Makamba: CCM ina jeuri ya kumbana Sitta
Mapokezi mazito ya Spika Sitta Tabora leo
na Deogratius Temba
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Luteni mstaafu Yusuf Makamba, amesema chama hicho kina haki ya kumhoji Spika wa Bunge, Samuel Sitta na wabunge wote wa chama hicho, kwani wote ni mali ya chama hicho tawala.
Kauli hiyo ya Makamba imekuja siku chache baada ya wadau mbalimbali, wakiwemo wasomi na wanasiasa wa vyama vya upinzani, kuhoji uhalali wa Kamati Kuu (CC) na Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kumuonya Spika Sitta, kutokana na hatua yake ya kutoa uhuru kwa wabunge wa chama hicho kuinyanyasa serikali na chama hicho tawala.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, muda mfupi mara baada ya kumaliza kuhutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Manzese Bakheresa, Wilaya ya Kinondoni, Makamba alisema CCM ina haki ya kumhoji mbunge yeyote wa chama hicho, na hata Spika wa Bunge, kwani Bunge hilo ni mali ya chama tawala.
Sisi ndio tunaotawala, tunayo haki ya kumhoji na kumuuliza namna anavyoliongoza Bunge. Serikali ni yetu, mnataka nani amuulize? alihoji Makamba na kuongeza:
Chama hakitaacha kuwahoji wabunge wanaotoka nje ya misingi ya chama na kutoa maneno yanayosababisha kukichafua. Kama wana maneno yao wayalete ndani ya chama, kwanini wakapige kelele za ufisadi nje ya chama?
Ukijichanganya ukatoa maneno ambayo hatuyataki, wenye chama chao watakuita na kukuuliza yanayohusu chama
kama ni ufisadi wayaseme ndani ya chama. Kama ni ya Bunge wayaseme ndani ya Bunge na si kwenda kuzungumza mitaani.
Alipoulizwa juu ya mkanganyiko wa kauli mbili za viongozi wa juu wa chama hicho, Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa, Kapteni mstaafu, John Chiligati na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Propaganda, Tambwe Hizza, zilizotofautiana, alisema kauli halali ya chama ni ile iliyotolewa na Chiligati.
Kauli halali ni ile ya Chiligati
hizo nyingine unazoniuliza sizijui mimi, ninachojua kauli ya NEC ni ile ya Chiligati, kwa sababu tulikuwa wote Dodoma, hizo nyingine mimi sizijui, alisema Makamba kwa mkato.
Makamba ambaye jana hakuwa tayari kutoa maelezo marefu kwa maswali aliyokuwa akiulizwa na waandishi wa habari, alisema kumekuwepo na wanasiasa wengi ndani ya chama hicho wanaojitokeza na kutoa maoni mbalimbali ya kupinga maamuzi ya chama.
Wakati Makamba akitamba kuwa chama hicho kina haki ya kumhoji Sitta kama kilivyofanya katika vikao vyake vilivyopita, juzi Tambwe alitoa tamko kwa vyombo vya habari linaloonyesha dhahiri kupindisha tafsiri ya maamuzi ya vikao hivyo, baada ya maamuzi hayo kuonekana kupata upinzani mkubwa kutoka kwa wadau mbalimbali nchini.
Katika tamko hilo, Tambwe alisema vikao hivyo havikujadili ajenda yoyote iliyowahusu Sitta na wabunge wenzake, wala iliyomhusu Makamba, aliyedaiwa kuwa ilikuwa nusura angolewe.
Katika NEC hakukuwa na ajenda yoyote iliyomjadili Sitta na wala hayo yaliyoandikwa eti wajumbe walitaka Sitta anyanganywe kadi ya CCM hayakutokea. Na hakukuwa na ajenda yoyote katika Kamati Kuu wala NEC iliyomjadilli Makamba. Kwanza wakati wao wanasema hivyo, ndiyo kwanza vikao vilimpongeza Makamba kwa kufanya kazi zake vizuri, alisema Tambwe.
Akizungumza na wananchi wa Manzese katika mkutano huo, Makamba aliwataka viongozi wa CCM ngazi ya wilaya na mkoa kuwasimamisha wagombea wanaopendwa na wapiga kura na kuacha upendeleo wa kindugu na kupokea rushwa.
Ninawataka mhakikishe viongozi wanaopewa nafasi ya kugombea ni wale wenye sifa, na ambao wanapendwa na wananchi, nyie viongozi muache kula rushwa, upendeleo wa kindugu katika uchaguzi acheni.
Kama wewe humpendi mtu, lakini chama kinamtaka mpe nafasi asimame na agombee, usitunyime ushindi CCM. Tumekuwa tukishindwa sana katika chaguzi nyingi kutokana na kuwasimamisha wagombea wasio na sifa.
Huyo mtu unayemuona wewe kuwa anakufaa wewe, kwetu CCM hatufai, huyo unayemuona kuwa hakufai wewe, kwetu anatufaa, tupatie huyo mwambie humpendi, lakini unamtoa kwa ajili ya chama, alisema.
Alisema ubaguzi ndani ya chama hicho umekuwa chanzo cha kushindwa kila chaguzi, na kama utaachwa katika kipindi hiki muhimu cha uchaguzi wa serikali za mitaa, kitaweza kushinda mitaa mingi.
Makamba aliyekuwa amefuatana na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Taifa, Sofia Simba, jana alikibomoa Chama cha Wananchi (CUF), ngazi ya taifa, baada ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa Baraza la Wanawake Taifa - CUF, Ashura Amanji, kukihama chama hicho na kukabidhiwa kadi ya CCM.
Ashura ambaye pia ni Mkurugenzi wa Wanawake wa CUF Taifa, alisema amekuwa kiongozi mkubwa ndani ya chama hicho, lakini amegundua kuwa anateseka bure kutumikia chama ambacho hakina demokrasia.
Viongozi wetu wa makao makuu wamekuwa wabaguzi, nimekitumikia chama sana katika ngazi za juu, lakini sijaona mafanikio kutokana na ubaguzi na baadhi ya wakubwa wa chama. Mkubwa mmoja akikutaka ndipo utapewa cheo la sivyo hupati, alisema Ashura na kusababisha watu kucheka.
Wengine ni Fatuma Aly Sadiq, ambaye ni mjumbe wa Baraza Kuu Taifa (wanawake), Sara Babavua, Mjumbe wa Baraza la Uongozi wa Taifa Wanawake, na Zainab Yusuf, Mjumbe wa Mkutano Mkuu, Mkoa wa Kigoma.
Mbali na viongozi hao wa kitaifa, pia chama hicho pamoja na Chama cha Tanzania Labor (TLP) vilipata pigo, kwani wanachama wake zaidi ya 220, walirudisha kadi na kukabidhiwa za CCM.
Wakati huo huo, Kituo cha Msaada wa Kisheria nchini (LHRC), jana kilitoa tamko la kulaani hatua ya NEC na Kamati Kuu CC kutaka kumwengua uanachama wa CCM, na kumvua madaraka ya uspika, Spika Sitta.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari, kituo hicho kimeona kuwa hayo ni matokeo ya mfumo mbaya wa utawala ambao nchi imeridhia kutoka kwa Wakoloni.
Haya ni matokeo ya mfumo mbaya tuliorithi kutoka kwa Wakoloni, ambao tunauendeleza ambapo kiranja wa shughuli za Bunge anatoka katika chama fulani cha siasa.
Kinachotokea kwa Spika Sitta, ni kwamba anasongwa na chama chake kutokana na malalamiko ya kutokilinda chama chake bungeni, hasa wakati huu ambao nchi inakumbwa na matukio mengi ya ufisadi, ilisema taarifa hiyo.
Wakati kituo hicho kikitoa tamko hilo la kumtetea Sitta, leo Spika huyo anatarajiwa kupata mapokezi makubwa atakapowasili mkoani Tabora.
Habari ambazo zimepatikana na kuthibitishwa na viongozi mbalimbali wa CCM mkoani humo, zinasema kuwa Sitta atawasili kwa ndege ya kukodi, ambayo pia itakuwa na viongozi na waandaaji wa tamasha la nyimbo za injili litakalofanyika kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.
Mara baada ya kuwasili mjini Tabora, Spika ataelekea moja kwa moja wilayani Urambo lilipo jimbo lake la uchaguzi, ambako ameandaliwa mapokezi makubwa yatakayopambwa na pikipiki na teksi na baadaye kufanya mkutano wa hadhara.
Hata hivyo, viongozi wa kisiasa wilayani humo walipohojiwa kwa njia ya simu kuhusu mapokezi ya kiongozi huyo, hawakuwa tayari kuelezea ratiba ya mapokezi na maandalizi ya ugeni huo, kwa madai kuwa wao wamesikia juu ya ujio huo kupitia vyombo vya habari.
Haya, maneno ya Katibu wako Mkuu hayo hapo, amempinga Tambwe na kuungana na Chiligati. Sasa wewe bado upo na Tambwe ambaye hata hicho kikao hakuwa mjumbe. masiki Pundamilia07, hiyo ndo CCM yenu, kama hukubaliani na kilichotokea, usijifariji kuwa hakikutokea, pole sana.