*MKUFU WA MALKIA II -- 53*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Bella na Lucy, aliyetokea nyuma, wakamtazama. Lucy akabinua mdomo wake na kusema:
"Amekwisha."
Bella akamalizia.
"Tufanye upesi!"
ENDELEA
Baada ya muda mchache, ikagundulikana Tattiana amedondoka chini. Hata mfalme akaamshwa na kujuzwa hilo. Ilikuwa bado ni usiku wa manane. Tattiana hakuwa anajielewa, na kama kuna hatua basi za kuelekea kifoni, yeye alikuwa amebakiza moja tu.
Hakuwa anaelewa chochote kile. Hakuwa hata na punje ya fahamu. Alipoteza damu nyingi. Mifupa yake mingi ilikuwa imevunjikavunjika. Hata kama angelipona, basi kamwe asingeliweza kurejea kwenye hali yake ya kawaida.
Angeweza kupooza mwili ama kuwa mlemavu wa kudumu.
Mfalme akachanganyikiwa sana. Ni nini kilitokea? Tattiana alifika huko kufanya nini? Ilikuwaje akaangukia chini? Vijakazi wote pamoja na walinzi wakaitwa na kuulizwa kilichotokea.
Nani alimwona Tattiana na mpaka anadondoka walikuwa wapi?
Kukawa kimya. Hakuna aliyesema jambo. Kila mtu aliogopa kwani kama ingebainika anahusika, angechukuliwa hatua kali maana mfalme anampenda sana Tattiana.
Lakini baadae, baada ya kubanwa sana wakitishiwa kufungwa maisha yao yote, Bella kwa uoga akasema huwa anamwona Tattiana majira ya usiku akizungukazunguka.
"Sijui huwa anafanya nini," akaeleza. "Ila si mara moja wala mbili."
Kidogo naye mmoja wa wanajeshi walinzi wa kasri akasema pahali pale alipotelezeaTattiana na kudondoka palikuwa pana mafuta. Hicho ndicho kimemwangusha.
Maneno haya yakawa mengi sana lakini ukweli ukabakia kwamba mtu pekee atakayetoa taarifa sahihi ni Tattiana na si mwingine. Mdomo wake ndio pekee utakaoeleza ukweli wa mambo.
Lakini sio leo wala kesho. Mwili wake ulikuwa umekusanyiwa kitandani daktari akihangaika kuokoa uhai wake.
"Itachukua muda mrefu sana kurejea. Amedondoka vibaya na kuathiri uti wake wa mgongo," daktari alieleza.
Mfalme akamsihi arejeshe uhai wa mwanamke huyo kwa namna yoyote ile. Hatamwelewa kabisa mwanamke huyo akifariki. Yupo tayari kwa gharama yoyote na chochote atakachohitaji atampatia.
"Umenielewa?" Mfalme akamkaba daktari.
"Ndio, nimekuelewa," daktari akasema kwa hofu.
Baadae taarifa zikasambaa himaya nzima. Melkizedek na mkewe wakashtushwa mno na habari hizo hata wakafunga safari upesi kwenda kumwona mtoto wao.
Mama alipomwona akalia sana. Akamuuliza mwanaye aliyekuwa hamsikii, nini ilikuwa shida? Kwanini amejiingiza matatizoni hivyo?
Kwa uchungu aliokuwa nao, hakutaka kurudi na mumewe nyumbani. Alitaka kubaki na mwanaye hapo kasrini anapotibiwa. Kwa mfalme hakuwa na shaka, akaona kheri.
Mama huyo akaketi kandokando ya mwanae akimtazama, machozi yanambubujika.
"Nitahakikisha kila kitu kinakuwa sawa," mfalme alimtoa hofu Melkizedek. "Nitampatia kila huduma na ulinzi wa kutosha. Usijali."
"Nashukuru sana," Melkizedek akampatia mkono mfalme. "Natumai mkononi mwako yupo salama."
Mfalme akamsindikiza mpaka nje, bwana huyo akaenda zake.
**
"Sasa tunafanyaje?" Aliuliza Bella akimtazama Lucy aliyekuwa amejilaza kitandani. Walikuwa ndani ya chumba peke yao. Wakati Lucy akiwa amejilaza miguu ipo chini, Bella alikuwa ameketi kitako.
Wote walionekana kutingwa na mawazo. Hawakuwa na raha. Hawakuwa na amani.
"Mimi nilidhani atakufa!" Akalalama Lucy. "Mwanamke ana roho ngumu yule. Kudondoka kote huko!"
"Tunafanyaje sasa?" Bella akarudia swali lake ambalo halikupatiwa jibu. Alikuwa ana hofu mpaka anatetemeka. "Akiamka si atatutaja?" Akaendelea kulonga. "Na akitutaja si ndo mwisho wetu huo!"
"Usijali," Lucy akampoza. "Hawezi amka yule. Hata akiamka atakuwa bubu, si kwa namna alivyodondoka."
"Mmh," Bella akaguna. "Unadhani itakuwa hivyo? Mfalme ameweka madaktari wote nguli ndani ya himaya wamtimbu mtu mmoja. Unajua hilo?"
"Najua!" Lucy akajibu akinyanyuka. "Lakini kifo kamwe hakizuiliki hata uwe na madaktari wangapi. Kikija kinakuja tu. Cha muhimu ni kumtazama kwa jicho makini. Tukimwona anapata ahueni, ama anaelekea kupona, basi tunammaliza!"
"Utaweza kwa namna anavyolindwa vile?" Bella alikuwa na shaka.
"Inawezekana!" Lucy akajibu akibinua mdomo. "Hakuna lisilowezekana, kumbuka tupo chini ya paa moja."
Kisha akauliza:
"Zile maiti umezihifadhi vizuri?"
"Za wale maaskari?" Bella akauliza.
"Ndio, kwani kuna zingine?" Lucy akabweka.
"Nimezihifadhi pazuri hamna shaka," Bella akachonga.
"Sasa inabidi tumalizie lile zoezi letu," Lucy akahusia. "Ila itabidi tutulie kidogo kwani kwa sasa ulinzi utakuwa mkubwa sana."
**
Baada ya kutembea kwa muda mrefu, Waheed akawaasa wapumzike angalau kidogo wavute pumzi. Wakaketi na kunywa maji kulainisha makoo yao.
Kulikuwa na ka giza hafifu kama vile jioni. Walitulia hapo kana kwamba wapo msibani. Hakuna mtu aliyekuwa anamwongelesha mwenzake wala kuongea. Hawakuwa na furaha. Haikuhitaji kusoma vitabu kulijua hilo.
"Tutadumu humu mpaka siku gani?" Fluffy akauvunja ukimya. Aliuliza akiwa amejikunyata kana kwamba anasikia baridi kali.
"Siku tatu," Waheed akajibu. "Vipi kuna tatizo?" Kisha akauliza.
Fluffy akamtazama kama mhaba wa matumaini, alafu akasema:
"Nataka kutoka nje."
Wenzake wote wakamtazama.
"Nataka kwenda nyumbani na kuachana na haya yote," akaongezea. Na punde macho yake yakawa mekundu kama bendera. Mara yakavujisha maji.
"Usilie, Fluffy," Seth akamuasa akimshika bega. "Yote yanakaribia kwisha. Tumeshamaliza."
"Sidhani," Fluffy akajibu akivuta makamasi. "Nimechoshwa na haya. Nini maana ya safari hii kama tunatoka tofauti na tuliongia? Hata tutakapopata hicho tunachokihitaji, nini itakuwa furaha yake?"
Maneno haya yakamgusa kila mmoja isipokuwa Waheed. Alikuwa anamtazama mwanamke huyo kwa mapuuzo akitamani hata kumziba mdomo.
"Tumehangaika mno kufika hapa, alafu tunakuja kupotezea hapa! Yale yote ya mwanzoni yanakuwa bure? Tuliyafanya yanini?" Fluffy aliendelea kumwaga maneno.
Alikuwa na uchungu kifuani mwake na kadiri alivyokuwa anaongea ndivyo akawa anazidi kuupata zaidi. Machozi yalizidi kummiminika na ikafikia pahala akawa hawezi hata kuongea.
Kifua kilimbana. Kwikwi zilimzidi na kuubana ulimi. Seth akahangaika kumbembeleza pasipo mafanikio. Ikafikia kipindi sasa Waheed akashindwa kuvumilia.
Akatamani kuropoka, ila akaona hamna haja hiyo. Akajitahidi sana kudumu na hasira yake. Alisimama akawaambia waondoke kwani muda wa kupumzika sasa umekoma. Alifanya hivyo kukatisha yaliyokuwa yanaendelea.
Basi wakanyanyuka na kuendelea na safari yao. Wakatembea kwa umbali wa nusu kilomita kabla hawajakutana na njia panda. Hapo wakasimama kidogo kutafakari.
Lakini ndani ya Waheed kulikuwa na roho ya kidhalimu. Roho ya kinyama.
Katika hali ya mshangao akachomoa kisu chake kiunoni alafu haraka, kufumba na kufumbua, akamkita Alk kifuani, akamkita pia na Fluffy!
Wakadondoka chini wakiugulia maumivu makali. Waheed, pasipo huruma, akamkita pia na Seth aliyekuwa hawezi kujitetea kwa kujaa na majeraha miguuni.
Wote wakalala chini wakiwa wanavuja damu lukuki, kisu cha Waheed kikichuruza kwa kushiba damu.
Waheed akatabasamu. Sasa alikuwa amekamilisha kazi. Akasimama kuwatazama watu hao wakikata roho. Na walipotimiza zoezi hilo, akaendelea na safari yake roho ikiwa nyeupe.
Hakuwahitaji tena watu hao. Hawakuwa na faida tena kwake. Alikopita huko ndipo alipokuwa anawahitaji kama sadaka. Sasa aendako ni kushuka tu. Anaweza maliza mwenyewe.
***