Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu amehamishwa gereza la Keko alikokuwa akishikiliwa, huku mahali alikohamishiwa pakiwa hapajulikani.
Msemaji wa Jeshi la Magereza, Elizabeth Mbezi alipoulizwa kuhusu taarifa hizo alisema bado hajazipata.
halipoulizwa kama kuhamisha watuhumiwa na wafungwa ni siri, amesema, "Inategemea na makosa, yapo makosa wanahamishwa kwa siri na yapo makosa hawahamishwi kwa siri." Alipoulizwa kuhusu tuhuma za Lissu, alisema, "Ngoja nifuatilie kwanza."
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa ,Mawasiliano na Uenezi, Brenda Rupia leo Ijumaa, Aprili 18, 2025, imesema viongozi wa Chadema akiwamo Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Wakili Ali Ibrahim Juma, Mawakili, wanafamilia na wanachama kwa nyakati tofauti, wamefika katika Gereza la Keko kumwona Lissu, lakini hawakufanikiwa kumwona.
“Juhudi zao za kumuona Mhe. Lissu hazikufanikiwa baada ya kuelezwa kuwa hayupo katika gereza hilo, cha kusikitisha, hawakupewa maelezo yoyote rasmi juu ya alipopelekwa.”
Chama hicho kimelitaka Jeshi la Magereza, mamlaka husika na vyombo vya Dola kutoa taarifa wazi na za haraka kwa umma kuhusu mahali alipopelekwa Lissu.
“Iwapo bado anashikiliwa katika Gereza la Keko, ni haki ya familia, viongozi na wanachama kumuona - ni haki ya msingi ya kibinadamu na kikatiba,” amesema Brenda.