SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 19*
*Simulizi za series*

Phares alipotelea ndani akimuacha Rhoda anamtazama. Mwanamke huyo alipoteza kama dakika tatu kufikiria, akiwa amesimama.

Alitoka zake ndani kwenda kumtafuta kibaraka wake, kuna mambo alitaka ayaweke sawa. Baada ya punde alimpata, wakasogea kando pasipo na watu.

“Nimeshaongea naye,” alisema Rhoda. “Ila bado sijapata kujua msimamo wake haswa kwenye hili jambo.”

“Kwahiyo tunafanyaje?” akauliza kibaraka. Mwanaume mlinzi mwenye mwili wa mapambano.

“Inabidi tuendelee kumtia hamasa,” alisisitiza Rhoda. “Kama tukimuacha, anaweza akapoteza hili jambo akilini mwake.”

“Sawa.”

“Jitahidi. Nadhani hujasahau kama kuna pongezi kubwa ndani ya hili.” Kibaraka alitikisa kichwa chake kuridhia. Rhoda aliaga akiahidi wataonana kesho, ila kuna jambo mwanaume akalikumbuka.

Alimuita Rhoda akamwambia kwa sura yenye ukakamavu. “Keshokutwa kuna wito wa baraza.”

Rhoda akapigwa na bumbuwazi. “Kweli?”

“Ndio.”

“Umepata wapi hizo taarifa? Mbona Phares hajaniambia.”

“Nakaa, nakula na kulala humu kasrini. Natambua kila korido.”

Rhoda aliinamisha chini kichwa chake akitafakari. Hili jambo lilikuwa ni nyeti na muhimu.

Inampasa ahakikishe kwamba Phares anabakia madarakani, la sivyo, haja zake zote zitakuwa zimekoma. Na kama kuna sehemu ya kuhakikisha hilo, basi ni barazani.

Ila hana nafasi yoyote kwenye baraza. Ni kwa namna gani mawazo na mapendekezo yake yakatasikilizwa na kutiliwa maanani? Anapata mashaka.

“Namjua mzee mmoja tu wa baraza, anaishi nyumba ya tatu mashariki ya kasri hili. Unawafahamu hao wengine?”
“Ndio, nawafahamu. Hawana muda mrefu barazani.”

“Kivipi naweza kuwajua?”

“Kwa kumtumia huyo unayemjua. Ana ushawishi mkubwa barazani kwa uzoefu wake.”

Macho ya Rhoda yalisadifu akili yake inayotatua mawazo. Aling’ata lips kisha akaliza vidole vyake.

“Tuonane kesho.” Aliondoka upesi akishikilia gauni lake lisimkinge kutembea. Alikwea mgongo wa farasi wake mweupe aliyekuja naye, akapotea eneo hilo la utawala.
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
.
.
“Tokea amenikabidhi sijaona chochote. Ndege hasogei na hakuna linalotukia. Nashindwa kuelewa.” yalikuwa maneno ya Sultan aliyekuwa amejilaza kwenye kitanda kikubwa, pembeni yake akiwa na mwanamke mwembamba mrembo, mke wake wa tatu.

Yalikuwa ni majira ya jioni, hali ya baridi ikipuliza kwa mujibu wa vipindi vya msimu. Sultan pamoja na mkewe walikuwa wamejifunika shuka zito la manyoya lililokuwa linajitahidi kwa kiasi kikubwa kupambana kuwapa joto.

Mandhari yalikuwa yanavutia, vitu vikiundwa na madini ya silva ama vumbi la dhahabu. Chumba kilikuwa kinameta. Nadhani si vema kujadili gharama ya samani hizo kwakuwa zaweza kutupa mishtuko ya moyo.

Mwanamke huyu, mke wa tatu wa Sultan, alikuwa mrembo haswa. Japokuwa hakuwa ametia kiungo chochote usoni mwake, bado alikuwa anavutia. Macho yake kama ya mtu aliyetoka usingizini. Mdomo wake, mdogo mwekundu, ni kana kwamba anabusu muda wote. Nywele zake ndefu nyeusi ya bendera zilikuwa zinamsumbua kiuno.

Macho yasikulaghai, mwanamke ni ndani. Hata kama awe ameumbwa siku Mungu hana msongo wa mawazo, kama ndani ni shetani, uzuri wake unakuwa vumbi peponi.

Mwanamke huyu anamtazama Sultan, kisha anapeleka vidole vyake vilaini kumchezea chezea mwanaume huyo ndevu.

“Pole sana mpenzi wangu,” anasema kwa sauti ya puani. “Sasa umepanga kufanya nini?” aliuliza kiudadisi. Sultan alisafisha koo lake na kutulia kwanza kwa sekunde sita kabla ya kufungua lips zake kavu kusema:

“Nitamfunda adabu, naona ananichezea. Kesho nitatuma jeshi langu likamtie nguvuni. Nitachoma dhana zake zote na kumtia ndani ajifunze.”

Mke akatabasamu kwa mbali. “Sasa kama ukimkamata na kumfunga, utapataje hicho kitu unachokitafuta?” Aliuliza kwa sauti ya upole iliyobembeleza masikio ya Sultan, ila swali hilo lilikuwa gumu, Sultan hakuwa na jibu.

“Sijui nafanyaje. Naelekea kukata tamaa sasa.”

Mwanya huu ulikuwa adhimu kwa mke huyu wa tatu. Alishusha mikono yake mpaka kwenye kifua cha Sultan, akawa anachezea nywele za mwanaume huyo akimtazama kana kwamba chakula kitamu kinachomtesa kwa harufu.

“Mpenzi, huna haja ya kukata tamaa,” alinong’oneza na kuendelea: “Ulifanya makosa kutonishirikisha. Laiti kama ningelikuwa nalijua, ungelishapata kito chako hicho cha thamani.”

Sultan hakuwa amemueleza mke huyu kama anachotafuta ni mkufu, bali kito fulani cha thamani. Baada ya hiyo kauli alimtazama mwanamke huyu kwa macho ya kuguswa, akauliza:

“Ungelifanyaje?” Mwanamke akatabasamu.

“Ningelitimiza wajibu wangu kama mkeo, kwa kukushauri namna ya kupata mwarobaini wa tatizo.”

Sultan alikaa kimya, asitie neno. Kwa muda kidogo kulikuwa kimya, ila mke akiendelea kukanda kifua cha mumewe katika namna lainishi.

“Najua hupendi nikimuongelea mke wako wa kwanza, ila jua ya kwamba Karim ana kiburi cha udugu nawe. Anajua hata asipofanya yanayokupendeza, damu ya mkeo itamlinda. Kama mke wako angelitumia ushawishi wake kwa nduguye, haya yangekuwa historia.”

Bado kulikuwa kimya kwa Sultan.

“Hakuna mtu yeyote mwenye uwezo kumzidi Karim maili za mbali sana pande zote za dunia toka kwenye kasri yako. Haingii akilini kuniambia ameshindwa.”

Hapo Sultan akaguna kuashiria kukubali. “Inahitaji theluthi tu ya uwezo wa Karim kupata hicho kito,” aliendelea kusema Mke huyu wa tatu.

“Auhitaji jeshi, wala vita. Naomba unipe nafasi hiyo nami nijaribu kukusaidia. Pengine naweza leta matokeo chanya.” Sultan alinyamaza kwa dakika kama moja. Alikuwa anatafakari. Alitazama dari kana kwamba anaona ramani. Alishusha pumzi ndefu, akamtazama mkewe kwa macho yaliyojawa uchovu.

“Nisingependa kukubebesha shida zangu ...”

“Hapana!” mke akadakia upesi. “Ni faraja kwangu kumhudumia na kumsaidia mtu ninayempenda.”

Ni kama vile mawazo yalimtinda zaidi Sultan. Aliwaza, ila mwishowe akaamua.

“Sawa, unaweza ukanisaidia.” Mke alimbusu shavuni na kumshukuru. Baada ya lisaa limoja, Sultan alijiandaa na kuondoka akirejea kasrini. Alipoyoyoma, mke huyu naye alijiandaa upesi, akiwa ameongozana na walinzi wake wanne, alikwea farasi wake na kuanza safari ya kuelekea kaskazini ya mbali na makazi yake.

Alikuwa amevalia gauni refu zito, jeupe kwa rangi. Kola yake ilikuwa na mawe madogo madogo mengi yenye rangi ya dhahabu. Juu ya gauni hilo alivalia koti kubwa lenye manyoya mengi ya mnyama. Nywele zake ndefu alikuwa amezibana. Uso wake usiwe na kikolombwezo chochote, ila alipendeza. Miguu yake mirefu ilikuwa imefunikwa na viatu imara vya ngozi.

Safari yake ilidumu kwa masaa manne, alifika ikiwa ni usiku. Mbele ya nyumba ndogo yenye chumba kimoja na sebule, ila ikiwa imefumwa kwa ustadi. Mlango wake ulikuwa mkubwa, madirisha madogo. Bomba kubwa refu la kutoa moshi lilikuwa linatazama angani.

Mke huyo wa tatu wa Sultan aliwaamuru walinzi wake wangojee hapo nje wakati yeye akienenda ndani. Walinzi wakatii. Aliugonga mlango mara tatu akiita bibi. Punde mlango ukafunguliwa na mzee wa makamo ya umri wa miaka hamsini na ushee.

Nywele zake zilikuwa nyeusi, mvi za kutafuta. Alikuwa amejitanda shuka kubwa lililofunika mwili wake wote kuanzia shingoni mpaka miguuni. Uso wake ulifanana na wa mgeni wake. Japo alikuwa mzee, hakuwa haba kwenye kujitunza.

Alijikuta anatabasamu punde tu alipomwona mgeni. Alimkumbatia na kumkaribisha ndani kwa furaha.

“Umenikumbuka mjukuu wangu, mbona muda huu?”

“Nina shida, bibi,” alisema mke wa tatu wa Sultan. “Nimeshindwa kuvumilia mpaka usiku ukome.”

“Shida gani hiyo? Ni kuhusu Sultan?”

“Ndio.”

“Umefanya nini tena? Sina nguvu ya kukimbizana barabarani kwenda kuwasuluhisha, mjukuu wangu.”
“Sio hivyo, bibi. Kuna kitu nataka unisaidie. Ni muhimu sana. Lina uzito sawa na lile ulilowahi fanya miaka miwili nyuma.”

Kabla ya miaka hiyo miwili nyuma, mke huyu wa Sultan hakuwa kitu mbele ya jamii. Hakuna aliyekuwa anamjua wala kumheshimu zaidi tu ya kutamaniwa na wanaume mbalimbali, aliowaona wa hovyo.

Siku moja Sultan akiwa anakatiza maeneo ya karibu na bibi huyo aliyekuwa anaishi na mke huyu wa tatu wa Sultan, ndipo maisha yalipobadilika. Bibi huyu akiwa anafahamu fika mjukuu wake ni mrembo, na Sultan angevutiwa naye, basi anaamua kutumia ulozi.

Anasema maneno kadhaa akiwa ameshikilia pindo la gauni lake chakavu, basi Sultan anakatiza kando kando ya kisima alipokuwapo mjukuu wake akifua nguo. Na kutokana na joto la kipindi hicho, binti huyo alikuwa amevalia nguo nyepesi iliyoonyesha umbo lake zuri.

Sultan alisimamisha msafara wake akaagiza aitiwe mwanamke huyo aliyemuuliza maswali kadhaa kisha akaondoka. Baada ya siku moja, vibaraka wa Sultan walitumwa kwenda kumtwaa mwanamke huyo na hayo mengine yote yakawa historia. “Mjukuu wangu, unanitisha,” alisema bibi. Mjukuuye akamshika mkono.

“Si kikubwa, bibi. Kuna kitu Sultan anakitaka. Kinamnyima furaha na amani kabisa. Endapo nikimsaidia kupata kitu hicho, ni wazi nitakuwa nimeteka nafasi kubwa ya moyo wake. Mtoto wangu anaweza akarithi kiti cha utawala.”

Bibi aliukunja uso wake.

“Kitu gani hicho?”

“Ni kito fulani cha thamani. Je bibi una namna yoyote ambayo inaweza ikasaidia kukipata na huku kipo mbali na himaya yetu?”

“Inawezekana, ila kuna baadhi ya mambo inabidi kwanza yawekwe sawa.”

“Yapi hayo?”

“Punguza hamu, mjukuu wangu. Bila shaka leo unalala huku. Pumzika, tutayajenga.”
.
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
.
.
.
.
.
Baada ya kufuatilia kwa takribani siku nzima pasipo mafanikio, ikiwa ni usiku sasa, vikongwe watatu wa Tanashe wanafika kwenye mpaka wa mashariki wa himaya yao. Walidumu hapo kwa muda mchache kabla hawajagundua nyayo za binadamu.

Nyayo hizo zilikuwa ni za mguu wa kike. Walizitazama wasichukue muda mrefu kuugundua ukweli mchungu, nyayo zile zilikuwa za mtu wanayemtafuta, si mwingine bali Malkia. Hakuna mwenye nyayo kama zile Tanashe nzima.

“Ameshaondoka, imewezakanaje?” aliuliza kikongwe mmoja. Nyuso zao zilijawa na huzuni.

“Sijui ni nini kilitokea. Siju ni nini kimempa uhai?” Kulikuwa kimya kwa muda kidogo kabla mmoja hajauliza:

“Itakuwa tulifanya makosa kumlaza na mkufuwe. Hakuna kingine kilichompa uhai zaidi ya mkufu ule. Ule ni mkufu wake na hatukufanikiwa kuchukua kibali hicho kwasababu ya Faki.”

Kukawa kimya tena kidogo. Upepo ulikuwa unapuliza, giza lilikuwa limetanda.

“Kwanini hatukumuona upesi kwenye rada zetu na ilhali alikuwa ndani ya Tanashe? Au atakuwa alitoka nje ya himaya hii tukiwa kwenye mapambano?”

“Yote yanawezekana. Kama bado alikuwa ndani ya Tanashe wakati tunamsaka, basi itatuwia vigumu sana kumrudisha mikononi mwetu. Maana itakuwa inamaanisha hatuna uwezo wa kumuona tena. Sijui uwezo huo ameutoa wapi?”
Akadakia mwingine:
“Na Sijui atakuwa ameelekea wapi? Kufanya nini?”

Walitamani sana kufahamu lakini haikuwezekana. Hawakujua kwa wakati huo Malkia alikuwa juu ya farasi aliyemkwapua hatua chache baada ya kutoka Tanashe akielekea himaya ya masonara.

Mwanamke huyo kifuani alikuwa amebebelea mkufu. Ngozi yake ilikuwa laini inayong’ara. Uso wake ulikuwa na uhai. Nywele zake zilikuwa ndefu, nyeusi. Alikuwa ni yule Malkia! Malkia wa Goshen tuliyekuwa tunamfahamu, mzuri atakayekufanya uache shughuli zako kumtazama.

Alikuwa amedumu kwenye safari hii kwa masaa kadhaa, na sasa alikuwa anaingia msituni kabla hajaumaliza na kudaka jangwa. Alipomaliza msitu huo mpana wenye miti na mandhari ya kuogofya, alimuacha farasi hapo atumie miguu yake kusema na jangwa.

Hakugeuza shingo nyuma kutazama alipotoka. Hakuwa na dalili hata ndogo za kuogopa. Baridi kali lililokuwa linampiga lilimfanya ajikunyate, lakini si kusitisha safari yake. Alizamisha miguu yake ndani ya mchanga na kuichomoa. Hakuchoka.

Safari yake inakuja kukoma katikati ya usiku. Alisimama kana kwamba aliona jambo. Alichota mchanga akaujaza kiganjani mwake kisha akaumwagia mbele yake kama hatua moja, mara shimo kubwa likatokea hapo. Lilikuwa ni lile lililommeza Zura.

Malkia alirusha macho yake ndani ya shimo hilo, hakuona kitu. Kulikuwa ni totoro haswa. Alisimama hapo kama anayechambua kiza anachokiona. Mara akajirusha kuzama humo ndani!

Kishindo kiliashiria amefika chini. Alikuwa haonekani kabisa. Hakukuwa na mwanga wowote ule. Punde baada ya kishindo hicho, sauti ya farasi inasikika. Sauti hii haikomi baada ya mara moja, inaendelea zaidi na zaidi. Inakuwa kelele sasa.

Malkia anasogea taratibu, vishindo vyake vya miguu vinasema. Haichukui muda mrefu, kidani chake cha mkufu kinawaka, sasa anaona anapopakanyaga, anaona pia anapoelekea. Ila mbele bado ni kiza. Haoni komo la shimo.

Anatembea kama hatua nane akiangaza, mara anasikia vishindo vya watu vikikatiza upesi, anasimama! Anaminya kidani cha mkufu wake na mara kunakuwa giza totoro. Alitembea hatua mbili, akaachia kidani hicho, mara mwanga ukachipuka haraka. Uso kwa uso Malkia akaona kundi la watu wa ajabu mbele yake!

Tabasamu linamtoka usoni.
.
.
.
.
.
.
.
****
.
.
LAKO JICHO!
.
.
.
.
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 20*
Simulizi za series


Watu hawa walikuwa ni wakazi wa humo shimoni. Nyuso na miili yao ilikuwa kama fuku. Haijulikani ni lini waliwahi toka nje wakaona mwanga wa jua. Japokuwa tulipata kuwajua watu hawa pale walipomtia Zura nguvuni, ila hii jamii ilikuwapo, haswa wakielezewa vizuri vitabuni.

Ni miaka kadha wa kadha iliyopita. Kwa mujibu wa imani ya hawa watu wa shimoni, binadamu aliumbwa kwa mchanga, hivyo basi ndani ya mchanga ndipo mahali anapotakiwa kuishi. Ndipo kwenye uhai wao. Harufu ya mchanga na udongo ndiyo sahihi kwao, na si marashi ya ‘hovyo’.

Kwa karne lukuki jamii hii imekuwa chini, ikidharauliwa, ikipuuzwa na kutotiliwa maanani. Imekuwa inayodharauliwa na hata wengine wakidhani viumbe hawa ni simulizi tu, hawajahi kuwepo! Sasa hii ilikuwa ni fursa yao ya kurudi na kuudhirishia ulimwengu kwamba wapo, na ni wenye nguvu kuliko ilivyowahi kuwa.

Watadhihirisha hili wakiupata mkufu. Mkufu ambao wamekuwa wakifuatilia kwa muda mrefu kwa macho yao ya tatu. Walijua Zura waliyemteka, atamleta Malkia. Na kweli sasa Malkia amekuja, yu mbele yao.

“Tunaomba mkufu!” alisema mwanamke mwenyeji akimnyooshea Malkia kiganja cha mkono wake. Mwanamke huyo alikuwa anatisha kiasi cha kutosha kabisa kumtishia mtoto anayegoma kunywa uji.

Meno ya mwanamke huyo hayakueleweka rangi. Macho yake yalikuwa mekundu uso ukiwa umefunikwa funikwa na mapande ya mchanga. Wenzake nao pia walikuwa vivyo hivyo kimavazi na kimuonekano.
Mwanamke huyu pasi na shaka ndiye alikuwa kiongozi. Ungeweza kumtambua kwa wepesi kwa nywele zake, aina ya rasta, ndefu zilizokuwa zinagusa kiunoni. “Mkufu upi unaozungumzia wewe?” aliuliza Malkia. Uso wake ulikuwa umejaa kebehi ila mikono yake ikiwa imejiandaa kwa ajili ya vita.

Kwa wakati huo bado farasi alikuwa anaendelea kulia, zaidi na zaidi.

Katika namna ya kipekee kabisa, Malkia anatetema maneno kadhaa yasiyoeleweka, maneno haya yalikuwa kwenye lugha isiyofahamika. Mara ghafla, anawaka kama jua! Wenyeji wanaficha macho yao kwa ukali wa mwanga, pale mwanga unapozima, taswira ya Malkia inaonekana akiwa amevalia nguo za mapambano mkononi akiwa amebebelea panga refu linalong’aa.

Nywele zake zilikuwa zimepigwa pasi vema. Nguo yake ya ngozi ilikuwa imembana katika namna vema ya kumlinda. Sketi yake ilikuwa imecharangwa, na kiunoni ikikobelewa na mkanda wa chuma. Miguuni alikuwa amevalia buti nyembamba za ngozi zenye ncha ya chuma. Kichwani alikuwa amevaa shada la malkia: rangi ya dhahabu lenye ncha ya msalaba mdogo.

Alikuwa mithili ya Malkia wa shaba! Malkia wa falme kubwa ya uajemi!

Vita ilianza, mtu mmoja akipambana na lukuki. Malkia alikuwa mwepesi mno kucheza na ncha ya panga lake. Hakuna shambulizi liliilomgusa hata kidogo. Kila mkono uliomgusa ulikatiwa chini, kila adui aliyesogea karibu aliishia kulazwa chini hajiwezi.
Mkuu wa wenyeji wa shimoni, yule mama, alikuwa amesimama kando akitazama namna wapambanaji wake wanavyopukutishwa. Ilikuwa ni kama miujiza. Watu wake walikuwa wenye kasi mno, ila bado hawakuweza kumkabili Malkia aliyekuwa akiruka, kupotea, na kurusha panga lake kana kwamba mkufunzi mkubwa.

Kwa namna alivyokuwa akishuhudia, mwanamke huyu kiongozi, akaona hitaji la kutafuta namna ya kufanya. Baada ya dakika kama tano, Malkia anawamaliza maadui aliokuwa anapambana nao, ambao wote wanageuka kuwa michanga wakitengeneza kifusi. Anarusha macho yake huku na huko kumsaka mwanamke yule kiongozi, hamuoni!

Alitazama huku na kule. Alisogea akaangaza, bado hakuona jambo. Haikujulikana ni wapi mwanamke yule alipoelekea. Baada ya Malkia kutofanikiwa kumuona adui yake, aliamua kuendelea na safari. Alifuata sauti ya farasi, lakini bado mkononi mwake akiwa amebebelea panga lake refu katika njia ya tahadhari.

Alipiga takribani hatua tano. Mara nyuma ukutani, macho yanafunguka na kumtazama Malkia. Usingeweza kubashiri kama pale kuna mtu. Kumbe ndio alikuwa amejificha mwanamke yule kiongozi!

Rangi ya mwili wake ilikuwa ndiyo ile ile na ya ukuta, mchanga! Endapo akifunga macho basi usingeweza kabisa kabisa kusema kama kuna mtu papo. Alimtazama Malkia kwa macho makali. Malkia akisogeasogea mbali, basi akawa anayafumba macho hayo na punde basi tunayaona macho hayo karibu tena na Malkia.

Mtu huyu alikuwa anasogea ukutani!

Malkia alisonga na kusonga na safari yake. Alikaribia kabisa sauti ya farasi. Alipochukua kona yake ya kushoto, shukrani ziende kwa mwanga wa mkufu, akaona banda la ukubwa wa wastani. Ndani yake lilikuwa limemtunza farasi mkubwa mweupe anayevutia.

Mara tabasamu linachipuka kwenye uso wa Malkia. Alikuwa ni farasi wake, Rob! Farasi aliyekua naye tokea utotoni. Mnyama anayemchukulia kama familia yake. Kwake kumwona farasi huyo ilikuwa ni miujiza, hakutegemea kabisa! Alijikuta akijawa na furaha mno. Machozi yalimlenga. Farasi naye alipiga kelele za furaha.

Pasipo kupoteza muda, Malkia alianza jitihada za kuuvunja mlango amweke huru farasiwe. Alitumia kitako cha panga kutwangia komeo. Alipiga mara ya kwanza na pili, komeo likatenguka. Ila kabla hajamalizia, mara ghafla anapigwa na rungu nyuma ya kichwa, anadondoka chini kama mzigo.

Macho yake yanapoteza uwezo, anaona maruweruwe! Mwili nao unakosa nguvu anashindwa kujinyanyua chini. Anabakia akigugumia kwa maumivu akijibaraguza.

Sauti kali ya cheko ilivuma toka kwa mwanamke yule mchanga. Sasa alikuwa anaonekana vema baada ya kujibandua toka ukutani. Alimtazama Malkia aliyekuwa hajiwezi, akang’aka:
“Amka sasa!” Aliangua tena kicheko. Malkia alijitahidi kunyoosha mkono kufuata panga lake lililokuwa kando, mara adui yake akalipiga teke panga hilo kwenda mbali.

Mwanamke huyu aliyeumbwa kwa mchanga, sasa alikuwa amejiona yeye ni mshindi. Ilikuwa imebakia kitu kidogo sasa kumaliza kazi. Alinyanyua mkono wake wa kuume, uliobebelea rungu zito, tayari kwa ajili ya kummalizia Malkia aliyekuwa hajiwezi pale chini.
Kabla mkono huo haujatekeleza kazi, ghafla anasikia sauti ya mlango wa banda. Anatazama huko. Kabla hata hajapumua, uso kwa uso alikumbwa na farasi aliyemsukuma na kumrushia mbali kama pande la gogo!

Farasi wa Malkia alivunja mlango uliokuwa umebakizwa na komeo goigoi. Mwili wake mzito na wenye nguvu ulitosha kabisa kufanya tukio hilo, hakuwa radhi kumuona Malkia akiuawa mbele ya macho yake. Alipiga kelele kali akisugua kwato za miguu yake kwenye udongo.

Mwanamke yule aliyeumbwa na michanga akanyanyuka kwa hasira. Macho yake makali yalimtazama farasi aliyemjeruhi. Alikwapua rungu lake lisilofahamika wapi alipolitoa, akamuenendea farasi kwa pupa. Loh! Hakufika. Mara akaanza kupuputika kuwa mchanga!

Ncha ya panga la Malkia lilikuwa limetoboa mgongo wake na kutokea kwa mbele, tumboni. Malkia alikuwa ameshafika nyuma yake na kumshindilia chuma hicho mwilini. Kasi yake ilikuwa ya kushangaza sana, hata adui yake hakupata kubashiri.

Alipapasa kichwa cha farasi wake, akasema:
“Anayetaka kukudhuru, inabidi apitie kwangu kwanza.” Alimkumbatia farasi wake kwanguvu. Alimkwea na kuanza kusaka ndani ya eneo hilo kumsaka Zura. Eneo lilikuwa kubwa mno kuliko alivyotarajia. Alizunguka sana pasipo mafanikio. Alipaza sauti yake kuita, lakini bado hakufua dafu, akakata tamaa.
Akiwa anarudi alipotokea, yani kwenye mdomo wa shimo, akapata wazo. Aliona ni vema kunena na mkufu wake. Aliuvua akaufichama kwenye kiganja akiacha kauwazi kadogo alimotia mdomo na kunong’oneza:

“Zura, Zura, Zura upo wapi?” Aliposema hayo alitulia kwa dakika moja kabla hajarudia tena kunong’oneza:

“Zura, Zura, Zura upo wapi?” Sauti yake japokuwa ilikuwa ya kunong’oneza, ilifika kwenye kila kona ikibembeleza kuta. Aliweka mkono wake huo uliofichama mkufu sikioni, akasikia sauti kwa mbali ikigugumia. Ilikuwa ni ya Zura! Alisema na moyo wake. Alizidisha sauti yake kwa kusema:

“Zura! Zura! Zura, upo wapi? Zura! Zura! Zura, upo wapi?”

Sauti yake ilifika vizuri kwenye masikio ya Zura aliyekuwa amelala kizani. Zura alikuwa amechoka mno kiasi cha kushindwa kuongea.

“Zura! …” Malkia aliita, kabla hajaendelea, sauti ikamjibu kwa kukoroma:

“Malkiaa … aa … Malk …” Malkia alichanganyikiwa.

“Upo wapi?” aliuliza kwa pupa. Bado sauti ya Zura ilikuwa ni ya kukoroma, hakuweza kuisikia vema. Aliendelea kuuliza na kuuliza, akaambulia la maana moja:

“Nipo kwenye shimo, shimoni.” Baada ya hapo Malkia hakusikia lingine la maana zaidi tu ya pumzi ya Zura iliyokuwa inafoka kwanguvu.

Alitafuta na kutafuta hilo shimo ndani ya shimo kwa dakika kadha wa kadha. Alikuja kugundua mahali fulani penye uchohoro finyu, hilo ni baada ya farasi kusimama hapo akigoma kuondoka.

Alishuka toka kwenye farasi wake akapenya uchochoroni. Alikutana na ngazi zilizomzamisha shimoni, huko akamkuta Zura akiwa amelala chini.

“Zura!” Malkia alijikuta akiita kwa furaha. Alimgeuza Zura akamtazama usoni. Kwa msaada wa mwanga wa mkufu wake akauona uso uliochoka, macho yaliyopanda juu na mdomo mkavu mno.

Akamnyanyua Zura huyo kama karatasi akamweka begani. Alitembea naye kurudi huko alipotokea, alipofika kwenye uchochoro akapata kazi maradufu. Ilimbidi amsimamishe Zura ndipo apite naye. Akafanya vivyo na kufanikisha. Alimkweza Zura kwenye farasi kisha naye akafuata, farasi akatimka.

Ndani ya muda mfupi, walifika kwende domo la shimo. Mwanga wake ulikuwa hafifu mno na kama isingelikuwa kumbukumbu basi huwezi jua kama hapo ndipo unapotulia pindi unapozama shimoni humo.

Farasi alisimama akiwa hajui pa kuelekea. Malkia aliufichama mkufu wake mikononi , kiganjani, akasema maneno kadhaa ya ajabu, mara kufumba na kufumbua yeye, farasi pamoja na Zura wakapotea! Walitokea kwenye fukwe ya bahari wakiwa wamejilaza.

Wimbi la bahari liliwamwagia maji, farasi na Malkia wakashtuka. Malkia alimtoa Zura toka eneo la bahari kisha akaanza kuangaza angaza mahali alipo. Palikuwa ni pageni kwake. Hakuwa anapafahamu kabisa. Palikuwa pametulia na kusionekane kama kuna dalili yoyote ya makazi ya watu.

Alimpakia Zura kwenye mgongo wa farasi kisha akaanza safari ya kutafuta msaada wa makazi. Muda ulikuwa ni alasiri sasa.
.
.
.
.
.
.
.
. ***
.
.
.
.
*** .
. .
.
. “Bibi, mimi naenda,” ilisema sauti ya kike ndani ya kijumba kidogo maridadi. Sauti hii ilikuwa ni ya mke wa tatu wa Sultan Mansoor aliyekuja kuonana na bibiye kwa ajili ya msaada ghafi.

“Mbona mapema hivyo mjukuu wangu? Haungoji jua lichomoze kuondoa hili baridi?” alisema bibi akiwa amevalia shuka zito lililomfunika gubigubi. Macho yake yalikuwa mekundu yakionyesha ametoka usingizini. Miguu yake ilikuwa ndani ya viatu vyepesi vyenye malighafi ya sweta.

Mke wa Sultan alikuwa amevalia gauni zito jembamba linalombana. Mikono yake ilikuwa imefunikwa na soksi nyeusi za mikononi.

Shingoni alikuwa amejiviringishia kitambaa kizito cha kaki, kichwani akivalia kofia kubwa nyeusi. Shukrani ziende kwa bibi yake anayemtunzia nguo.

“Singoji tena, bibi,” alisema Mke huyu wa Sultan. “Nimengoja vya kutosha. Inabidi niondoke sasa.”

“Aaahaa! Kwakuwa umepata ulichokuwa unakitaka enh?”

“Hapana, bibi! Unataka nikae hapa mpaka lini? Nilimuahidi Sultan kuwa ntampatia suluhisho la tatizo lake haraka. Unataka nipoteze imani yake kama ilivyopotea kwa mke wake wa kwanza?” Bibi akawa kimya. Alimsogelea mjukuu wake akamshika mikono na kumtazama machoni.

“Kuwa makini sana,” alisema. “Hakikisha unafuata kila nilichokuagiza usisahau hata tone.”

“Ndio, bibi. Usijali.”

“Embu niambie nilikuambia nini?”

“Jamani, bibi. Yani nianze kuyasema yooote yale tuliyaongea. Nakumbuka bana.” Bibi alimbusu mjukuu wake kwenye paji la uso kumuaga. Mke huyo wa Sultan akatoka na kuungana na walinzi wake, safari ikaanza kurudi kwenye makazi ya sultana huyu mdogo, mbichi.

Mpaka kwenye majira ya mchana uliokomaa wakawa wamewasili. Kitendo tu cha mwanamke huyu kuingia ndani na kujimwagia maji, Sultan Mansoor anaingiza miguu yake.
Ujio wa Sultan huyo ulimpatia tabasamu pana mke. Alioga vema na kujinyunyuzia marashi. Alivalia nguo sisimuzi tayari kwa ajili ya kumalizia kazi. Kazi ambayo tayari bibi yake alishaimaliza kwa utalaamu wake wa mikono.

Lakini maskini sultana huyu hakujua. Dawa aliyopewa na bibiye aliidondosha njiani akiwa anarejea. Miruko ya farasi aliyempanda ilitoa dawa hiyo toka kwenye mfuko mdogo wa ngozi uliokuwa ubavuni mwa farasi. .
.
.
.
.
.
.
***
.
. .
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom