Alaa! Baada ya kumsikiliza Sitta na Mwakyembe sasa nimeelewa kwa nini Slaa na Zitto wamenunua ajenda ya Dowans dhidi ya Shelukindo. Kumbe kweli hii ni Operesheni Sangara. Dili ni kufufua ishu ya Richmond bila kuinyanyulia bango Tanesiko ya 'Dakta wa Vijisenti' ili 'Vilongola' walioponea chupuchupu nao pia waingie kitanzini. Si unakumbuka aliyekuwa Waziri Mkubwa alisema nini wakati analalama kuwa 'amedhalilishwa sana' , 'amesononeshwa sana' na 'amefedheheshwa sana'? Alisema hivi: 'Put in on the table, who is Richmond', yaani, 'Iweke wazi mezani, Richmondi ni nani'? Operesheni Sangara ya Dowans-Richmond ya Zitto-Slaa ikifanikiwa basi ukweli wote utawekwa mezani. Hapo ndipo nchi itatikisika hasa. Ole wetu. Namalizia kwa nukuu hii ya Mwalimu Nyerere kutoka kwenye ukurasa wa 46 wa kitabu chake cha 'Uongozi Wetu na Hatma ya Tanzania':
"Narudia: Kumbadili Waziri, hata Waziri Mkuu, si jambo la ajabu. Anaweza kujiuzulu, anaweza kufukuzwa, na Nchi isitikisike. Lakini huwezi kumtikisa Rais wa Nchi bila kuitikisa Nchi yenyewe. Ni vizuri jambo hili likatamkwa wazi wazi na likaeleweka sawa sawa. Maana watu wengine wananong'ona nong'ona kuwajibika kwa Rais kana kwamba ni jambo la mchezo mchezo tu. Kulazimika kumchukulia hatua Rais wa Nchi ni mkasa na balaa kwa Nchi yoyote ile. Ndiyo maana tunatakiwa kuwateua na kuwachagua Marais wetu kwa uangalifu mkubwa; na ndiyo maana wakishachaguliwa, wanatakiwa wajiheshimu na kuwa waangalifu sana" - JKN, 1994
Mwenye sikio na asikie Mwalimu anacholiambia Taifa. Mungu Ibariki Tanzania. Wabariki viongozi wake. Amina.