Posted Date::4/14/2008
Serikali isisubiri taarifa imchunguze Chenge
Mwananchi
SIKU chache baada ya gazeti la The Gurdian la nchini Uingereza kuchapisha habari kwamba uchunguzi umeanza kufanyika dhidi ya Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge, kuhusiana na akaunti yake iliyoko katika benki moja ya nchini humo kukutwa na dola za Marekani zaidi ya 1 milioni (Sh1.2 bilioni), serikali imeahidi kuchukua hatua za kisheria kupata uhakika wa jinsi fedha hizo zilivyopatikana.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Sofia Simba alisema mwishoni mwa wiki iliyopita kwamba, wakipata taarifa rasmi juu ya suala hilo, taratibu za kisheria zatafuatwa kwa kuangalia kwenye kumbukumbu za Waziri Chenge, kama alijaza fomu za viongozi za kutaja mali zao, kikimwemo kiasi hicho cha fedha na kuonyesha jinsi alivyozipata.
Kauli hiyo ya serikali inatia moyo kama kweli hatua hizo zinachukuliwa na kusimamiwa vizuri kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni njia mojawapo muhimu ya kukabiliana na ufisadi wa viongozi wa umma hapa nchini.
Ni jambo la ajabu sana kwa kiongozi wa umma, tena wa ngazi za juu serikalini kuwa na kiasi hicho kikubwa cha fedha katika benki za nje ya nchi, wakati uchumi wa nchi yetu unaendelea kudorora.
Hata kama alizipata fedha hizo kwa njia halali, kwa nini azifiche nje ya nchi yetu wakati hapa nchini kuna benki zinazoweza kumtunzia vizuri na wakati huo huo kuwasaidia Watanzania kutokana na kodi na riba zinazokatwa kwenye fedha hizo pamoja na kutumika kwenye miradi mingine kwa njia ya mikopo inayotolewa na benki kwa watu na mashirika mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya taifa letu?
Kama tatizo ni la thamani ya fedha ya nchi yetu kutokuwa imara kutokana na hali ya uchumi kuwa mbaya, karibu benki zote hapa hapa nchini zina akaunti za fedha za kigeni ambazo angeweza kuzitumia na bado zikawanufaisha Watanzania na taifa kwa ujumla.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, inadaiwa kuwa waziri Chenge alikiri kuwa na kiasi hicho cha fedha kwenye akaunti ya benki moja iliyoko kwenye kisiwa cha Jersey na kufahamisha kuwa hakuzipata kwa njia ya ufisadi.
Hata hivyo, kauli ya serikali haijatoa picha maalumu juu ya hatua itakazochukua katika suala hilo, hivyo kuifanya jamii kuwa na hofu kwamba huenda kale katabia ka kulindana kanapewa nafasi kama inavyokuwa kwenye mambo mengine yanayohusiana na masuala kama hayo ambayo humalizwa kimyakimya.
Si hivyo tu, badala ya serikali kusubiri taarifa ya uchunguzi kutoka kwa taasisi maalumu ya kuchunguza makosa makubwa ya jinai nchini Uingereza ya Serious Fraud Offence (SFO), inafaa kwa kutumia vyombo vyake nayo ifanya uchunguzi wake wa kina ili kujiridhisha na suala hilo.
Tusema hivyo kwa sababu, hata kama suala hilo linamhusu Chenge binafsi, ni wazi tuhuma hizo ni kashfa kubwa kwa serikali kwa sababu ni mmoja wa mawaziri wake mwenye dhamana ya kuiwakilisha nchi kwenye maeneo mbalimbali, kwani kwa wadhifa wake huo anaweza kuingia mikataba na mashirika ya nje kwa niaba ya Watanzania.
Inashangaza kuona kwamba serikali inashindwa kubaini viongozi wake wanaoficha fedha zao nje ya nchi badala ya kuzihifadhi hapa nchini, ili zitumike kuimarisha uchumi wa nchini yetu.
Kwa ujumla, tunalaani kitendo cha viongozi wetu wa ngazi za juu serikalini kuficha fedha zao nje ya nchi, ikimaanisha kwamba wanahamisha utajiri wa nchi yetu na pia wanaonyesha kwamba hapa nchini mambo si shwari, hivyo kuwafanya wananchi kuwa na hofu na mwelekeo wa taifa lao kiuchumi.
Tunaomba serikali isingoje taarifa za wakaguzi wa nje juu ya suala hilo, bali ishiriki kikamilifu kufuatilia suala hilo nchini Uingereza na mahali pengine na lisiishie kwa Chenge tu, bali hata kwa viongozi wengine pia.