BigTall
JF-Expert Member
- Mar 9, 2022
- 422
- 1,049
Jumla ya kesi 42 za vitendo vya udhalilishaji zimeripotiwa katika Ofisi ya Naibu Mrajisi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Kisiwani Pemba kwa mwaka 2021.
Naibu Mrajisi, Hidaya Omar Khamis amesema bado tatizo la udhalilishaji kwa wanafunzi lipo na ni changamoto kubwa.
Mrajisi huyo alieleza kuwa kesi ambazo ziliripotiwa katika ofisi yao ni pamoja na ubakaji, mimba kwa wanafunzi, udhalilishaji pamoja na kulawitiIwa ambapo jumla ya matukio hayo ni 42.
"Kwa upande wa Wilaya ya Wete, kesi ambazo ziliripotiwa ofisini kwetu ni (11), ambapo kesi za udhalilishaji zilikuwa (4), ubakaji (2), udhalilishaji (4), mimba (1) huku kesi za ndoa ikiwa hamna," alieleza.
Sambamba na hayo naibu huyo alieleza kuwa kwa upande wa Wilaya ya Micheweni kesi ambazo ziliripotiwa ni (10) ikiwa ni kesi ya ndoa (1), mimba 8), ulawiti (1) huku vitendo vya Udhalilishaji na ubakaji ikiwa hamna.
Upande wa Wilaya ya Chake Chake, Naibu Mrajisi alieleza kuwa kesi zilizoripotiwa ni (10), ambapo kesi za udhalilishaji ni (1), ubakaji (2), mimba (5) kesi ya ndoa ni (1) ulawiti (1)
"Kwa Wilaya ya Mkoani, kesi ambazo tulizipata ni kesi (11), ambao kesi za ubakaji ni (4), kesi za ulawiti ni (1), udhalilishaji (2), mimba (4) huku kesi za ndoa ikiwa hamna," alisema Naibu Mrajisi.
Aidha, Mrajisi Hidaya alibainisha kuwa changamoto kubwa ambayo wanakabillana nayo ni wazazı kuwaoza watoto wao wa kike kwa siri.
Aidha kwa wale ambao kwa bahati mbaya wanaopata ujauzito (mimba) wakati bado ni wanafunzi, wanapojifungua (wanapozaa) hukataa kurudi tena.
"Changamoto kubwa ambayo tunayo ni wazazi kuwaozesha waume watoto wa kike wakati bado ni wanafunzi, lakini pia wale ambao kwa bahati mbaya walipata ujauzito (mimba) wakati bado wanasoma, hutakiwa kurudi tena skuli kuendelea na masomo yao lakini hukataa kufanya hivyo,"alisema Hidaya.
Naibu Mrajisi Hidaya alitoa wito kwa wazazi na walezi kushirikiana pamoja ili kutokomeza vitendo vya udhalilishaji ambavyo bado ni hatari sana kwa jamii.
Chanzo: Nipashe