Viongozi CCM kuzunguka nchi nzima kujibu hoja za wapinzani
Abdallah Bawazir na Muhib Said
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimepanga kutumia viongozi wake wa kitaifa hadi matawi kueleza ukweli wa shutuma zilizotolewa na Mbunge wa Karatu, Dk Wilbroad Slaa, dhidi ya viongozi wa serikali na chama.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Aggrey Mwanri, alisema ili kujisafisha na tuhuma hizo, viongozi wa chama hicho kuanzia ngazi ya taifa hadi matawi, watazunguka nchi nzima kueleza ukweli wa suala hilo ili kuisafisha serikali na CCM.
�Chama chetu kina mtandao mkubwa, tutatumia njia ya kujisafisha kwa kuwaeleza wananchi ukweli. Viongozi wetu watazunguka nchi nzima kuzungumza na wananchi ili wazipuuze kauli za wapinzani ambao wao wenyewe wamedai kuwa nia yake ni kuwafanya wananchi wakichukie serikali ya chama hicho, jambo ambalo hatulikubali,� alisema.
Alipotakiwa na waandishi wa habari kueleze kama tuhuma zilizotolewa hazina ukweli ni kwanini chama hicho kisichukuwe hatua za kisheria, alisema chama chake hakina mpango wa kwenda mahakamani.
�Tunaamini kuwa Watanzania wanaheshimu utawala wa sheria, hivyo kama kuna mtu yoyote mwenye ushahidi kuhusu tuhuma za ubadhirifu au rushwa katika vyombo vya umma, basi aupeleke ushahidi huo katika vyombo vya dola kama Takukuru, polisi, Usalama wa Taifa na vinginevyo,� alisema.
Katika tamko hilo alisema chama hicho pia kinaunga mkono kauli ya serikali iliyotolewa hivi karibuni na Waziri Nchi, Ofisi ya Rais ( Siasa na Uhusiano wa Jamii), Kingunge Ngombale-Mwiru kuhusiana na tuhuma za Dk Slaa.
Akisoma tamko la CCM kuhusiana na tuhuma hizo za wapinzani Mwanri, alidai kuwa chama hicho kimebaini kuwa nia ya vyama vya upinzani ni kutaka kukichafua na kukichonganisha na wananchi, jambo ambalo halitakivumilia.
�Shabaha ya vyama vya upinzani ni kuichafua serikali ya CCM mbele ya umma ili kujitafutia umaarufu wa kisiasa nchini. Wanataja majina ya viongozi hadharani bila ya kuwa na ushahidi wowote , kinachosikitisha anatajwa hata Rais aliyechaguliwa na asilimia 80.2 ya wananchi kutokana na imani waliyonayo kwake. Jambo hili halikubaliki hata kidogo,� alisema Mwanri.
Nao Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), umesema unaunga mkono kauli ya Kingunge na kusema wanaamini tuhuma hizo zimejaa upotoshaji wenye lengo la kujenga chuki dhidi ya serikali, kuwapaka matope viongozi na kuhatarisha amani.
Taarifa ya UVCCM iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana ilieleza kuwa kitendo cha kutunga tuhuma za uongo na kisha kuanzisha kampeni maalum ya kuzizungumza ili kuwafanya wananchi waziamini imekuwa ikifanywa na wapinzani kwa muda mrefu sasa.
"Mfano hai ni tukio la hivi karibuni la kusema uongo bungeni lililofanywa na Zitto kuhusiana na mkataba wa mradi wa mgodi wa dhahabu wa Buzwagi. Alishindwa kuthibitisha madai yake akasimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge kwa kusema uongo.
Ni wapi mtu muongo akaitwa shujaa? Hizi ni propaganda za wapinzani kuficha ukweli, alisema sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa na Katibu Mkuu wa UVCCM Taifa, Amos Makalla na kuongeza:
"Kwa hulka hiyo UVCCM haishangazwi na hatua nzima ya umoja wa wapinzani ya kuja na madai mengine dhidi ya viongozi wa CCM, serikali na taasisi zake".
Source-MWANANCHI