Wakili wa Moyo-24
ILIPOISHIA:
Hapo ndipo ninapochanganyikiwa, mama kitendo walichonifanyia familia ya kina Hans, sitawasahau.
Umeona eeh, nilikueleza toka zamani familia ile ilikuwa haikupendi kama ungeolewa na Hans ndoa yako isingedumu. Mungu amekuletea mwanaume wa maisha yako unamchanganya.
Mama nimesha fanya kosa, naomba msaada wako, nitamweleza nini Colin anielewe.
Wala usiwe na wasi kamwambie kuwa ulimtuma Brenda cheni ambayo ulipanga kumpatia kama surprise umekuta hajaitengeneza na kujikuta umekasirika na kuanza kulia.
Mmh! Atanieleza? Naona kama utetezi mwepesi.
Walaa, ye anajua ulikuwa kwa Brenda, nilimwambia kuna kitu mmeshindwa kuelewana ndiyo maana ulirudi katika hali ile.
Mmh! Basi ngoja nidanganye hivyo.
Wakiwa katikati ya mazungumzo simu yake iliita, ilikuwa ikitoka kwa mama Colin.
SASA ENDELEA...
Mkweo, mama Mage alisema.
Mmh! Lazima ataulizia kilichotokea.
Ngoja nimsikilize, alisema huku akibofya cha kupolelea na kuweka simu sauti ya nje.
Haloo mama Colin.
Eeh! Dada kuna nini huko?
Kwani vipi?
Naona Colin ananichanyanyia maneno wala simuelewi.
Wala hakuna kitu cha kutisha bali mkweo aliudhiwa na shoga yake, lakini kwa sasa yupo sawa na wakati wowote atakuja huko.
Mmh! Afadhali maana nilikuwa na wasiwasi.
Wa nini?
Nilijua Colin kisha mtibua mkwe wangu.
Walaa, sema mkweo ana hasira za kitoto kitu kidogo analia kama kafiwa.
Basi nikuacheni muendelee na mambo mengine.
Baada ya simu kukatwa mama Mage alimgeukia mwanaye na kumwambia.
Unaona ulivyotaka kumsababishia matatizo mwenzako?
Mama lazima niende sasa hivi najua mpenzi wangu hayupo kwenye hali nzuri.
Fanya hivyo na... mama Mage alinyamaza baada ya mlango kugongwa.
Unasemaje? aliuliza kwa sauti.
Kuna wageni.
Nakuja, mama Mage alitoka nje kwenda kumsikiliza mgeni.
Alitoka hadi getini na kukutana wa wanaume wawili na mwanamke mmoja, aliwatazama walikuwa wageni kwake.
Karibuni.
Asante.
Aliwakaribisha hadi sebuleni, baada ya kuketi mama Mage alitaka kujua wana sida gani.
Ndiyo jamani mna shida gani?
Sisi ni maafisa wa polisi, walitoa vitambulisho vyao.
Ndiyo, mna shida gani?
Tuna imani hapa ndipo anaishi Magreth Chogo.
Ndiyo.
Yupo?
Mna shida gani?
Kabla hajajibu Mage alitoka chumbani ili awaone wageni ni kina nani, askari mmoja baada ya kumuona alijua ni Mage alibahatisha kwa kumwita jina.
Mage.
Abee.
Upo chini ya ulinzi, alisema askari wa kike.
He! Kwa kosa gani? Mage alishtuka.
Kutokana na tukio lililomtokea mpenzi wako wa zamani.
Sasa mimi nahusika kivipi?
Utajua yote kituoni.
Mi siendi, Mage alitaka kugoma kwenda.
We nenda wala usihofu, ila jamani chondechonde mwanangu asiguswe wala kulazimisha kusema uongo tutaelewana vibaya.
Hakuna tatizo, atakuwa salama baada ya mahojiano atarudi.
Itaendelea...................