Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Kanga zina mambo mengi, zina mengi hizo kanga,
Kanga zinaficha vingi, vinavyofichwa na kanga,
Kanga zina siri nyingi, zina siri hizo kanga,
Kanga unapoachiwa, ana penzi mwenye kanga!
Kanga zinaona mengi, chumbani ziliko kanga,
Kanga zahifadhi vingi, vyasitiriwa na kanga,
Kanga zafunika mengi, visivyoonwa bila kanga,
Kanga unapoachiwa, ana penzi mwenye kanga!
Kanga zinagusa vingi vinavyoguswa na kanga,
Kanga zapangusa pengi, papanguswapo na kanga,
Kanga zina hisa nyingi, za wadau wenye kanga,
Kanga unapoachiwa, ana penzi mwenye kanga
Kanga zinaganda vingi, visivyoganduka bila kanga,
Kanga zinashinda nyingi, kweli vitenge si kanga,
Kanga zina rangi nyingi, na misemo kwenye kanga,
Kanga unapoachiwa , ana penzi mwenye kanga.
Kanga hata kama nyingi, atakupa moja kanga,
Kanga itasema mengi, kubwa ni hilo la kanga,
Kanga yatangaza vingi, hakuna kuzidi kanga,
Kanga unapoachiwa, ana penzi mwenye kanga.
UKIMPENDA ITUNZE.
Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)
(picha kutoka Mombasa Events)