Wakili wa moyo 42
ILIPOISHIA:
Cecy hebu nisikilize. Ungekuwa na shida na mimi ungenifuata nyumbani kwetu. Colin aliamini kabisa Cecy alikuwa amechukizwa na kitendo cha kumtelekeza na ahadi za uongo. Alitoka mbio kumuwahi Cecy nje, alimkuta amekaribia getini, akamfuata na kumshika mkono asiondoke. SASA ENDELEA
Cecy najua nimekukosea,naomba unisamehe. Colin najua hunipendi bali mimi najipendekeza kwako,endelea na Mage wako. Hapana Cecy,nakuapia haki ya Mungu wewe ndiye moyo wangu, Colin alipiga magoti mbele ya Cecy ambaye siku ile alionekana mrembo maradufu.
Colin wewe ndiye wa kunifanya hivi au kwa vile mimi ni maskini,mbumbu sijui lolote? Asante, Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
Ha..ha...Si..si
Colin alinyamaza baada ya kusikia honi lakini alishindwa kunyanyuka kwa vile alikuwa bado kamshika mkono Cecy akimuomba msamaha. Geti lilifunguliwa na gari la mama Colin liliingia na kushangaa kumuona mwanaye amepiga magoti mbele ya binti mrembo.
Cecy alipomuona mama Colin akiteremka kwenye gari,alimsukuma Colin na kutimua mbio kwenda nje. Cecy
Cecy rudi na..na..
Cecy hakugeuka,alitoka hadi nje ya geti, bahati nzuri aliona Bajaj inapita, aliisimamisha na kupanda kisha alimweleza dereva ampeleke nyumbani kwao.
Colin alipotoka nje alikuta ameshaondoka. Alirudi ndani mbio na kumwambia mlinzi afungue geti,alipanda kwenye gari alilokujanalo mama yake na kumfukuzia Cecy kwa kuamini hasira za Cecy hazikuhitaji kupewa muda zaidi ya kutulizwa haraka,la sivyo atakosa Bara na Pwani.
Mama Colin,tangu afike alikuwa akijionea vioja asijue kumetokea nini na yule binti mrembo ni Cecy gani. Alimsogelea mlinzi na kumuuliza. Eti yule msichana ni nani?
Hata sijui,alikuja na kuuliza kama upo, nikamwambia haupo,akaniuliza Colin, nikamwambia yumo ndani. Basi aliingia hata hajakaa,niliona akitoka mara nikamuona Colin akimkimbilia na kumshika yule msichana,akawa mkali. Nilishangaa kumuona akipiga magoti kumuomba msamaha. Nimesikia anamwita Cecy,ni Cecy yupi?
Mmh! Ndiyo leo namuona. Sasa atakuwa amekwenda wapi? Hata najua! Labda atakuwa amemfuata huyo msichana. Colin aliendesha gari kwa kasi kuitafuta Bajaj ambayo ilikuwa imeshapotea kuonesha Cecy alimwambia dereva aikimbize. Alikanyaga mafuta kuitafuta Bajaj kuelekea nyumbani kwao Cecy. Alipokaribia nyumbani kwao alimuona akiteremka kwenye Bajaj na kuingia ndani.
Colin alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka,hakufunga mlango alikimbilia ndani,Cecy alishangaa kumuona Colin pale,alimuuliza kwa sauti ya juu. Colin umefuata nini hapa kwa masikini? Cecy mpenzi naomba unisikilize.
Nikusikilize nini,ni wazi nalazimisha mapenzi,nenda kwa Mage,mwanamke mwenye uwezo na elimu,niache mimi masikini nisiye na elimu.
Ukifanya hivyo utakuwa ukinifunga mikono na kunipiga,sitaweza kujitetea,naomba unipe nafasi. Umetudhalilisha vya kutosha kwa kutudanganya kuishi maisha ya peponi,leo yapo wapi? Najua una chaguo lako,naomba uondoke utuache na umasikini wetu.
Cecy najua nimewakosea lakini nami ni mwanadamu ninayehitaji kusamehewa kwa vile si mkamilifu. Mama Cecy aliyekuwa nyumba ya pili akichota maji,aliporudi alishangaa kumkuta Colin kampigia magoti Cecy.
Kuna nini? aliuliza kwa mshangao. Mama huyu si alikuja hapa kusema nini na alifanya nini? Cecy aliuliza kwa sauti hasira. Mama najua sikuwa mkweli lakini mpango wangu upo palepale.
Baada ya kukataliwa na Mage eeh? Cecy alimuuliza huku amemshikia kiuno. Hapana,majukumu yalinibana,mama naahidi nikitoka hapa kila nilichoahidi nisipofanya hivyo chukua uamuzi wowote.
Tuchukue uamuzi gani ikiwa hatukudai ni hiyari yako si lazima, mama Cecy alisema. Mama nilikuwa katika kipindi kibaya ambacho naamini ningelazimisha,ningeweza kuwatia kwenye matatizo.
Colin,maisha yetu ndiyo haya,hatuhitaji msaada wako,hatujaja kwenu kuomba msaada,hata masikini ana nafasi kwa muumba, Cecy alisema huku machozi ya uchungu yakimtoka. Cecy usifike huko,najua unanipenda. Nakuhakikishia kulipa upendo mara mbili.
Sihitaji, Cecy alijibu kwa nyodo japokuwa moyo wake wote ulikuwa kwa Colin,alitaka kutikisa kibiriti kuona kama kimejaa.
Cecy najua nimekukosea lakini amini huu ni wakati wako wa kuponya maumivu ya moyo wako. Cecy msamehe mwenzako, mama Cecy aliingilia kati.Basi amka, Cecy alimnyanyua Colin ambaye alikuwa bado amepiga magoti kama muumini aliyekuwa akiungama dhambi kanisani.
Colin alinyanyuka na kukumbatiana na Cecy ambaye alijilaza kifuani kwa mpenzi wake, mama yake alikuwa pembeni,alitabasamu huku akiomba dua Colin amuoe Cecy ili kutimiza ndoto ya mwanaye. Cecy nataka kukuhakikishia mbele ya Mungu,mama yako na mchana wa jua kuwa wewe ndiye mke wangu wa maisha.
Muongo Colin unanidanganya, Cecy alisema kwa sauti ya kudeka. Unataka nifanye nini ili uamini ninayosema. Nioe niwe mkeo.
Nakuhakikishia kukuoa uwe mke wangu na mimi niwe mumeo. Asante.
Naomba sasa hivi twende nyumbani nikamueleze mama mbele yako. Akikataa?
Hawezi,hii ni nafasi yangu ambayo hakuna wa kuiingilia,naomba uniamini. Mmh! Sawa wacha nikaoge ili tuondoke. Colin alipewa kiti ili amsubiri Cecy aliyeingia ndani kubadili nguo,alitoka amejifunga upande wa kanga na kutoka kuelekea bafuni kuoga.