Sehemu ya 87
“Ngo, ngo, ngo!” niligonga mlango. Ukimya ulikuwa umetawala. “Ngo, ngo, ngo!” niligonga tena.
Nikasikia mchakacho wa hatua za mtu akisogea getini. “Nani wewe!” sauti ya kike ilisikika.
Mungu wangu!. Ilikuwa ni sauti ya Lawalawa. Mapigo ya moyo yalienda kasi. “Dawa ya mganga imefanya kazi? Huyu Lawalawa kweli ametoka huko mashariki ya mbali alikokuwa ameolewa na karudi Tanzania, nguvu za dawa hizi kweli? Ama kaja kwa mambo yake mengine tu?” Nilijiuliza kimoyomoyo. “Nani wewe?” Lawalawa aliendelea kuuliza akiwa ndani. “Mimi!” hatimaye nikamjibu.
Mlango ukafunguliwa. Macho kwa macho na Lawalawa. Kwa pamoja tukabaki tukitizamana kwa sekunde kama nne ama tano, kisha chotara huyo akanirukia na kunikumbatia kwa furaha. “Ajibu!!...Ajibu jamani Ajibu!!” aliniita huku akiwa amenishika kwa nguvu. “Naam mpenzi.” “Ajibu mume wangu mpenzi, ulikuwa wapi miaka yote hiyo?” “Nilikuwepo Lawalawa”
Alitoka mwilini mwangu, akaniangalia usoni kwa hisia kali. Machozi ya furaha yakajikusanya machoni mwake. “Karibu ndani baba, pita ndani mpenzi wangu.”
“Ndani kwenu!!” niliongea kwa wasiwasi.
Nilitambua mwanamke huyo alikuwa akiishi na baba yake, sasa vipi anikaribishe mimi mpenzi wake ndani ya nyumba ya mzee wake. Adabu gani hiyo? “Ndio pita, usigope?” alisema. Akanishika mkono na kunipeleka ndani.
“Wewe Lawalawa humwogopi baba yako, si mke wa mtu wewe?” “Njoo...Pita usiogope.” Binti alizidi kunivutia. Tukaingia ndani sebuleni. Nilimkuta baba mmoja mzee sana, alikuwa hajiwezi kutokana na uzee, aliketi sofani huku akionekana kuchoka kwa kutafunwa na maradhi ya utu uzima.
Alikuwa ni mwarabu, ngozi ya mwili wake ilikuwa ikining’inia mwilini, nywele zake zilikuwa nyeupe kama sufi, zilionesha kunyonyoka kwa kukosa afya. Macho yalimtumbukia ndani na midomo ilimtepeta.
Alikuwa na umri kati ya miaka 90 ama 95. Alikuwa ni kikongwe aliyebahatika kuwa hai. “Huyu ni baba yangu,” alinitambulisha, akaendelea. “Baba huyu anaitwa Ajibu, ndiye mwanaume niliyekuwa nakwambia habari zake,” alimwambia yule mzee, sikujua aliposema ‘Ndio mwanaume niliyekuwa nakwambia habari zake’ aliwahi kumweleza nini baba yake.
TUKUTANE KESHO.