Hadithi: Wakili wa moyo

Hadithi: Wakili wa moyo

Aisee ukiwa unaiendeleza hii hadithi uwe unanitag ... sawa? ?? Lasivyo manundu yatakuhusu.

Hahahaaa., acha mkwara mbuzi bucho, kwanza leo lazima fimbo zikuhusu, umechezea sembe ya familia.
 
Hahahaaa., acha mkwara mbuzi bucho, kwanza leo lazima fimbo zikuhusu, umechezea sembe ya familia.

Haha.... nishakula mikwaju ya kutosha. Hapa nipo kwenye gunia. Dingi ameniweka tokea asubuhi
 
Kwa heshima na taadhima naomba niendeleze hii hadithi hadi mkuu mkuu mizambwa arudi. Kisha ataebdelea kutokea hapo.

Hahahaha., bucho avatar yako tu inaonesha ulivyo mbishi, ila mizambwa naye anazingua bana., Big up mkuu
 
Last edited by a moderator:
Hahahaha., bucho avatar yako tu inaonesha ulivyo mbishi, ila mizambwa naye anazingua bana., Big up mkuu

Hahahaha...yan mkuu umenena haswaaa....mi nikiangalia hyo avatar nikarelate na mambo ya mwenye hyo avatar sina mbavu....
 
Last edited by a moderator:
Buchooo upo wapi njoo upande huu uendeleze hii kitu.
Au wewe ni yule bucho wa film ya desperado na salma hayek yule mwanamama wa kimorocco
 
Hivi kumbe bado mnahangaika huku basi ngoja nifanye msaada ili jahazi lifike
 
Daudi1 watu watakudunda ukishindwa kuendelea. mizambwa na bucho wameingia mtini na watu wana hamu kujua kinachoendelea
 
Last edited by a moderator:
WAKILI WA MOYO-45

ILIPOISHIA:
“Juzi tulikuja huku na Mage kuvunja uchumba wetu ambao ulinishtua sana na kuumiza moyo wangu japokuwa haikuwa hoteli hii, lakini ni hukuhuku Bagamoyo.
SASA ENDELEA…

“Lakini leo nimezaliwa upya kwa kulipata penzi la kweli ambalo naamini nilitaka kulipoteza, haya ni machozi ya uchungu na furaha.”
“Nafurahi kusikia hivyo, lakini moyo wangu bado haujaamini kama tayari wewe ni wangu.”
“Kwa nini Cecy?”

“Naogopa Mage anaweza kurudi na wewe kunitosa, nitaumia mara mbili kwa vile nimeonja utamu wa mapenzi naweza kufa kwa presha kama utafanya hivyo,” Cecy alisema kwa sauti ya kulalamika.
“Cecy unataka kuamini vipi wakati penzi langu lilikuwa wazi mbele ya mama yangu.”
“Mama yako alikuitia nini pembeni?”

“Tulikuwa na yetu wala haikuhusiana na sisi,” Colin alitengeneza uongo ili kuendeleza furaha ya siku ile.
“Mmh! Nilikuwa na wasiwasi labda chokoraa nimeingia kwenye nyumba ya malkia,” Cecy alitania utani wenye ukweli.

“Hapana wewe ndiye malkia wangu.”
“Nashukuru kusikia hivyo,” Cecy alimkumbatia mpenzi wake kwa furaha bila kujua palichimbika mpaka yeye kuwa pamoja muda ule.

***Mage na Hans waliwasili katika ardhi ya Tanzania katika Jiji la Dar na ndege ya Shirika la Afrika Kusini. Nje ya uwanja wa ndege walisubiriwa na gari la kifahari aina ya Land Cruiser V8 nyeusi. Baada ya ndege kutua waliteremka na kwenda moja kwa moja ndani ya gari lililokuwa likiwasubiri na kuingia.
Gari liliondoka kuelekea Mikocheni anapoishi Hans, njiani Mage alikuwa na furaha ya ajabu kurudi mikononi kwa mpezi wake mwanaume wa maisha yake. Baada gari kuingizwa ndani na kusimama, Hans alizunguka upande wa pili na kumfungulia Mage mlango na kumkaribisha.”
“Karibu utamu wangu.”

“Asante raha zangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani, mapokezi ya familia ya Hans yalikuwa tofauti na siku za nyuma, waliufurahia ugeni wa Mage huku wadogo zake wakimwita wifi na shemeji na wazazi wakimwita mkwe.
Ilikuwa ni faraja kubwa moyoni kwa Mage, aliona sawa na ngamia kupita katika tundu la sindano kukubalika katika familia ile.
Moyoni alijilaumu kukubali kuolewa na Colin kumbe ahadi ya kuvumilia ili ndoto yao ya muda mrefu waliyoahidiana kutenganishwa na kifo ilikuwa njiani. Familia haikuwa na tatizo tena kuingilia uamuzi wa mtoto wao kwa vile chaguo lao ni la Mungu, hawakuwa na jinsi.

Baada ya mapokezi mazuri katika familia ya mpenzi wake, Mage na Hans walielekea Kigamboni nyumbani kwa kina Mage ili kujitambulisha rasmi kwa mzazi wake.
Walipofika Kigamboni, Mage alimkaribisha Hans nyumbani kwao.

“Karibu mume wangu.”
“Asante mke wangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani kwa mwendo wa mahaba, sebuleni walimkuta mama Mage. Mage alimuachia mkono Hans na kumkimbilia mama yake na kumkumbatia.
“Waaawoo mama.”

“Mage mwanangu karibu mama.”
“Asante mama.”
Mage alichukua nafasi ile kumtambulisha Hans.
“Mama leo nimemleta mume wangu chaguo la moyo wangu.”
“Nimemuona, karibu baba,” mama Mage alisema kwa sauti ya unyonge.
“Asante mama.”
“Mama mbona unaonekana mnyonge, unaumwa?” Mage alimuuliza mama yake.
“Walaa mwili umechoka tu.”

Mama Mage alinyanyuka na kuelekea chumbani kuwapisha, alipoondoka eneo la sebule alimwita mwanaye.
“Mage mama njoo mara moja.”
“Nakuja mama,” kabla ya kuondoka alimuaga mpenzi wake.
“Mpenzi nakuja.”

“Hakuna tatizo msikilize mama.”
Mage alimbusu shavuni Hans na kuchepua mwendo kwenda kumsikiliza mama yake.
“Abee mama.”
“Njoo chumbani.”
Waliongozana hadi chumbani, walipofika mama yake alisimama na kumwambia Mage akae kwenye kochi, baada ya kukaa alimgeukia na kumwita.
“Mage.”
“Abee mama.”
“Hivi ndiyo umeamua kunivua nguo?”
“Kukuvua nguo! Kivipi mama.”
“Kwa hiyo hutaki kuolewa na Colin?”
“Mamaaa! Mbona hilo tuliisha limaliza, si nimekueleza ukweli wangu na Colin anajua kila kitu. Sasa swali kama hilo linatoka wapi?”
“Mage kwa nini unalamba matapishi yako?”
“Mama Hans si matapishi ni chakula kilichowekwa kwenye hot port, nimekipakuwa bado kina moto. Unajua jinsi gani nilivyoteseka baada ya Hans kulazimishwa kuoa mwanamke mwingine. Ni wewe uliniambia niwe na subira sasa leo karudi mikononi mwangu unaniuliza hivyo.”
“Kama ungekuwa huna mchumba nisingekuuliza lakini wewe tayari umeshakuwa mchumba wa mtu tena upo kwenye hatua za mwisho za ndoa.”
“Mama wewe ndiye unayekuza mambo, Colin tumesha malizana na sasa hivi tunatoka nyumbani kwao Hans ambako sikuamini kama wangenipokea kama malkia. Yaani mama nimefurahi kukubalika katika familia ya mpenzi wangu.”
“Mwanangu siku zote mkataa pema pabaya panamwita.”
“Mamaa maombi gani hayo?”
“Nakuambia utamkumbuka Colin, ipo siku Hans atakukimbia na kurudi kwa Colin utambembeleza ukitembea kwa magoti, kibaya ukute ameoa mwanangu utakuja jutia uamuzi wako,” mama alitoa tahadhari.
“Mama kuwa na Hans sitajuta katika maisha yangu ni chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Kuonesha Hans hataki kunichezea, wiki ijayo barua inakuja na baada ya majibu maandalizi ya harusi yanaanza mara moja. Kinachotakiwa vikao vya harusi visogezwe mbele ili michango ya harusi yangu na Colin iwe yangu na Hans. Hapo nina imani hakuna kitakacho haribika.”
“Sawa, siwezi kukuingilia kwa vile umeamua mwenyewe, ila kila aliyae hushika kichwa chake.”
“Mama hiyo misemo, ninachoshukuru nimepata tiba ya moyo wangu, kuna lingine?”
 
WAKILI WA MOYO-46

"Sawa, siwezi kukuingilia kwa vile umeamua mwenyewe, ila kila aliyae hushika kichwa chake."
"Mama hiyo misemo, ninacho shukuru nimepata tiba ya moyo wangu, kuna lingine?"
SASA ENDELEA…


"
Hakuna."
"Basi mama yangu naomba unipe baraka zako kinyongo chako kinaweza kuvuruga ndoto zangu."
"Siwezi kuwa na kinyongo kwa vile nipo kwa ajili ya kuyaona maisha yako yanakuwa mazuri na salama."
"Asante mama," Mage alimshukuru mama yake kwa kumkumbatia.

Mage baada ya kuachana na mama yake alikwenda sebuleni alipokuwa amemuacha mpenzi wake.
Alirudi sebuleni na kumvamia Hans kwa mahaba motomoto bila kujali yupo sehemu gani.
Mama yake hakutoka ndani alijikuta moyo ukimuuma na kuanza kulia peke yake huku akilaumu mapenzi ya baba yake yalivyomharibu mtoto.

***
Siku ya pili, Colin na Cecy alirudi nyumbani, alimpitisha nyumbani kwao kisha yeye alirudi nyumbani kwao kwa vile kulikuwa na mambo ya kufuatilia kuhusiana na shughuli zake alizoanza ikiwemo kupata kibali cha kuanzisha kampuni ya mitindo na mavazi ambayo alipanga kumtumia Cecy kwa ajili ya maonesha ya mitindo ya nguo.

Walipofika kabla ya kuondoka Colin alimwambia Cecy:
"Mpenzi pumzika ila jioni nitakufuata tutakuwa na mazungumzo marefu ila utarudi kulala nyumbani najua bi'mkubwa amekumisi."
"Hakuna tatizo msalimie mkwe."
"Kuanzia wiki ijayo nategemea kutimiza ile ahadi."
"Ahadi gani?"

"Ya ujenzi wa nyumba yenu, leo nitamtuma mtu awatafutie nyumba ili kesho mhame ili kupisha ujenzi."
"Kama ni kweli tutashukuru."
Colin alimwita mama Cecy na kumpa laki mbili.
"Mama utakunywa soda."
"Asante baba."

"Hakuna tatizo."
Colin aliaga na kuondoka kuwahi nyumbani ili awahi mjini kwenye mipango yake na kumuacha Cecy akikumbatiana na mama yake kwa furaha. Kwa vile alikuwa na haraka alipofika nyumbani hakukaa, alibadili nguo na kuvaa suti ili kwenda kwenye miadi yake.
Wakati anatoka alikutana na mama yake sebuleni.
"He! Baba umerudi saa ngapi?"

"Sasa hivi mama, leo nina miadi ya jamaa wale wa kampuni ya matangazo."
"Na mwenzio yupo wapi?"
"Nimemuacha kwao."
"Sawa baba, baadaye."
‘Sawa mama."

Colin aliagana na mama yake na kutoka nje ambako alichukua gari kuwahi Posta Mpya katika Jengo la Benjamini Mkapa ghorofa ya kumi na nne.
Baada Colin kuondoka, mama yake aliamini ile ndiyo nafasi ya kwenda nyumbani kwa kina Cecy ili kuhakikisha ndoa na mwanaye haifungwi.

Alioga harakaharaka na kutoka kwenda nyumbani kwao Cecy, aliendesha gari kwa kasi kidogo ili kuwahi kabla mwanaye hajarudi.

Aliamini kutumia fedha zake ataweza kuisambaratisha ile ndoa. Alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka.
Alimkuta mama Cecy amekaa kwenye kibaraza cha nyumba, alipomuona alimkaribisha kwa furaha na bashasha.

"Ooh! Karibu dada."
"Asante, za hapa?"
"Nzuri, karibu japo maisha yetu ya kuungaunga."
"Aah! Kawaida tu wala msijali."

Alipotaka kumkaribisha ndani alikataa, alisimama mbele ya nyumba, aliyatazama mazingira wanayoishi Cecy na mama yake, moyo wake ulichefuka kwa kuona jinsi gani mwanaye alivyopotea maboya kutaka kumuona mwanamke fukara kama yule ambaye halingani na sifa na hadhi ya familia yao.
Lakini alijenga tabasamu la uongo ili kuonekana amefurahi kuonana naye.
"Dada karibu ndani."

"Napita tu siku nyingine nitaingia, vipi mkwe wangu yupo?"
"Mmh! Amerudi muda si mrefu alikuwa na mwenzake muda si mrefu na kufikia kulala."
"Naomba uniamshie."
"Hakuna tatizo dada."

Mama Cecy alikwenda kumuamsha mwanaye.
"Cecy mwanangu amka kuna ugeni mzito."
"Nani tena mama?"
"Mama Colin."
"Uongo!"

"Kweli, amekataa kuingia ndani ana shida na wewe mara moja."
Cecy aliamka na kujifunga kanga na nyingine alijitanda mabegani na kutoka nje, alipofika nje na kumuona mama Colin, aliteremka ngazi haraka na kwenda kumkumbatia kwa furaha.
"Waaawooo! Jamani mama mzaa chema."
"Ndiye mimi."

"Mama mbona umeishia nje si uingie ndani?"
"Hapana nina haraka kidogo naomba tuzungumze kwenye gari."
"Hakuna tatizo."

Cecy na mama Colin waliingia kwenye gari na kumuacha mama Cecy amekaa kwenye kibaraza huku akiamini ile ni dalili njema ya ndoa ya mwanaye baada ya adui kugeuka rafiki.
Baada ya kuingia kwenye gari walifunga vioo vyote na kuwasha AC, Cecy alikuwa mtulivu ili kumsikiliza mama mkwe kipi kimemleta. Baada ya kimya kifupi Cecy alikuwa wa kwanza kuzungumza.
"Ndiyo mama, una habari gani?"

"Cecy nataka kukuliza kitu kimoja, umempenda mwanangu kwa ajili ya mapenzi au kufuata fedha?"
"Kimapenzi."

"Muongo, wewe mwanangu unampenda kwa ajili ya fedha hivyo nataka uniambie unahitaji fedha kiasi gani ili umuache mwanangu?"
"Mmh! Haya yameenza lini mama na kipi nilichokiomba toka katika familia yenu kuonesha nahitaji fedha?"

"Sikiliza Cecy narudia tena, mwanangu huna mapenzi naye sitaki yatokee ya Mage hivyo naomba uachane naye. Sema unataka kiasi gani?"

"Kuachana na Colin wala sihitaji pesa yako mimi ni maskini niache na umaskini wangu. Unaweza kununua kila kitu lakini huwezi kununua moyo wa mtu."
"Sikiliza Cecy, nitayabadili maisha yenu kwa kuwajengea jumba la kisasa na kuwanunulia wewe na mama yako magari ya kutembelea pia kukufungulia duka kubwa la nguo na vipodozi katikati ya jiji ili tu uachane na Colin."

"Nimeridhika na umaskini wangu wala usipoteze fedha na nguvu nyingi kuliua penzi letu."
 
WAKILI WA MOYO-47

ILIPOISHIA:
"Nimeridhika na umaskini wangu wala usipoteze fedha na nguvu nyingi kuliua penzi letu."
SASA ENDELEA…


"Cecy nielewe si kuliua penzi lenu bali kumuokoa mwanangu na mateso, kingine sitaki nawe kuingia kwenye mkumbo huo kwa vile Colin bado anampenda Mage, wakirudiana watakuumiza."
"Sawa nimekuelewa unaweza kwenda," Cecy alisema kwa mkato.

"Ila ukitoka hapa naomba hili libakie siri yetu."
"Sawa, ila nami nakutuma kitu kimoja, ukitoka hapa kamkanye mwanao asije hapa la sivyo!"
"Utamfanya nini?"

"Siyo nimfanye nini asije hapa na wewe ukiondoka hapa usikanyage tena, nenda kwa matajiri wenzio," Cecy alisema kwa hasira.

"Cecy usifanye hasira hujui vitu gani vizuri nilivyovipanga kwako."
Mama Colin alifungua mkoba na kutoa mabunda matano ya milionimilioni na kumpa Cecy huku akisema:

"Ukiachana na Colin utapata zaidi ya hizi."
Cecy alizipokea na kumfanya mama Colin atabasamu kwa kuamini fedha ni sabuni ya roho. Alizitazama zile fedha kwa uchungu huku machozi yakimtoka na kuona jinsi gani umaskini wao ulivyotumiwa kama kisu butu cha kuupasua moyo wake bila ganzi. Alitulia akilia huku machozi yakidondokea kwenye zile fedha.

Kwa hasira alizinyanyua na kumpiga nazo usoni mama Colin na kutoka ndani ya gari, kitu kilichomuacha mdomo wazi mama Colin. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye akitoka ndani ya gari akilia.
"Cecy kuna nini?"

"Mama niache kwanza, huyu mama ni mchawi."
"Mchawi! Kafanya nini?" mama yake alishtuka.
Wakati huo mama Colin kwa aibu aliwasha gari lake na kuondoka bila kuaga. Aliushangaa ujasiri wa Cecy, msichana maskini lakini mwenye kujiamini kupita kiasi kwa kukataa fedha zile na ofa ya kuyabadili maisha yao.

Hakuamini binti muuza ndizi kukataa fedha zile wakati maisha yao ya kubahatisha. Lakini alijiapiza kwa nguvu, kwa hiyari kwa fedha, kwa damu, lazima Cecy ataachana na Colin.

Mama Cecy alimfuata mwanaye aliyeingia chumbani huku akilia na kushindwa kuelewa mazungumzo ya ndani ya gari yalikuwa ya nini. Alimkuma akiendelea kulia kitu kilichomfanya ajiulize kipi kikubwa walichokizungumza ndani ya gari.

Alikuwa amelala kifudifudi akilia kwa sauti ya kwikwi, wasiwasi wake labda Colin amepata tatizo.
"Cecy mwanangu kuna tatizo gani tena?"
"Mama inaumiza sana."

"Kuna nini? Mpenzi wako kapata tatizo?"
"Mama mtu anaweza kuununua moyo wangu hata kuuchukua bure nikiwa nimekufa, lakini nikiwa hai siuuzi kwa gharama yoyote kwa vile furaha ya mtu hainunuliwi dukani."
"Una maana gani?" mama yake alikuwa bado njia panda.

Cecy alimweleza mama yote aliyozungumza na mama Colin, mama yake macho yalimtoka pima kusikia taarifa ile baada ya kuamini kila kitu kilikuwa vizuri kilichobakia ni ndoa ya mwanaye na Colin.
"Mmh! Mbona makubwa madogo yana nafuu," mama Cecy alisema akiwa amechoka na maneno yale.
"Mama mimi na Colin basi," Cecy alisema kwa hasira.

"Huo ni uamuzi wa hasira lazima umsikilize mwenzako si amesema atakupitia jioni basi msubiri umsikilize naye anasemaje kama lao moja na mama yake una haki ya uamuzi wako."

"Mama kosa langu nini? Yaani anatumia fedha zake kuinunua furaha yangu?" Cecy alisema kwa uchungu.

"Mwanangu, kama Colin si chaguo la Mungu basi hamtaoana lakini kama ni chaguo la Mungu hakuna kitakachozuia."

"Yule mwanamke ni mnafiki, akiwa na mwanaye ananichekea kicheko cha mamba lakini kumbe anatamani kunimeza."
"Wee yaache tusubiri jioni."

"Sawa, lakini nina amini hakuna ndoa na Colin labda mapenzi ya sisi wenyewe lakini mama yake hanipendi na yupo radhi kutumia njia yoyote kukwamisha mapenzi yetu."
"Ngoja tumsubiri Colin anasemaje."
"Namsubiri kwa ajili yako lakini ningekuwa peke yangu asingekanyaga hapa."
***
Majira ya jioni, Colin alimpitia Cecy kama alivyomueleza, aliposimamisha gari alishangaa kutomuona mpenzi wake kama kawaida, kwani alishamzoesha vibaya kumpokea kwa kumrukia kwa mahaba motomoto.

Baada ya kusimamisha gari, aliteremka na kwenda ndani huku akiita jina la Cecy mkononi alikuwa amebeba zawadi za mpenzi wake.
"Beeeebi."

Hakuwa na jibu zaidi ya kusikia sauti ya kilio toka ndani kitu kilichomshtua na kufanya akimbilie ndani kwa kuamini mpenzi wake yupo kwenye matatizo. Alimkuta Cecy amelala kifudifudi akilia kilio cha sauti.
"Cecy mpenzi una nini?"

"Colin unaweza kununua kila kitu chini ya jua lakini si furaha ya mtu," Cecy alisema bila kugeuka.
"Kuna nini mpenzi wangu?" Colin alishangaa.
"Umenikuta maskini hata siku moja sikuja kwenu kuomba pesa ya kula, nimeishi kwa kuuza ndizi nitaendelea kuuza ndizi lakini hamuwezi kuutumia umaskini wetu kama silaha ya kununua haki ya moyo wangu."

"Cecy hebu gauka mpenzi wangu, kipi nimekukosea mpaka useme maneno makali hivyo?"
"Najua hunipendi lakini usitumie gharama kubwa kuniacha, tamko lako ni tosha kuliko gharama na nguvu mnayotaka kuitumia.

Ni kweli nakupenda jambo ambalo lipo wazi mbele ya Muumba. Lakini ni vigumu kulazimisha mapenzi ni sawa na kumvuta punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji."
"Cecy mpenzi wangu mbona toka jana tumekuwa na siku nzuri ambayo nilitegemea kuimalizia leo.

Kipi nilichokufanyia ikiwa nimekuaga nimekwenda kwenye mipango ya maisha yetu ya mbeleni. Nimekuja na furaha ili kukujulisha nimekupatia chuo cha mambo ya urembo ambacho utasoma miezi sita na ukitoka hapo utakuta nimeshakufungulia kampuni yako ya urembo.

"Kwa nini wanawake mnapenda kuumiza moyo wangu, Cecy kabla hatujaanza mapenzi ulionesha kunijali lakini kuanza kwa ukaribu wetu hata mwezi bado unataka kuupasua moyo wangu bila ganzi.

Cecy niliamini wewe ndiye tiba ya moyo wangu, lakini unataka kuongeza msumari wa moto kwenye kidonda. Naomba basi mnihurumie nami binadamu ninayehitaji upendo.

Mapenzi yangu yamekuwa kama mtu anayemwaga maji baharini yasiyoonekana.
"Kwa nini hukuniambia mapema Cecy umeacha...
 
WAKILI WA MOYO-48

ILIPOISHIA:
Naomba basi mnihurumie nami binadamu ninayehitaji upendo. Mapenzi yangu yamekuwa kama mtu anayemwaga maji baharini yasiyoonekana.
SASA ENDELEA…

"Kwa nini hukuniambia mapema Cecy umeacha nijirushe juu ya ghorofa ya mapenzi nikiamini utanidaka, lakini najiona naangukia pabaya nawe umekataa kunidaka nitakufa kifo kibaya.

Cecy utajiri wetu hauingiliani na mapenzi yetu, fedha inaweza kununua kila kitu lakini si penzi la kweli bali upendo wa dhati toka chini ya uvungu wa moyo wa mtu mwenye mapenzi ya kweli asiyeangalia kitu bali mtu mwenyewe alivyo.

"Ni kosa gani nililokufanyia mpaka kufikia kusema maneno mazito yaliyoushtua moyo wangu, kama moyo ungekuwa ukitoka nje naamini ungekuwa unavuja damu kutokana na mshtuko na maumivu ya kuona unatolewa sehemu salama na kutupwa kwenye miba."

Maneno ya Colin ambaye alionekana hajui kilichokuwa kikiendelea, yalimfanya Cecy aongeze sauti ya kilio na kujinyanyua alipokuwa amejilaza na kwenda kujitupa kifuani kwa Colin kitu kilichomshangaza mpenzi wake.

"Cecy mpenzi wangu hebu kuwa mkweli tatizo nini mpaka kusema maneno makali? Nipo radhi kujitoa muhanga ili kuliokoa penzi letu."

"Colin najua unanipenda lakini mama yako hanipendi," Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
"Bebi, maneno gani hayo ikiwa jana uliona alivyokufurahi, yasahau yote yaliyopita."
"Colin, mama yako mnafiki, ana tabia ya unafiki wa mamba anakuchekea machoni lakini moyo anakuchukia."

"Kwa nini unasema hivyo?" Colin alishtuka kusikia vile.
"Mama yako hataki tuwe pamoja yupo radhi kutumia gharama yoyote kuhakikisha anatutenganisha."
"Lakini mbona yaliisha."

Cecy aliamua kumweleza ukweli, ujio wa mama yake na ahadi na fedha aliyotoa kwa ajili kulivunja penzi lao. Colin alibakia macho yamemtoka pima asiamini maneno ya Cecy.
"Cecy unayosema ni kweli?"

"Nimzulie uongo mama yako ambaye kama tungeoana angekuwa mama mkwe wangu?"
"Kama kafikia hatua hiyo naomba kwanza unisamehe sana, najua nitafanya nini. Ila nakuahidi kwa kuonesha msimamo umezidisha upendo moyoni mwangu, pia hela aliyotaka kukupa nitakupa mara kumi yake na kutimiza ahadi yangu kwa kulijenga penzi letu."

"Colin, narudia huwezi kuununua moyo wangu."
"Kwa nini unasema hivyo?"

"Sihitaji pesa zako kwa ajili ya kuonesha kuwa unanipenda bali mapenzi ya dhati toka kwako. Pendo langu halina gharama japo ni ghali kwa vile nilikubali kukupenda kama ulivyo wala si kwa ajili ya gari, majumba au fedha zenu."

"Asante kufahamu hivyo, basi naomba ukaoge ili twende nilipokueleza jana."
"Sawa mpenzi wangu."
"Pia, kesho mtahama ili kupisha ujenzi wa nyumba yenu kwa muda, nimewatafutiea nyumba nzima ambayo nimelipia kwa mwaka mzima."

"Kwani hiyo nyumba unachukua muda gani kujengwa?"
"Nataka ijengwe vizuri hata miezi miwili au mitatu."
"Basi si ungechukua miezi mitatu?"

"Msiwe na wasi, niliwaambia wakakataa mwaka mzima."
"Ipo wapi?"
"Kimara Baruti."

"Asante mpenzi wangu," Cecy alimkumbatia Colin kwa furaha na kuyasahau maumivu yote.
Cecy alikwenda kuoga akimuacha Colin ambaye alihisi kichwa kinataka kupasuka kwa mawazo kutokana na alichokifanya mama yake aliyeamini ndiye muongozo wake na kuitengeneza furaha lakini kwake ilikuwa kinyume.

Alipanga akitoka pale kwenda na Cecy nyumbani kwao ili mama yake akayasema yale mbele yake.
Baada ya Cecy kumaliza kuoga na kubadili nguo ambazo zilizidi kumpandisha chati na kumfanya aonekane binti mrembo kuliko wanawake wote duniani mbele ya Colin.

Walishikana mikono na kuelekea ndani ya gari na kuelekea moja kwa moja nyumbani kwao Colin.
"Colin unanipeleka wapi?" Cecy alishtuka.
"Usihofu naomba uambatane na mimi."

"Mmh! Sawa."
Gari lilipiga honi na geti lilifunguliwa na Colin kuliingiza ndani, kama kawaida alizunguka na kumfungulia mlango kisha alimshika mkono na kuingia naye ndani. Sebuleni alikuwa mama Colin akizungumza na msichana wa kazi alipomuona Colin alinyanyua macho na kumuona ameongoza na hasimu wake.

Alijikuta akiponyokwa na glasi ya juisi aliyokuwa ameshikilia.
Cecy alisogea hadi karibu na mama Colin na kumsalimia.
"Shikamoo ma mkwe," kama kawaida alipiga goti la heshima mpaka chini.

Mama Colin alinyanyuka alipokuwa amekaa na kumfuata Cecy na kumnyanyua alipokuwa bado amepiga magoti na kumkumbatia kwa muda huku machozi yakimtoka.
Colin alishangazwa na mama yake kufanya vile aliamini alifanya vile kujitakasa mbele ya macho ya mwanaye lakini moyoni alikuwa na nia mbaya kuliko bomu la kutegwa.

Alijiuliza mama yake atamwambia nini kwa kitendo cha kigaidi alichokifanya cha kusambaratisha penzi lake.

"Cecy," alimwita huku akimshika mabegani na kumtazama usoni kwa macho yaliyojaa machozi.
"Abee ma'mkwe," Cecy aliitikia huku naye machozi yakimtoka.

"Najua siku ya leo huenda hutanielewa, wewe ni msichana wa kwanza kunionesha kitu si cha kawaida. Lakini nilichokifanya leo ni mtihani wangu wa mwisho kwako, nakiri kwa moyo wangu katika wasichana niliowapenda ulikuwa wewe namba moja.

"Lakini sikumaanisha kuwa utakuwa mke wa mwanangu kwa vile nilikuwa na malengo makubwa kwa mwanangu baada ya kutumia kiasi kikubwa kumsomesha.

Niliamini mwanamke atakayemfaa ni mwenye elimu kama yake pia anayetoka katika familia yenye uwezo ambaye atakuwa na mapenzi ya kweli na hatafuata mali aliyonayo mwanaume.

"Niliamini chaguo langu lilikuwa sahihi la kumchagua Mage kwa vile ni msomi tena anatoka katika familia yenye uwezo pia mama yake ni shoga yangu.

Lakini kumbe siyo, nakiri toka moyoni mwangu mapenzi niliyokuwa nikimpenda Cecy yaligeuka na kumuona ni adui namba moja anayetaka kuvuruga ndoto zangu.

"Mwanzo nilidhani utani lakini siku ya birthday ya Colin nilivyokuona ulivyopendeza mpaka kukusahau na picha nilizomkuta nazo Colin niliona ndoa hakuna.
"Moyo wangu ulikosa amani mpaka mipango ya harusi kwenda vizuri huku nikiwa sisikii taarifa yako.
 
WAKILI WA MOYO-49

ILIPISHIA:
"Mwanzo nilidhani utani lakini siku ya birthday ya Colin nilivyokuona ulivyopendeza mpaka kukusahau na picha nilizomkuta nazo Colin niliona ndoa hakuna. Moyo wangu ulikosa amani mpaka mipango ya harusi kwenda vizuri huku nikiwa sisikii taarifa yako.
SASA ENDELEA...

"Kwa kweli niliumia sana kwa kitendo cha Mage kuuvunja uchumba tukiwa katika hatua za mwisho. Kwa kweli siku zote nilikosa usingizi nimekuwa nikipungua siku hadi siku. Kitendo cha kuibuka wewe kwa kweli kilinichanganya sana, sikuamini kama una mapenzi ya kweli na mwanangu zaidi ya kufuata mali zetu.

Mtihani niliokupa leo umenipa sababu sahihi ya mwanangu kukuchagua wewe kuwa mkewe.
"Cecy kitendo cha leo kimefukua mapenzi yote ya nyuma na kukiri mapenzi si elimu wala mali bali upendo wa dhati toka moyoni mwa mtu.

Umenionesha jinsi gani unavyompenda mwanangu mapenzi ya dhati si kwa ulichonacho. Napenda kuwaomba radhi wote kwa kuwakwaza kwa namna moja ama nyingine.
"Colin mwanangu nataka kukutamkia hili mbele ya mpenzi wako na Mungu shahidi yangu kama nitakwenda kinyume, naomba anifanye kitu chochote kibaya.

Kuanzia leo namtambua rasmi Cecy kama mkwe wangu na mipango ya harusi itaanza mara moja. "Cecy mkwe wangu kuna zawadi nitakupa kwa kuonesha msimamo na mapenzi ya dhati kwa mwanangu naamini wewe ndiye mke aliyechaguliwa na Mungu."

Mama Colin alisema huku machozi yakimtoka, kila mmoja alitokwa na machozi, yalikuwa maneno yenye kuumiza moyo yaliyotaka moyo wa chuma kukufanya usidondoshe chozi.
Colin hakuwa na haja ya kumuuliza mama yake baada ya kila kitu kuwekwa wazi.

Mama yao aliwakusanya na kuwakumbatia wote kisha aliwaachia na kutaka kupiga magoti kuwaomba msamaha lakini walimuwahi mama yao kabla hajapiga.

"Hapana mama huna kosa, bali sisi ndiyo tulikwenda tofauti na mawazo yako, tunaomba utusamehe sana. Ombi letu utupe idhini toka moyoni mwako ili tufunge ndoa yenye Baraka," Colin alimwambia mama yake.

"Mungu ananisikia nimeibariki ndoa yenu duniani na mbinguni."
"Ma' mkwe, naomba usinipe zawadi yenye gharama kubwa bali kunipa mume wa ndoto yangu, inawezekana uliponiita mkwe na kunieleza nitaolewa na mwanao anayesoma Ulaya ulidhani utani. Na siku nilipomuona nilichanganyikiwa zaidi, moyoni niliamini nimeokota dhahabu katikati ya soko.

"Lakini niliumia siku nilipojua kumbe kuna chaguo sahihi la Colin, kuanguka kwangu si ugonjwa bali presha ilipanda na kushindwa kujizuia. Niliamua kujitoa na kukaa pembeni huku nikiwa nimejikatia tamaa.

Niliumia zaidi siku Cecy alipomshusha Colin kwenye gari na kumdhalilisha, kwa kweli japo nilikuwa sipendwi niliingilia ugomvi kwa vile chenye thamani kwenye moyo wangu nilikiona kikidhalilishwa.
"Mpaka leo mama unasema maneno matamu kama haya si kwa urahisi bali nimetoka jasho na damu. Nashukuru mama mkwe, nakuahidi kuwa mke bora na kufurahia chaguo lako la awali."

Ilikuwa furaha siku hiyo iliagizwa shampeni na kufurahi kutambulika rasmi kwa Cecy katika nyumba ya kina Colin.
***
Mipango ya harusi ya Hans na Mage ilikwenda vizuri, mama Mage hakuwa na haja ya kukusanya tena michango ya sherehe zaidi ya kugawa kadi za ‘Send Off' ya harusi ya mwanaye.
Katika watu waliopelekewa kadi ya Send Off ya Mage ni familia ya mama Colin, tena Mage alisisitiza Colin ahudhurie sherehe yake.

Taarifa zilifika, Colin alikubali kuhudhuria kwa kujua hataumia kwani Cecy alikuwepo.
Siku ya Send Off, Colin na Cecy waliingia wakiwa watu wa mwisho, ilikuwa siku ambayo Cecy aliitafuta kwa udi na uvumba kuwaonesha walimwengu kuwa kila mguu hutulia kwenye kiatu saizi yake wala si kuvaa kikubwa kikakupwaya au kidogo kikakubana lakini kwake kilikuwa kimetulia.

Wakiwa wamependeza, Colin katika vazi la shati refu la kitambaa cha maua laini na suruali nyeusi na viatu vyeusi vilivyochongoka kidogo mbele Cecy alitupia gauni refu jekundu la mikanda mabegani la kitambaa chepesi na viatu virefu vilivyoongeza uzuri wake.

Waliingia taratibu huku Cecy akiuweka mkono wa Colin kwapani kwake na kuushika kwa mbele. Waliingia taratibu na kufanya watu wote wageuze shingo kuwatazama wapenzi wawili walioonekana kama ndiyo wamepata shahada ya mapenzi muda si mrefu.

Mage alishtuka kumwona Colin akiwa amependeza sana akiwa na msichana mrembo ambaye alimsahau kama ndiye aliyempa kipigo siku alipomdhalilisha Colin. Moyo ulimlipuka na kujikuta akiingia wivu, Colin alikuwa na tofauti kubwa na Hans kimuonekano alikuwa ana mvuto kwa mwanamke yoyote.

Lakini mapenzi yake Hans yalikuwa makubwa kuliko kitu chochote chini ya jua. Colin pamoja na umbile na sura nzuri lakini kwake moyoni kwake alikuwa na nafasi ndogo.
Naye mke mtarajiwa naye alipendeza katika gauni la kitenge aliloshonewa kwa ustadi mkubwa na kumwongezea urembo wake.

Aliamini kabisa msichana aliyechukua nafasi yake alikuwa kama maji ya bahari na yeye, kuvunja uchumba na Colin ilikuwa sawa na kuchota maji kwa kikombe ndani yake na kufanya pengo lake lisionekane kabisa. Sherehe ilienda vizuri kila mtu aliyekuwepo aliisifia jinsi ilivyofana kwa burudani iliyoandaliwa ambayo ilifanya wageni wasichoke kuwepo ukumbini pale.

Katika watu waliokuwa na furaha siku ile alikuwa mama Colin baada ya kumwona mwanaye alivyopendeza akiwa na Cecy msichana aliyekuwa kama dhahabu iliyokuwa imechafuliwa na tope lakini mwanaye aliisafisha na thamani yake kuonekana mbele ya macho ya watu.

Katika kitu kilichomvutia siku ile ni jinsi Cecy alivyojiamini sana, kwake lilikuwa kama jibu ambalo alitamani siku moja Mage alipate baada ya kumuacha mwanaye. Kitendo cha kuonesha mapenzi mazito kwa mwanaye kilimpa faraja kubwa moyoni mwake na kujiapiza kumpa zawadi kubwa japokuwa alionesha Cecy hahitaji zawadi ambayo aliitafsiri kama hongo.

Alipanga siku ya harusi ya mwanaye ampe Cecy zawadi ya nyumba ambayo ataanza kuijenga wakati wowote na zawadi ya gari la kifahari ili kurudisha shukurani kwake kumwokoa mwanaye aliyeachwa ghafla kama chuma cha moto kilichozimwa kwa kumwagiwa maji, lazima kipinde.

Aliamini kitendo cha Mage kumuacha ghafla lazima angekuwa kwenye hali mbaya lakini yeye alikuwa mwokozi wake na kulipigania penzi la mwanaye mpaka mwisho kuibuka mshindi.

Itaendelea wiki ijayo
 
Furaha ya moyo hainunuliwi kwa pesa ila ni kwa hadithi tamu,yenyekusismua na kuleta matumaini kama hii.Mungu akjaze hekima.
 
Back
Top Bottom