Halima Mlacha
Daily News; Saturday,August 02, 2008 @00:01
Aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, aliyekufa ajalini Jumatatu wiki hii, siku inayofuata ilikuwa awasilishe ombi la dharura mahakamani akitaka iamuru arejeshwe katika wadhifa wa Makamu Mwenyekiti wa Chadema, HabariLeo imebaini.
Wakili wa mwanasiasa huyo ameliambia gazeti hili kwamba walipanga waiwasilishe hati hiyo ya dharura Mahakama Kuu Dar es Salaam Jumanne asubuhi. Wakili huyo, Mathew Kakamba wa Kakamba and Partners Advocates, alisema katika hati hiyo Wangwe alikuwa aiombe Mahakama isimamishe kwanza uamuzi wa kusimamishwa kwake wadhifa wa umakamu hadi kesi ya msingi aliyokuwa ameifungua juu ya suala hilo itakapokamilika.
Alisema kabla mbunge huyo hajaondoka Dodoma, alizungumza naye kwenye simu saa tisa alasiri ambako aliahidi kuhudhuria mahakamani kesho yake kama ilivyopangwa. "Kusema ukweli majira ya saa tisa siku aliyoondoka nilizungumza naye na akaahidi kuwahi kesi, nilipomuuliza kwa nini anaondoka usiku, alisema ni kwa sababu anataka pia awahi maziko ya mwanasiasa Bhoke Munanka," alisema Kakamba.
Alisema kesi ya msingi ya Wangwe dhidi ya wadhamini wa chama hicho, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu wa chama hicho Dk Wilbrod Slaa, tayari ilishafunguliwa tangu Julai 21, mwaka huu katika Mahakama Kuu. Alisema katika kesi hiyo ya msingi ya madai pamoja na mambo mengine, Wangwe alisema mkutano uliofanyika Dodoma na kumsimamisha umakamu, haukuwa halali na kwamba uamuzi waliotoa haukuwa wa haki.
Kwa mujibu wa hati ya kesi hiyo, Wangwe alitaka Mahakama itoe agizo kuwa mkutano uliofanyika Juni 28, mwaka huu, pamoja na uamuzi wote uliotolewa ni batili. Alitaka mahakama itoe amri ya kumruhusu kuendelea na wadhifa wake wa umakamu mwenyekiti wa Chadema Bara na itoe amri ya kisheria ya kudumu dhidi ya Mbowe, Dk Slaa na wakala wao na kuwazuia kuchukua hatua yoyote ya kumsimamisha wadhifa wake au uanachama.
Gazeti hili pia lina taarifa za kuaminika kuwa baadaye Jumanne, Wangwe alikuwa azungumze na waandishi wa habari Dar es Salaam juu ya alichoamini kuwa ni jaribio la kuvuliwa wadhifa wake na uanachama wa chama hicho. Baadhi ya masuala ambayo dondoo zake alizisambaza kwa watu wake wa karibu (gazeti hili linazo), Wangwe alikuwa azungumze kuwa sababu zote zilizotolewa na Mbowe dhidi yake, hasa suala la kuvujisha siri za chama hicho kwa CCM ni za uzushi.
Dondoo zinaonyesha angezungumzia kukerwa na mtiririko wa mgogoro ndani ya Chadema, kiasi cha kuonekana inaendeshwa "kiujanja ujanja." Wakati huo huo, Mwandishi Wetu anaripoti kutoka Tarime kuwa utata uliogubika kifo cha Wangwe, jana ulitatuliwa baada ya uchunguzi wa mwili wake kubaini kuwa kifo chake kilitokana na ajali na hakupigwa risasi.
Uchunguzi huo uliochukua zaidi ya saa tano, uliwashirikisha madaktari watatu ambao waliombwa na familia kuufanyia uchunguzi mwili huo. Wanafamilia waliongozwa na Profesa Samwel Wangwe na madaktari hao ambao hata hivyo, walikataa kutaja majina yao. Uchunguzi huo ulianza saa tano na kumalizika saa 10.00 jioni.
Madaktari hao, mmoja alitoka Dar es Salaam, daktari mwingine alitokea Musoma na mwingine alikuwa mwakilishi wa hospitali ya wilaya ya Tarime. Uchunguzi huo ulifanyika chini ya usimamizi wa Polisi kwa lengo la kujiridhisha. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kiliongozwa na Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe. Wangwe alisema sasa familia imejiridhisha na uchunguzi wa marehemu na walilazimika kufanya hivyo kutokana na utata ulioigubika, hivyo kulazimika kuwaita madaktari wao.
"Sasa hatuna shaka na mtu yeyote wala chama chochote," alisema Wangwe na kuongeza kuwa wanaenda kuzika na hawana hofu. Juzi ndugu wa Wangwe waligoma kuzika mwili wa marehemu, kwa maelezo hawakuwa wanaamini kuwa ndugu yao amekufa kwa ajali ya gari. Hivyo walilazimika kuahirisha maziko hayo ili kujiridhisha zaidi, kwani Wangwe alikuwa kiongozi wa watu. Maziko yalifanyika kijijini hapo jana jioni na kuhudhuria na umati wa watu ambao haukulingana na waliokuwapo juzi.
Baadhi ya viongozi wa upinzani waliokuwapo katika maziko hayo yaliyofanyika kwa amani walikuwa ni pamoja na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia.
Habari zinasema Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alishauriwa asihudhurie maziko hayo jana kutokana na vurugu zilizotokea juzi baada ya yeye kufika msibani hapo.