*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 20*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Asubuhi...
Mfalme Phares akiwa anapata kifungua kinywa, haraka anaingia kamanda wa vita na kusimama kando kando yake, akatoa heshima zake na kumwambia mfalme ya kwamba kuna msiba, wa yule kijakazi wake aliyekuwa yu hoi kwa kuumwa!
Mfalme akasikitika sana kwa kupoteza dhana yake muhimu.
Kabla hajasema neno lolote, yule kamanda akaongezea taarifa ya kwamba kila mtu anaogopa kuushika wala kuuzika mwili wa mtumishi huyo.
ENDELEA
Mfalme upesi akaacha chakula chake na kukimbilia huko kwenye mazishi. Akakuta watu wachache waliokuwa wamejifunika pua zao na watu kadhaa kwa mbali wakiwa wanateta - hawa walikuwa wanataka kuuzika mwili huo.
Wote wakamsalimu mfalme na kumkaribisha eneoni .
"Mfalme, japo tumetangaza dau kubwa kuuzika mwili huu, hakuna anayethubutu," alisema mwanaume aliyekuwa anasimamia shughuli.
Akampeleka mfalme kuutazama mwili wa marehemu kisha akaagiza watu wauzike upesi kama mfalme alivyoagiza. Wanaume watatu waliovalia mifuko wakatekeleza agizo hilo.
Mfalme akakaa na kutazama mpaka shughuli hiyo ilipoisha, kichwani akiwa ana maswali lukuki ambayo hakuyapatia majibu.
Punde akakumbuka kuna kazi alimpatia daktari kuhusu marehemu, hivyo haraka akaagiza daktari huyo aje upesi kumdadavulia asichokifahamu. Ndani ya muda mfupi mlengwa akaja.
"Samahani, mkuu. Hivi ndiyo nilikuwa najiandaa kuja kukuona," akasema daktari kwa unyenyekevu. Mfalme asijali akamtaka ampe maelezo ni nini kilimuua mtumishi wake hadidi?
Basi daktari akatoa makaratasi yake na kuanza kuyapitia kabla hajasafisha koo lake na kusema:
"Mfalme wangu, sumu iliyotumika kumuulia mtumishi wako ni kali sijapata kuona tangu nianze kazi hii. Inafelisha viungo vya mwili kwa taratibu lakini kwa uhakika. Mwili hukakamaa na kwa wakati mmoja kumenyeka kana kwamba nyama iliyochemshwa kwa juma zima!"
Maneno ya tabibu huyu yakazidi kumpa maswali mfalme, ni nani amempatia mtumishi wake sumu hiyo? Na kwanini?
Alirudi kwenye ngome yake kisha akaitisha kikao cha dharura na matabibu wote wa kienyeji ndani ya himaya, akawauliza nani ana ujuzi wa kutengeneza sumu hiyo; ajabu hakuna aliyekuwa anaijua!
Hata nao walikuwa kwenye bumbuwazi.
"Pengine ungeuliza na wazee wa baraza!" Akashauri mtabibu mmoja.
"Kwanini nifanye hivyo?" Mfalme akauliza.
"Kwasababu wao hujua mengi, wana maarifa makubwa yaliyojenga misingi kwenye himaya hii!" Mtabibu akajibu.
***
Mchana wa jua la utosi...
Baada ya kijakazi wa Sultan kuingia ndani ya chumba, akainamisha kichwa chake na kumwambia Sultan wake:
"Ameamka!"
Haraka Sultan akiongozana na Sultana mdogo wakatoka ndani na kwenda chumba kingine walipomkuta Bibi akiwa amelala anatazama paa. Wakamjulia hali.
Bibi alikuwa amechoka, hata kuongea kwake ilikuwa tabu. Alimuuliza Sultan juu ya maendeleo ya mkewe mkubwa, wakamwambia bado naye yu usingizini.
"Inawezekana akawa amepona?" Sultan akauliza.
Bibi akatikisa kichwa chake;
"Hapana, bali ametulia. Nilifanya makosa sana, hata nisingekuwa hai mpaka sasa. Tatizo lake ni kubwa mno, siwezi kulimudu."
Sultan akafa moyo.
"Kwahiyo umeshindwa? Kabisa? Haitawezekana kumrejesha kwenye hali yake?"
Bibi akashusha kwanza pumzi ndefu. Akawaambia anahitaji muda na pia watu wa kuonana nao.
"Sitaweza peke yangu, inabidi nifunge safari kwenda ng'ambo ya Mashariki."
"Itachukua muda gani?" Sultan akauliza.
"Siku moja tu," Bibi akajibu, kisha akatulia akifikiria. Punde akamwambia Sultan.
"Lakini ni kwa sharti moja."
Sultan akamuuliza ni lipi hilo? Bibi akamtazama machoni na kumshika mkono wake wa kuume.
"Utimize agizo langu la mwisho nitakalokuomba."
Basi Sultan akaapa atatimiza lolote lile atakalotaka Bibi huyo endapo tu akimrejesha mkewe mkubwa kwenye hali yake ya awali.
Na basi akawaagiza vijakazi wake wajiandae kwa safari ya kumsindikiza Bibi kwenda ng'ambo ya Mashariki. Baada ya muda mfupi, maandalizi yakawa tayari. Bibi akapata chakula na kisha kuanza safari.
Akadumu juu ya mgongo wa farasi kwa takribani masaa mawili kabla hajawasili mbele ya ngome kubwa ya mishumaa. Akawazuia vijakazi aliokuja nao wakati yeye akizama ndani ya ngome hiyo.
Baada ya kama nusu saa, akatoka akiwa mpweke. Akakwea farasi na kutazama ngome hiyo kana kwamba kuna kitu anangoja kitokee.
"Hatwendi?" Akauliza kijakazi.
"Hapana!" Akajibu Bibi. "Tutangoja hapa mpaka itakapofika zamu yangu kuingia ndani."
Hakuna kijakazi aliyeelewa, ila wakanyamaza kwa maana haikuwa kazi yao. Wakaendelea kungoja.
Ikapita lisaa bado wakingoja tu.
Likapita na lisaa lingine la pili. Kijakazi akauliza mbona wameketi hapo kwa muda na hakuna kitu wala hawaoni mtu wanayemngoja?
Bibi hakujibu kitu, kama dakika mbili mbele, akashuka toka kwenye farasi akazama tena ndani ya ngome. Mara hii akatoka na mwanamke mwembamba mrefu, akakwea naye farasi wakaanza safari ya kurudi nyumbani.
Ajabu ni kwamba hata pale vijakazi walipotazama nyuma kuangalia ngome ile ya mishumaa, hawakuiona tena! Ilikuwa imefutika.
Waliwasili nyumbani, wakaandaa mazingira ya kazi, na punde zoezi likaanza. Mungu si Athumani, kila jambo likaenda kama lilivyopangwa. Wakafanikiwa kutoa roho ya mfu ndani ya sultana mkubwa.
"Samira!" Bibi akaita. Sultana mkubwa akafungua macho yake na kuitika. Sultan akafurahi sana! Hatimaye alikuwa ameshinda vita.
Akamuuliza Bibi ni nini angependa amfanyie kama zawadi ya kumtendea wema usio na kipimo kwake. Bibi akamvuta kando na kumwambia ana ombi moja tu, nalo ni la mjukuu wake kuwa mke mkubwa.
Hapo Sultan akahisi mwili wake umekuwa wa baridi. Alidhani pengine Bibi huyo angeomba theluthi moja ya utawala wake, na angekuwa radhi kabisa kumpatia. Ila hili swala kwake lilikuwa gumu.
Lakini atafanyaje na ingali alijifunga na kinywa chake kwa kiapo cha kutimiza chochote? Akainamisha kichwa chake chini.
"Atakuwa anakaa hapa?" Akauliza.
"Ndio," Bibi akajibu. "Na mjukuu wangu atahamia kasrini."
Sultan akasita kutoa maamuzi, Bibi akamsihi afanye upesi kwani anataka kumruhusu mgeni wake toka kwenye ngome ya mshumaa aendeze.
Baada ya dakika tano, Sultan akarejea na Bibi ndani ya chumba. Wakateta kidogo na mara akaomba faragha na mkewe mkubwa. Akatumia fursa hiyo kumueleza kwamba atamwacha hapo kwasababu za kiusalama na maendeleo yake kiafya.
Ila Bi mkubwa akawa mwerevu kutambua kuna jambo halipo sawa, akamuuliza:
"Unampeleka kasrini?"
Sultan akahisi ulimi mzito.
****