4. KAFARA
Nilitumia dawa zile kwa wiki moja na hali yangu ilionekana kama kutulia, kaka mkubwa naye aliagizwa aende mazizini (Bagamoyo jirani na kwa Kafumbo ambaye alikuwa anamiliki mgodi wa kutengeneza chumvi), kule kulikuwa na mazizi mengi ya mifugo ambayo yalikuwa yanamilikiwa na wafugaji mbali mbali.
Siku hizi eneo hilo kumejaa mahoteli ya kitalii sijui kama bado kuna mazizi ya mifugo.
Baada ya siku kumi hivi tangia nitumie zile dawa kutoka Mlingotini, safari ya kwenda huko tena ikawadia ambapo safari hii Baba, Mama, kaka mkubwa, dada yangu tulienda wote. Baba alienda kwa mzee Kafumbo kuomba usafiri wa kutupeleka Mlingotini.
Mzee Kafumbo alikuwa na gari zuri Landrover 109 pickup TZ-61.
Tukapakia Kondoo wetu mwenye rangi mchanganyiko wa nyeupe na nyeusi kwa maelekezo ya mzee wa tiba, alikuwa na pembe zilizopinda na sikujuwa hata alinunuliwa kwa kiasi gani, baba na mama wakapanda mbele, mimi , kaka na dada tukapanda nyuma, dereva alikuwa mtoto wa mzee Kafumbo.
Haikuchukuwa muda mrefu tukafika, tukapokelewa kisha kijana wa Kafumbo akaondoka na land rover kurudi mjini kuendelea na majukumu mengine.
Ilikuwa majira ya saa tatu hivi asubuhi tulipo wasili eneo hilo kwa mzee wa tiba, tulikaribishwa vizuri kisha yule kondoo akachukuliwa na kijana wa mzee wa tiba na kufunga kwenye kigogo pembeni kidogo ya eneo la machinjio ya kuku.
“Tiba ya leo ni kiboko!” alisikika yule mzee akisema kwa sauti ya kawaida.
“Tiba hii kwa hapa Tanzania nimeifanya kwa watu wawili tu kwa umri wangu huu” aliendelea yule mzee wa tiba kuongea huku akiendelea kufanya kazi zake ndogondogo.
“Mtu wa kwanza kumfanyia tiba hii ni kiongozi mkubwa wa kisiasa na wa pili ni mama mmoja hivi miaka ya nyuma…” aliendelea huku akifungua kasha maalumu liliokuwa na vitu mfano wa visu.
“Kafara nyingi za wanyama wenye miguu mine huwa nafanya kwa kuchinja, lakini kwa aina ya maradhi ya huyu kijana imenibidi nifanye kafara hii ambayo najuwa haiwezi kudunda…” alisema kwa kujigamba.
Mara akamwita yule kijana msaidizi wake na kumkabidhi visu vikali vitatu na kumwambia akamchune / kukwangua yule kondoo manyoya yake abakie na ngozi tu tena akiwa hai.
Nilishtuka sana kuona kondoo anaenda kuchunwa ngozi akiwa hai, nikamuangalia kaka mkubwa naye akanitazama lakini hatukusema neno. Mganga akatuamuru sisi tubaki nje na yeye akaingia ndani na wazazi watu. Huko sikujuwa kilichoendelea.
Huku nje, yule kijana akawa anamnyoa manyoya yule kondoo, kidogo moyo wangu ukatulia maana nilidhani anachunwa ngozi akiwa hai. Kwa ustadi mkubwa aliendelea kumnyoa zoezi lililochukuwa saa kadhaa kabla ya kumaliza na wakati huo tayari juwa lilikuwa juu ya utosi, ambapo ndio muda aliosema mzee wa tiba kuwa unafaa kwa kuanza kufanya kafara.
Kondoo akiwa hai, tayari akiwa amekwanguliwa manyoya yake karibu yote, akachukuliwa na mzee wa tiba na kuanza kumchorachora mavitu ambayo sikuyaelewa kwenye mwili wake kwa kutumia kijiti maalum na wino mwekundu (zafarani?)
Wakati yeye akiendelea kumchora yule kondoo, alimuambia yule kijana aandae ‘ziara’. Sikuelewa mara moja ziara ipi tena lakini nikaona yule kijana ameenda kuchukuwa jembe na sepetu / beleshi (spade) na kwenda pambeni kidogo ya msitu wa miembe iliyopo hapo jirani na kuanza kuchimba. Baadaye nilikuja kujuwa kumbe alikuwa anachimba kaburi. Moja kwa moja nikajuwa hapa ndipo atakapozikiwa huyu kondoo.
Muda wa kula ukafika, safari hii tulikuwa kwa jumuiya lakini wanaume peke yetu na wanawake peke yao na wala hapakuwa na vibakuli vya kupimiwa finyango za nyama ya kuku. Tulikuwa vyema tukashiba kisha mzee wa tiba akaendelea na zoezi lake la kuandika kwenye mwili wa kondoo na yule kijana akimalizia kuchima kaburi maana ardhi ya eneo lile haikuwa ngumu.
Mzee wa tiba akamaliza zoezi la kuandika kwenye mwili wote wa kondoo kisha akachukuwa shuka nyepesi nyeupe nayo akaanza kuichorachora mistari mistari na mikato mikato isiyoeleweka na maandishi kama ya kiarabu lakini yenye usanifu tofauti kabisa sijapata kuona, shuka lile lote likaenea wino wa michoro na maandishi. Alikuwa ananakili kutoka katika kitabu fulani hivi kuukuu. Sanjali na kondoo pia kulikuwa na ‘nazi kavu’ saba (inasemekana zilizo anguka zenyewe kutoka juu ya minazi), mayai viza saba, chungu cha kupikia na vifaa ambavyo sikuona vyote mara moja kwenye ambayo vilikuwa kwenye ungo, lakini niliona chumvi, mtama, kitu kama buni (kahawa) na vingine vingi sivikumbuki.
Tukaiwa wote kwenye kilinge cha nje ya nyumba, tukakaa kama nusu duara hivi, kukaletwa jiko la mkaa na chungu kikabandikwa, kondoo akasogezwa jirani, mayai na nazi nazo ziliwekwa chini kwenye jamvi. Mzee wa tiba akaanza kwa kusoma pale haraka haraka sana kisha akawa anaweka mavitu yale yaliyokuwemo kwenye ungo ndani ya chungu huku yule msaidizi wa kike akikoroga…
Zoezi iliendelea kwa muda, yule kijana akaamriwa amfungue kondoo Kamba zote, muda wote kondoo alikuwa akilia kwa namna ya kuomba msaada
(wafugaji watanielewa)
Baada ya kufunguliwa Kamba, kondoo badala ya kukimbia, aliendelea kutulia huku makamasi yake yakimchuruzika. Mzee alizidi kusoma mavitu yake, chungu kilizidi kukarangizwa mavitu yasiyoeleweka na kutatarika na kondoo alizidi kutulia, akaacha kulia na hatimaye akalala kwa namna ya kupumzika huku akihema kwa kasi.
Chungu kilikamilika kukarangizwa kikaipuliwa na kubandikwa chungu kingine chenye majani ya aina tofauti tofauti na kufunikwa. Kondoo aliendelea kulala chini na safari hii alilaza kichwa chake chini kama vile amezirai au amekufa. Yule mgaga akachukuwa lile shuka lenye maandishi mengi mekundu na kumfunika na akaendelea kusoma.
Baada ya muda mzee wa tiba alimuamuru yule kijana msaidizi wake ambebe yule kondoo akiwa na shuka lake waelekee kwenye kaburi. Pia sisi alitupa ishara ya kwamba tumfuate, tulienda sote isipokuwa yule dada msaidizi na mama. Kufika kule yule kijana akaambiwa amuweke kondoo kwenye kaburi, ambapo alivyomshusha tu, kondoo hakulala tena bali alisimama lakini bila kupiga kelele, alikuwa kama amezubaa hivi, huku akiwa na shuka lake mgongoni.
Mzee wa tiba aliendelea kusoma mavitu yake hadi kondoo akalala tena chini, kijana akaambiwa amfunike vizuri shuka kisha akaendelea kusoma huku anaweka udongo kwenye kaburi. Zoezi liliendelea hadi kondoo alipozikwa (akiwa hai?)
Juu ya kaburi halikuinuliwa kama makaburi mengine bali paliwekwa ‘levo’ ya usawa wa ardhi, kisha akatuambia turudi kule kilingeni zoezi bado linaendelea.
Kufika kule kilingeni nikapewa kidoga na kuamriwa nikae hapo, kisha kile chungu ambapo kilikuwa tayari kimechemka haswa kikaletwa mbele yangu na kisha nikaona nafunikwa shuka kubwa na kuambiwa niachame mdomo halafu chungu kikafunuliwa.
Lo salale! Hewa ikaanza kuwa nzinto ndani ya shuka nikawa kama nakosa hewa (nakosa pumzi), mwili wote ukajaa jasho kiasi cha nguo nilizovaa kulowa chapachapa. Baadaye nikazoea hali hile ya hewa chache na baada ya dakika chache tu nikafunuliwa wakaniangalia kisha wakanifunika tena. Zilikuwa ni zoezi la kama dakika kumi hivi lakini niliona kama ni saa nzima.
Baada ya zoezi hilo niliambiwa nikae kwenye mkeka nivue shati ambalo kwa wakati huo lilikuwa halitamaniki kwa jasho. Nikamuona yule dada msaidizi wa mganga ameshika kiwembe kipya aina ya topaz…
“Tulia nikuchanje eee mdogo wangu, utapona tu” alisema yule dada.
Kusema ukweli baada ya kutoka ndani ya lile shuka nilijisikia vizuri sana, nilipumua vizuri na kujihisi nina afya ‘tele’. Katika maisha yangu hadi wakati huo nilikuwa sijawahi kuchanjwa hata mara moja, hivyo lile zoezi lilikuwa la kuogofya sana kwangu. Nahisi yule dada aliniona na kuelewa hisia zangu ndiyo maana akanituliza kwa maneno yake na sauti nyororo ya kuliwaza.
Nilichanjwa kichwani chale mbili mbili utosini, kwenye paji la uso mwanzo wa nywele na kisogoni. Pia aliendelea kunichanja kifuani, mikononi na miguuni halafu akazunguka mgongoni ambapo alinichanja nyuma ya shingo na kiunoni. Mwote humo alikuwa akichanja chale mbilimbili ndogo ndogo kwa haraka sana na kila sehemu alipochanja damu ilikuwa inatoka.
Yule dada akaletewa kibuyu ambacho ndani kulikuwa na dawa ya kimiminika kama mafuta hivi meusi na kuanza kupipaka kwa mtiririko kama alivyo nichanja. Alipomaliza akapewa kikopo kingine cha dawa ya unga unga mweusi na kupaka sehemu zote zilizochanjwa bila kufuata mpangilio. Alipomaliza alinielekeza nitulie pembeni kwenye mkeka. Hapo nilikuwa nasikilizia maumivu ya chale pamoja na hii dawa ya pili ya unga unga maana ilikuwa inauma sana.
**********
Zoezi liliisha kwa wazazi wangu kupewa maelekezo mengine kisha wakapewa zile nazi zote na mayai yote tukaanza safari ya kurudi barabarani ili kufika njia kuu ya Kaolee. Wakati tupo njiani kabla ya kufika barabara kuu ya Kaole kuna njia panda fulani hivi za watembea kwa miguu, nikaona baba anavuja zile nazi moja baada ya nyingine huku mdomo kama anasema vitu ambavyo sikuvisikia. Nazi zote saba zikaisha, tukawa tunaendelea na safari ya kwenda barabara kuu.
Kabla hatujatokeza barabara kuu, nikapewa yale mayai moja baada ya jingine na kuamriwa kurusha kinyume nyume bila kuangalia nyuma hadi yakaisha yote. Muda huo wote tupo kimya na tukawa tumekaribia kabisa barabara kuu ambayo ilikuwa ni ya vumbi.
Ilikuwa inaelekea majira ya saa kumi na moja hivi jioni, hivyo tulichelewa lile basi la Mbegani, ikabidi tuketi chini kusubiria usafiri mwingine lakini ni wa kubahatisha maana mabasi ya kutokea Dar es Salaam yalikuwa yakipita njia ya Zinga-Kiromo-Ukuni hadi mjini Bagamoyo wakati sisi njia tuliyopo ni ya Zinga -Pande -Kaole -Mjini Bagamoyo.
Kwa bahati nzuri baada kama ya dakika arobaini hivi za kusubiri likaja basi moja kutoka Dar es Salaam linalomikikiwa na Shariff wa Bondeni, basi hilo kwa jina maarufu likikuwa linaitwa UWEMBE na kwa siku hiyo alikuwa analiendesha dereva mmoja aitwaye Mantibo.
Basi lilikuwa limejaza sana maana lilikuwa ‘linaokota’ abiria wote kwa kuwa njia hiyo haikuwa na mabasi mengi hivyo ilikuwa ni namna pia ya kusaidia abiria licha ya jambo la biashara.
Tulifika nyumbani jua likiwa limeshazama, Mama aliniambia nisioge siku hiyo hadi kesho, nikapewa dawa na mama za kunywa usiku huo na asubuhi pia na kuendelea kufanya hivyo kwa siku saba.
**********
Inaendelea