Pamoja na kukupa hongera zangu na pia pokea shairi hili.
[1]
Owa s'andame hadaa, moyo ukahadaiwa
Owa anaye kufaa, mke mwenye kusifiwa
Owa upate kuzaa, kama ulivyozaliwa
Owa ukijaaliwa, mupendane na mkeo
[2]
Owa aliye na kheri, muandamane kwa dini
Owa yai la johari, litiye nuru nyumbani
Owa mdomo mzuri, ukupambie lisani
Owa ungiye nyumbani, mupendane na mkeo
[3]
Owa moyo wa imani, usozumbua mafuja
Owa usiowe duni, anayeitwa kioja
Owa mtenda wa dini, ndiye mke mwenye haja
Owa utungiwe koja, mupendane na mkeo
[4]
Owa siowe tambara, linukiyalo vibaya
Owa mwanamke jura, mlekeze njema ndia
Owa usiowe sura, kutaka kuzangaliya
Owa mzuri tabiya, mupendane na mkeo
[5]
Owa kijana kitoto, mteshi wa kutekeya
Owa akwandike jito, mwenye kukuhurumiya
Owa usiowe zito, jabali likakwemeya
Owa aliye na haya, mupendane na mkeo
[6]
Owa s'andame uhuni, upate juwa kuzawa
Owa nami natamani, ela sijajaaliwa
Owa utiye chandani, pete uloiteuwa
Owa ujuwe kuowa, mupendane na mkeo
[7]
Owa uvishwe kilemba, na joho na mahazamu
Owa wapate kupamba, ukale twiba na tamu
Owa upambiwe chumba, upate tanganya damu
Owa usijidhulumu, mupendane na mkeo
[8]
Owa kinda la tausi, alo nadhifu mibele
Owa kiini cheusi, chendacho nyuma na mbele
Owa siowe tetesi, apaye watu uwele
Owa aliye lekele, mupendane na mkeo
[9]
Owa ualike watu, wahudhuriye arusi
Owa nawe uwe mtu, mkeo simnakisi
Owa muonyane utu, mukae mutaanasi
Owa mupane mepesi, mupendane na mkeo
[10]
Owa akukubaliye, akuizao siowe
Owa upendane naye, zamani sizo ujuwe
Owa akuridhiyae, mujikubali wenyewe
Owa mukae mutuwe, mupendane na mkeo
[11]
Owa chenye asimini, kikuba cha asiliya
Owa kilo na rihani, na waridi maridhiya
Owa kilicho na shani, na manukato kutiya
Owa ujuwe duniya, mupendane na mkeo
[12]
Owa utukuze cheo, na jina lipate kuwa
Owa apate mkeo, aambiwe meolewa
Owa kama waowao, moyo usiliye ngowa
Owa ujuwe kukuwa, mupendane na mkeo.
Dr Hamza Yosuf Al-Naamani
Doha. Qatar