Uongozi UDSM wapewa saa 48 kuwarejesha waliosimamishwa
Habari Zinazoshabihiana
SUA yasogeza tarehe ya wanafunzi kurejea chuoni 07.05.2007 [Soma]
UDASA yapinga UDSM kuwa na makamu watatu 14.04.2006 [Soma]
UDASA yapinga UDSM kuwa na makamu watatu 14.04.2006 [Soma]
*Ni uamuzi wa Bunge la dharura la Wanafunzi
*Ladai hawakuongoza mgomo, walitekeleza maamuzi
*Pia waazimia kukiburuza chuo mahakamani
Na Hassan Abbas
HALI ya mambo bado si shwari katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) baada ya wanafunzi waliorejeshwa jana kuibua hoja nzito wakiutaka uongozi wa chuo hicho kuwarejesha wenzao 56 waliosimamishwa, bila masharti hadi kufikia kesho saa 4 asubuhi, vinginevyo mgomo mkubwa utatangazwa.
Maamuzi hayo yalifikiwa kwenye kikao cha dharura cha Bunge la Wanafunzi wa Kampasi ya Mlimani (USRC) kilichofanyika jana jioni kwenye ukumbi wa Art Theatre B (ATB).
Habari za kuaminika kutoka ndani ya kikao hicho, zinaeleza kuwa awali Bunge hilo lilikumbwa na mgawanyiko katika suala la kugoma kabla ya kufikia muafaka.
"Kikao kimepitia tathmini ya mgomo na kuona kuwa viongozi waliozuiwa kuanza masomo wamesimamishwa kimakosa kwa sababu wao si chanzo cha mgomo, bali walisimamia maamuzi halali yaliyopitishwa na Bunge la Wanafunzi ambalo linatambuliwa katika kanuni na sheria za chuo,"kilisema chanzo chetu.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Bunge hilo pia lilikubaliana katika kipindi cha kusubiri kama uongozi wa chuo utatekeleza ombi lao hadi kesho, kuwasiliana na wataalamu wa masuala ya sheria ili pia kuangalia uwezekano wa kuchukua mkondo huo katika kuhakikisha wenzao wanarejea masomoni na kufanya mitihani inayoanza wiki ijayo.
Uamuzi huo wa Bunge umetokana na ukweli kwamba karibu viongozi wote wa Serikali za Wanafunzi kwenye Kampasi za Mlimani, Chuo Kikuu cha Ardhi na Usanifu wa Majengo (UCLAS), Chuo Kishiriki cha Elimu Chan'gombe (DUCE), Chuo Kishiriki cha Elimu Mkwawa (Iringa) na Taasisi ya Habari na Mawasiliano (IJMC), wamezuiwa kwa muda usiojulikana kuanza masomo yanayoanza leo.
Mbali ya kukosa masomo, wanafunzi wengi walioripoti jana wamekuwa wakiamini kuwa viongozi hao wametolewa kafara baada ya kusimamia hoja za msingi kwa niaba ya wanafunzi wenzao.
Wanafunzi kadhaa waliozungumza na Majira kwenye Kampasi ya Mlimani mapema jana, walikiri kuwa baada ya kurejeshwa masomoni, wengi wao wanaangalia mbele hasa wakijiandaa na mitihani inayoanza wiki ijayo lakini suala la wenzao 56 bado linawachanganya.
"Hakuna kiongozi aliyeanzisha mgomo. Mgomo ulikuwa wa wanafunzi wote walioamini kuwa walikuwa na hoja ya kutaka majibu kutoka serikalini," alisema mmoja wa wanafunzi wa shahada ya uchumi kwa sharti la kutotaja jina na kuongeza:
"Hivi sasa kama unavyoona wanafunzi wengi wanahangaika kujaza fomu ili kesho (leo) waanze masomo lakini hakuna mwenye furaha anapoona viongozi ambao hawakuwa na makosa wanatolewa kafara.
"Watu wanataka kujua hatma yao ila tatizo umoja haupo kwa sababu hakuna wa kuwaongoza wafanye nini."
Katika Kampasi za Mlimani na UCLAS, gazeti hili lilishuhudia wanafunzi wakijaza fomu za aina mbili; Fomu 'A' ambayo ni ya kukubali kutii kanuni na sheria za chuo, ambayo inawabana wote walioshiriki katika mgomo kutojiingiza tena katika suala kama hilo.
Pia wanafunzi hao walikuwa wakijaza Fomu'B' ambayo ni maalumu kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza walioshindwa kulipa asilimia 40, ambayo baadaye itafanyiwa tathmini na Bodi ya Mikopo ili kuona namna ya kuwasaidia.
Wakati wanafunzi hao wakiendelea kujaza fomu hizo imebainika pia kuwa uongozi wa chuo ulikuwa umeshatoa ratiba ya mitihani katika vitivo mbalimbali ambayo imepangwa kuanza Jumatatu ijayo.
Uongozi wa chuo hicho hadi jana haukuwa umetoa tamko lolote jipya kuhusu hatma ya waliosimamishwa, hali inayoashiria kuwa msimamo unaobaki ule wa mwishoni mwa wiki wa Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandala, aliyeahidi kuwa mchakato wa kuwahoji upya wanafunzi hao 56 ungefanyika na usingechukua muda mrefu.
Alipoulizwa jana jioni kwa njia ya simu kuhusu maamuzi hayo ya Bunge la Wanafunzi, Prof. Mukandala alisema hakuwa na taarifa za kikao hicho na kuahidi kuzifanyia kazi na kutoa taarifa.
"Ndio kwanza unaniarifu kuhusu uamuzi huo, sikuwa na taarifa. Tutaliangalia hilo katika taratibu zetu na kulitolea ufafanuzi," alisema.