JUMAMOSI, MACHI 16, 2013 05:46 NA KULWA MZEE, DAR ES SALAAM
*Washindwa kumfikisha mahakamani
JESHI la Polisi nchini, jana limeshindwa kumfikisha mahakamani Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare.
Hatua hiyo, ilionekana kuwachefua mawakili wa Lwakatare, ambao walifika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mjini Dar es Salaam, kwa ajili ya kumwekea dhamana.
Mawakili hao, walidai Jeshi la Polisi linaongoza kwa kuvunja sheria za nchi kwa kumshikilia mteja wao kwa siku tatu, bila kumfikisha mahakamani.
Mawakili hao, Tundu Lissu, Profesa Abdalaah Safari na Peter Kibatala, walitoa malalamiko hayo baada ya kusota siku nzima wakimsubiri mteja wao afikishwe mahakamani.
Akizungumza kwa niaba ya mawakili wenzake, Lissu alisema sheria inasema mtu akishikiliwa na polisi, anatakiwa kufikishwa mahakamani ndani ya saa 24, kinyume cha hapo ni uvunjifu wa sheria.
"Tangu asubuhi tuko hapa mahakamani, tulidhani wamemaliza uchunguzi wao watamfikisha mahakamani, hii ni makusudi kabisa ili wamweke rumande hadi Jumatatu…kisheria hawaruhusiwi kukaa na mtuhumiwa kwa siku tatu, wanatakiwa kumfikisha mahakamani ndani ya saa 24.
"Jeshi la Polisi Tanzania, wanafikiria sheria za nchi hii haziwahusu, wanaona wanaweza kumshikilia mtu wanavyotaka wao, hawa ndio chanzo cha ukiukwaji wa sheria za nchi.
"Nilimuuliza afande Kigondo ambaye ni Kaimu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai kujua wanafuata sheria zipi kukaa na mtuhumiwa siku zote hizo, alinijibu kwamba yeye ni mpelelezi tu, nimuulize afande Isaya Mangulu.
"Nimemuuliza Mangulu, ananijibu kwamba anayehusika ni Kigondo, lakini baadaye akanipigia simu na kuniambia hataletwa mahakamani, upelelezi bado unaendelea," alisema Lissu.
Lissu, alisema inaonekana wazi polisi hawajui kwa nini wanaendelea kumshikilia Lwakatare.
Alisema tuhuma zinazomkabili, zinaonekana wazi kuwa za mambo ya kisiasa zaidi.
Aliongeza kuwa, kama itafika Jumatatu bila kumpeleka mahakamani, watafanya utaratibu wa kukutana na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Said Mwema, ili kujua jeshi hilo, linatumia sheria gani kushikilia mtuhumiwa.
"Nawaambia Lwakatare hajafanya kosa lolote na hao wanaosema na kufikiria hivyo, walete ushahidi mahakamani tupambane.
"Haya ni maneno ya kina Mwigulu Nchemba (Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara), anayetangaza katika vyombo vya habari kwamba viongozi wa CHADEMA, wanapanga mauaji kama hayo, ndiyo yamefanya Lwakatare ashikiliwe na Polisi, nawaambia wajiandae sawa sawa," alisema Lissu.
Wakili Profesa Safari, akichangia hilo alisema, polisi wako kinyume na kifungu cha sheria namba 32 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, hivyo wanatakiwa kumpa dhamana mtuhumiwa ili kuepuka kujiaibisha.
"Tunamwambia IGP Said Mwema, wasijiaibishe, wampe dhamana Lwakatare, kwanza ni mgonjwa wa sukari wanataka kuhatarisha maisha yake," alisema Profesa Safari.
Lwakatare alikamatwa Jumatano asubuhi, kwa tuhuma za kuhusika na matukio ya mashambulizi dhidi ya watu hapa nchini.
Taarifa kutoka ofisi za makao makuu ya CHADEMA Kinondoni jijini Dar es Salaam, zinasema Lwakatare alikamatwa saa 7 mchana na watu wanne waliojitambulisha kama maofisa wa Jeshi la Polisi, ambao walifika na gari aina ya Toyota Land Cruiser jeupe lenye namba za usajili T 140 BLA, likiwa na chata ya kitalii.
Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, Advera Senso alisema Lwakatare amekamatwa kwa sababu ya kupanga mikakati mbalimbali ya kushambulia na kudhuru watu mbalimbali wakiwamo waandishi wa habari.