Kikwete avunja ukimya
2007-04-01 10:59:55
Na Mwandishi wetu
Rais Jakaya Kikwete, katika hali ya kuvunja ukimya, sasa ametoa wito kwa wananchi kila mmoja pale alipo kuhakikisha anachukua tahadhari zote muhimu kukabiliana na Homa ya Bonde la Ufa, ambayo hadi sasa imeua watu 33 na wengine 119 kuambukizwa.
Rais Kikwete alitoa wito huo jana alipohutubia Taifa kupitia redio na televisheni katika uratatibu wake aliojiwekea kila mwisho wa mwezi.
Alisema Mikoa ambayo watu wameathirika na hata baadhi yao kufariki dunia ni Manyara, Tanga, Dodoma na Morogoro na kwamba mikoa ya Dar es Salaam na Singida, pia inao wagonjwa wachache wenye kuonyesha dalili za maradhi hayo ambao wanaendelea kuchunguzwa.
Kwa upande wa mifugo, Rais Kikwete alisema mikoa iliyokumbwa na ugonjwa huo ni Dodoma, Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Tanga, Morogoro, Iringa, Singida na Mbeya.
Hata hivyo, alisema Serikali inatambua uzito wa tatizo hilo na inafanya kila iwezalo kuutokomeza ugonjwa huo.
Rais Kikwete alisema hadi sasa, serikali imechukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na ugonjwa huo ambao binadamu huupata kwa kula nyama ya mnyama aliyeathirika.
Aliitaja baadhi ya mikakati na hatua hizo kuwa ni kuzuia kufanyika kwa minada ya mifugo kote nchini, lengo likiwa ni kudhibiti kuenea kwa ugonjwa huo na kwamba minada itaruhusiwa tena kufanya kazi pindi hali itakaporejea kuwa nzuri.
Pia alisema serikali imeimarisha utoaji wa chanjo za mifugo dhidi ya ugonjwa huo kwenye maeneo yote yenye mifugo ambapo hadi sasa imetumia Sh. bilioni 1.7 kununulia chanjo na vifaa vingine vya kukabiliana na ugonjwa.
``Tayari tumeagiza dozi milioni mbili za chanjo ya RVF. Kati ya hizo, dozi 736,600 zimeshapokelewa na kusambazwa kwenye wilaya zilizoathirika na zile zilizo katika hatari ya kuambukizwa ugonjwa,`` alifafanua.
Kadhalika, alisema serikali imeandaa chini ya usimamizi wa Waziri Mkuu, mpango wa dharura wa kitaifa wa kudhibiti ugonjwa huo ambapo utagharimu dola za Kimarekani takriban milioni 12.3.
``Tunaendelea kuwasiliana na marafiki zetu wa nje kuhusu uwezekano wa kutusaidia kugharamia mpango huu mapema iwezekanavyo ili kunusuru mifugo yetu na maisha ya watu,`` aliongeza.
Aidha, alifafaunua kuwa, mnyama na mwanadamu wanaweza kupata ugonjwa huo kwa kuumwa na mbu wa aina ya Aedes mwenye wadudu wa maradhi hayo.
Alitoa wito kwa wananchi kuhakikisha kwamba, mifugo yote inapata chanjo kwa kuwa hiyo ndiyo kinga ya kwanza ya kupambana na ugonjwa huo.
Rais Kikwete alisema kwa upande wake, Serikali inafanya jitihada ili kuhakikisha kwamba dozi za kutosha za chanjo zinapatikana na kuwahimiza wana wote kupeleka mifugo yao ikachanjwe mapema iwezekanavyo.
Aliwataka pia watu kuacha tabia ya kuhamisha mifugo kutoka eneo moja kwenda eneo lingine kiholela kwa kuwa kufanya hivyo kunachangia katika kueneza ugonjwa na kurudisha nyuma jitihada za kuudhibiti.
Rais Kikwete aliwaasa watu kuepuka kuchinja wanyama na kuchuna ngozi bila kuchukua tahadhari za kujikinga pamoja na kutoshika damu, majimaji na nyama ya mnyama anayehofiwa kuwa na ugonjwa huo.
Vile vile, aliwataka watu kutokula nyama ya mnyama aliyekufa kwa ugonjwa huo na kuelezea kushangazwa kwake na taarifa za baadhi ya wanaodiriki kufukua mizoga iliyozikwa na kula nyama yake.
``Ndugu zangu, ni uchu wa kiasi gani huo unaotufanya hata tupuuze tishio kubwa kwa maisha ya mwanadamu kama hili la ugonjwa huu. Nawasihi tusikilize ushauri. Wahenga wamesema, asiyesikia la mkuu huvunjika guu,`` alihoji na kutolea mfano huo.
Hali kadhalika, alisema ni vema siku zote watu kunywa maziwa yaliyochemshwa vizur na kuwataka wataalam na watendaji kwenye ngazi ya wilaya na vijiji, kusimamia kwa ukamilifu utekelezaji wa Sheria ya Magonjwa ya Mifugo ili kudhibiti kuenea zaidi kwa ugonjwa huo.
Pamoja na yote hayo, Rais Kikwete alihimiza matumizi ya vyandarua hasa vile vilivyowekwa dawa ili kujikinga na mbu kwa kuwa ugonjwa huo huenezwa pia na mbu aina ya Aedes na kuongeza juhudi za kudhibiti mbu ili kupunguza kushamiri kwao kwenye maeneo mbalimbali nchini kwa kufukia mazalia yao na pale inapowezekana, kunyunyizia dawa.
Alivishukuru vyombo vya habari na kuvitaka kuendelea kushirikiana na kuwa na mawasiliano ya karibu na mamlaka husika na hasa wataalamu husika ili kuepuka kuandika au kutangaza habari ambazo hazijathibitika.
Alisema vyombo hivyo vinalo jukumu kubwa la kusaidia kuelimisha umma kuujua ugonjwa huu na jinsi ya kujikinga nao.
SOURCE: Nipashe