Hatimaye nipo huru

Hatimaye nipo huru

Sio busara kutaka kulinganisha watu wasiolingana. Mkuu JBourne59 amesoma elimu ya zamani sio kama hao uliowaita hapa. Kuna pengo kubwa sana kati ya elimu ya sasa na zamani.
Ni muhimu kuendelea kujifunza as long as elimination haina mwisho

Hapa sio kulinganisha zaidi ya kujua fasihi katika ubora wake...

Pole kama umekwazika!
 
Kipi hicho na ndio kwaanza Antonnia kakuita jana.
Mwenyewe ana muda sana hapa bado yuko ep 2, akawa anaulizika kama kuna nazani zingekuwepo angeshafika ep 16
Jamaniiii jamanii unanioneaaaa!! Mi hata sipendi hivo vitruuuu😎😎! Navichukiaaaaaaaaajeee! Nakuja kuendelea! Mwamba keshawafikia??? Yuko vizuri asee!!
 
Ni muhimu kuendelea kujifunza as long as elimination haina mwisho

Hapa sio kulinganisha zaidi ya kujua fasihi katika ubora wake...

Pole kama umekwazika!
Elimination? Umeniacha kidogo mkuu.
Wala sijakwazika nimekupa tu tahadhari in case kama ulikuwa hujui.
 
3. MIZUNGU

Kauli ile ya Sheikh kuwa kwa maradhi niliyonayo ni ya bara ilitukatisha tamaa kiasi cha kufanya tusijuwe la kufanya, tukarudi nyumbani kwa ajili ya kupeleka mrejesho na kufikiria kutafuta waganga wa kienyeji.

“Msiende kwa waganga wa kienyeji, nendeni kwanza kwa Shariff mtoto…” hii ilikuwa kauli ya baba baada ya kuona tutapotea njia maana yeye hakuwa mtu wa kufuatilia tabibu za kienyeji ingawaje pia hakuwa mtu wa kusali sana msikitini.

Shariff mtoto wakati huo alikuwa kiitwa Hanssen. Shariff huyu asili yao ni maeneo ya Mkwaja pia ambapo ndipo matatizo yangu yalipoanzia. Hakuwa mtoto kihivyo lakini watu walizoea kumwita hivyo maana alianza huduma za maombezi akiwa kijana mdogo kabisa.

Mashariff kwa mukhtadha wa hapa ni wale watu wanaume ambao wamekirimiwa zawadi na Mwenyezi Mungu ya kuweza kukusudia jambo na likawa. Watu walikuwa wanasema wana ‘makarama’. Wapo mashariff wa aina kuu nne kama sijakosea, wapo wale wa nasaba (kutokea kwenye kizazi cha wajukuu wa Mtume Mohammad, rehema na amani zimfikie), wapo wale wa ucha Mungu (kila mwenye kuitakasa nafsi basi aweza kuwa shariff) na wapo wale wa kukirimiwa tu na Mwenyezi Mungu kupitia mawalii wake. Inasemekana kuna hata kizazi cha paka (nyau / pussy, cats) ambao ni mashariff. Ndiyo maana haishauriwi kuwapiga paka hovyo bila sababu ya msingi maana kuna wengine ni uzao huo, wakikusudia baya basi litakupata, na hii imeenda mbali kwa viumbe wengine wengi wataambao, warukao na watembeao. Pia kuna Mashariff ‘jina’. Hawa wamepewa tu jina hilo na wazazi wao ama kujiita wao wenyewe pasi na karama zozote ama kwa kujifanya wana karama za kutibu nk.

(Habari za Mashariff ni pana na linafaa kuwa na uzi wake.)

*************

Siku iliyofuata tulienda kumtafuta Shariff mtoto, lakini hatukumkuta, tulirudi jioni nyumbani kwake ndipo tukamkuta lakini cha ajabu tulimkuta akiwa amelewa pombe aina ya mnazi.

Mnazi ni aina ya pombe igemwayo kutoka kwenye mti wa mnazi kama vile pombe aina ya ulanzi inavyogemwa.

“Njooni kesho asubuhi, muda huu siwezi kufanya kitu…” ilikuwa kauli ya Shariff Hanssen.

Tuliondoka kwa unyonge sana huku tukiwaza kama huduma ya maombezi itafanikiwa kwa hali ya ulevi ule wa pombe.

“Makarama yatamwisha huyu kwa sababu ya ulevi” kaka alisema kwa kulalamika wakati tunarejea nyumbani.

Asubuhi yake tulifika kwa Hanssen mapema ili kuona kitakachoendelea, alitukaribisha kwenye mkeka na baada ya maelezo marefu ya kaka akachukuwa kitabu kidogo akaanza kusoma kiarabu kwa haraka haraka sana kiasi kwamba hata sikuweza kujuwa anasoma kitu gani. Aliendelea kusoma hivyo kwa muda mrefu, kisha akaingia ndani akaleta ‘chetezo’ na ubani aina tatu tofauti na kendelea kusoma huku akiweka ubani kwenye chetezo chenye moto.

Baadaye akatuamuru tuwe tunaitikia dua kwa kusema ‘amin’, tulitikia dua kwa muda mrefu hatimaye akamaliza.
**********


Hali yangu kiafya ilitulia kiasi cha kama miezi miwili hivi lakini baadaye maruweruwe yakanirudia tena. Nakawa nikilala usiku naona ndoto za kama napaa hivi juu ya ardhi na kuiangalia dunia kama mwewe vile aangaliavyo chini akiwa hewani, siku nyingine naota nipo msituni peke yangu kama nimepotea hivi natafuta njia ya kutokea barabarani, siku nyingine naota nipo mwenye mji wa ajabu wenye miamba ya mawe mengi watu wakiwa wanataabika na hali za huko mie nakuwa nawasaidia nk.

Siku nikiota ndoto za namna hiyo tu, asubuhi yake napata homa kali kiasi cha kushindwa kula vizuri hali iliyopeleka afya yangu kuzidi kudhoofu, lakini pia nikawa kama vile naona yatakayotokea muda ujao japo siyo kwa asilimia mia lakini inakuwa vivyohiyo. Kwa mfano, naweza kulala hata mchana nikaona / kuota kama kutakuwa na msiba jirani, basi kweli haipiti muda tunapata taarifa za msiba na mambo ya ajabu ajabu kama hayo.

Hali yangu iliendelea kuwa mbaya mpaka familia ikaamua nianze kujaribu tiba za kienyeji. Ndipo nilipo pelekwa Mlingotini – Bagamoyo. Tulipitia njia ya kaole kisha kuingia ndani upande wa kulia ndani ndani kabisa kwa kuulizia kwa Mzee wa tiba, mganga maarufu Mlingotini. Nilikuwa kijana barobaro tu wa miaka kumi na mitano hivi kuelekea kumi sita na wala sikuwa nawajuwa wanawake.

Elimu ya sekondari sikuchaguliwa kuendelea na wala wazazi hawakujishughulisha kuhusu mimi kwenda Sekondari, haikuwa kipaumbele sana kwa watu wa ukanda wetu, tulikuwa tunarithi kazi za baba zetu tu.

Baada ya mapokezi ya pale kwa mganga tulisubirishwa na kundi wa wateja wengine wapatao wane hivi pale. Kila mmoja alikuwa anaitwa ndani kwenye kilinge cha Mzee wa tiba.

Ilipowadia zamu yangu niliitwa na kuelekezwa kukaa kwa kunyoosha miguu uelekea upande jua linapo chomozea (mashariki). Mpaka hapo hatukuwa tumesema chochote kwa mganga. Akauliza jina langu na la mama yangu kisha akaanza kusema maneno yasiyoeleweka pale na vimbwanga kibao hatimaye akatikisa kichwa na kutulia.

“Kijana!” aliniita yule mganga, nikatoa tu macho kwa kumuangalia. Yeye akaendelea kusema kwa sauti nzito…

“Kijana, umerogwa!”
“Umehangaika sana bila suluhu lakini hapa sasa umefika!”

Kwa mganga huyu tulienda watu watatu, yani mimi, Kaka mkubwa pamoja na mama yangu mzazi. Ilikuwa ni mwendo mrefu wa kutembea, maana tulivizia basi la MFDC (Mbegani Fisheries Development Centre) lililokuwa likiwapeleka wafanyakazi na familia za wafanyakazi kwenye Chuo cha maendeleo ya uvuvi Mbegani Bagamoyo. Tulishukia mbele kidogo ya kaole na safari ya kutembea kwa miguu ikaanza kuelekea huko kwa Mzee wa Tiba Milingotini ndani ndani.

“Eeee wanatakiwa kuku wawili, jogoo mwekundu na tetea mweusi…” alisema yule mzee wa tiba kwa sauti nzito.

“Eeee kuku wawe wamekomaa kiasi cha kuwa na ukucha mrefu juu ya miguu…” aliendelea.

Mimi na kaka tukawa tunatazamana, lakini mama akawa anasikiliza kwa makini.

“Baba, tumetoka mbali, hao kuku tutawapata wapi na ni hatua kurudi kuwatafuta…” Mama alimsemeza yule mganga.

“Hahahahhaa…. Hahahahaha…” Mganga alicheka kwa sauti nzito kisha akasema kuwa kuku watapatikana.

“kuku watapatikana, kuku watapatikana, kuku watapatikana…” sauti ya mganga ikawa inafifia kisha akainamisha kichwa.


Pale kilingeni kulikuwa pia kuna wasaidizi wawili wa mganga, mmoja ni kijana wa kiume na mwingine ni mdada wa makamo ambao wote walikuwa wamevaa kawaida tu isipokuwa mganga mwenyewe alikuwa amevaa kaniki, kilemba cheupe huku ameshika usinga wenye shanga kadhaa .

Pembeni ya chumba kulikuwa na makopo mengi yaliyo na mizizi iliyosagwa (dawa) na upande mwingine kulikuwa na vibuyu vidogo vidogo kadhaa ambavyo sikujuwa mara moja ndani yake kuna nini. Sehemu nyingine kulikuwa na kitambaa chekundu kilichofunika vitu ambavyo pia sikujuwa ni nini.

Mara yule mzee wa tiba akainua kichwa na kuwauliza wale wasaidizi wake…

“Wamesemaje…?” aliuliza mganga kwa sauti ya kawaida huku akiwaangalia wale wazaidizi wake.

Wakaumueleza kuwa kunatakiwa jogoo na tetea. Basi mganga akawambia yule kijana akachukuwe hao kuku bandani.

Kulikuwa na banda maalumu la kuku wenye rangi moja moja tofauti. Yani kuku weupe tu, kuku weusi tuu na kuku wekundu tu lakini wote waliweka pamoja.

“Tiba yako kijana itaanza kwa kafara ya kuku hao wawili… hebu nifuateni” alisema yule mganga huku akitoka nje ya kilinge na kwenda eneo la uwazi ambalo kwa dalili zote palikuwa panaonyesha kuwa ni machinjio ya kuku maana kulitapakaa damu za kuku zilizoganda.

Kuku wale walichinjwa kila mmoja kwa wakati wake, baada ya kuku kupapatika na kufa mzee wa tiba alikuwa ‘anatolea macho’ miguu, mabawa, shingo na ueleko wa kuku maana walikuwa wakichinjwa wanaachwa wapapatike hadi wafe.

“Njia imefunga” alisikika mganga akisema baada ya kumchinja yule tetea mweusi.
“Magharibi” aliropoka yule mzee wa tiba, hiyo ni baada ya kumchinja kuku wa pili ambaye ni jogoo.

Basi tukaambiwa tukae nje tusubiri na wale kuku walichukuliwa na yule mdada msaidizi na kutoweka nao upande mwingine wa nyumba.

Mganga aliingia tena kilingeni na kuita wateja wengine waliokuja baada ya sisi.

Tulisubiri pale nje hadi njaa ikaanza kuniuma maana ilikuwa inakaribia saa nane mchana. Mara akaja yule kijana msaidizi wa mganga na kutuita ulekeo wa jamvi safi kwa ajili ya chakula. Kilikuwa chakula maalumu kilichoandaliwa kwa ajili yetu sisi, kulikuwa na ugali, samaki pamoja na vibakuli vitatu vya finyango za kuku.

“Wewe bakuli lako hili” alisema yule kijana huku akinionesha upande wa kukaa.

Wakati nakula ndiyo nikagundua niliwekewa maini, firigizi na miguu ya kuku wakati mama na kaka wao niliona baadaye wakila vipapatio.

Kulikuwa na makundi mengi yanayokula muda huo na mtindo ulikuwa ni huo huo wa vibakuli vibakuli.

Baada ya maakuli, kila mteja alikuwa akiitwa kilingeni na kupewa dawa na maelekezo ya kutumia. Zamu yetu ilipofika mganga akasema, kazi yangu kubwa maana imeegemea magharibi na njia imefunga. Hivyo tujiandae kwa kafara kubwa ya kondoo. Tutafute wenyewe. Ujira wa kazi alisema tuweka kwenye mtungi kiasi chochote ambapo mama alienda kuweka, sikujuwa hata ameweka kiasi gani lakini nilisikia sauti za sarafu zikilia, pia tulilipishwa kuku wawili kwa bei ya sokoni tu.

Hata hivyo nilipewa dawa za kutumia na maelekezo yake. Baadhi ya dawa zilikuwa majani fulani sijapata kuyaona tangia nizaliwe, yanalowekwa kwenye maji ya kuogea kisha kila nikitaka kuoga niliambiwa niwe nachanganyia maji hayo ya majani ya ajabu ajabu, dawa nyingine ilikuwa ya kupaka kama mafuta lakini yalikuwa meusi ti! Yalikuwa kimiminika, unajipaka mwili mzima, kali kupita yote nilipewa mafuta fulani ya kupata nyayoni, viganyani na usoni usiku tu wakati nataka kulala lakini ilikuwa inanuka balaa! Ilikuwa inanuka kuliko mafuta yatumikayo ‘kukarafati’(siyo kukarabati) vyombo vya baharini kwa sufi na mafuta ‘makasamala’.
**********

Inaendelea
Waganga wanakula sana hivi vitoweo kuku mbuzi kondoo ng'ombe za wateja sanaaa!
leadermoe Bado naendelea
 
4. KAFARA

Nilitumia dawa zile kwa wiki moja na hali yangu ilionekana kama kutulia, kaka mkubwa naye aliagizwa aende mazizini (Bagamoyo jirani na kwa Kafumbo ambaye alikuwa anamiliki mgodi wa kutengeneza chumvi), kule kulikuwa na mazizi mengi ya mifugo ambayo yalikuwa yanamilikiwa na wafugaji mbali mbali.

Siku hizi eneo hilo kumejaa mahoteli ya kitalii sijui kama bado kuna mazizi ya mifugo.

Baada ya siku kumi hivi tangia nitumie zile dawa kutoka Mlingotini, safari ya kwenda huko tena ikawadia ambapo safari hii Baba, Mama, kaka mkubwa, dada yangu tulienda wote. Baba alienda kwa mzee Kafumbo kuomba usafiri wa kutupeleka Mlingotini.

Mzee Kafumbo alikuwa na gari zuri Landrover 109 pickup TZ-61.

Tukapakia Kondoo wetu mwenye rangi mchanganyiko wa nyeupe na nyeusi kwa maelekezo ya mzee wa tiba, alikuwa na pembe zilizopinda na sikujuwa hata alinunuliwa kwa kiasi gani, baba na mama wakapanda mbele, mimi , kaka na dada tukapanda nyuma, dereva alikuwa mtoto wa mzee Kafumbo.

Haikuchukuwa muda mrefu tukafika, tukapokelewa kisha kijana wa Kafumbo akaondoka na land rover kurudi mjini kuendelea na majukumu mengine.

Ilikuwa majira ya saa tatu hivi asubuhi tulipo wasili eneo hilo kwa mzee wa tiba, tulikaribishwa vizuri kisha yule kondoo akachukuliwa na kijana wa mzee wa tiba na kufunga kwenye kigogo pembeni kidogo ya eneo la machinjio ya kuku.

“Tiba ya leo ni kiboko!” alisikika yule mzee akisema kwa sauti ya kawaida.
“Tiba hii kwa hapa Tanzania nimeifanya kwa watu wawili tu kwa umri wangu huu” aliendelea yule mzee wa tiba kuongea huku akiendelea kufanya kazi zake ndogondogo.

“Mtu wa kwanza kumfanyia tiba hii ni kiongozi mkubwa wa kisiasa na wa pili ni mama mmoja hivi miaka ya nyuma…” aliendelea huku akifungua kasha maalumu liliokuwa na vitu mfano wa visu.

“Kafara nyingi za wanyama wenye miguu mine huwa nafanya kwa kuchinja, lakini kwa aina ya maradhi ya huyu kijana imenibidi nifanye kafara hii ambayo najuwa haiwezi kudunda…” alisema kwa kujigamba.

Mara akamwita yule kijana msaidizi wake na kumkabidhi visu vikali vitatu na kumwambia akamchune / kukwangua yule kondoo manyoya yake abakie na ngozi tu tena akiwa hai.

Nilishtuka sana kuona kondoo anaenda kuchunwa ngozi akiwa hai, nikamuangalia kaka mkubwa naye akanitazama lakini hatukusema neno. Mganga akatuamuru sisi tubaki nje na yeye akaingia ndani na wazazi watu. Huko sikujuwa kilichoendelea.

Huku nje, yule kijana akawa anamnyoa manyoya yule kondoo, kidogo moyo wangu ukatulia maana nilidhani anachunwa ngozi akiwa hai. Kwa ustadi mkubwa aliendelea kumnyoa zoezi lililochukuwa saa kadhaa kabla ya kumaliza na wakati huo tayari juwa lilikuwa juu ya utosi, ambapo ndio muda aliosema mzee wa tiba kuwa unafaa kwa kuanza kufanya kafara.

Kondoo akiwa hai, tayari akiwa amekwanguliwa manyoya yake karibu yote, akachukuliwa na mzee wa tiba na kuanza kumchorachora mavitu ambayo sikuyaelewa kwenye mwili wake kwa kutumia kijiti maalum na wino mwekundu (zafarani?)

Wakati yeye akiendelea kumchora yule kondoo, alimuambia yule kijana aandae ‘ziara’. Sikuelewa mara moja ziara ipi tena lakini nikaona yule kijana ameenda kuchukuwa jembe na sepetu / beleshi (spade) na kwenda pambeni kidogo ya msitu wa miembe iliyopo hapo jirani na kuanza kuchimba. Baadaye nilikuja kujuwa kumbe alikuwa anachimba kaburi. Moja kwa moja nikajuwa hapa ndipo atakapozikiwa huyu kondoo.

Muda wa kula ukafika, safari hii tulikuwa kwa jumuiya lakini wanaume peke yetu na wanawake peke yao na wala hapakuwa na vibakuli vya kupimiwa finyango za nyama ya kuku. Tulikuwa vyema tukashiba kisha mzee wa tiba akaendelea na zoezi lake la kuandika kwenye mwili wa kondoo na yule kijana akimalizia kuchima kaburi maana ardhi ya eneo lile haikuwa ngumu.

Mzee wa tiba akamaliza zoezi la kuandika kwenye mwili wote wa kondoo kisha akachukuwa shuka nyepesi nyeupe nayo akaanza kuichorachora mistari mistari na mikato mikato isiyoeleweka na maandishi kama ya kiarabu lakini yenye usanifu tofauti kabisa sijapata kuona, shuka lile lote likaenea wino wa michoro na maandishi. Alikuwa ananakili kutoka katika kitabu fulani hivi kuukuu. Sanjali na kondoo pia kulikuwa na ‘nazi kavu’ saba (inasemekana zilizo anguka zenyewe kutoka juu ya minazi), mayai viza saba, chungu cha kupikia na vifaa ambavyo sikuona vyote mara moja kwenye ambayo vilikuwa kwenye ungo, lakini niliona chumvi, mtama, kitu kama buni (kahawa) na vingine vingi sivikumbuki.

Tukaiwa wote kwenye kilinge cha nje ya nyumba, tukakaa kama nusu duara hivi, kukaletwa jiko la mkaa na chungu kikabandikwa, kondoo akasogezwa jirani, mayai na nazi nazo ziliwekwa chini kwenye jamvi. Mzee wa tiba akaanza kwa kusoma pale haraka haraka sana kisha akawa anaweka mavitu yale yaliyokuwemo kwenye ungo ndani ya chungu huku yule msaidizi wa kike akikoroga…
Zoezi iliendelea kwa muda, yule kijana akaamriwa amfungue kondoo Kamba zote, muda wote kondoo alikuwa akilia kwa namna ya kuomba msaada
(wafugaji watanielewa)

Baada ya kufunguliwa Kamba, kondoo badala ya kukimbia, aliendelea kutulia huku makamasi yake yakimchuruzika. Mzee alizidi kusoma mavitu yake, chungu kilizidi kukarangizwa mavitu yasiyoeleweka na kutatarika na kondoo alizidi kutulia, akaacha kulia na hatimaye akalala kwa namna ya kupumzika huku akihema kwa kasi.

Chungu kilikamilika kukarangizwa kikaipuliwa na kubandikwa chungu kingine chenye majani ya aina tofauti tofauti na kufunikwa. Kondoo aliendelea kulala chini na safari hii alilaza kichwa chake chini kama vile amezirai au amekufa. Yule mgaga akachukuwa lile shuka lenye maandishi mengi mekundu na kumfunika na akaendelea kusoma.

Baada ya muda mzee wa tiba alimuamuru yule kijana msaidizi wake ambebe yule kondoo akiwa na shuka lake waelekee kwenye kaburi. Pia sisi alitupa ishara ya kwamba tumfuate, tulienda sote isipokuwa yule dada msaidizi na mama. Kufika kule yule kijana akaambiwa amuweke kondoo kwenye kaburi, ambapo alivyomshusha tu, kondoo hakulala tena bali alisimama lakini bila kupiga kelele, alikuwa kama amezubaa hivi, huku akiwa na shuka lake mgongoni.

Mzee wa tiba aliendelea kusoma mavitu yake hadi kondoo akalala tena chini, kijana akaambiwa amfunike vizuri shuka kisha akaendelea kusoma huku anaweka udongo kwenye kaburi. Zoezi liliendelea hadi kondoo alipozikwa (akiwa hai?)

Juu ya kaburi halikuinuliwa kama makaburi mengine bali paliwekwa ‘levo’ ya usawa wa ardhi, kisha akatuambia turudi kule kilingeni zoezi bado linaendelea.

Kufika kule kilingeni nikapewa kidoga na kuamriwa nikae hapo, kisha kile chungu ambapo kilikuwa tayari kimechemka haswa kikaletwa mbele yangu na kisha nikaona nafunikwa shuka kubwa na kuambiwa niachame mdomo halafu chungu kikafunuliwa.
Lo salale! Hewa ikaanza kuwa nzinto ndani ya shuka nikawa kama nakosa hewa (nakosa pumzi), mwili wote ukajaa jasho kiasi cha nguo nilizovaa kulowa chapachapa. Baadaye nikazoea hali hile ya hewa chache na baada ya dakika chache tu nikafunuliwa wakaniangalia kisha wakanifunika tena. Zilikuwa ni zoezi la kama dakika kumi hivi lakini niliona kama ni saa nzima.

Baada ya zoezi hilo niliambiwa nikae kwenye mkeka nivue shati ambalo kwa wakati huo lilikuwa halitamaniki kwa jasho. Nikamuona yule dada msaidizi wa mganga ameshika kiwembe kipya aina ya topaz…
“Tulia nikuchanje eee mdogo wangu, utapona tu” alisema yule dada.

Kusema ukweli baada ya kutoka ndani ya lile shuka nilijisikia vizuri sana, nilipumua vizuri na kujihisi nina afya ‘tele’. Katika maisha yangu hadi wakati huo nilikuwa sijawahi kuchanjwa hata mara moja, hivyo lile zoezi lilikuwa la kuogofya sana kwangu. Nahisi yule dada aliniona na kuelewa hisia zangu ndiyo maana akanituliza kwa maneno yake na sauti nyororo ya kuliwaza.

Nilichanjwa kichwani chale mbili mbili utosini, kwenye paji la uso mwanzo wa nywele na kisogoni. Pia aliendelea kunichanja kifuani, mikononi na miguuni halafu akazunguka mgongoni ambapo alinichanja nyuma ya shingo na kiunoni. Mwote humo alikuwa akichanja chale mbilimbili ndogo ndogo kwa haraka sana na kila sehemu alipochanja damu ilikuwa inatoka.

Yule dada akaletewa kibuyu ambacho ndani kulikuwa na dawa ya kimiminika kama mafuta hivi meusi na kuanza kupipaka kwa mtiririko kama alivyo nichanja. Alipomaliza akapewa kikopo kingine cha dawa ya unga unga mweusi na kupaka sehemu zote zilizochanjwa bila kufuata mpangilio. Alipomaliza alinielekeza nitulie pembeni kwenye mkeka. Hapo nilikuwa nasikilizia maumivu ya chale pamoja na hii dawa ya pili ya unga unga maana ilikuwa inauma sana.
**********

Zoezi liliisha kwa wazazi wangu kupewa maelekezo mengine kisha wakapewa zile nazi zote na mayai yote tukaanza safari ya kurudi barabarani ili kufika njia kuu ya Kaolee. Wakati tupo njiani kabla ya kufika barabara kuu ya Kaole kuna njia panda fulani hivi za watembea kwa miguu, nikaona baba anavuja zile nazi moja baada ya nyingine huku mdomo kama anasema vitu ambavyo sikuvisikia. Nazi zote saba zikaisha, tukawa tunaendelea na safari ya kwenda barabara kuu.

Kabla hatujatokeza barabara kuu, nikapewa yale mayai moja baada ya jingine na kuamriwa kurusha kinyume nyume bila kuangalia nyuma hadi yakaisha yote. Muda huo wote tupo kimya na tukawa tumekaribia kabisa barabara kuu ambayo ilikuwa ni ya vumbi.

Ilikuwa inaelekea majira ya saa kumi na moja hivi jioni, hivyo tulichelewa lile basi la Mbegani, ikabidi tuketi chini kusubiria usafiri mwingine lakini ni wa kubahatisha maana mabasi ya kutokea Dar es Salaam yalikuwa yakipita njia ya Zinga-Kiromo-Ukuni hadi mjini Bagamoyo wakati sisi njia tuliyopo ni ya Zinga -Pande -Kaole -Mjini Bagamoyo.

Kwa bahati nzuri baada kama ya dakika arobaini hivi za kusubiri likaja basi moja kutoka Dar es Salaam linalomikikiwa na Shariff wa Bondeni, basi hilo kwa jina maarufu likikuwa linaitwa UWEMBE na kwa siku hiyo alikuwa analiendesha dereva mmoja aitwaye Mantibo.

Basi lilikuwa limejaza sana maana lilikuwa ‘linaokota’ abiria wote kwa kuwa njia hiyo haikuwa na mabasi mengi hivyo ilikuwa ni namna pia ya kusaidia abiria licha ya jambo la biashara.

Tulifika nyumbani jua likiwa limeshazama, Mama aliniambia nisioge siku hiyo hadi kesho, nikapewa dawa na mama za kunywa usiku huo na asubuhi pia na kuendelea kufanya hivyo kwa siku saba.
**********

Inaendelea
"Hii kafara ya Leo kiboko Nimetibu Watu wasiliana tu mmoja akiwa kiongozi maarufu" Mganga alikua na mbwembwe huyooi doh!!
leadermoe hivi Kwanini njiapanda inatumika sana katika hayo mambo ya 👽???
Bado Naendelea kusoma 🙇
 
"Hii kafara ya Leo kiboko Nimetibu Watu wasiliana tu mmoja akiwa kiongozi maarufu" Mganga alikua na mbwembwe huyooi doh!!
leadermoe hivi Kwanini njiapanda inatumika sana katika hayo mambo ya ???
Bado Naendelea kusoma
Kwa kweli labda mshana ana jb mie walaaa, mweupe pande hizo
 
Niwache na sauti yangu ya kukotoma ka churaaa🙃
Hiii sister mawigi Antonnia naijua hiyoi
Screenshot_20230219-035232_1.jpg
 
Back
Top Bottom