PREMJI KANOON aliteremshwa kutoka katika kile kiti akakanyaga chini kwa miguu yake na moja kwa moja akaingia kwenye kijimlango kidogo na kujifungia. Akateremshwa chini ya ardhi ambako kulikuwa na kasri lake lisilo na bugudha. Alipofika tu akapewa huduma zote zilizomstahili ikiwa pamoja na kukandwakandwa mabegani, kuoshwa miguu kupakwa mafuta ya kunukia katika nyayo zake na amambo mengine mengi. Chumba chote kilinukia udi, aliinuka na kusogea karibu na sanamu moja lenye ukubwa wa wastani, akainamisha kichwa chake huku akiwa kabana viganja vya mikono yake kifuani kwa uchaji wa hali ya juu. Sekunde kadhaa akamaliza na kutoka eneo hilo huku akimwagiwa maua mazuri ya kunukia naye akakanyaga juu yake.
Hatua chache akalifikia sanamu linguine, akasimama mbele yake na lile sanamu likasogea pembeni taratibu, akapita na likarudi mahala pake. Kilikuwa chumba kidogo chenye giza, kikamteremsha chini zaidi na huko akaingia kwenye ukumbi wa wastani uliokuwa uking’azwa kwa taa zinazobadilisha rangi. Akaketi kwenye kiti kimoja kikubwa kilichokuwa nyuma ya meza kubwa yenye nakshi za kupendeza. Mbele yake kulikuwa na watu wane, vijana wakakamavu wenye miili ya wastani, vichwani mwao walivaa vilemba ambavyo viliwatambulisha kuwa wao ni Singasinga.
Akajikohoza kidogo na wale vijana waliendelea kusimama pale wakiwa kimya kabisa. Pancho Panchilio au wao wanamwita Premji Kanoon.
“Sina lingine, nataka auawe au wauawe,” akasema.
Wale jamaa wakaitikia kwa vichwa tu, hawakuongea lolote; pembeni yao kukatokea picha kubwa ya Amata.
“Mnamwona huyu?” akawauliza, wote wakageuka na kuitikia kwa vichwa.
“Mna uhakika ndiye mliyemwona uwanja wa ndege?”
Wakajibu tena kwa vichwa.
“Vizuri, sasa nataka auawe mara moja yeye na Yule wa mwanzo, watu wa jamii kama hii hawafai kuishi kwa sababu huaribu mipango ya watu. Sikilizeni, huyu mnayemwona kwenye picha ni mtu hatari sana, mnapokwenda kumshambulia hakikisheni mmejipanga vizuri, mnanielewa?” akawauliza.
“Ndiyo, tunakuhakikishia jua la kesho hawezi kuliona kamwe!” mmoja aliyesimama mbele ya wenzake akajibu kwa ushupavu. Zile taa zikazimika na Pancho akapotea kwenye milango yake ya siri.
† † †
MKESHA WA DIWALI
“Kamanda Amata!” SaSha akaita kwa sauti ya chini.
“Niambie motto mzuri,” Amata akajibu.
“Unalala hapa siyo?”
“No! natoka sasa maana usiku huu tuna kazi ya kufanya. Kesho uje pale Grand Hyatt Hoteli, utanikuta,” kamanda akamwelekeza.
“Mmmmm! Nikikufumania maana wewe huwezi kulala bila mwanamke,”
“Acha uongo,” akamjibu huku akijinasua kutoka katika mikono ya SaSha iliyokuwa imembana pale kitandani, akaingia bafuni na kujiweka sawa, alipojitumbukiza ndani ya suti yake na kutokomea nje ya jengo lile.
“Swiiiiiiiiiih!” sauti ya mruzi ilimshtua Amata akasimama na ghafla gari moja ikatokea mbele yake na kusimama.
“Twenzetu kumekucha!” Ilikuwa sauti ya Chiba, akajipakia garini na wakaondoka kwa kasi.
“Kamanda tuko matatani, jamaa wamejipanga wanajua kama upo hapa, nilichofurahia ni kuwa wanakuzungumzia wewe na hawajui kama mimi niko hapa,” Chiba akaeleza huku akiongeza kasi ya gari yake.
“Asee, watakuwa wamejuaje kama niko hapa?”
“Ah hapo ni sehemu mbili tu ama uwanja wa ndege au hotelini, watu kama hawa huwa na macho mengi na masikio kila mahali,” Chiba akaongea harakaharaka.
“Sasa Chiba na sisi tugeuze kibao, kazi yetu tuifanye leo hii hii usiku tukichelewa kitanuka, maana wanaweza kusali wale tukageuka panya kwenye nchi ya watu,” Kamanda akaongea huku akijiweka vizuri kitini,
“Twende hotelini, nikachukue begi langu niliweke humu garini maana kuanzia sasa kambi popote”.
Chiba akakunja kona kali na kujikuta kapita katika taa nyekundu, honi za magari zikasikika kila upande, lakini hakusimama akakanyaga mafuta na ile gari ikazidi kuunguruma kwa nguvu.
HOTELI YA GRAND HYATT
GIZA LILIKUWA likishindana na taa za umeme zilizopendezesha jingo hilo la hoteli. Siku hiyo ambayo ilikuwa ni usiku wa kuamkia sherehe kubwa sana kwa dini za Kihindi ulijawa na watu wengi. Wale waliopenda ibada walienda mahekaluni na wale waliopenda starehe walienda kwenye makasino.
Gari moja ndogo nyeusi ikaegesha katika maegesho na vijana wawili wakateremka, vijana hawo wenye mandevu na maviremba vichwani mwao hawakuwa na la kuongea wala kusalimiana na yeyote waliomuona. Mmoja wao akainua simu na kupiga, akaongea maneno machache na kuiweka mfukoni ile simu kisha akauendea mlango mkubwa wa ile hoteli. Moja kwa moja alisimama mbele ya kaunta na kubadilishana maneno kadhaa na mhudumu aliyekuwa hapo na kutoka kuelekea kunako lifti za kupanda juu.
Yule mwenzake alibaki kwenye makochi ya mapokezi akivuta gazeti hili na lile, mtego.
† † †
“Chiba wewe nisubiri upande uleeee, mi naingia kutoa begi tu napitia mlango wa nyuma kisha tunaondoka bila kuaga,” Amata akamwambia Chiba wakati akiufunga mlango wa gari hiyo na kumwacha Chiba akiondoka taratibu kuelekea upande wa pili wa ofisi hiyo. Amata akavuta hatua za nusu kukimbia na nusu kutembea, akazikwea ngazi na moja kwa moja akaifuata kaunta na kukaribishwa na yule binti wa jana yake, Sukaina.
“Ndiyo mrembo! Ujumbe wangu wowote?” akauliza.
“Ujumbe wako nimekupelekea chumbani tayari,”
“Sasa mbona hukusubiri hukohuko unikabidhi?” Amata akaanza maneno yake ya ubembe.
“Mmmm na wewe, tangulia nakuja,”
“Waja kweli au ndiyo kunipaka mafuta kwa mgongo wa chupa?”
“Naja kweli we tangulia dakika kumi nitakuwa nimefika maana ndiyo nafunga ofisi natoka. Nikukute kitandani sawa bebi?” Sukaina akarusha maneno ya kumlegeza Amata huku akijuwa wazi kuwa ni kitu gani kitakachomtokea kijana huyo. Yule jamaa aliyekaa pale kwenye kochi akamwoneshea ishara ya dole gumba Sukaina na kunyanyuka taratibu kuelekea kule ndani alikoenda Amata.
Kamanda Amata alibofya kitufe cha kuiita lifti lakini alihisi vinyweleo vyake vikisimama na mwili ukisisimka, akarusdi nyuma hatua mbili na kugeuka akapanda kwa ngazi za kawaida mpaka ghorofa ya nne kulikokuwa na chumba chake. Alipoufikia mlango, akautazama juu hadi chini, kisha akatupa jicho pale kwenye kitasa kile cha kielektroniki ambacho kufungua ulipaswa ku-chanja kwa ‘smart card’ kisha mlango ungefunguka. Moyo wake ukawa mzito kufanya jambo hilo, jicho lake lilipotua kwenye ile sehemu akagundua uwa mlango ule umefunguliwa kwa maana alama yake ya kiuzi alichokitengeneza kama kifundo Fulani na kukipachika katika ule mfereji wa kuchanjia kadi haukuwepo. Akachomoa bastola yake ‘Berreta’ na kupichika kile chombo cha kupoteza sauti kisha akachomo kadi yake nyingine na kuchanja, mara mlango ukajinasua loki zake. Akaufungua ule mlango kwa kasi na kubamiza kwa nyuma kumbe Yule mjinga alijificha upande huo. Akajikuta akipigwa na mlango usoni, akatoka pale huku bastola ikimwanguka chini na mkono kajishika pua.
Amata alirudisha bastola yake kikobani na Yule bwana alipogeuka, alikutana na makonde mawili ya maana yaliyopita yote usoni, akayumba na kujibamiza mezani kabla hajaenda chini ambako hata hakufika kwani teke kali la Amata lilitua usoni na kumtupia upande wa pili wa kitanda. Kamanda Amata akaweka tai yake vizuri na kufunga upya saa yake, kisha akaruka kitanda na kutua upande wa Yule jamaa ambaye alikuwa akijiandaa kunyanyuka ilhali hali yake tayari ilikuwa tete. Lipotu sakafuni alihisi mlango ukifunguka tena nyuma yake, bila kuuliza, alichomo bastola na kujirusha chini huku tayari keshafyatu risasi mbili zilizoishia tumboni mwa Yule mjinga wa pili na kumbwaga chini huku akigombania roho yake isimwache. Amata akageuka haraka na kumrudia Yule wa kwanza ambaye tayari alikuwa amesimama na kujiandaa kwa mapambano.
“Umemuua Rajiv! Sasa zamu yako,” akaunguruma huku shati lake likiendelea kulowa kwa damu zilizokuwa zikichirizika kutoka puani mwake.
“Tulia mpumbavu wewe,” Amata alimjibu kwa lugha hiyo ya Kihindi aliyokuwa akijarobu kumwemwesa japo maneno mawili.
“Tupa bastola tupambane,” lile jamaa likamwambia Amata.
“Hamna tabu,” Amata akaipachika kwenye kikoba chake. Wakati akifanya hilo Yule jamaa alitua kifuani mwa Amata kwa miguu yake miwili. Amata akapepesuka na kujibamiza ukutani huku akimwona Yule mtu akitu sakafuni kwa miguu yake ileile. Kabla hajatulia, Amata alijizungusha huku akiwa amebonyea na kuwa mdogo kama mbuzi, mguu wake wa kulia uliozunguka kwa kasi ulimchota ngwala Yule bwana aliyekuwa akijaribu kuruka ili akwepe pigo hilo, lakini haikuwa hivo kwani alichotwa vibaya na kubamiza kisogo chini huku kiwiliwili kikimfuatia juu yake. Alijitahidi kunyanyuka lakini guu la Amata likatua kwa nguvu kifuani na kumafanya ateme damu.
“Unamjua Premji Kanoon?” akamwuliza.
“Husilitaje bure jina la mtu huyo,”
Kamanda Amata akamwinamia na kumchapa kofi moja kali lililomwacha taabani.
“Nani mshirika wenu hapa?”
“Hatuna mshirika,” akajibu kwa taabu. Kamanda Amata akachomoa kisu cha kukunja na kukifyatua hewani, ile ncha yake ikachachamaa juu, alipokishusha kilitua kwenye nyama ya paja.
“Aaaaaiiiiiggghhhh! Sukaina wa mapokezi,” akajibu huku akifumba macho na kubana meno.
“Shenzi kabisa wewe,”
Akakichomo na kukifuta damu kwa nguo za Yule jamaa huku akisimama na kukipachika mahala pake. Damu ilikuwa ikimbubujika Yule jamaa pale chini, Amata akafungua kabati na kutupia vitu vyake ndani ya begi lake, ‘haina haja ya kupoteza muda’ akawaza na kuivuta bastola yake.
“We mjinga salamu hii umpe mungu wako Premji Kanoon, mwambie Kamanda Amata yuko hapa,” akafytaua risasi na kuvunja goti la mguu wake mmoja, kisha akasonya na kupotea akiacha maumivu, kifo na kilio ndani ya chumba hicho.
† † †
Amata akatupi begi lake katika kiti cha nyuma na kujiweka kiti cha mbele.
“Vipi?” Chiba akauliza.
“Mmoja kafa, mwingine atakuwa kiwete milele na wengine tunawafuata leo hii hii,” Kamanda akajibu huku Chiba akiondoka eneo lile na kutokomea gizani.
“Itawezekana kufunga kazi usiku huu? Maana nilikadiri saa sabini na mbili,” Chiba akauliza huku akiicha barabara kubwa na kuingia kwenye barabara ya vumbi iliyopita katika miti mingi ambayo moja kwa moja ilikuwa ikielekea Bahrain House.
“Usijali, hapa kazi tu, ndani ya saa hizi arobaini na nane tayari huyu mtu atakuwa mikononi mwetu. Naamini Madam atafanya ulivyomwambia,” Kamanda akaeleza huku akiweka bastola yake na silaha nyingine tayari tayari.
“Usihofu juu ya Madam, ameona jua kabla yetu”.
Chiba akaegesha gari ndani ya jingo hilo na kuteremka kisha akaingia mahala Fulani na kuchukua silaha mbili tatu na mavazi ya kutumia katika hali halisi itakayowakumba, mabomu ya machozi na vinyago vya kuzuia sumu hiyo, mavazi ya kuogelea na mitungi ya hewa mine. Sehemu nyingine ya jingo hilo akafungua boti ndogo iliyokuwa kwenye kitoroli na kuivuta kwa mikono yake mpaka, ndani yake akatupia vile vitu na kuisukuma mpaka majini. Bahari haikuwa mbali na jingo hilo kuukuu: Kamanda Amata na Chiba wakaingia kwenye boti na kuiwasha, safari ikaanza.
† † †
Chiba alizima mlio wa injini ya boti na kuiacha iseleleke taratibu mpaka ilipo karibia umbali kama wa mita mia tano hivi. Wakati huo Amata alikuwa tayari amekwishavaa nguo zake za kupigia mbizi, mitungi yake mgongoni na begi dogo lilisiloingia maji mbele ya tumbo lake.
“Chiba, hapa kazi tu, mi naingia kwa njia ya maji nafikiri ni njia rahisi kama ulivyonambia, na wewe pitia hii hii lakini upande wa pili sote tukaibukie ndani na kutafuta njia ya kumnasa mtu huyo, tukishamtia mkononi kila mtu aangalie ustaarabu wa kuitoka hiyo himaya lakini tukutane Bahrain,” Kamanda Amata alimweleza mkakati mzima Chiba kisha akajitupa majini na kupotelea humo.
Chiba akaendele kupiga kasia kuisogeza ile boti mpaka kwenye mimea ya baharini iliyojazana upande mmoja wa peninsula hiyo. Akaegesha naye akavaa vifaa vyake na kujitupa majini kwa uelekeo mwingine.
† † †
Ndani ya hekalu hilo sherehe za mwanga ‘Diwali’ zizliendelea, watu walikuwa wakiimba na kucheza, kwa ujumla palichangamka. Pancho Panchilio alikuwa ameketi sehemu ya juu kabisa akifuatilia michezo na burudani zote zilizokuwa zikiendelea katika ukumbi huo. Kando yake alikaa na watu wengine kadhaa huku wanawake kama nane hivi warembo wa kuvutia walikuwa wakimpepea, wengine wakileta vinywaji na kadhalika. Nyuma yake alisimama mtu mmoja, mwanaume mwenye tambo kubwa, aliyefuga sharubu zake na kuzichanua huku n kule kama askari wa kijerumani enzi za mkoloni. Mikono yake aliifungamanisha nyuma. Macho yake yalionekana kutotopepeswa upande wowote ule. Na katika kila upande au kona ya jingo lile walionekana vijana waliovalia sare na virmba vyao vichwani mwao wakirandaranda huku na kule.
Kamanda Amata aliibuka majini na kujikuta kwenye chumba maalum ambacho ndani yake kuna boti kubwa la kifahari lililoegeshwa. ‘Nimekuja wakati mzuri, ningekuja mchana kusingekuwa na maji hivi,’ akawaza huku akivua ule mtungi na kuuweka kando, akatoa nay ale mavazi yake kisha akafungua begi lake na kujipachika kila silaha aliyoihitaji mwilini mwake. Sauti ya viatu vya mtu aliyekuwa akija upande huo vilimfanya atulie tuli huku kisu chake kikiwa ngangari kiganjani.
“Inabidi tuiwashe kwanza ipate moto. Mkuu anasema hana budi kwenda Punjawar usiku huu,” Sauti ya kwanza iliongea.
“Mbona ghafla hivi wakati sherehe hii yote kaandaa kwa ajili ya watu wake?” Sauti ya pili ikauliza.
“Mi mwenyewe sielewi aisee, ngoja tuwashe kabisa yeye akifika ni kuondoka tu,” ile sauti ya kwanza ikarudia.
‘Nimsubiri kwenye boti?’ Amata akajiuliza moyoni, ‘Uamuzi mbaya utakuwa’ akajijibu mwenyewe na nukta hiyohiyo Yule jamaa akaibukia kwenye mlango mmoja wa chumba hicho. Amata akaruka kwa wepesi na kumvami huku akiwa tayari kamdidimiza kisu moyoni. Akamshusha chini taratibu na kumsukumia kwenye maji. Kisha akatulia kwani bado mwingine alikuwa akija upande huo.
“Kumar! Kumar!” Yule wa pili akaita. Lakini hakukuwa na jibu kutoka kwa swahiba wake, akaendelea kwenda na alipofika kwenye kile chumba hakuamini anachokiona. Mwili wa Kumar ulikuwa ukielea kifudifudi majini. Mshtuko wake ulikuwa zahiri shahir, akainua redio yake na kuomba msaada.
“Kumar mara cuka hai! Kumar mara cuka hai!” (Kumar amekufa! Kumar amekufa), Amata akajibana kimya nyuma ya pipa kubwa lililojaa vipuli mbalimbali. Dakika hiyohiyo watu kama saba wenye silaha wakaingia katika kile chumba.
‘Nimecheza blanda’ akajiambia, akachomoa bastola yake iliyofungwa kifaa cha kuzuia sauti na kuiweka tayari. Risasi ya kwanza akapiga mtungi wa kuzimia moto na poda iliyokuwa ndani yake ikatoka kwa kasi na kuwachanganya wale jamaa. Kamanda Amata akapita kwa kasi huku watatu waliokuwa mbele yake wakiwa chali kwa risasi kutoka kwenye bastola yake, sekunde mbili tu alikuwa keshafika mlangoni na kuufunga kwa nje akiwaachia kizaazaa. Ujia mrefu ulimkaribisha. Ving’ora vya hatari vikalia kila kona, mvurugano ukaanza kila kona, burudani zikasimama na kelele za vilio nzikaanza huku na kule.
† † †
Chiba aligundua hali ile baada ya kusikia kelele za watu, akapachika head set yake masikioni tayari kwa kazi.
“Amata vaa barakoa yako kazi inaanza,” Chiba akaongea kwenye kile kifaa na kisha akavaa kinyago chake cha kuzuia gesi ya machozi na kinachoweza kumfanya aone gizani bila tabu. Akatazama huku na kule akaona sense ya moshi ambayop ikipata moshi basi huruhusu maji kumwagika, akatazama huku na kule akaona ua jirani, akavuta karatasi la urembo lilikuwa hapo akawasha moto na kisha akasogeza karibu na ile sensa, nukta hiyohiyo jingo zima likaanza kutiririsha maji, Chiba akaifuata swichi kubwa ya umeme na kuizima kisha akoundoa fyuzi na kuzitupa mbali. Sasa jingo lote lilikuwa giza na jenereta liligoma kuwaka, tayari kijana huyo wa TSA alishapita na kuondoa betri.
† † †
UKUMBI wote ulishikwa na kimuhemuhe, Amata alichomoa bastola yake yenye mabomu ya machozi na kutawanya huku na kule. Moshi huo mzito uliwafanya watu kukohoa bila kikomo, wakiishiwa nguvu na wengine kuanguka chini hawajiwezi.
Pancho Panchilio, aliinuliwa pale alipoketi na vijana wake kama saba hivi wakawa wamemzunguka kwa kumlinda wakiwa na silaha zisizojua huruma. Kutokana na gia lile walishindwa kumwona sawasawa Amata hivyo ilikuwa ni rahisi kwake kuwatawanya kwa risasi. Zilipomwishia akaruka sarakasi na kutua karibu kabisa na Pancho Panchilio huku miguu yake ikiwatandika mateke walinzi wawili waliobaki. Pancho alitaka kukimbia kuingia kwenye mlango mmoja lakini hakufanikiwa, ngwala moja maridadi ilimbwaga chini vibaya, wale vijana walipojaribu kunyanyuka, risasi za Chiba ziliwarudisha chini na Amata akapata nafasi ya kuinuka na kukutana uso kwa uso na Pancho.
“Twende nyumbani mwanaharamu wewe!” kamwambia huku akimtandika konde moja kali lililomfanya ayumbe na kupoteza mwelekeo. Konde la pili likamrudisha chini akiwa hoi, pamoja na ule moshi kumlegeza. Amata alijikuta akishikwa na hasira akikumbuka mtu huyo alichowafanyia yeye na wenzake kule Kerege katika mkasa uliopewa jina la Kitisho.
Kabla hajafanya lolote, akajikuta akipigwa na kitu kizito kisogoni, lakini mpigaji hakulenga sawasawa, Amata akageuka na kupeleka mashambulizi makali yaliyolifanya lile jitu lipoteane lenyewe kwa lenyewe. Lilipotulia likajikuta likitandikwa risasi mbili za kifua.
“Hatuna muda wa kupoteza, nasikia ving’ora vya wanoko huko nje,” Chiba alimwambia Amata, na wakati huo huo, Amata akamkamata mkono Pancho na kumkokota kwa nguvu. Mirindimo ya risasi bado ilikuwa ikiendelea, moshi wa machozi ulikuwa umechanganyika na ule wa baruti na kulete harufu ya tatu.
“Ondoka naye Amata, mi nalinda mkia wako,” Chiba alimwambia tena braza ake na Kamanda Amata akatoka na Pancho, alipoona upinzani umekuwa mkali akambeba Pancho na kuruka naye ghorofa ya chini yake wakafika hoi. Amata akawahi kunyayuka na kutumia bastola yake nyingine kupambana na wawili watatu waliokuiwa mahali hapo na kujaribu kumletea zengwe.
Haraka akaiwahi gari iliyokuwa imeegeshwa hapo na kufungua mlango. ‘Asante sana’ akashukuru baada ya kukuta funguo ikining’inia, akafungua buti.
“Ingia!” akamwamuru Pancho huku akiwa amekiinua kile kinyago chake na kukiweka kwa juu, Pancho akapigwa butwaa kumwona kiumbe huyo matata.
“Unashangaa nini? Ingia unanipotezea muda,” kamanda akang’aka lakini Pancho hakutaka kufanya hivyo. Konde moja la tumbo likamfanya Pancho ajiinamie huku amejishika tumbo lake, teke la kusukuma lilipeleka mpaka kwenye buti na Kamanda Amata akamalizia kufunga buti hilo kwa mguu kisha akaingia kwenye usukani, akaiwasha gari hiyo na kutoka kwa kasi huku akigonga geti na kukunja kushoto. Mfukuzano na gari za polisi ulichukua nafasi katika barabara za Bombay. Amata aliwapeleka nje ya mji kwenye barabara ya hatari kabisa, yenye mteremko mkali na wenye kona za ajabu, ambapo wengine waligwaya na waliojaribu walijikuta wakiishia shimoni.
Baada ya kuhakikisha wote kawaacha mbali Amata alichukua uelekeo wa Bahrain house na kuliacha jiji hilo.
Saa tisa za usiku akaegesha gari ndani ya jingo hilo kuukuu, akateremka akiwa hafai kwa vumbi lililomkaa mwilini.
Akafungua buti na kumtoa Pancho aliyekuwa kajikunyata ndani yake.
“Shuka!” akamwamuru naye akashuka. Akamkokota mpaka ndani ya chumba kimoja kikubwa.
“Pancho Panchilio au Premji Kanoon, karibu katika himaya yangu, mara hii ni zamu yako,” Sauti ya Madam S ikasikisa na taa yenye nuru hafifu ikawaka. Madam S akainuka alipoketi na kumjongelea mtu huyo. Kofi moja kali lilitua shavuni mwa Pancho na kumwacha akitetemeka.
“Ulifikiri utafanikiwa kunikimbia? Twende nyumbani nikakuoneshe kama mimi ni Head of T.S.A,” Madam akaunguruma na kumpa pingu Amata naye akamfunga mikono yake na mnyororo akautia miguuni mwake. Akamkokota mpaka kwenye ile gari waliokuja nayo na Chiba.
“Nafasi yako ni kwenye buti tu, akamwingiza na kulifunga kisha akatulia nyma ya usukani huku kushoto akimwacha Madam S.
“Chiba, Chiba, wapi?” Kamanda akauliza kwenye kile chombo chake.
“Naegesha boti nimefika,” akajibu.
“Weka kiberiti,” akampa agizo. Baada ya sekunde chache Chiba aliungana na wenzake na kuingia siti ya nyuma.
“Mzigo uko wapi?” akauliza Chiba.
“Upo mahala pake,” akajibu huku akiondoka eneo lile na kupita njia za vichochoroni.
“Kilomita ishirini na mbili kijiji cha Malve” Madam S alimwambia Amata na moja kwa moja akaelekea huko nje kabisa ya mji.
Hali ya utulivu ilitawala kijiji kile watu wote walikuwa wamelala ndani ya nyumba zao, ni miti tu iliyokuwa ikitikiswa na upepo wakati Amata akiegesha ile gari katika moja ya kichaka karibu na barabara kubwa inayoelekea baharini, barabara ya vumbi. Dakika mbili tu Scoba akatua na ndege ndogo aina ya Boeing yenye uwezo wa kubeba watu watano lakini yenye nguvu na kasi ya kutosha. Akatumia barabara hiyo kutua kwa kutumia mwanga wa tochi alizowasha Madam S akiwa chini kwa ishara aliyompatia. Hakuna kusubiri, walimkokota mtu wao na kumpakia ndegeni, huku kwa mbali wakisikia ving’ora vya polisi vikielekea upande wao.
“Haraka, haraka, haraka,” Madam alihimiza na mlango ukafungwa, Scoba moja kwa moja aliiongeza nguvu ile ndege na kuodoka kwa kasi huku akiwaacha wale polisi wakijaribu kufyatua risasi bila mafanikio. Dakika moja ndege ile ikawa angani ikikata bahari na kuelekea katika anga ya kimataifa ambako huna ruhusa kuifanya lolote.
† † †
“Na leo hii utatakiwa kusema siri zote ulizozificha mwanaharamu wewe!” Madam S alimwambia Pancho kwa ukali mara baada ya ndege ile kukaa sawa angani na kila mtu kuweza kufanya shughuli yoyote. Pancho Panchilio alitulia kimya akiangalia kwa jicho la kukata tama huku mwili wake ukionekana bado kukosa nguvu kwa kipigo cha rasha rasha alichokipata kutoka kwa Amata.
“Kamanda mwondoe hapa mpeleke kwenye chumba cha mwisho,”
Kamanda Amata akanyanyuka na kumchukua Pancho kwa kuushika ukosi wa shati lake, akamkokota mpaka katika chumba hicho na kumtupia humo. Mlango ukafungwa na ukimya ukatawala.
“Najua hauko peke yako kwenye mtandao huu, Mahmoud na mwenzake tulishawakamata wewe ukatutoroka kijanja. Na wale vibaraka wako wengine kule Kerege tumewakamata na wengine wamekufa wenyewe lakini wewe bado umetukimbia. Hukutukimbia tulikuwa tunaendelea kukuchunguza na sasa arobaini zako zimefika, haya nitajie mmoja baada ya meingine kabla hatujatua Dar es salaam,” Madam S alionekana kuwa na hasira kali juu ya mtu huyo.
Pacho alibaki kimya hakuzungumza lolote.
“Jeuri!” Amata akasema, kisha ghafla akapiga teke kwenye korodani lililomfanya Pancho apige kelele za maumivu na kuikusanya mikono yake yenye pingu katika eneo hilo.
“Utasema?” Kamanda akauliza. Lakini Pancho bado alibaki kimya huku akigugumia kwa maumivu makali. Amata akachukua kiberiti cha gesi na kukiwasha kisha moto wake akauweka chini ya kidevu cha Pancho. Maumivu aliyoyapata kwa moto ule uliokuwa ukiichoma ngozi akashindwa uvumilivu.
“Aaaaaaiiigghhh! niache! niache! nasema! nasema!” akapiga kelele.
“Sema, upon a nani kwenye mtandao?” Amata akauliza.
“Kamba Sebule, Kamba Sebule,” akataja jina la mtu mkubwa ambaye ni balozi wan chi Fulani hapa Tanzania.
“Na mna misheni gani hapa?”
“Mapinduzi ase aaaaiyyayayay aaaaiiiggghh! We muuaji wewe,” akalia kwa uchungu.
“Mwingine nani?”
“Alibaki huyo huyo, aaaaaaghhh!”
“Hutaki kusema ee? Sasa nakutupa nje kwa huna faida wewe,” Kamanda akamwambia Pancho kisha akamtazama Madam S.
“Madam! Jisjike vyema namtupa nje huyu mshenzi,”
Akabonyeza kitufe Fulani na mlango ukafunguka taratibu, upepo mkali ukaingia ndani na kuleta ufumbufu mkubwa.
“Utasemaaa au husemiii?” Kamanda aliuliza kwa kelele huku akimtazama Pancho. Akabaki kimya bila jibu. Amata akamsukuma na kumtanguliza kichwa nje, akamsukuma nje. Pancho akatoka mlangoni na kuning’inia vibaya.
“Aaaaaiihhhh, weweeeeeee! Niache nasema kila kituuu, ohhhhh! Nooooo!” Pancho akapiga kelele.
“Sema, mna misheni gani?”
“Mapinduzi, mapinduzi asee,” kutokana na upepo mkali Pancho aliyumba na kujigonga kwenye ubavu wa ndege. Kamanda Amata akatumia nguvu zake zote na kumvuta ndani akambwaga kando huku ule mlango ukijifunga taratibu. Pancho alipoteza fahamu na kutulia kimya.
“Kamba Sebule,” madam S akarudia jina hilo.
“Vipi?” Amata akauliza.
“Inabidi achunguliwe mara kwa mara asije kutupotea kuanzia sasa,” akajibu.
Madam S na Amata wakatoka katika chumba kile na kumwacha Pancho akiwa hajitambui damu ikitiririka usoni huku pingu na mnyororo vikiwa vimemdhibiti.
“Vipi?” Chiba akauliza.
“Poa, yupo huko kapumzika,”
“Yuko down?” (amekufa?)
“Hapana anaelea tu,” (hapana amezimia tu)
“Kinachoendelea?” Chiba akauliza.
“Kamba Sebule, yupo kwenye mtandao,” Amata akajibu huku akiketi sawia kitini. Chiba alibaki kakodoa macho kwa taarifa hiyo, hakutegemea mtu kama Kamba Sebule kuhusika kwenye mtandao wa maovu kama huo.
DAR ES SALAAM – saa 2:30 asubuhi
Saa tano ziliwaweka hewani na asubuhi ya saa mbili na nusu waliwasili uwanja wa ndege wa jeshi, Dar es salaam. Gari nyeusi yenye boksi kubwa nyuma ilisogea taratibu mpaka kwenye ile ndege na kusimama jirani kabisa. Pancho Panchilio aliteremshwa na kuingizwa kwenye hiyo gari haraka na kufungiwa humo, askari wawili wenye silaha wakaingia pia sehemu ya nyuma, milango ikafungwa na safari ikaanza.
“Asanteni sana kwa kazi vijana,” Madam S aliwashukuru Amata na Chiba.
“Ndiyo wajibu wetu,” Chiba akaitikia.
“Sasa mpumzike kisha kesho jioni tuonane ili tuweke mambo sawa juu ya mtu huyu,” madam akamaliza kusema na kuingia garini, Scoba akaondosha gari iliyombeba Madam S, Chiba na Amata waliingia kwenye gari nyingine ambayo alikuja nayo Gina wote wakaondoka uwanjani hapo.
SIKU HIYOHIYO
SEHEMU FULANI HUKO BAGAMOYO
VIJANA KAMA SABA hivi walikuwa katika chumba kimoja cha jingo lililochini ya ardhi katika kisiwa kimojawapo kati ya visiwa vine katika bahari ya Bagamoyo. Vijana hao wote walivalia mavazi meusi na kofia zao zilificha hadi nyuso na kuruhusu macho tu kuonekana. Mikono yao waliifutika kifuani na kufanya wote wawe katika mtindo mmoja wa kupendeza. Kati yao mmoja ndiye alikuwa na mkanda mpana mwekundu katika kiuno chake.
“Komredi ametekwa,” akawaambia wale vijana wengine.
“Usiku wa kuamkia leo pale Bombay, washenzi wamemchukua komredi na mpaka tunavyoongea sasa ameshafikisha hapa nchini,” akaendelea kusema; “Hii inaonesha dharau kubwa sana kwetu, kwa kuwa wale jamaa tulifanikiwa kuwateka wote wakatutoka kwa namna ya kibabe sasa naona wametugeukia sisi. Hatuwezi kuwaacha, sasa ni vita na vita hii ninaitangaza sasa. Komredi lazima akombole ndani ya saa sabini na mbili hata kama atakuwa amefichwa Ikulu, ohi?”
“Oha!” wakajibu kwa pamoja kumaanisha kuwa wanajua na wanaelewa kile walichoambiwa. Baada ya mazungumzo mafupi wakatawanyika na wawili kati yao wakabaki pamoja na Yule aliyevaa vazi lenye mkanda mwekundu wakaketi katika meza hiyo ya duara pamoja wakijadiliana jambo.
“Tutatumia gharama yoyote tumpate,” mmoja wao akasema.
“Hilo ndilo hasa nalitaka tuzungumze, mambo waliyoyafanya Bombay kule si madogo, wamedhalilisha hekalu la Hanuman,” mwingine akadakia.
“Yote tuyaache, mpango wao ukoje mpaka sasa na wapi amehifadhiwa?” Yule wa kwanza akavunja mazungumzo.
“Kutoka chanzo chetu cha habari wanasema jamaa kahifadhiwa Keko, lakini kesho kutwa atafikishwa Kisutu mahakamani,” Yule kiongozi akajibu.
“Baaasi mpaka hapo kazi imekwisha, lazima atekwe ama anavyokwenda au anavyotoka,” mwingine akajibu huku akipiga ngumi mezani.
“Nani wa kulainisha mipango? Si unajua wote wapo lupango,” Kiongozi akauliza.
“Aaaaa Mkuu hilo ni dogo, Kamba Sebule na Maliapopo si wapo? Watafanya kazi,”
“Na hata hizi habari ni Maliapopo aliyenipatia na yuko sambamba na kila linaloendelea atatujulisha,” akamaliza na kuwaomba vijana wakae tayari kwa lolote watakaloambiwa.
GEREZA LA KEKO
PANCHO PANCHILIO aliketi sehemu ya peke yake, mikono yake ikiwa na pingu kama alivyoletwa siku iliyotangulia. Chumba chenye mtindo wa duara kilichojengwa kwa vyuma imara pande zote ndimo alimohifadhiwa mtu huyo. Taa yenye mwanga mkali wa watts 750 ikawashwa na kummulika mtu huyo.
“Aaaaaigh Shit!” aling’aka baada ya taa ile kummulika usoni moja kwa moja.
“Acha kupiga makelele ya kitoto bwege we!” Madam S alimwambia huku akisogea taratibu na vijana wake Chiba na Amata wakiwa nyuma yake.
“Kesho mahakamani,” akamwambia.
“Afadhali haki ikatendeke maana hapa mnanionea tu,” Pancho akajibu.
“Haki? Unaijua haki wewe? Ungeijua haki ungefanya yote uliyoyafanya? Pancho au nikuite Premji Kanoon, nchi iliyokulea unaweza kuifanyia haya? Kudhulumu haki, haki ya mwananchi mdogo anayevuja jasho la chumvi na kulilamba kwa kukosa maji safi ya kunywa lakini wewe na mabwanyenye wenzio wenye matum,bo makubwa yasiyo na shukrani mnahamisha fedha na kuzificha ughaibuni.
Pancho! Kweli kabisa unadiriki kukifutilia mbali kikosi hiki unachokiona ili tu uendeleze biashara yako haramu, unaniteka mimi wewe, unateka vijana hawa uwaue halafu ufanye nini kwenye nchi hii? Kila anayekaribi kung’amua madhambi yako unataka ummalize. Siku yako imefika, nimekufuata India kwa gharama ili nikuoneshe kama mimi ndiye Madm S, mwanamke wa chuma tena chuma cha pua, kama kukuua ningeshakuua long time ila nilitaka kwanza nikuoneshe jeuri yangu kisha nikusweke jela maisha yako yote …”
“Kamwe, Pancho Panchilio hawezi kuingia jela, ha! Ha! Ha! hiyo sahau we mwanamke, utaiona miujiza yangu kabla ya kufika jela au hata mahakamani, mtatafutana ninyi nakwambia na hapo ndipo mtashuhudia mmoja mmoja wenu akianguka na kufa wakati mi narudi kuishi maisha yangu ya anasa. Ikitokea wewe ukabaki hai basi nitakualika kwenye tafrija kubwa pale Kilimanjaro Hoteli kisha utaona nani na nani wamealikwa, ndipo utakapojiona upumbavu wako we mwanamke ni mwanamke tu…”
Madam S alijikuta akishikwa na hasira akachomoa bastola yake.
“Rudia maneno yako nikupasue fuvu hilo,” aliongea kwa hasira.
“Ha! ha! ha! ha! Muoneni bibi yenu huyu, hana akili kabisa,” aliwaambia kina Chiba na Amata.
“Funga domo lako wewe! Usifikiri tunacheka na punguani,” Amata akaunguruma.
“Tena wewe! Wewe! Wewe! Ipo siku yako. Nitakutoa huo utumbo niuanikie nguo,” Pancho alimwambia Amata.
“Utafanya hayo kabla bastola yangu haijafumua ubongo wako,” Amata akamaliza na kumtazama Madam S aliyekuwa amekunja sura kwa uchungu.
“Kesho Mahakamani,” Madam akamwambia Pacho na kugeuka kuanza kutoka ndani ya chumba kile maalum.
SIKU ILIYOFUATA
Asubuhi ya siku iliyofuata Pancho Panchilio aliandaliwa tayari na kupelekwa mahakamni ili kusikiliza shitaka lake.
Mahakama ilifurika watu kama kawaida, waandishi wa magazeti na wale wa televisheni walikuwa bize kutafuta habari lakini zaidi kuipata picha ya mtu huyo. Baada ya yote kukamilika na shauri hilo kuahirishwa, Pancho alitakiwa kurudishwa rumande mpaka baada ya mwezi mmoja ambapo ushahidi utakuwa umekamilika. Gari ile iliyomchukua kutoka uwanja wa ndege ndiyo iliyokuja gerezani hapo kumbeba kwa mara nyingine na sasa ilikuwa na kazi ya kumrudisha Keko. Alitolewa akiwa chini ya ulinzi mkali mnyororo wake miguuni na pingu mkononi, moja kwa moja akaingizwa ndani ya gari hiyo isiyo na dirisha hata moja katika eneo la kuifadhi wahalifu. Baada ya kufungwa mlango wake askari wawili wenye silaha walikaa katika kijichumba kidogo wakiwa na bunduki zilizoshiba vyema.
Msafara ukaanza kutoka katika gereza hilo, gari ya polisi ikatangulia mbele ikipiga ving’ora vya kuomba njia, kisha ikafuatia hiyo ilimbeba mhalifu na mwisho kulikuwa na gari nyingine iliyobeba askari magereza wenye silaha, safari kuelekea Gereza la Ukonga na sio Keko tena ikaanza kwa kasi huku gari nyingine zikiacha njia na kuupisha ule msafara uende. Kasi iliyokuwa kwa gari zile haikuwa ya kawaida, kila mtu alishangaa na kujiuliza ‘kuna nini?’
WAKATI HUOHUO
Barabar ya Shaurimoyo na Nyerere
“Mko tayari? Tunafanya kazi sasa, dakika tatu kila kitu kiwe kimekamilika, kwa kuwa wao hawajajiandaa kwa hilo basi itakuwa ushindi ni upande wetu, ohi?”
“Oha!” wakaitikia vijana wa kazi waliovalia nguo za khaki, na bunduki zenye risasi tele migongoni mwao, nyuso zao zilikuwa tayari kufunikwa na barakoa za kukinga gesi ya machozi, walikamilika.
Kiongozi wa operesheni hiyo aliinua redio yake ya upepo na kuiweka karibu na kinywa chake.
“Namba one, namba one, stand by!” akaongea.
“Umesomeka, namba one stand by,” akajibiwa.
“Namba one on your marks! Get set, go!” Yule kiongozi alitumia mtindo unaotumika na wanariaadha kutimua mbio.
Kutoka upande wa Keko, karobu kabisa na eneo la daraja la leri pembezoni mwa kiwanda cha uchapaji cha Taifa, liliwashwa tingatinga na kuchomoka kwa kasi kuelekea barabara ya Nyerere. Hamad! Wakati ule msafara unafika na lile tingatinga linafika, ajali mbaya isiyosemeka ikatokea. Lile tingatinga likaigonga gari ya mbele ya polisi na kuharibu vibaya, haikuishia hapo, iliigonga ile gari ya kubeba mhalifu na kuikunga njia, ikaibana karibu na gema la daraja. Mtafutano wa watu ukaanza asubuhi hiyo katika eneo lile.
Kutoka kwenye ile gari ya askari maalum wa magereza, waliruka na kutua nje kila mmoja akachukua sehemu yake kwa kuangalia nini kinatokea. Kabla hawajakaa sawa, gari aina ya Range Rover ikaingia kwa kasi na vijana kama sita hivi wakateremka haraka na kulizunguka eneo lile, mabomu saba ya machozi yakatua ardhini na wao wakavaa barakoa zao tayari kuzuia adha ya gesi ile ya machozi. Wawili kati yao haraka wakaenda kuufungua ule mlango wa lile gari, risasi zikaanza kulindima kutoka kwa wale vijana wa magereza na polisi, wakashambuliana na wale majambazi. Jambazi mmoja akapigwa risasi na kudoindoka lakini hakufa bali alijeruhiwa vibaya.
Mlango ukafunguka, mmoja wa askari bado alikuwa ana nguvu zake, alimpiga Yule jambazi kwa kitako cha SMG kichwani, Yule jambazi akapepesuka na kushindwa kustahimili akaaguka chini, Yule mwenzake akatumia risasi ya moto na kupiga askari wote wa ndani kisha akaingia na kumfungua bosi wake. Mabomu ya machozi yaliongezwa na mosi ukatapakaa eneo lote.
Yule jambazi aliyetoka na Pancho akapiga aina Fulani ya mluzi na wale wenzake wote wakakimbili garini, lakini jambazi mmoja aliyekuwa mwisho ambaye kiutaratibu lazima apande mwisho, akamchapa risasi Yule jambazi mwenzake aliyekuwa na hali mbaya pale chini ili kuzuia asije ongea lolote, nukta hiyo hiyo ukasikika mlio wa helkopta eneo lile, nalo likazidisha vumbi, wale majambazi na mtu wao wakajitupa ndani yake na lile dege likapotelea angani.
“Upo Salama Mkuu,” Kiongozi akamwambia Pancho.
“Yeah, hongereni kwa kazi,” akawapongeza wakati huo wakimwondoa ile minyororo na pingu mikononi mwake.
“Ha! Ha! Ha! Ha! mmewapiga chenga ya mwili,” Pancho aliwasifu vijana wake kwa lugha ambayo Yule dereva hakuielewa.
“Ijapokuwa tunasikitika tumepoteza wawili,”
“Usijali, hiyo ni najali kazini,”
“Sawa Boss”.
† † †
DARAJANI
Dakika tatu tu tukio lile lilishafanyika na utulivu ukarudi, kilichobaki kilikuwa na mtapakao wa moshi na harufu ya baruti inayoishia kwa upepo. Watu walikuwa wakisogea taratibu kuona kulikoni. Polisi nao walifika na kuweka ulinzi eneo hilo ikiwa pamoja na kufunga barabara.
Mkuu wa polisi mkoa wa Dar es salaam alikuwa hapo akiangalia hali halisi, sura yake ikikunja ndita sehemu ya juu ya macho yake, hasira isiyojificha ilionekana wazi wazi.
“Wanaharamu hawa,” akang’aka kwa hasira.
Wakati polisi wengine wakiendelea kupima hapa na pale yeye bado alikuwa akiendelea kuwasiliana kwa redio yake.
“Nipo eneo la tukio, mmeona helkopta yoyote ikipita maeneo hayo?” akawauliza polisi wa anga ambao daima kazi yao ni kuvichungulia vya juu.
“Vipi Mkuu?” sauti ya Inspekta Simbeye ilimfanya Yule RPC kushtuka na kumwangali mtu huyo. Wakapigiana saluti za kijeshi kisha mazungumzo yakaendelea.
“Kwa hiyo wamekuja na helkopta mpaka hapa na kumchukua mtu wao?”
“Ndiyo, ilikuwa nishambulizi la ghafla na la ufundi wa hali ya juu ijapokuwa hata vijana wetu wamefanya kazi kubwa mpaka kuwalaza hawa wawili, sema tu ndiyo hivi wameshakufa, laity wangekuwa hai pangechimbika,” akamaliza kusema RPC na kumwacha Simbeye akikagua hapa na pale kuona kama kuna lolote la ajabu katika ajali hiyo, alitazama hiki akagusa kile, alipindua hiki na kusimamisha kile kule arimuradi tu afanye kitu.
SHAMBA
MCHANA HUOHUO
Simu ya mkononi ya Madam S iliita kwa fujo, alipotupa jicho mezani akaona simu inayowakawaka ni ile ya taarifa nyeti.
“Shiit, nini tena?” akaongea kwa sauti ya kuonesha kuwa hajafurahia simu hiyo, akainyakuwa na kuitega sikioni kwanza.
“Hello Madam!” mara moja akaitambua sauti hiyo.
“Ndiyo Simbeye vipi (…) what! Unasema, (…) acha masihara katika kazi asee,”
“…Madam habari ndiyo hiyo, Pancho Panchilio kaokolewa na jamaa zake kwa njia za kikomandoo”.
Madam S akakata simu na kuitupia mezani kisha yeye mwenye akajitupa kitini na kushusha pumzi ndefu. Akawaita vijana wake wote na kuwapa taarifa hiyo ambayo iliwachanganya mpaka wakachanganyikiwa.