Jojina funguo hakuna Jojina, ile bahasha tuliyopoteza katika chumba chako kwenye operesheni mbwa okoa, ndani yake kulikuwa na funguo!!
Ni hizo na ninao uhakika kuwa Ezekiel alimaanisha kitu aliponipatia zile funguo!!
Nilimaliza kuongea nikamsikia Jojina akishusha pumzi zake kwa nguvu sana. Ni kama alikuwa ameungana nami katika kukata tamaa.
“Kweli huo ni mtihani mgumu, lakini Sam unakumbuka kuwa kila jaribu linalokuja kwa mwanadamu huwa linayo njia yake ya kutokea? Basi amini kuwa hata kikwazo hiki tukakiruka. Kama unaweza kwenda tena kwa huyo Masawe basi hakikisha kuwa unachukua alama ya hilo tundu ili tuweze kuchonga ufunguo wa bandia…….” Alianza kushauri Mama lao. Nikaingilia kati na kumweleza kuwa kile kitasa ni cha aina yake na hata ule funguo ulikuwa wa aina yake. Mama lao akasihi kuwa ni heri kujaribu kuliko kupuuzia.
Nikakubaliana naye, lakini kila nilivyoujengea picha ule ufunguo chakavu alionipatia Ezekiel na umbo lake la kustaajabisha niliamini kabisa kuwa zile zilikuwa mbio za sakafuni tulizokuwa tunajaribu kukimbia.
Lazima ziishie ukingoni tu!!
Tukaagana na mama lao, na kuahidia kupeana matokeo kwa siku inayofuata.
Huo ukawa usiku wenye matumaini kiasi fulani, lakini sikujua kama asubuhi ya siku inayofuata ingekuwa asubuhi ya kustaajabisha ndani ya jiji la Dar es salaam na wakati huo mjini Iringa!!!
Ni heri tusingefikia maamuzi yale!!
Lakini hatukujua!!!

***

**HARAKATI zinaendelea kushika kasi!! Je uwepo wa Matata utaleta unafuu ama utata mpya??
***SAM atafanikiwa katika harakati za kuupata ufunguo kwa kuchonga??
**Hii ni ya jana..... Itaendelea tena kesho saa KUMI KAMILI
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU
SIMULIZI: ANTI EZEKIEL
MTUNZI: George Iron Mosenya

SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU


“Kweli huo ni mtihani mgumu, lakini Sam unakumbuka kuwa kila jaribu linalokuja kwa mwanadamu huwa linayo njia yake ya kutokea? Basi amini kuwa hata kikwazo hiki tukakiruka. Kama unaweza kwenda tena kwa huyo Masawe basi hakikisha kuwa unachukua alama ya hilo tundu ili tuweze kuchonga ufunguo wa bandia…….” Alianza kushauri Mama lao. Nikaingilia kati na kumweleza kuwa kile kitasa ni cha aina yake na hata ule funguo ulikuwa wa aina yake. Mama lao akasihi kuwa ni heri kujaribu kuliko kupuuzia.
Nikakubaliana naye, lakini kila nilivyoujengea picha ule ufunguo chakavu alionipatia Ezekiel na umbo lake la kustaajabisha niliamini kabisa kuwa zile zilikuwa mbio za sakafuni tulizokuwa tunajaribu kukimbia.
Lazima ziishie ukingoni tu!!
Tukaagana na mama lao, na kuahidia kupeana matokeo kwa siku inayofuata.
Huo ukawa usiku wenye matumaini kiasi fulani, lakini sikujua kama asubuhi ya siku inayofuata ingekuwa asubuhi ya kustaajabisha ndani ya jiji la Dar es salaam na wakati huo mjini Iringa!!!
Ni heri tusingefikia maamuzi yale!!
Lakini hatukujua!!!

***

ASUBUHI baada ya stafutahi ya wastani nilijongea katikati ya mji huku na kule nikitazama hiki na kile na hatimaye nikapata mahali ambapo wanachonga funguo. Nikawaeleza shida yangu, wakanielewa na kunitaka nilete alama ya tundu la kitasa ambacho nahitaji kuchonga funguo zake.
Wakanieleza kuwa alama sahihi nitaichukua kwa kutumia kipande cha sabuni.
Nilipotoka pale moja kwa moja nikaenda dukani kwa Masawe.
Alinipokea kwa furaha zote, alikuwa anatabasamu pana ambalo bila shaka lilionyesha dalili ya tumaini jipya!!
Akanisabahi kisha akanihoji kuhusu kutoweka kwangu siku iliyopita bila taarifa.
“Kwanza nilivyokuagiza ulivipata?” nilipoteza uelekeo wa swali lake.
“Sijakosa hata kitu kimoja ati! Vyote nimepata tena kwa bei poa tu!” alinijibu huku akisahau kuwa sijamjibu swali lake la awali!!
Nikataka kutia neno, Masawe akaendelea kuzungumza.
“Nikaona nom asana kuviweka humu ndani maana bosi angevikuta ingekuwa kesi, hachelewi kusema kuwa namwibia. Vipo hapo kwa jirani yangu mmoja…..”
Neno la mwisho la Masawe likanipa mwanga na akili ikafunguka!! Huo ulikuwa mwanya mwingine wa kuweza kufanya jambo.
Nikamsihi aende kuleta vitu baadhi alivyonunua niweze kuvitazama.
Masawe akatoweka akiliacha duka lake wazi. Mguu wake ukitokomea mimi nikaingia ndani ya kile kibanda, moja kwa moja katika lile tundu la funguo. Nikailowanisha sabuni kidogo kutoka katika duka la Masawe kisha nikagandamiza na kuipata alama kama walivyonielekeza mafundi.
Nikaifunika ile sabuni na kuitia mfukoni.
Masawe aliporejea mimi sikuwa na habari, nilichokitaka nilikuwa nimekitimiza tayari.
Mazungumzo kati yetu niliyaona kama kelele tu zinazonisumbua masikio, nikamzuga Masawe kuwa nimepigiwa simu fulani. Nikampa pesa kidogo na kumshukuru kwa wema wake wote. Nikatoweka nikiwa katika haraka, nikapita huku na kule nikachukua taksi.
Nikamwelekeza dereva wapi pa kunipeleka.
Akatia gari moto na kuanza kuitafuta sehemu.
Dereva huyu alikuwa muongeaji sana, akanieleza juu ya jaribio la wizi wa taksi lililofanywa na shanta mmoja akishirikiana na mteja wake. Akanielezea gari ilipokutwa!!
Nikatambua anaizungumzia gari ambayo niliitumia siku iliyopita nikiwa na shanta aliyeingia matatani na kisha kutoweka. Nikajifanya kushiriki katika maongezi yale lakini nilikuwa katika kumchimba tu nipate mawili matatu kuhusiana na na usalama wangu!!
Hali ilikuwa shwari hakuna hata mmoja aliyebahatika kukumbuka walau nguo nilizokuwa nimevaa!!!
Alinifikisha nilipohitaji nikamlipa chake na kuingia katika harakati za kuusaka ufunguo.
Nikawaonyesha wale mafundi alama ya tundu lile, wakalitazama kwa makini na kukiri kuwa hawawezi kutengeneza huo funguo na badala yake wakanielekeza kwa mzee Sendeu. Mkongwe katika kuchonga funguo za kila aina. Hata hao mafundi walikiri kuwa alikuwa kiboko yao na walimkuta katika ufundi huo.
Nikaongozwa hadi katika kibanda chake kidogo!! Akanipokea vyema na kisha tulipobaki wawili akabaki kunisikiliza. Wakati nazungumza niligundua kitu, kuwa mzee yule hakuwa na amani sana na ile miwani yake usoni haikuwa ya heri sana. Nikajipa jibu kuwa huenda huwa anawachongea majambazi funguo bandia maalum kwa shughuli zao, ama la yeye mwenyewe si mtu mwema.
Lakini hayo yote hayakuwa yakinihusu hata kwa mbali, kilichonihusu ni kuupata funguo wangu kwa ajili ya manufaa yangu!!
Nikamweleza shida ileile na kisha kumpa ile sabuni yenye alama.
Ama! Akaiachia ghafla ile sabuni!! Ikaanguka chini, akataka kutoa miwani yake usoni akasita. Akapigwa na bumbuwazi la waziwazi usoni!!
Nikaduwaa zaidi yake!! Na wala hakujishughulisha katika kuiokota ile sabuni!!
“Wewe ni nani? Aliniuliza… nikakosa cha kumjibu na nisijue nini maana ya swali lake. Nikiwa bado naduwaa niliona akibonyeza namba za simu lakini hakuzungumza chochote kile, uso wake ulitawaliwa na ghadhabu!! Nilitaka kuondoka lakini nikajiuliza ni kwanini niondoke. Yawezekana kukutana na mzee yule ni njia mojawapo ya kuifikia siri kuu!! Na mbaya zaidi kuondoka kwangu kusingesaidia chochote kile.
Lakini kubaki na mtu nisiyemjua hili lilikuwa tatizo zaidi.
Nikaamua kusimama niweze kuondoka!! Akabonyeza tena simu yake.
Milango ikajifunga tena!!
“Wewe ni nani nakuuliza??” sasa alikuwa ametoa miwani yake usoni na alikuwa anakanisogelea!!! Nikajaribu kurudiu nyuma.
Mzee alikuwa na miguu ya bandia na hata jicho lake moja!!
Hakuwa na jicho moja!!!
Alitisha kumtazama.
“Naitwa Dickson naitwa Dickson mzee wangu….” Nilijikuta nalainika na kujibu alichouliza japokuwa nilikuwa nadanganya.
Nilidhani jibu lake litamfanya aweze kutulia, lakini mara akaurusha mkono wake. Nilikuwa sijajiandaa kwa tukio hilo, kiganja chake kizito kikatua katika shavu langu.
Naam!! Maumivu makali haswa yakasambaa katika uso wote na kichwa kikakumbwa na maumivu!!
Hakuishia pale yule mzee wa kutisha.
Mara akarusha gongo alilokuwa anatumia, hata hili pia sikulitarajia lakini sijui ilikuwaje nikawahi kujikinga uso wangu. Likanikung’uta mikononi. Maumivu mapya kabisa.
“Kwa hiyo nd’o mnataka kuniua eeh!!” akatokwa na kauli hiyo. Sasa alikuwa ameikamata shingo yangu.
Uso wenye jicho moja ukawa unatisha zaidi ulipokuwa karibu nami!!
“Nilitamani kusema neno lakini alikuwa amenikaba haswa! Macho yakamsihi lakini ni kama hakutambua hilo.”
“Kindo na mwenzake wapo wapi?” aliniuliza swali lile huku akiamini kuwa jibu ninalo basi tu ni kiburi.
Akaniachia ghafla nikawa nakohoa kwa fujo!!
Na hapo akatoa kisu kikali sana.
“Usipojibu maswali yangu nakufanya kama nilivyofanywa, nang’oa jicho, nakata miguu na masikio, nakung’oa na hiyo pua yako mwanaharamu wewe…” Akazungumza haya huku akitetemeka.
“Naitwa Sam mzee wangu, hakuna nijualo kuhusu hayo unayoniuliza niamini mzee wangu sijui lolote na mimi ni mtafutaji tub ado sijapata chochote.” Nilizungumza huku nikitokwa machozi.
Akanisogelea kwa kuchechemea, akanifikia.
“Unataka kufa eeeh!!” akasema kwa sauti ya chini inayosihi.
“Bonge waitio amekutuma kitu gani kwangu? Na nd’o nani huyo bonge waiti…..” akaniuliza tena, ni kweli niliwahi kuyasikia hayo majina mahali lakini sikuwa na maelezo yoyote ya kuweza kujibu.
“Mzee wangu, nipe dakika tano tu za kujieleza kinaga ubaga na baada ya hapo nitakuruhusu unifanye utakavyo iwapo tu itakuwa ni haki yangu kuuwawa kinyama namna hiyo. Na kama ikithibitika mimi ni mtu mbaya mzee wangu, usisite kunisulubu. Lakini amini kuwa ukifanya suluba hiyo bila kunisikiliza basin a kilio changu kiwe juu yako milele.” Nikajitutumua na kutokwa na kauli ile ya mwisho ambayo sikutarajia inaweza kuwa chachu ya kutuliza munkari ya yule mzee mwenye jicho moja!!
Kwa ishara ya kichwa akanipa nafasi ya kuzungumza!! Kisu kikiwa mikononi mwake imara.
Huo haukuwa wakati wa kuficha siri tena, nilikuwa katika dakika za mwisho za uhai wangu.
Nikamweleza mzee juu ya uhalisia wa jina langu, wapi natoka na kisha nikamweleza juu ya kukutana na kijana shoga aitwaye Ezekiel jijini Dar es salaam, nikakumbuka kumwelezea mwonekano wa Ezekiel na sikusahau tarehe za kukutana kwetu.
Nikagusia juu ya utata wa Ezekiel wa Ubungo na yule maiti wa Temeke Dar es salaam.
Sikuuyumbisha ukweli nikamweleza juu ya mke wangu kupotea na kisha mimi kuanza kuzushiwa juu ya mambo kadha wa kadha ikiwemo kifo.
“Wewe kumbe nd’o Samson….. Sam….” Alitokwa na maneno yale mzee huku kisu kikiwa kimemtoka tayari. Alikuwa ameduwaa haswa.
Mara akafungua makablasha kadhaa akatoka na magazeti kadha wa kadha, akachomoa mojawapo. Akakutana nna habari yangu, akaitazama ile sura na kujihakikishia kuwa sikuwa nimemdanganya hata kidogo.
“Sam… umewakwepa vipi hadi sasa hawa watu wasijulikana sura zao” aliniuliza huku akinisaili kwa chati.
Sikuamini kama uso wa yule mzee unaweza kulainika na kuwa katika masikitiko kiasi kile.
Sikuwa na uwezo wa kujibu chochote kile. Ni kama nilikuwa ndotoni tu!!
Mzee akajishughulisha zaidi akachukua pamba na kunifuta damu mdomoni, kisha akaniomba niketi tuzungumze.
Mzee Sendeu!! Akanielezea juu ya mkasa wake. Mkasa uliowahusisha Kindo na mwenzake ambaye hakuwa akimtambua jina lakini alikiri kuwa sura yake na ya huyo Ezekiel niliyemtaja ni kitu kimoja!!
“Wale vijana waliniletea tenda ya kutengeneza funguo, hakuna funguo iliyonitia wazimu kama ile pale. Kila nikijaribu kutengeneza wanaenda na kurejea wakidai haifungui ule mlango. Natengeneza tena na wao wanalipa pesa nzuri tu… nikakataa tenda zote nikabaki na tenda moja tu ya kutengeneza ule funguo wa ajabu. Kila nilipowasihi waende kunionyesha kitasa wakadai kuwa ni mbali sana. Kwa sababu ni wao walikuwa wanasema basi mimi nikaendelea kukuruka huku na kule nifanikishe kuwafurahisha wateja wangu.
Mara ya mwisho kuonana nao wote kwa pamoja ilikuwa ni siku ambayo walidai kuwa walau ule funguo unazo dalili za kufungua japo kwa kulazimisha.
Baada ya hapo wakatoweka moja kwa moja!! Na hapo nikaanza kuandamwa na watu nisiowajua wakinihoji juu ya mambo nisiyoyajua vilevile.
Siku moja nikakamatwa na polisi, lakini sikupelekwa rumande nikafungwa kitambaa usoni na kwenda kukutana na mtu aliyeitwa bonge waiti. Alikuwa anazungumza kiingereza na walitafsiri nami nikawa najibu.
Yule mtu akaniomba funguo! Nikasema sijui lolote juu ya funguo. Ebwana walinishushia kipigo cha hali ya juu sana ndugu yangu!!
Nakuja kupata fahamu nikiwa porini huko, mguu mmoja haufanyi kazi, na jicho moja likiwa halioni, meno yote haya ya mbele unayoyaona ni ya bandia sina meno Sam. Wale watu ni zaidi ya majasusi na sijui niliweza vipi kupona kutoka katika kifo kile.
Niliokotwa na mmoja kati ya majangili ambayo huwa nayatengenezea funguo kwa ajili ya kwenda kuvamia wanapojua wao. Tena waliniokota wakiwa katika shughuli zao za kijangili.
Wakanichukua hadi katika machimbo yao.
Amakweli tenda wema uende zako bila kuangalia ni nani ulimtendea wema. Wale watu walimtafuta daktari na kunipatia tiba, mguu ulikuwa si mguu tena ukakatwa, jicho haliukuwa jicho tena likang’olewa na kubaki na jicho moja.
Nilikuwa naitwa Masta key kabla sijatekwa na kupotezwa, basi nikalazimika kufuga ndevu tele na kisha wale majangili wakanitengenezea maficho haya niendelee na shughuli zangu nikiwa katika usalama wa hali ya juu. Na hapo wakaniita mzee Sendeu. Na hilo nd’o jina langu maarufu kwa sasa.
Watu wanaamini kuwa mimi ni mrithi wa Masta Key ambaye wanadai alitoweka kishirikina.
Hawajui kuwa nd’o mimi hapa.
Sasa leo ulipouleta ufunguo ulionisababishia majanga haya nikakuona kuwa wewe naye ni mmoja wa watu wabaya wanaofahamu siri yangu!! Sam kiuhakika nisingekutambua basi ungekufa kifo kibaya sana leo.” Alimaliza mzee yule kunieleza juu ya simulizi ile ya kutisha na kusisimua.
Mwili ulisisimka haswa nikijaribu kujenga picha juu ya mwanadamu kung’olewa jicho na kukatwa mguu.
Watu ninaokabiliana nao walikuwa wanyama haswa!!!

Wakati nikiendelea kufikiria juu ya tukio hilo la maajabu. Mara katika simu yangu ukaingia ujumbe!!
Hakuwa mwingine alikuwa ni Mama lao..
“SAM HALI SI SHWARI MZEE MATATA MATATANI”
Nilichoka!!!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom