WAKATI UTATA WAGUBIKA KUJIZULU KWAKE
Gavana Ballali harudi
MWANDISHI WETU
Dar es Salaam
WAKATI taarifa za kujiuzulu na hali ya afya ya Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zinazidi kutatanisha, imefahamika kwamba Gavana huyo, Dk.Daudi Ballali, hatorejea nchini.
Imeelezwa kwamba Gavana Ballali ameshauriwa kuendelea kupata matibabu huko Boston, Marekani hadi hapo hali yake ya afya itakapotengemaa kabisa ili kuepuka ‘mazonge' akiwa nchini Tanzania.
Tayari, Ofisi ya Rais, kupitia Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Salvatory Rweyemamu, imekwisha kusema kwamba haina taarifa ‘rasmi' kuhusu kujiuzulu kwa Dk. Ballali na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji naye amesema hana taarifa.
Hali ya Ballali bado ni ya kutatanisha baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa na Rais Jakaya Kikwete, amethibitisha kufahamu kwake kuhusu ugonjwa wa Dk. Ballali alipozungumza na waandishi wa habari Ikulu, Jumatano wiki hii.
Habari kutoka BoT, zinaeleza kwamba kabla hata ya taarifa za kujiuzulu kwake, Dk. Ballali aliondoka nchini akijua kwamba hatarejea tena nchini hasa baada ya serikali kuteua Manaibu Gavana wawili, Juma Reli aliyekuwapo na Prof. Benno Ndulu.
"Alipondoka sisi wote hapa BoT tulijua kwamba hatorudi tena nchini kwani, mbali ya maofisa wa serikali, hata jamaa zake walimshauri asirudi tena nchini kutokana na jina lake kuchafuliwa mno na vyombo vya habari," alisema ofisa mmoja mwandamizi wa BoT.
Ofisa huyo alisema baada ya kufanya kazi ndani na nje ya nchi kwa miaka mingi na kujijengea heshima kubwa, watu walio karibu na Gavana Ballali, walimshauri aende kupumzika na kuangalia zaidi afya yake nje ya nchi na zaidi Marekani ambako tayari alikwishakupazoea.
"Hivi unadhani hata kama ni wewe, watu wengi wamehusika na ulaji wa BoT, halafu wewe ndiye unabebeshwa lawama na kuharibiwa jina kwa hiyo kwa kuwa ni mgonjwa ni bora akapumzike na kupata matibabu akiwa na familia yake bila kupata bughudha," anasema ofisa huyo wa BoT.
Hata hivyo, Mbunge wa Karatu (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa, ameliambia KULIKONI kwa simu jana kwamba suala la Ballali kutorejea alikwishalizungumzia Juni 15, 2007 na hivyo haoni ajabu kusikia Gavana amejiuzulu akiwa nje ya nchi.
Hata hivyo, Dk. Slaa anasema kama kweli serikali inaendeshwa kwa haki, Ballali anastahili kurejea ama kurejeshwa nchini na kujibu tuhuma ama kushitakiwa.
"Kama kuna watuhumiwa na washitakiwa wanaolazwa pale Muhimbili (Hospitali ya Taifa ya Muhimbili) wakiwa na pingu mikononi na miguuni, kwanini hawa wakubwa nao wasifungwe pingu hata kama wanaumwa? Hatuwezi kuwa na huruma kwa wakubwa na kuwahukumu wadogo," alisema Dk. Slaa.
Alisema Ballali anashauriwa asirejee nchini kwa kuwa mbali ya yeye binafsi kuhusika na tuhuma mbalimbali, wako watu wazito ndani ya serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaohusika na ufisadi ndani ya BoT na hivyo kurejea kwake nchini kunaweza kuibua mambo mengi zaidi.
"Mbali ya hayo, kuna kosa la jinai ambalo Ballali amelifanya kwa kughushi taarifa aliyoiwasilisha kwa Waziri wa Fedha, , taarifa ambayo ilikabidhiwa kwa wabunge, sasa hilo ni kosa la mtu kufungwa kwanini aachwe huko nje?" alihoji Dk. Slaa.
Habari za awali zilizoifikia KULIKONI juzi zilieleza kwamba Gavana Ballali ameomba kujiuzulu rasmi wadhifa wake, kupitia barua yake ya kujiuzulu kwa Rais Kikwete Jumatano wiki hii akitoa sababu za matatizo ya kiafya kuwa ndio zimemfanya achukue hatua hiyo.
Ballali ambaye amekuwa Gavana wa Benki Kuu kwa miaka saba sasa amekuwa akipatiwa matibabu katika hospitali moja mjini Boston, huko Marekani kwa takriban miezi mitatu iliyopita, lakini kabla ya kuanza tiba alikuwa nchini akipambana na shutuma nzito za ufisadi dhidi yake na taasisi ya umma anayoongoza.
"Gavana ametaja sababu za matatizo ya kiafya kufuatia operesheni ya upasuaji aliyofanyiwa kuwa ndio sababu kuu ya kujiuzulu kwake," chanza cha habari serikalini kimesema.
Chanzo hicho kiliongeza: "Tunatarajia Rais atakubali kujiuzulu kwake kwa kuwa tunatambua shutuma za ufisadi zilizokuwa zinamkabili pia."
Vyanzo vya uhakika vinasema, Dk. Ballali alikutana na Rais Kikwete wakati alipokuwa katika ziara ya kikazi nchini Marekani hivi karibuni ambapo alisisitiza nia yake ya kujiuzulu. Pia watendaji waandamizi wa serikali wamefanya mazungumzo ya siri na Dk. Ballali nchini Marekani.
Inafahamika pia kwamba Dk. Ballali, ambaye amekuwa nje ya nchi kabla ya mchakato wa kuchunguza ufisadi ndani ya Benki Kuu haujaanza rasmi, atakuwa anakamilisha tu hatua ambayo ilitarajiwa kwani isingekuwa rahisi kwake kujisafisha dhidi ya shutuma nzito zilizokuwa zinamkabili.
Serikali nayo kwa upande mwingine imekuwa ikishinikizwa sana na wafadhili na wahisani wa nje ili kuchukua hatua dhidi ya tuhuma za ufisadi ndani ya Benki Kuu na sehemu nyingine za sekta mbalimbali.
Baadhi ya wafadhili wakubwa wa serikali wamefikia hatua ya kutishia kuchelewesha utekelezaji wa ahadi zao za misaada kwa Tanzania wakitaka hatua kali zichukuliwe dhidi ya mafisadi.
Kwa miezi kadhaa sasa, Ballali amekuwa akikataa kujiuzulu wadhifa wake licha ya kutakiwa kufanya hivyo na raia kadhaa wakiwemo pia wabunge.
Katika mkutano na waandishi wa habari makao makuu ya Benki Kuu Julai mwaka huu, Ballali alisema hawezi kujiuzulu na kwamba tuhuma dhidi yake ni za "uzushi na uongo mtupu."
Tuhuma mojawapo inayomkabili, Dk. Ballali ni ujenzi wa jengo jipya la Benku Kuu - BoT Twin Tower – kwa gharama kubwa kuliko gharama halisi.
Dk. Ballali anatuhumiwa pia kwa kuidhinisha malipo ya dola za Marekani milioni 200 (takriban bilioni 250/-) kwa ajili ‘miradi isiyoeleweka' na kuidhinisha ada kubwa za mawakili wa kutetea kesi za Benki Kuu.
Kujiuzulu kwa Gavana Ballali bado kutaacha tatizo kuhusu gharama za jengo jipya ‘BoT Twin Tower' zinazokadiriwa kufikia dola milioni 340 (takriban bilioni 425/-). Tathmini ya wataalamu wa ujenzi zinasema gharama hizo ni mara mbili ya gharama za kujenga jengo la aina hiyo katika miji maarufu ya nchi zilizoendelea kama London, New York au Tokyo.
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imekuwa inachunguza tuhuma hizi pamoja na malipo ya mamilioni ya dola kwa kampuni mfu za Meremeta Gold Mine Company Limited, Tangold, Mwananchi Gold Company, Alex Stewart Asseyors na kadhalika.
Wakati Dk. Ballali anataka kujiuzulu Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utuoh, anatarajia kuwasilisha serikalini taarifa rasmi kuhusu ukaguzi aliofanya ndani ya Benki Kuu hususan katika kijengo cha malipo ya madeni ya nje, kinachoshutumiwa zaidi kwa ufisadi.