Na Said Kubenea
JAKAYA Mrisho Kikwete, mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) taifa, anapaswa kushitakiwa kwa uchochezi.
Akifungua mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama chake mjini Dodoma leo, Kikwete alichochea wanachama wa CCM kuwapiga wapinzani kwa kudai kuwa, Uvumilivu una kikomo.
Amewataka wana CCM kuacha unyonge kwa madai kwamba wapinzani wamekuwa wakiwapiga huku wao wakisubiri polisi kuchukua hatua za kisheria.
Hii ina maana kwamba, Kikwete ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano, amewataka wanachama wa CCM, kuchukua sheria mkononi. Ametaka wananchi kuumizana, kupingana na kuuana. Huu ni uchochezi unaoweza kuingiza nchi katika machafuko ya kisiasa, kidini na kijamii.
Kama Kikwete alitaka urais, bila shaka alijipima na kujiona anaweza kufanya kazi hiyo. Kama alikuwa anajua anakwenda Ikulu kujaribu, basi alikuwa amekosea. Ikulu siyo sehemu ya kujaribu.
Kauli ya Kikwete ya kutaka wananchi wajibu mapigo, ni ishara kwamba ameomba kazi ambayo haiwezi.
Rais wa nchi hawezi kuchochea raia wake kupigana. Anapaswa kutumia vyombo alivyonavyo kusimamia sheria.
Ni lazima akumbushwe kwamba nchi hii ikiingia katika machafuko au mauaji ya halaiki, yeye ndiye atakuwa wa kwanza kuulizwa. Anaweza asiulizwe na vyombo vya sheria vya hapa, lakini ataulizwa na vyombo vingine vya dunia.
Yeriko hampaswi kumsuta JK kwa kauli yake, mnapaswa kujiuliza kama aliyoyasema ni ya kweli na kamani ya kweli basi muone umuhimu wa kubadilika amani ya Tanzania haitalindwa na rais KIKWETE au CCM peke yao, ni jukumu la taifa zima mkiwemo ninyi mnaolalamkiwa.