SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 51*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Rhoda akatazama dirishani njia ya kuelekea Goshen. Akakamata nondo za dirisha na kusaga meno. Akatazama njia hiyo kwa sekunde kadhaa, alafu akasema kifuani mwake.

"Goshen, hata ukinitupia katikati ya mamba nikaliwe, bado nitarejea nikiwa nawaongoza mamba hao."

ENDELEA

Sasa akakubaliana na kichwa chake kwamba kazi aliyonayo ni kutafuta namna ya kurejea tena Goshen. Arejee kwa nguvu zote. Arejee kama Malkia.

Huko ndipo alipozaliwa na ndipo atakapofia. Si pengine pale.

"Twende tukale malkia wangu," Venim akamwambia akimtoa hapo dirishani. Wakaongozana mpaka chini mezani. Rhoda alikuwa na njaa na hakuona haja ya kubisha. Tumbo lake lilikuwa tupu kwa kutokula muda mrefu.

Meza ikachafuliwa kwa masinia ya vyakula na mabilauri kedekede. Lakini Rhoda akashindwa kula. Hakukuwa na chakula cha kumridisha wala kuendana naye pale mezani.

Masinia yalikuwa yamejaa viungo vizima vizima kama vile macho, masikio ya wanyama mbalimbali na hata binadamu! Viungo hivi vilikuwa vimechemshwa tu na kutiwa siniani.

Kutazama bilauri, zote zilikuwa zimejawa na damu. Hazikuwa za mvinyo kama vile Rhoda alivyokuwa amewaza. Basi tumbo likaanza kumchefua. Akataka kutapika lakini hakuwa na kitu tumboni.

Haraka akatoka katika meza ile iliyokuwa inamkifu, akaenda zake kando akapate hewa safi. Pale mezani palikuwa pananuka, na kama angeendelea kuketi hapo basi angejikuta anapoteza fahamu kwa ubongo kukosa hewa ya oksijeni.

"Nini shida Malkia wangu?" Venim akamuuliza. "Je hujapenda chakula tulichoandaa kwa ajili yako?"

"Chakula gani kile?" Rhoda akafoka. "Unadhani mimi ni kama nyie kunilisha vyakula vya ajabu?"

"Samahani sana, Malkia wangu," Venim akamwambia akimshika mkono. "Ni makosa yangu. Hatufahamu nini binadamu hupendelea hivyo tukaandaa chakula chetu bora kabisa. Niambie unataka nini, nami nitakuletea mezani kufumba na kufumbua."

"Inawezekana?" Rhoda akauliza

"Hakuna kisichowezekana kwa Malkia wangu," Venim akamjibu. "Kama nilimtoa sadaka kaka yangu kwa ajili yake, nitashindwaje kumuwekea chakula mezani?"

Rhoda akatabasamu. Kauli hii ilimkonga moyo. Lakini pia ikaonyesha mwanzo mzuri kwenye harakati zake.

'Hakuna kisichowezekana kwa Malkia wangu.'

Akajikuta anatabasamu tena alafu kwa madaha akasema chakula anachokitaka na namna anavyopenda meza iwe. Ndani ya muda mfupi, meza ikajawa na nyama za kuokwa, mbogamboga mbalimbali na matunda ya kila aina.

Mabilauri yakajaa mvinyo mwekundu na meza ikapambwa kwa maua ya uwaridi. Pakavutia haswa. Sasa Rhoda akajongea kitini na kula atakavyo. Venim akawa anamtazana Rhoda akitafuna na kunywa. Moyoni akajihisi faraja.

Alikuwa anapenda kila kitu kuhusu Rhoda. Alifurahi sana kumwona mwanamke huyo karibu yake na akajiapia hatomruhusu tena aende mbali na upeo wa macho yake.

Ilikuwa ni kama bahati mwanamke huyo kurejea tena mikononi mwake. Ulikuwa ni kama muujiza. Akajiwekea agano la kumlinda kadiri ya uwezo wake na kuhakikisha mwanamke huyo anapata furaha mbele ya macho yake.

"Venim," Rhoda akaita akiwa ameshikilia kipande cha nyama mkononi.

"Itapendeza ukiniita mumeo," Venim akamrekebisha kwa tabasamu na kumuuliza: "Unasemaje Malkia wangu?"

"Nina ombi moja mume wangu," Rhoda akasema kwa sauti ya chini. Venim, moyo wake ukiwa umepozwa na sauti hiyo, akauliza kwa staha:

"Lipi hilo?"

"Nataka unifunze ulozi," Rhoda akajibu kwa uhakika. Venim akastaajabu. Ila si kwa ubaya, alipenda wazo hili. Hakutegemea kama Rhoda angelipenda kujua ulozi. Sasa akaona dhamira yake ya kuwa Malkia kamili wa himaya yake inaenda kutimia.

"Kweli unataka kujua, malkia wangu?"

"Ndio. Sidhani kama ni vibaya?"

"Hata kidogo. Nitajivunia kukuelekeza hayo. Ukiyajua, utajua Malkia wa himaya yangu vema. Tutatengeneza himaya imara na yenye nguvu kuwahi kutokea."

Rhoda akatabasamu. Akaupumzisha mdomo wake kuongea akaendelea kutafuna, lakini kichwani mwake akiendelea kuyapanga mambo. Hakutaka kupoteza muda kabisa. Kila sekunde kwake ilikuwa inahesabika.

Ilikuwa na thamani mpangoni mwake.

**

"Vipi, mmepaonaje hapa kwangu?" Aliuliza kuhani Raam akikuna ndevu zake nyeupe. Mbele yake alikuwa wamesimama Oragon na Ottoman wakiwa wamevalia nguo nadhifu. Sasa wamekuwa vijakazi wa mwanaume huyo maarufu himayani kama kuhani.

"Tunakushukuru sana," akasema Oragon. "Hatukuwa na pa kwenda ukatupatia hifadhi. Hata hapa si tu tunaishi bali tunapata kila hitaji letu."

Raaam akatabasamu.

"Msijali. Kuleni na mnywe. Ishi kama mpo nyumbani. Binadamu tuneumbwa kutegemeana na kusaidiana."

"Ahsante sana," Ottoman akasema akikumbatisha viganja vyake. "Hatuna cha kukulipa kabisa. Umekuwa mkarimu sana kwetu."

Raam akaenda zake. Oragon na Ottoman wakaendelea na kazi zao za hapa na pale lakini kumbe Raam alikuwa amesimama kwa mbali akiwatizama.

Akikuna ndevu zake, akawatazama wanaume hao kwa muda wa dakika kadhaa kisha akatabasamu tena na kwenda zake akiyoyoma sasa.

Vijana wale wa Harid wakamaliza kazi zao na kuketi mezani kujipatia chakula cha mchana. Ndani ya muda mfupi, wakaja wanaume wengine wawili, ambao nao walikuwa vijakazi wa Raam, wakaungana nao mezani kula.

"Ni raha iliyoje mnaipata hapa?" Akauliza Ottoman. "Mnakula kama si vijakazi. Mnavaa kama si vijakazi. Mna uhuru kama wanawe!"

Vijana wale wawili wasiseme jambo wakamtazama Ottoman kisha wakaendelea kula. Kukawa kimya kidogo kabla Oragon hajauvunja kwa kuuliza:

"Raam hana familia?"

"Hana," akajibu kijakazi mmoja. "Anaishi mwenyewe na vijakazi wake."

"Na uzee wake wote, hana hata mtoto wa kurithi mali zake na kumlinda?" Oragon akaendelea kuuliza.

"Hana," akajibu kijakazi mwingine. "Umwonavyo ndivyo alivyo."

"Kwanini?" Ottoman akadakika kuuliza.

Wale vijakazi wawili wakatazamana alafu mmoja wao akasema:

"Msijali. Kadiri mnavyoendelea kukaa hapa mtafahamu kila jambo. Kwahiyo tunzeni macho na masikio yenu."

Oragon na Ottoman wakatazamana. Hawakuuliza tena wakajaza midomo yao na vyakula.

**

"Nakuomba mara moja," ilikuwa sauti ya Raam ikimwambia Oragon. Majira yalikuwa ni usiku. Oragon alikuwa akifutafuta buibui konani mwa nyumba.

Akaacha kazi yake na kuitikia wito. Akaongozana na Raam mpaka chumbani kwake, Raam akaketi kitandani wakati Oragon akiwa amesimama.

Raam akamtazama Oragon kisha akamwambia
"Njoo uketi hapa," akionyeshea mkono kandokando yake.

"Hapana," Oragon akajibu. "Hapa panatosha tu mkuu."

Raam akaminya mdomo wake na kuuliza:

"Kuna kitu nilishawahi kukuomba tangu umekanyaga hapa?"

"Hapana," Oragon akajibu akitikisa kichwa.

"Basi hiki ndiyo cha kwanza," Raam akasema. "Njoo ukae hapa!"

Oragon akatii agizo. Akaenda kuketi kando na Raam. Raam akatabasamu. Akaweka mkono wake begani mwa Oragon alafu akamwambia mwanaume huyo:

"Tangu siku ya kwanza nilipowaona, nilivutiwa nanyi. Mlionekana vijana watanashati, wenye nguvu zao. Nisingeweza kukataa kuwasaidia."

Akiwa anaongea hayo akawa anasogezasogeza pua yake shingoni mwa Oragon. Oragon akakereka mno lakini akazuiza hasira zake.

"Niliwaona mkiwa watupu hamna nguo. Hicho kikawa kitu changu kizuri kabisa kukiona kwa siku hiyo nzima. Miili yenu iliyojawa misuli na umbo la ukakamavu. Hakika mlinivutia."

Akatulia kimya. Oragon akasali moyoni mwake isiwe kama ambavyo ameshaanza kuwaza. Mwili ukamtetemeka. Akatamani hata ayayuke na kupotea.

"Natamani niwaone kama nilivyowaona siku zile," Raam alimnong'oneza Oragon sikioni, kisha akamng'ata kidogo. "Unaweza ukanionyesha tena uufanye usiku wangu kuwa wa kipekee?"

Oragon akashindwa kuvumilia. Akanyanyuka haraka na kumtazama Raam kwa macho ya mshangao. Akamuuliza:

"Ni nini unataka kwangu?"

Raam akacheka.

"Ni mjinga tu ndiye atakuwa hajanielewa ni nini nataka," akajibu akitazama sehemu za siri za Oragon.

"Siwezi!" Oragon akafoka. "Sahau kabisa hilo. Siwezi nikafanya huo ushenzi!"

Raam akaguna kwa kebehi kisha akanyanyuka.

"Pengine wewe ni mgeni inabidi nikupe elimu kidogo. Ndani ya himaya hii mimi ni kuhani. Kila mtu ananiheshimu na kunisikiliza. Unadhan kama ukikataa nitakuacha hai uende huko kutema maneno?"

Akapiga hatua kumsogelea Oragon.

"Utachagua moja. Unihudumie ama nikuue kisha nikuzike asijue mtu yoyote yule!"

Raam akavua nguo zake na kubaki mtupu. Akamsogelea Oragon kwa ukaribu na kuweka mkono wake sehemu za siri za mwanaume huyo. Akazipapasa akitabasamu.

Oragon akakosa uvumilivu. Akamsukuma Raam kwanguvu, mzee huyo akadondoka na kujikita kichwa kwa mbao ya kitanda. Akakata moto.

Oragon akatoa macho kwa mshangao.

**

"Ottoman, amka! Amka twende!" Oragon alipaza sauti akiunyaka mkono wa kaka yake na kumvuta toka kitandani.

"Nini? Mbona hivyo?" Ottoman akastaajabu.

"Nahisi nimemuua Kuhani!" Oragon akajibu kwa sura ya mkanganyiko. "Twende kabla hatujakamatwa!"

Lakini getini kulikuwa kuna walinzi. Wanaume watatu waliobebelea silaha. Wangefanyaje?

Na wakiendelea kukaa hapo, sebuleni wakiwa hawajui la kufanya, wale vijakazi wengine wawili watakawakuta. Watawaacha?

**
 
*MKUFU WA MALKIA II -- 52*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Lakini getini kulikuwa kuna walinzi. Wanaume watatu waliobebelea silaha. Wangefanyaje?

Na wakiendelea kukaa hapo, sebuleni wakiwa hawajui la kufanya, wale vijakazi wengine wawili watakawakuta. Watawaacha?

ENDELEA

Hakukuwa na namna. Iliwabidi waruke ukuta kwa kusaidiana wakatokea huko upande wa pili na kuanza kukimbia. Hawakujua wanapoelekea ila alimradi waondoke na kuacha mbali nyumba ya kuhani huyo.

Walipokimbia sana, wakasimama wapumzike. Mapafu yalikuwa yamekaukiwa. Wakashika magoti yao wakihema kama mbwa.

Walikuwa wanavuja jasho haswa. Macho yamewalegea kana kwamba wamepigwa na moshi. Ottoman hata akaketi chini baada ya kuhisi viungo vinamuuma haswa.

Hapa ndiyo akamuuliza mwenzake, nini kilimsibu kujaribu kumuua kuhani? Oragon akamwambia mwanaume huyo alimtaka kimapenzi.

Ottoman akatoa macho.

"Una maanisha nini?"

"Alitaka nimlale!" Oragon akajibu kwa midadi.

Ottoman akashika mdomo wake kwa mshangao. Ilikuwa ngumu kuamini mzee yule, mwenye nafasi yake kubwa ndani ya himaya, alikuwa na michezo hiyo.

Kumbe ndiyo maana hana mke wala mtoto! Wakang'amua. Lakini sasa tunafanyaje na wapi tunaenda? Swali lilikuwa hapa. Na wapi pia watapata chakula?

Wakakaa hapo kama kinda za ndege zilizompoteza mama yao. Na kwakuwa walitoka mbio kwa kuhani, hawakuwa wamebeba chochote kile mikononi mwao. Hata 'vituguo' vya kujihifadhi ama kujifunikia.

Wakalala wakiwa wamejikunyata, miili yao ikipambana na baridi kali. Wakisimamisha masikio yote kusikia ujio wa shari toka pande yoyote ya dunia.

**

"Mbona nakuita muda wote huo, hukunisikia?" Raam alifoka. Alikuwa yupo uchi chini sakafuni akiwa ameshikilia kichwa chake kinachomimina damu. Sakafu ilikuwa imetapakaa damu. Na mwili wake ulikuwa umeshika damu upande wake wa kushoto alioulalia.

Mbele yake alikuwa amesimama bwana Marimari mmoja wa vijakazi wake wa ndani.

"Sikukusikia, mkuu," akasema Marimari. Alikuwa amepigwa na butwaa kumwona mkuu wake katika hali ile aliyomkuta.

"Wako wapi wale vijana wapya?" Akauliza Raam. Kabla hajasubiria majibu akaagiza: "wakamateni na muwamalize mara moja!"

"Hawapo!" Marimari akampasha. "Sijawaona kwa muda sasa hapa ndani hata nikajua umewatuma huko nje."

Raam akashika kichwa chake kwa maumivu. Habari hizo zikamuumiza kichwa zaidi. Akajitahidi kunyanyuka akisaidiwa na Marimari, akajiveka joho jepesi na kutoka ndani kwenda kuonana na walinzi wake langoni.

Akamtaka abakie mlinzi mmoja tu, hao wengine wote, pamoja na wale ambao hawapo zamu, wajumuike wakawatafute wakina Oragon popote pale walipo.

"Mtakapowakamata, muwamalize asijue mtu yeyote yule. Sawa?"

"Sawa, mkuu!" Wakaitikia kwa ukakamavu.

"Ni wageni himayani hivyo hawatawasumbua kabisa. Mkiulizia mtawapata kwa urahisi, na hata wakichangamana na wenyeji mtaweza kuwachambua. Vilevile mkiwaua hakuna atakayewaulizia wala kusumbuka nao," Raam aliwapasha zaidi. Baada ya maelezo hayo, wanajeshi wakaenda zao kwenda kuwasaka vijana hao.

**

Kwa mbali wanaume wawili walionyeshea kidole upande wao wa kulia wakinong'onezana. Mmoja alikuwa mwanaume mfupi na mwingine mrefu. Kwakuwa ilikuwa giza, ilikuwa ngumu kuwatambua.

Baada ya kunong'onezana huko wakasogea kwa haraka na kusimama mbele ya wanaume waliokuwa wamejilaza chini.

Walikuwa ni wakina Oragon!

"Nyie!" Wakawaamsha wakiwasukuma na miguu. "Amka! Amka! Amka!"

Wakina Oragon wakamka kwa hofu kubwa wakidhani wameshatiwa nguvuni. Walipotazama vema wakagundua ni wale wanaume waliowakwapulia kila kitu chao. Wakataka kuzua ugomvi, lakini mara wanaume wale wakachomoa jambia zao na kuwatishia kuwanyofoa uhai.

"Tulieni hivyo hivyo kabla hatujawatoboatoboa!"

Wakanywea akama ukili majini. Wanaume hao wakawasachi mifukoni lakini hawakupata kitu. Badala yake wakina Oragon ndiyo wakawaomba wawafadhili kwani hawana mbele wala nyuma.

"Naomba mtupatie fedha kidogo," akasema Oragon. "Hatuna hata cha kutia mdomoni."

Wale wanaume wakatazamana, alafu yule mfupi akarudishia jambia lake kiunoni na kuwaambia kama wanataka kula basi waungane nao la sivyo waozee hapo.

"Mnafanya shughuli gani?" Ottoman akauliza.

Wanaume hao wakacheka alafu mrefu akasema:

"Yani mpaka sasa hamjajua tu tunafanya shughuli gani?"

Kisha wakacheka tena.

**

"Mwambie ntalizingatia, anipatie muda tafadhali," alisema Phares akimwambia mwanaume mgeni aliyekuwa ameketi naye. Mwanaume huyu alikuwa ana ndevu za wastani, nywele nyeusi ti ndefu mpaka begani, na kwenye kifua chake upande wa kushoto alikuwa ametundika alama ya ndege, ishara ya himaya ya Maam.

Mwanaume huyo, mjumbe wa Maam, akanyanyuka na kumpatia mkono mfalme.

"Nitamfikishia habari hizo, lakini nisiwe muongo, hamna muda wa kungoja tena. Keshokutwa anaapishwa kuwa mfalme na hawezi akaapishwa pasipo kuwa na mke."

Mjumbe huyo akashusha pumzi ndefu na kutengenezea nguo yake.

"Kwahiyo kiuhalisia muda ulionao ni kesho tu mpaka majira ya jioni," akasema mjumbe kisha akaondoka zake mfalme akimsindikiza kutoka naye nje. Mjumbe huyo alipoyoyoma mfalme akarudi zake ndani akiwa na mawazo.

Sasa ni rasmi kijana wa mfalme alikuwa anamtaka Tattiana akawe malkia wake. Harid alishampasha habari kijana huyo kuwa Tattiana ndiye mrembo himaya nzima.

Na ubaya zaidi, hata mjumbe huyu aliyetumwa kuja hapo himayani, alikutana na Tattiana akasadiki hayo maelezo. Akasema Alah! Kweli huyu afaa.

Sasa afanyaje?

Mfalme akahisi kichwa kinamuuma. Hakuwa radhi kumpoteza Tattiana hata kidogo.

**

Ni usiku sasa. Tattiana hakuwa katika chumba kimoja na mfalme kama inavyotakiwa, bali katika kile chumba alimokuwa anaishi malkia Vedas.

Humo alikuwa tayari ameshafungua kabati na kuchukua chupa ile ya maajabu. Anaitazama na kujiuliza maswali kichwani.

Anaisikiliza chupa hiyo na kusikia ikidunda mapigo ya moyo. Anasikiliza tena na kuhakiki kweli, yalikuwa ni mapigo ya moyo.

Leo anapata wazo na kuanza kung'amua kitendawili hiki. Alijiuliza:

"Nimelala na mfalme kwa muda wote huo, amekuwa baridi mpaka nashindwa kulala. Lakini pia sijawahi kusikia mapigo yake ya moyo, hata nilipolaza kichwa changu kifuani mwake.

Ina maana hana moyo?" Akajiuliza akitazama chupa ile.

"Au moyo wake ndiyo huu chupani?"

Habari hiyo ikaleta mantiki.

"Lakini nani kauweka moyo huo humo? Inawezekanaje mfalme akaishi na huku moyo wake upo chupani?" Maswali hayo yalimpasua kichwa. Na kama haitoshi basi, yule kiumbe anayetoka nje ya chupa pale ifunguliwapo, ni nani?

Akakumbuka yale maneno yake: "Nefil njhami khatu habab?" Anamaanisha nini?

Ikiwa ni usiku sasa mkali, akiwa ndani ya mawazo haya, mara anasikia harufu ya ajabu. Akanusanusa kuhakiki. Hakuijua harufu hiyo ni ya nini. Na kadiri na muda ilikuwa inaongezeka!

Akashindwa kuipuuzia. Akaificha chupa kabatini na kuanza kuifuatilia harufu hiyo. Akafungua milango na kutembea akikatiza korido kadhaa akiacha pua ifanye kazi yake.

Mwishowe akajikuta amefika kwenye kingo ya kasri. Kwenye kakona kidogo alikuwa amesimama Bella akiwa ameshikilia miti kadhaa mikononi mwake. Miti hii ilikuwa inafuka moshi mweupe.

"Bella," Tattiana akaita. "Unafanya nini hapo muda huu?"

Bella hakujibu. Akawa anamtazama Tattiana kana kwamba alikuwa anamtarajia. Tattiana akasogea karibu zaidi. Kuangaza akaona askari kadhaa wakiwa wapo chini.

Hakuelewa kilichokuwa kianendelea pale.

"Bella, unafanya nini hapa? Na hao maaskari mbona wapo chini?"

Tattiana akawatazama vema wale maaskari. Akagundua walikuwa wamekufa. Macho na midomo yao ilikuwa wazi!

Akamezwa na hofu. Lakini kufumba na kufumbua, kabla hajatenda hata jambo, akasukumizwa kwanguvu na mtu tokea nyuma. Akajigonga na kizuizi cha kibaraza, akabinuka na kudondokea chini!

Bella na Lucy, aliyetokea nyuma, wakamtazama. Lucy akabinua mdomo wake na kusema:

"Amekwisha."

Bella akamalizia.

"Tufanye upesi!"


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom