KIKAO cha wakuu wa Jumuiya ya SADC kitafanyika nchini kuanzia leo, kikiwa na malengo ya kuzungumza mambo mbalimbali yanayohusu sehemu hii ya Afrika.
Miongoni mwa mambo hayo ni hali ya kisiasa huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na pia hali ya kisiasa huko Zimbabwe.
Kuhusu suala la Zimbabwe, nchi za Kiafrika zimeshindwa vibaya kusimamia maslahi ya watu wa Zimbabwe na hivyo kuacha serikali yao kuendelea kutenda kazi kana kwamba imesimikwa na Mungu.
Hali ya kisiasa ya Zimbabwe inasikitisha na haikubaliki!
Ni kwa sababu hiyo basi, kikao hiki cha viongozi wa SADC kina nafasi ya pekee ya kuonyesha msimamo mmoja wa viongozi hao na hatimaye kuwa sauti ya wale "wasio na sauti" wa Zimbabwe.
Kuendelea kufumbia macho kinachoendelea Zimbabwe, ni kuhalalisha serikali ya kidikteta na kufumbia macho uvunjaji mkubwa wa haki za binadamu.
Tanzania ina nafasi ya pekee katika kuona kuwa suala la Zimbabwe linatafutiwa suluhisho la kisiasa, ambalo litaheshimu Katiba ya Zimbabwe na kulinda haki za raia wote bila kujali vyama vyao au itikadi zao.
Viongozi watakaokutana kwenye mkutano huu, ni lazima wakubali kuwa ile "diplomasia ya ukimya" ambayo imekuwa ikifuatwa hadi hivi sasa katika kulikabili tatizo la Zimbabwe, imefeli, na haina nafasi katika kutafuta suluhisho la kudumu.
Wakati umefika kwa viongozi wetu kuweka mambo kadhaa wazi kabisa kwa Serikali ya Rais Mugabe.
Kwanza, licha ya mchango mkubwa wa Rais Robert Mugabe katika kutafuta uhuru wa Zimbabwe, mchango wake huo si leseni ya utawala wa mabavu au wa kidikteta.
Viongozi wa SADC waseme wazi kuwa, linapokuja suala la haki za raia wote na ulinzi wa utu wa watu wetu, hakuna mtu yeyote ambaye ana haki ya kuvunja, kuondoa, au kuzuia upatikanaji wa tunu hizo.
Kama tulimkatalia Amin, Bokasa, Mengistu na wengine, wakati umefika Waafrika tutambue kuwa Mugabe kwa kuridhia vitendo vya ukiukwaji haki za binadamu, na matumizi ya nguvu katika kuendeleza utawala wake, basi matendo yake mengi yanaanza kupakana na utawala wa kiimla, hivyo lazima abadili mwelekeo au atatengwa.
Pili, wananchi wa Zimbabwe kama walivyo wa sehemu nyingine yoyote ile, wana haki ya kufurahia uhuru wao na haki zao kama raia bila kujali itikadi za vyama vyao au vitu vingine vinavyowatofautisha kama mtu mmoja mmoja.
Katika Zimbabwe ya sasa, kama wewe hauko kwenye chama tawala, basi nafasi yako ya kufanikiwa ni kama sifuri!
Viongozi wa SADC wanapokutana hapa nchini, ni lazima waweke hilo wazi kuwa, tofauti za kisiasa au kimtizamo si sababu hata chembe ya kuwagawa Wazimbabwe na kuwafanya wale walio kwenye chama tawala ndio wazalendo hasa na wale wanaopinga si wazalendo.
Ni wazi kuwa Tanzania ni vigumu kwake kuja na msimamo kama huo, kwani utaakisi mahusiano ya chama tawala hapa nyumbani na wapinzani wao.
Itakuwa sawa na mtu kujaribu kutoa kibanzi kwenye jicho la jirani yake wakati boriti bado liko kwenye jicho lake.
Zimbabwe lazima ionyeshwe upotovu wake huo na itakiwe ijirudi, si kwa ajili ya kuyaridhisha mataifa makubwa bali kwa ajili ya watu wake na hatma ya nchi hiyo.
Tatu, wapinzani wa Serikali ya Zimbabwe ni lazima nao wapewe nafasi ya kusikilizwa na hoja zao kufanyiwa kazi.
Kitendo cha mkuu wa kambi ya upinzani kupigwa na kunyanyaswa pamoja na watu wengine, ni mwanzo mbaya na ni hatua mbaya ambayo viongozi wetu wanapokutana hawana budi kuilaani kwa maneno makali.
Inapofikia kuwa tofauti za kisiasa zinaanza kusababisha watu wapigwe na kufungwa, basi tujue ya kuwa, Zimbabwe imeanza kuunusa mstari utenganishao utawala wa sheria na haki kutoka maisha ya vurugu na uchokozi.
Ukweli ni kuwa, inavyoendelea kuungua Zimbabwe, ndivyo nchi jirani na hususan eneo hili la Afrika zinavyozidi kupoteza sifa zake na kubebeshwa mzigo wa matatizo yanayotokana na Zimbabwe.
Endapo itatokea kuwa serikali ya Mugabe iendeshe operesheni ya kukamata wapinzani wake na kuwafunga, basi jumuiya hii itakuwa imepoteza umuhimu wake na kubakia kuwa klabu ya kupigiana soga, na baraza la kuchukuana picha.
Nne, wapinzani wa Mugabe nao waambiwe wazi kuwa, lolote watakalofanya kama ni kinyume cha sheria za nchi, watasababisha kugongana na serikali.
Hivyo ni lazima watiwe moyo, watumie njia zinazokubalika kisiasa ili kufikia malengo ya kisiasa.
Ingawa jambo hili kwa sasa ni kama haliwezekani, lakini jumuiya ya SADC ni lazima ichukue nafasi ya makusudi na ya wazi ya kutafuta suluhisho la kudumu, ambalo litaheshimu uhuru wa Zimbabwe kujiamulia mambo yao, litatambua haki za raia wa Zimbabwe kuishi kwa uhuru bila hofu ya serikali yao, na kusimamia utaratibu wa ujenzi wa hatua za kisiasa ambazo zitarudisha umoja na heshima kati ya makundi mbalimbali ya kisiasa nchini humo. Katika hili Tanzania ina nafasi ya pekee.
Katika kutafuta suluhisho la swali la Zimbabwe, Tanzania inaweza kuonyesha njia kwani sisi ni marafiki, ambao wakati mwingine inabidi tuwaambie rafiki zetu ukweli.
Maneno makali yanapotoka kwa wakubwa kuzungumzia suala la Zimbabwe, inaonekana wana ajenda ya siri na hilo sisi sote tunajua.
Waingereza wanapozungumzia suala la Zimbabwe, si kwa sababu wana uchungu na maisha ya watu weusi wa Zimbabwe, bali wana uchungu na ndugu zao Wazimbabwe weupe ambao wamenyang'anywa ardhi na wengi kulazimika kutimka.
Lakini sisi Watanzania na watu wa bara hili la Afrika, hatuwezi kukaa kimya wakati ndugu zetu wa Zimbabwe wanazidi kujichimbia shimo ambalo jinsi ya kutoka haionekani.
Hapa, Tanzania inaweza kufanya jambo ambalo litasaidia kuondoa mgogoro wa ndani wa Zimbabwe na ule dhidi ya mataifa ya Magharibi.
Tanzania baada ya mkutano huu wa viongozi wa SADC, ikubali jukumu la kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa hali ya kisiasa ya Zimbabwe kwa kuitisha mkutano usio na masharti wa wadau wa hali ya kisiasa wa nchi hiyo.
Wakati umefika wa Tanzania kutoa mwaliko kwa Serikali ya Zimbabwe, vyama vya upinzani vya nchi hiyo na taasisi za kiraia kukaa pamoja na kutafuta chanzo cha mgogoro na kutatufa utatuzi wa mgogoro wa Zimbabwe.
Hatuwezi kuendelea kukaa kimya hadi tuone ndugu zetu, wanaharakati za ukombozi wenzetu wakiendelea kudidimia katika hali mbaya ya kiuchumi huku maisha yao ya kisiasa yakiwa matatani.
Ingawa Tanzania inaweza kufanya hili, lakini kwa Serikali ya Kikwete kuamua kujaribu kutafuta suluhisho la Zimbabwe, inawezekana ikawa ni "kinyume nyume" kwani wakati tunahangaika kutafuta suluhisho la matatizo ya Zimbabwe, ya kwetu bado yanatuzungusha kichwa.
Hata hivyo, hilo lisiwe kizuizi cha kujaribu kutatua mgogoro wa Zimbabwe, kwani kutatupa na sisi ari zaidi ya kushughulikia matatizo yetu kabla hayajafikia mahali pa yale ya Zimbabwe.
Kwa kuanzia hata hivyo, tuwasaidie Zimbabwe waondokane na hali ya wasiwasi ya sasa, mgongano wao wa ndani, uhasama na nchi za Magharibi na uundaji wa mazingira mapya ya kisiasa ambapo kila Mzimbabwe atafurahia matunda ya uhuru wa nchi yake bila kujali rangi zao, itikadi zao, au mfungamano wowote wa kisiasa.
Tukifanikiwa kufanya hivyo, basi wito wetu kama Watanzania tunaojigamba nao wakati wa kukimbiza mwenge kila mwaka utatimia, nao ni "kuleta matumaini mahali ambapo hakuna matumaini, upendo mahali ambapo pana chuki, na heshima ambapo pamejaa dharau."
Hakuna mfano mzuri wa mahali kama hapo kuliko Zimbabwe ya sasa.