Wakili wa Moyo - 15
Kwa kitendo walichonifanyia siendi tena kwao kuuza ndizi."
Kauli ya Cecy iliyochanganyika na kigugumizi na kilio ilimshtua.
"Cecy nini mama?"
"Ningejua nisingeenda," alisema kwa sauti ya kilio.
"Kwa nini?"
"Yaani wameniita kuniumiza! Nimewakosea nini?"
"Kukuumiza! Kivipi?"
"Mama yaani sijawahi kuumizwa moyo wangu kama leo.
SASA ENDELEA...
"Najua unaniona mtoto mdogo lakini nina hisia kama mtu mwingine, mama inaumaa," Cecy alisema kwa uchungu huku akishika mkono kifuani.
"Kuna nini mbona huniweki wazi?" mama yake alishtuka.
"Mama, Colin wa kuniita kunionesha mchumba wake?"
"Kukuonyesha kivipi?"
Cecy alimweleza kila kitu kilivyokuwa katika sherehe, mama yake alishtuka na kusema:
"Mwanangu unataka kujiua bure, nilikueleza na mapema tajiri na sisi kina pangu pakavu wapi na wapi?"
"Kwa nini mama yake ananiita mkwe wakati mwanaye ana mwanamke mwingine?" Cecy aliuliza macho yakijaa machozi.
"Kuna siku alikutamkia suala la uhusiano kati yake na wewe?"
"Hapana."
"Sasa kuumia huko kumetoka wapi?"
"Mama! Nampenda sana Colin."
"Ulimwambia unampenda?"
"Nilikuwa naona aibu."
"Siku zote moyo ni mfungwa wa mapenzi hasa kumpenda asiyejua anapendwa mdomo wako ndiyo wakili wa kuutetea moyo wako. Bila hivyo upendo wako utateketea kama mwanga wa mshumaa mchana wa jua kali, hakuna atakayeuona mwanga wake."
"Mama, Colin alionesha ananipenda."
"Nilikueleza toka zamani ule ni utani tu wala hakuna ukweli wowote."
"Kwa kitendo walichonifanyia siendi tena kwao kuuza ndizi."
"Mwanangu nikueleze mara ngapi kila kitu kinatokana na baraka za Mungu. Muombe yeye ndiye atakayekuchagulia mwanaume wa maisha yako."
"Asante mama kwa kunitia moyo."
"Basi badili nguo kisha uoge ule ulale."
"Mama hata hamu ya kula ninayo, wacha tu nikalale."
Cecy aliingia chumbani kwake kulala na kumuacha mama yake akiwa amesimama akiyafikiria aliyoambiwa na mwanaye. Alimuonea huruma kwa kujiingiza kwenye mapenzi ya kumpenda mtu mwenye mpenzi mwingine anayempenda.
Kingine kibaya ilikuwa hali yao duni ambayo ilikuwa tofauti na matajiri na wasomi. Alijiuliza kwa hali iliyomtokea mwanaye iliyopelekea kupatwa na presha kupelekea kukimbizwa hospitali itachukua muda gani kumtoka.
Aliamini ingemtesa mwanaye kwa kipindi kirefu na kumfanya akose amani ya moyo wake. Lakini aliamini atampatia ushauri nasaha utakaomrudisha katika hali ya kawaida. Aliachana na mawazo yale na kwenda chumbani kwake kulala.
Siku ile ilikuwa mbaya kuliko zote maishani mwake, aliyakumbuka maneno ya mama yake kuhusu Colin kumtamkia mpenzi wake zaidi ya utani wa uchumba.
Kwa vile kichwa kilikuwa kikimuuma, alimeza dawa za usingizi na kupanda kitandani kuitafuta siku ya pili.
***
Wakati hayo yakiendelea, Colin na Mage walikuwa kwenye furaha ya ajabu. Mage hakuamini tukio lililotokea usiku ule la kuvalishwa pete ya uchumba mbele ya watu.
Kilikuwa kitu kikubwa sana katika maisha yake, pamoja na kupendana sana na Hans kwa muda mrefu lakini hakikufanyika kitu kama kile. Aliamini Hans alikuwa mwamaume aliyeletwa kwake na Mungu kwa kuonesha ana mapenzi ya dhati na yeye.
"Colin asante sana mpenzi wangu," Mage alisema huku akiitazama pete yake ya kito cha Tanzanite.
"Kawaida tu, nina vitu vingi vya kukufanyia mpenzi wangu," Colin alijibu huku akichezea vidole vya mikono ya Mage.
"Colin nakuahidi kuwa mke mwema."
"Nashukuru, nataka harusi yetu isichukue muda mrefu."
"Hujui tu, ukitaka sasa hivi nipo tayari hata unioe bure kwa vile upendo wa kweli ni ghali kuliko kuitafuta fedha. Nakuhitaji kuliko kitu chochote chini ya jua."
Mage alisema huku machozi yakimtoka akikumbuka alichofanyiwa na mpenzi wake Hans, mwanaume aliyeamini ndiye wake wa kufa na kuzikana.
Lakini kilichotokea kilikuwa kinyume na matarajio yake, kiliufanya moyo wake kuingia wasiwasi wa kumkosa hata yule.
"Mage usilie nataka ulie kwa furaha ukiwa nami si kwa huzuni," Colin alimwambia Mage huku akichezea vidole vyake na macho yake kutazama usoni kwake.
"Nina wasiwasi naweza kutendwa tena, Colin ukinitenda nitakufa mwenzio nakuona wewe ndiye uliyeshika uhai wangu," Mage alisema kwa sauti iliyohitaji huruma.
"Nakuhakikishia furaha yako itapitia mikononi mwangu."
"Kweli Colin?" Mage aliuliza huku ametoa macho.
"Amini nakupenda sana Mage, wewe ni ua la moyo wangu sitachoka kulitunza na kulimwagilizia ili liendelee kustawi na kuchanua."
"Asante Colin, nami nitahakikisha chaguo la mama yako hutajutia maishani mwako. Hazina yote ya mapenzi nahamishia kwako."
"Asante mpenzi wan gu nami nitakuwa benki yenye usalama kwa ulichokiweka kila sekunde kinaongezeka faida ya upendo."
"Nimefurahi kusikia hivyo, nina imani kovu la kutendwa litaondoka."
"Niamini nikisemacho, kwa vile nami nahitaji furaha yangu itoke kwako."
"Asante mume wangu mtarajiwa," Mage alisema huku akimkumbatia Colin kwa mahaba mazito.
Baada ya sherehe, Mage alikataa kuondoka na mama yake na kulazimisha kubaki na Colin.
"Mage mwanangu muda wa kuwa karibu na Colin bado."
"Hapana mama, alichokifanya leo ni zaidi ya ndoa. Naomba uniache nina mengi ya kuzungumza naye usiku wa leo."
"Mama Mage mwache mtoto abakie na mwenziye, bado wana mengi ya kuongea wakiwa karibu," mama Colin aliingilia kati na kufanya mama Mage kukubaliana na mzazi mwenzie kumuacha Mage alale na Colin siku ile.
ITAENDELEA.................