C/HQ/ADM/SG/02/185 30 Julai, 2008
MKUU WA JESHI LA POLISI,
P.O.BOX DAR ES SALAAM ,
TANZANIA.
YAH; KIFO CHA MHESHIMIWA CHACHA ZAKAYO WANGWE MBUNGE WA TARIME.
Kutokana na ajali iliyotokea tarehe 28 Julai 2008 katika eneo la Pandambili Wilaya ya Kongwa Mkoa wa Dodoma na kusababisha kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime Marehemu Chacha Zakayo Wangwe, ninalazimika kukuandikia rasmi kuhusiana na taarifa mbalimbali ambazo zimekuwa zikiripotiwa na vyombo mbalimbali vya Habari hapa nchini juu ya utata ambao umekighubika kifo hicho na haswa mazingira ya ajali yenyewe. Katibu Mkuu wa CHADEMA, katika mahojiano yake na TBC1 katika mahojiano yake kwenye kipindi cha Jambo Tanzania alielezea pia utata huo na kutaka Jeshi la Polisi lifanye uchunguzi wa kina.
Maelezo ya Ndugu Deus Mallya ameyatoa kwenye vyombo mbalimbali vya habari kuhusiana na jinsi ajali hiyo ilivyotokea na eneo ambalo yeye alikuwa amekaa wakati ajali inatokea , pamoja na kusema kuwa yeye alikuwa amekaa kiti cha nyuma huku Dereva wa Gari akiwa ni Marehemu Chacha Wangwe yameongezea kwenye utata huo.
Taarifa ambazo zimetolewa na watoto wa Marehemu kama walivyohojiwa na vyombo mbalimbali vya habari na kuripotiwa na vyombo hivyo na haswa maelezo yaliyorushwa na Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC), na vituo vingine vya Television, pamoja na Habari za Magazeti mbalimbali ya tarehe 30-07-2008 ,kama vile Magazeti ya The Guardian, Nipashe, Tanzania Daima ,Mwananchi na mengineyo ambayo yaliandika kuhusiana na maelezo aliyotoa Ndugu Deus Mallya pamoja na watoto wa Marehemu yakilinganishwa na maelezo ya Deus Mallya yanahitaji kupatiwa majibu ya kina, jambo ambalo CHADEMA kama mwathirika wa ajali hiyo isingeliweza kulifumbia macho.
CHADEMA , tumefuatilia kwa kina sana kuhusiana na maelezo hayo ambayo yametolewa kwa nyakati tofauti na watu tofauti kuhusiana na ajali hiyo na hatimaye msiba huo.
Hivyo basi , Chadema kama Chama kilichoathirika kwa kumpoteza Mbunge wake, Mwenyekiti wake wa Mkoa na aliyekuwa Makamu Mwenyekiti na hivyo kuwa na maslahi ya karibu sana katika uchunguzi huu, tunalitaka Jeshi la Polisi wakishirikiana na vyombo vingine vya Usalama kufanya uchunguzi wa kina kuhusiana na mambo yafuatayo;
1. Kujua huyu ambaye alikuwa (Deus Mallya) na Marehemu kwenye gari lake wakati anafariki ni nani na anafanya shughuli gani.
2. Deus Mallya alienda Dodoma kufanya shughuli gani na ana uhusiano gani na Marehemu na au Familia ya Marehemu.
3. Ndugu Deus Mallya alikuwa amekaa kwenye kiti gani wakati ajali inatokea.
4. Ni nani alikuwa anaendesha Gari wakati ajali na hatimaye umauti unamkuta Mheshimiwa Chacha Wangwe.
5. Ni mazingira gani yaliyopelekea na au kusababisha ajali hiyo kutokea .
6. Tunataka Polisi wachukue hatua stahiki za kisheria ili Deus Mallya akaisaidie Polisi na kuhojiwa kwa kina juu ya suala hili kwani maelezo yake yana utata mkubwa sana.
7. Jeshi la polisi liitoe ripoti ya uchunguzi huo mapema na kuiweka ripoti hiyo hadharani.
Tunapendekeza hatua hizo zichukuliwe mara moja kwani tunaamini kuwa kifo hiki kimeghubikwa na utata mkubwa sana na haswa kutokana na maelezo ambayo yamekuwa yakitolewa na aliyeshuhudia ajali (Deus Mallya) pamoja na watoto wa marehemu.
Tunaamini kuwa utatupatia ushirikiano wa kina ili kuhakikisha kuwa hatua za haraka na za dharura zinachukuliwa mara moja kwa ajili ya kuujua ukweli wa kifo hiki tata.
Pamoja na hayo, hivi karibuni wabunge wa CHADEMA wamekuwa wakipata taarifa za vitisho pamoja na kuzushiwa vifo kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu za mkononi na ujumbe huo kusambazwa sana kama ilivyoripotiwa kwako na Mheshimiwa Zitto Kabwe (MB).
Tunaomba wabunge wetu wapatiwe Ulinzi na pia taarifa hizo zifanyiwe kazi kwa kina.
Nakutakia kazi njema.
Wako katika ujenzi wa Demokrasia na Utawala Bora.
……………………
John Mnyika - 0754694553,
Kaimu Katibu Mkuu,
Na Mkurugenzi wa Vijana Taifa ,
Nakala:
1. Mhe.Lawrence Masha – Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi
2. Mhe.Dr. Willbrod Slaa (MB) - Katibu Mkuu CHADEMA .
3. Robert Manumba -Mkurugenzi wa Upelelezi na Makosa ya Jinai.