SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 22*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Kwa hofu, na tahadhari yakinifu akaanza kupekua jengo mahali kwa mahali. Miguu yake ilikuwa inabembeleza sakafu usisikie chochote hata akipita nyuma yako.

Akakaribia kumaliza jengo lote hili pasipo kumwona mfalme! Hapa sasa moyo wake ukaanza kwenda mbio kwani aliwaza mawazo mabaya, pengine wale walozi wamekwisha mkwapua!

Akiwa amesimama anawaza la kufanya, mara anajikuta ameshikwa mkono! Na mara amezibwa mdomo na kuamriwa anyamaze kimya. Anapata hofu nzito.

Akiwa ameminywa hivyo na mikono ya kiume, sauti ikamuuliza yeye ni nani, ametoka wapi na pale anafanya nini?

ENDELEA

Kwakweli Malkia alibanwa na hofu. Alijua sasa mwisho wake umefika. Aliwaza mengi kichwani kwa wakati mmoja. Alifikiria namna ya kujichoropoa lakini hakuwa na mabavu ya kujichoropoa dhidi ya nguvu zilizomshikilia.

Mwanaume yule aliyemkaba akamvutia ndani ya chumba cha mfalme kisha akafunga mlango. Malkia akamtazama usoni na kugundua kumbe alikuwa ni Phares!

"Nimekuwa nikitegemea ujio wako hapa hivi karibuni!" Akasema mfalme akitabasamu, kisha akaketi na kumtazama Malkia kwa macho ya maulizo.

Akamwambia bila shaka yeye ni Sandarus, Malkia akastaajabu amejulikanaje? Lakini Mfalme akamwambia yote ni kwakuwa amekuwa akisikia habari zake kila uchwao. Hakuna mtu atakayekuja Goshen asimtambue.

"Lakini niliambiwa umekufa ... niliambiwa haupo himayani hapa ... na wengine wakanambia upo mbali huko kusikojulikana. Yote haya yanawezekanaje kwa wakati mmoja na wewe kuwa hapa?"

Malkia akamwambia Phares hataweza kuelewa kwani ni kisa kirefu mno. Kwa sasa amekuwa akiitazama na kuilinda Goshen kwani ndipo nyumbani kwake hata akienda pande ipi ya dunia.

Phares akataka kufahamu ni wapi alipo na anawezaje kufika ndani ya kasri ingali kuna walinzi kedekede huku na huko. Anawezaje kuingia ndani ilhali malango yamefungwa?

"Mfalme, siwezi kuzuiwa na kuta wala kufuli yoyote kutembelea sehemu yoyote ya Goshen," Malkia akajibu kwa kujiamini. Phares akashusha pumzi ndefu na kumtazama mwanamke huyo vema. Kichwani alikuwa na maswali mengi lakini alianza kufadhaika kwa kukosa majibu mujarabu toka kwa Malkia.

Akachakata na kuchuja maswali yake, akaamua kuuliza swali kuu lililobeba dhamira.

"Nini kimekuleta hapa kwangu?"

"Kukutahadharisha!"

"Juu ya nini?"

Kabla Malkia hajasema kitu, maginga ya moto yakaanza kufinyafinya kana kwamba yamepitia shurba ya pepo kali. Wakatahamaki!

Wakasikia ardhi ikitetemeka na vitu vikianguka. Wakajiuliza ni nini hiko, mara ghafla maginga ya moto yakazima kukawa kiza totoro!

Mfalme akapapasa papasa, akamuita Sandarus lakini hakupata majibu yoyote. Muda si mrefu akasikia mlango wake ukigongwa kwanguvu!

Mara mlango ukavunjwa wakaingia wanaume wawili wakiwa wamebebelea maginga ya moto. Wakapaza sauti kumuita mfalme. Walikuwa ni wanajeshi.

"Nipo hapa!" Phares akajitokeza. Lakini akaangaza huku na huko kumtafuta Malkia, hakumwona. Alitwaa ginga moja la moto na kuangaza kila mahali ndani ya chumba, hakumwona Malkia!

Akabakiwa na maswali kedekede kichwani.

Wakati huo upande wa pili wa shilingi!...

"Amepotea!" Akafoka bibi mlozi akipiga kofi la lawama. Alikuwa na mwenzake wakiwa wanatazama chupa mithili ya chemli mezani.

Ndani ya chupa hiyo kulikuwa kuna mwanga na taswira ya kile kilichokuwa kinaendelea ndani ya ngome ya mfalme! Walikuwa wanamwona mfalme akiwa na walinzi wake wakiangaza na kuangaza huku na kule.

Chumba kilikuwa kimejawa na giza. Na ni chupa ile ya chemli peke yake na macho ya walozi hawa ndiyo yalikuwa yaking'aza.

"Tulikuwa tumeshampata! Hii ilikuwa ni tende jangwani!" Akalalama mmoja wao akitikisa kichwa. Mwenzake akamshtumu:

"Ni wewe ndiye ulipuliza kwanguvu!"

Naye akamrudishia kwa kumuuliza:

"Na wewe ulivyotikisa kama kibuyu?"

Wakarushiana lawama kama watoto kila mmoja akimlaumu mwenzake kwa kupoteza nafasi ile adhimu ya kumtia mikononi Malkia. Sasa amekwishapotea na hata hawajui wapi alipoenda, wala alipotokea.

Walipotuliza shurba zao, wakaulizana juu ya nini cha kufanya. Kwa muda wakafikiria na kupendekeza kumalizana na mfalme kwa usiku huo. Yaani wahakikishe kila jambo wanamaliza.

"Huwezi jua Sandarus alikuwa amekuja kufanya nini? Anaweza kumuepusha kwa kumtahadharisha, kitumbua kikaingia mchanga!" Akasisitizia mmoja.

Kwa pamoja wakakubaliana kuwa usiku huo ulikuwa wa dhahabu kwao hivyo basi waufanye uwe kheri. Wakaandaa kila wanachotakiwa kuwa nacho. Wakaketi sasa kungojea tu muda muafaka uwasili wakati huo Wakitazama chupa yao.

Mfalme akalala. Wakamhesabia muda. Waliporidhika sasa atakuwa amelowea usingizini, wakajivika majoho mekundu yenye kofia za kujishkiza, alafu wakashikana mikono na kuteta maneno ya kigeni, mara wakapotea!

---

Ndani ya chumba kulikuwa ni kiza. Mfalme alikuwa mwenyewe juu ya kitanda kikubwa akiwa amejichanua kama ua bustanini.

Juu ya mwili wake alikuwa amejifunika shuka kubwa zito la manyoya manyoya. Si kwamba kulikuwa kuna baridi kali, la hasha! Hali ya hewa ilikuwa ya kawaida, na kwa watu wengine ambao wamezoea baridi, huu ulikuwa wasaa wao wa kuyasahau mashuka na kujitutumua ndani ya nguo nyepesi nyepesi.

Kulikuwa kuna ukimya wa kutosha kwa mtu kulala na kunogewa usingizini. Kwa mbali kama ungelisikiliza kwa umakini basi ungegundua mfalme alikuwa anakoroma.

Punde! Bibi walozi wanatokea konani. Wameifungua mikono yao wakiiangaza huku na kule kana kwamba wanapungia umati mikono. Walipoona shwari, wakatoa kitabu chao ndani ya joho alafu wakakiweka mezani na meza wakaisogezea karibu na kitanda alipokuwa amelala mfalme.

Upesi, mmoja akafungua ukurasa nambari mia tatu ishirina na nane, wakavuta pumzi na kuanza kusoma wote kwa pamoja, wakienda sawa kituo kwa kituo!

Wakamaliza ukurasa wa kwanza, wakahamia wa pili na kisha wa tatu mpaka wakamaliza hiyo sura! Ajabu hakukuwa na mabadiliko yoyote. Mwili wa mfalme ulikuwa umelala kama hapo awali!

Wakatazamana na kuulizana kama kuna kitu hakijaenda sawa. Kuhakikisha, wakarudia tena zoezi lao! Sasa wakilifanya kwa utaratibu na umakini mkubwa.

Lakini bado matokeo yakawa yaleyale! - hakuna kilichobadilika. Hapa sasa wakakubaliana kuna jambo halipo sawa!

"Tunafanyaje?" Mmoja akauliza.

"Turudie tena! Mara hii utaweka kiganja chako kwenye paji lake la uso."

Wakakubaliana. Wakarudia tena zoezi lao ambalo bado halikuleta matunda yoyote yale zaidi ya fadhaiko. Wakakata tamaa na kuondoka zao wakiwa wamejawa na maswali chungu nzima!

Imewezekanaje?

Mahali pekee ambapo zoezi hilo haliwezi kufanya kazi ni endapo tu mhanga anayefanyiwa akiwa mlozi ama si binadamu. Ina maana mfalme ni mlozi? Ina maana mfalme si binadamu?

Wakabaki kama mbweha aliyepokwa mnofu na mwewe!
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 23*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lakini bado matokeo yakawa yaleyale! - hakuna kilichobadilika. Hapa sasa wakakubaliana kuna jambo halipo sawa!

"Tunafanyaje?" Mmoja akauliza.

"Turudie tena! Mara hii utaweka kiganja chako kwenye paji lake la uso."

Wakakubaliana. Wakarudia tena zoezi lao ambalo bado halikuleta matunda yoyote yale zaidi ya fadhaiko. Wakakata tamaa na kuondoka zao wakiwa wamejawa na maswali chungu nzima!

Imewezekanaje?

Mahali pekee ambapo zoezi hilo haliwezi kufanya kazi ni endapo tu mhanga anayefanyiwa akiwa mlozi ama si binadamu. Ina maana mfalme ni mlozi? Ina maana mfalme si binadamu?

Wakabaki kama mbweha aliyepokwa mnofu na mwewe!

ENDELEA

Hawakujua cha kufanya. Walikuwa wameganda kwa mawazo kwa muda usiojulikana. Mambo yalikuwa mazito wasijue namna ya kuyamaliza. Wakajadili na kuamua kufanya utafiti kumhusu mfalme.

Inabidi wajue ametokea wapi, familia yake, na yeye ni nani haswa? Njia pekee ya kuyafahamu hayo yote ilikuwa kumtumia Rhoda kwa macho ya mapenzi.

Atamlainisha mfalme na mwisho wa siku wakapata wanachokitaka.

"Tutafanyaje sasa tukigundua naye ni mlozi?" Akauliza kikongwe mmoja. Mwenzake akamung'unya kwanza lips zake akifikiria. Akajibu:
"Hakutakuwa na namna, itabidi tuenende katika hiyo njia!"

"Unasema?!" Mwenzake akatahamaki. "Kwahiyo tutarudi tena Tanashe?"

"Ndio! Unajua fika dawa ipo kule. Ni lazima turudi kule kama kweli tukigundua mfalme ni mlozi kama sisi!"

Hapana, roho ya huyu mmoja ikasita kabisa. Alihofia mno kurudi Tanashe. Alijiona ni kama wanarejea kwenye mdomo wa simba waliyemkwepa. Lakini mwenziwe akamtoa hofu:
"Tuna mwili wa binadamu, nini kitashindikana? Tutatoka na kuingia kama tufanyavyo chumbani!"

Japo kishingo upande akaridhia. Pasipo kupoteza muda, wakaadhimia patakapokucha waende kuonana na mfalme wakiwa wamejivika mwili wa Rhoda, na wafanye kila walijualo kuupata ushindi!

***

Kama ulidhani usiku ulikuwa umekoma, basi umekosea. Bado kulikuwa na kiza kinene na kukiwa kimya. Kwa majira ya sasa, tungesema ni mishale ya saa tisa kasoro ya usiku.

Wote walikuwa wamejilaza wakiuzingira moto ambao umefifia ukilinganisha na hapo awali, lakini Zura alikuwa bado yu macho. Aligeuzia mwili wake juu akitazama anga na huku mawazo yake yakiwa yanamsumbukia Malkia.

Muda unazidi kwenda sasa, wala harudi. Nini kimemkumba huko aliko? Japo hakuwa anajua, alihisi kuna kitu hakipo sawa na nafsi yake. Alihisi Malkia si mzima.

Ni kheri akiwa fikirani, akahisi kitu kizito kimedondoka kando yake. Na mara sauti ya mtu akikohoa kwa pupa!

Basi haraka akageuka na kutazama, kifuani akijazwa na hofu. La haula! Akamwona Malkia akiwa amejilaza, amechoka! Anakohoa pasipo kupumzika.

Akamfuata upesi na kuuliza nini kimetokea. Lakini Malkia hakuweza kumjibu mpaka pale alipokoma kukohoa na kisha akavuta pumzi ya kutosha.

Akamweleza Zura namna gani mambo yalivyotokea kule Goshen alipotaka kumhabarisha Mfalme juu ya walozi. Punde akajikuta yupo kizani, pumzi imekuwa nzito, anaishiwa na nguvu!

Wazi akatambua lilikuwa shambulizi toka kwa wale vikongwe kwani hawakutaka amhabarishe mfalme juu ya njama zao. Kwa haraka, kwakuwa alipoteza dhana yake ya kujichanja, akajing'ata apate damu kumruhusu arudi pale.

Zura akashangazwa sana na hiyo habari. Akamwonea huruma Malkia lakini pia akajawa na hofu kuhusu Goshen.

"Ina maana walikuwa wanatarajia ujio wako?" Akauliza Zura.

"Pasi shaka, hata na mfalme pia alikuwa akinitarajia!" Malkia akajibu.

"Kwahiyo wote wanajua sasa kama upo hai! Na kama upo hapa!"

"Hapana! Hawafahamu nilipo, ila wamefahamu kuwa nipo."

Zura akatulia kwa sekunde kadhaa akimtazama Malkia. Akautazama mkono wake aliojing'ata, akakabwa na donge la huruma. Akatikisa kichwa chake na kumwambia Malkia.

"Inabidi uache sasa. Kwa hakika!"

Malkia akamtazama asiseme kitu. Zura akaendelea kumhasa kuwa yu hatarini kwa sasa. Adui zake wameshajua kuhusu uwepo wake na hivyo basi watajipanga kumdhibiti, ama kummaliza kabisa!

"Maadui? - maadui wangapi?" Malkia akauliza. Alikuwa akiamini maadui zake ni walozi tu. Ila Zura akamfungua macho kwa kumweleza hata mfalme ni adui yake.

"Uongozi ni mtamu. Uongozi hulevya. Kiti cha mfalme hupambwa na nadiri za dhahabu. Ni kiti aghali na chenye mamlaka. Ni kiti juu ya viti na nyumba zote. Sasa nani atataka kukiacha kwa wepesi?"

Zura akamshika mkono Malkia.

"Hata mfalme anahofia kiti chake. Wewe ni tishio kwake, tambua hilo. Habari zako anazo. Hafurahishwi na ushawishi wako ndani ya himaya ... atakumaliza hata kama aonyesha tabasamu kwa sasa. Mkono unaobebelea kisu waweza kufichwa nyuma ya mgongo!"

Baada ya Zura kusema hivyo, akamwacha Malkia ayameze maneno yake. Yeye akageukia upande wa kushoto apate kulala, lakini Malkia akamuuliza:

"Huyo ameenda wapi?"

Zura kutazama akagundua jitu moja halikuwapo. Akastaajabu kwani hakukumbuka ni muda gani mtu alitoka hapo ingali alikuwa macho! Akanyanyuka na kuketi kitako, akaangaza.

Hapa akawaza pengine mawazo aliyokuwa nayo yalimfanya asisikie kitu. Akamtazama Malkia na kumwambia hajui jitu hilo limeenda wapi!

Basi haraka wakamwamsha Seth na Fluffy, wakawaambia habari hizo. Wakaulizana na kuona kuna haja ya kufanya msako kumtafuta. Wakawasha maginga ya moto na kuanza msako!

Jitu lile lingine lililokuwa lipo usingizini, hakuwa anajua hata kinachoendelea. Alikuwa usingizini akikoroma kama mlevi.

Wakina Malkia wakatazama huku na huko, wakatembea kule na kule, hawakumwona mwenzao! Wakatembea kwa muda wa kama dakika ishirini, hawakufanikiwa!

Seth akatoa angalizo huenda wakapotelea huko kadiri wanavyozidi kwenda, hivyo warudi na wataendelea kesho jua likichomoza.

"Hapana!" Malkia akakataa. "Kama yupo matatizoni huoni kesho tutakuwa tumeshachelewa? Tumtafute hivi sasa. Sitaweza nikapata usingizi nikalala."

Basi wakaendelea na kutafuta. Baadae kidogo, wakasikia kishindo! Wakaangaza, hawakuona mtu. Lakini kabla hajawapiga hatua zozote kusonga mbele, wakasikia sauti ya mtu akitafuna.

Kwa ujasiri wakasonga kufuata sauti hiyo, njiani wakaona vipande vipande vya mwili wa mnyama, kama vile miguu na kichwa. Kusonga mbele, wakamkuta mtu wanayemtafuta.

Alikuwa ameketi akiwa anamla mnyama, mithili ya swala, akiwa mbichi atiririkaye damu!

Wakamwambia wamekuwa wakimtafuta, kwanini aliondoka pasipo kuaga. Akajitetea kuwa alienda kutafuta chakula kwani hakuridhika na tumbo lilikuwa linalalama njaa!

Basi wasipoteze muda wakamtaka afungashe warejee. Jitu lile likasomba nyama zake na wakafunga safari wakitembea upesi. Kufika mahali walipokuwapo, wakastaajabu kutomkuta yule waliyemuacha amelala!

"Mungu wangu!" Malkia akashika kichwa.


***
 
*MKUFU WA MALKIA II -- 24*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Basi wakaendelea na kutafuta. Baadae kidogo, wakasikia kishindo! Wakaangaza, hawakuona mtu. Lakini kabla hajawapiga hatua zozote kusonga mbele, wakasikia sauti ya mtu akitafuna.

Kwa ujasiri wakasonga kufuata sauti hiyo, njiani wakaona vipande vipande vya mwili wa mnyama, kama vile miguu na kichwa. Kusonga mbele, wakamkuta mtu wanayemtafuta.

Alikuwa ameketi akiwa anamla mnyama, mithili ya swala, akiwa mbichi atiririkaye damu!

Wakamwambia wamekuwa wakimtafuta, kwanini aliondoka pasipo kuaga. Akajitetea kuwa alienda kutafuta chakula kwani hakuridhika na tumbo lilikuwa linalalama njaa!

Basi wasipoteze muda wakamtaka afungashe warejee. Jitu lile likasomba nyama zake na wakafunga safari wakitembea upesi. Kufika mahali walipokuwapo, wakastaajabu kutomkuta yule waliyemuacha amelala!

"Mungu wangu!" Malkia akashika kichwa.

ENDELEA

Walichoka lakini wasingeweza kulala. Ilibidi naye huyo wamtafute wapi alipoelekea. Walihofia usalama wake, wapi alipo na nini atakuwa anafanya.

Je naye atakuwa ameenda kutafuta chakula kama mwenzake, yaani hakushiba? Seth akakataa.

"Alikuwa ameshiba. Nilimpatia kipande cha nyama akasema hataweza hata kutafuna!"

Sasa basi kaenda wapi usiku wote huo? Wakaanza kusaka huku na kule. Wakiangaza chini alama za miguu. Wakaenda mbali sana. Hata wakaanza kutumia jina la jitu huyo kumsakia, wakimuita huku na kule. Wakisahau ya kwamba walikatazwa kuitana majina wakiwa safarini!

Na basi, punde kifupi wakaanza kusikia sauti za watu kwa mbali masikioni mwao. Sauti hizo zilikuwa ni mwangwi wa zile sauti walizokuwa wanaita.

Wakatazama huku na huko kutazama sauti hizo zinatoka wapi, hawakuona mtu yeyote. Hapo Malkia akakumbuka onyo lile walilopewa na mama yake Fluffy, upesi akawakataza wenziwe kuita majina. Lakini tayari alishachelewa!

Bado sauti zile zilizokuwa zinahakisi za kwao, zikaendelea kururuma na kuwaogopesha. Lakini zaidi ya hapo, ilikuwa kheri kwani hawakudhurika na lolote lile.

Shida ikawa kwa yule aliyekuwa anaitwa. Akiwa yupo mbali kabisa na ulimwengu wa wenzake, na pengine akiwa hajui kwanini na kivipi yupo huko, akawa anaendeshwa kama toroli bovu!

Macho yake yalikuwa yamepanda juu mithili ya mtu aliyelewa madawa. Miguu yake ilikuwa inatembea kwa kuburuza. Mdomo wake ulikuwa wazi, mikono yake ikiwa imelegea kana kwamba amepooza.

Masikioni mwake alikuwa anasikia sauti ya kike ikimwita jina. Na hakuwa na nafasi ya kukataa sauti hiyo. Mwili ulikuwa umekubali, akili haikuwapo!

Kwa takribani dakika kumi na, akawa anatembea na mwishowe akakaribia shimo la tewa! Shimo lenye mdomo mkubwa kama kinywa cha mamba. Shimo jeusi linalomeza watu. Shimo lisilo na kikomo!

Na kadiri alivyokuwa akisogelea shimo hilo, basi na ile sauti inayomuita ikazidi kulowana utamu. Kwa sauti ya kinubi ikawa inaita.

Jitu hili, ambalo lilifanywa kama mtoto sasa, likawa limebakiza hatua nne tu kudumbukia shimoni. Halikusikia chochote na masikio yake, bali sauti ya kumwita ... sauti ya kumvutia shimoni..

Lakini ghafla,

"Heeey!" Sauti ya kiume ikaita nyuma yake ".. heeey! ... simama! Simamaa!"

Wala hakusikia. Sasa akawa amebakiza hatua moja tu azame shimoni! Huku nyuma yake kukavuma vishindo vya miguu vikija upesi, na mara mtu akamrukia na kummwagia pembeni.

Alikuwa ni Seth! Lakini kumwokoa jitu hilo kukamtia yeye hatiani. Akaserereka na kuzamisha mwili wake ndani ya shimo, akibakiza mikono tu iking'ang'ania kingo ya shimo!

Kama si haraka wenzake kumuwahi, basi alikuwa anazama. Walifanikiwa kumdaka mikono na kumvuta kwanguvu. Lakini hawakufua dafu! Seth alikuwa anavutwa shimoni pia!

Mikono meupe iliyotokea kwenye kuta za shimo, ilikamata miguu yake na kumvutia ndani kwanguvu. Seth akajitahidi kuchoropoa miguu yake kwa nguvu lakini kazi ikawa kinyume na alivyofikiria. Hakuweza kuishinda nguvu mikono ile!

Basi ikawa vuta n'kuvute! Kila pande iking'ang'ania mwili wa Seth.

Ni bahati wakati zoezi hilo likiendelea, lile jitu lililookolewa na Seth likarejea fahamuni! Lilkahema mafundo makubwa makubwa kana kwamba limetoka kunusurika kuzama na maji.

Lilipotazama kando ndipo likawaona wenziwe waking'ang'ana, basi upesi likawaongezea nguvu kumvuta Seth, wakafanikiwa!.

Wote wakajilaza pembeni wakihema kwa shughuli pevu! Walifanikiwa kumkomboa Seth lakini alikuwa amejeruhiwa miguuni kwa kucha za mikono ya shimoni, hivyo hakuweza kusimama wala kutembea.

Wenziwe wakambeba na kurejea kule walipokuwapo mwanzoni. Wakakuta moto ushazima, wakauwasha na kuketi kumganga Seth. Yale majitu mawili yakitafuna majani waliyochuma kwenye miti kadhaa na kisha kumuwekea kwenye majeraha.

"Ulifikaje kule?" Malkia akamuuliza yule jitu waliyemkomboa. Jinale aliitwa Ghaut. Kwa msaada wa ukalimani toka kwa Seth, wakawa wanawasiliana.

"Anasema wakati amelala alisikia kishindo cha mtu akiwa anakimbia kumzunguka. Akakurupuka na kutazama, akajikuta yu mwenyewe! Na kwa mbali alipoangaza, akamwona mtu akiishia akikimbia," Seth alikalimani maneno ya jitu.

"Ulifanikiwa kumtambua mtu huyo na alipoelekea?" Malkia akauliza.

Jitu likatikisa kichwa, likajibu huku Seth akikalimani.

"Japo nilimkimbiza nikidhani anaweza kuwa ni wa miongoni mwetu, sikufanikiwa kumwona. Kila nilipokimbia, akafichwa na miti. Akamezwa na miti. Zaidi nikajikuta nikipotelea ndani ya msitu nisijue wapi nilitokea!"

Simulizi hiyo ikatetemesha mioyo yao. Mule msituni hawakuwa wenyewe. Na sasa kwa matendo walikuwa wamejifunza kuwa hawatakiwi kuachana hata mara moja!

"Kesho tutaumaliza msitu huu endapo tutatembea kwa zaidi ya masaa nane pasipo kupumzika. Na baada ya hapo, tutaingia kwenye jangwa la Medek-taum kabla ya kwenda kukutana na bahari," alisema Seth akitoa ramani ya mwenendo wao.

"Na je kuna cha kukitarajia huko?" Zura akauliza upesi. Wote wakamtazama Seth kwa jicho la shauku.

Seth akapandisha mabega na kusema:
"Pengine yapo ya kuyatarajia. Kwakuwa jina la jangwa hilo humaanisha kifo-mezani. Sidhani kama jina hili liliwekwa kwa bahati mbaya."

Moto ukaendelea kuwaka na kuwaka. Hakukuwa na mtu mwenye dalili ya kulala tena.

***


"Kila kitu kipo sawa?" Akauliza kikongwe. Mwenzake akatikisa kichwa pasipo kutia neno, lakini uso wake haukuwa wenye furaha.

Juu ya kitanda kulikuwa kuna furushi kubwa jeusi. Wao wenyewe walikuwa wamevalia mashela meusi mikononi wakifunikwa na glovu za nyavu.

"Hatuna namna. Lazima tufanye hivi," akaendeleea kusema kikongwe wa kwanza kufungua mdomo.

"Lazima turudi Tanashe. Twende kule tukachote dawa za kuja kumaliza kazi. Umeona mwenyewe mambo yalivyogoma.

Mwenzake akamtazama akiwa kimya kwa muda kidogo, alafu akamwambia:
"Hili si chaguo jema."

Baada ya hapo hakusema tena kitu. Wakazama ndani ya mwili wa Rhoda na safari ya kwenda Tanashe ikaanza.

Yalikuwa ni majira ya saa kumi ya usiku! Huko nje hakukuonekana na mtu yeyote akirandaranda bali hali ya ukimya mkubwa. Kwa mtu wa kawaida, angeliogopa. Angelitembea kwa kutazama nyuma kila saa.

Walozi hawa, pasipo tembe ya hofu, wakakata safari wakijongea kwenda mpakani mwa Goshen na Tanashe. Japo miili yao bado ilikuwa ndani ya Goshen, akili zao zilishafika Tanashe wakiwaza yatakayojiri huko.

Lakini wakiwa wamekaribia mpakani, wakagundua hawakuwa wenyewe safarini! Kuna watu walikuwa wanawasindikiza. Na watu hawa si wengine bali wanajeshi waliowekwa na yule Afisaa usalama, bwana Alphan baada ya shuku za hapa na pale!

Wanajeshi hawa walikuwa kazini wakitimiza maagizo ya kufuatilia kila jambo alifanyalo Rhoda.


NINI WALOZI HAWA WATAFANYA WAKIWA NDANI YA RHODA?
 
*MKUFU WA MALKIA II -- 25*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Yalikuwa ni majira ya saa kumi ya usiku! Huko nje hakukuonekana na mtu yeyote akirandaranda bali hali ya ukimya mkubwa. Kwa mtu wa kawaida, angeliogopa. Angelitembea kwa kutazama nyuma kila saa.

Walozi hawa, pasipo tembe ya hofu, wakakata safari wakijongea kwenda mpakani mwa Goshen na Tanashe. Japo miili yao bado ilikuwa ndani ya Goshen, akili zao zilishafika Tanashe wakiwaza yatakayojiri huko.

Lakini wakiwa wamekaribia mpakani, wakagundua hawakuwa wenyewe safarini! Kuna watu walikuwa wanawasindikiza. Na watu hawa si wengine bali wanajeshi waliowekwa na yule Afisaa usalama, bwana Alphan baada ya shuku za hapa na pale!

Wanajeshi hawa walikuwa kazini wakitimiza maagizo ya kufuatilia kila jambo alifanyalo Rhoda.

ENDELEA

"Tukimbilie Tanashe!" Kikongwe mmoja akasema ndani ya Rhoda. Lakini mwenzake akapinga hiyo hoja. Endapo wakiwaacha wanajeshi hawa hai, basi habari zao zitasambaa na hata watakaporudi Goshen mbivu na mbichi zitakuwa bayana.

"Kwahiyo inabidi tuwaue. Hatakiwi kubaki hai hata mmoja wao!"

Basi kufumba na kufumbua, vikongwe wakatoka ndani ya mwili wa Rhoda kimiujiza! Haraka wakatapakaa na kuwakamata wanaume watano waliokuwa wamebebelea silaha. Wakawaviringita na kuwanyofoa uhai mara moja, kisha wakaendelea na safari yao kuzama Tanashe.

Baadae jua lilipochomoza, watu wakazingira miili ile ya wanajeshi wakiwa wamestaajabu. Habari zikasambaa ndani ya himaya nzima, muda si mrefu wakafika wanajeshi wengine kuja kuchukua miili ya wenzao.

Kitendawili kikawa ni nani aliyewaua wanajeshi hao? Na kafanya hivyo kwa dhamira gani? Wakapembua mazingira ya tukio, wakagundua hakukuwa na mabaki yoyote kumwonyesha muuaji - si alama za miguu, wala chochote alichoacha.

Muda kidogo, Alphan, mkuu wa jeshi, akawasili eneoni kuja kuhakiki taarifa alizopata.

Alikuwa mchovu na uso wake ukiwa mweusi kwa mbali. Kiafya hakuwa sawa. Alikuwa anakohoa mara kwa mara. Macho yake yalijifinya na shingo yake ilikuwa na alama za mikwaruzo na mgandamizo.

Akatazama miili ya wanajeshi wake kisha akasonya na kutikisa kichwa. Akaamuru itolewe pale ikahifadhiwe kisha, akiwa ameongozana na wanajeshi wanne, akaelekea mpaka nyumbani kwa Rhoda.

Baada ya kugonga kwa muda pasipo majibu, wakachukua hatua ya kuvunja mlango. Wakasaka nyumba nzima, wasifanikiwe kumwona Rhoda popote pale.

Hapo Alphan akatengeneza makisio kichwani. Moja kwa moja akaenda kuonana na mfalme, wakapata chai pamoja mezani.

Akamweleza mfalme juu ya makisio yake.

"Rhoda ameenda Tanashe," akafungua mjadala kwa kauli hiyo. Mfalme akamkabidhi macho na masikio yake apate kusikia.

"Tanashe?"

"Ndio. Ameenda huko ... inaweza kua ajabu lakini ndio ukweli. Askari wangu niliowaweka kumtazama kila nyendo zake, wamekutwa mpakani mwa Tanashe wakiwa wamekufa. Wamefikaje huko? Wakiwa wanamfuatilia Rhoda, pasi na shaka. Na hivi tunavyoongea, Rhoda nyumbani kwake hayupo!"

Maneno hayo yakajenga jumba la ukweli ndani ya kichwa cha mfalme. Aliacha hata kunywa chai akawa anaskiza na kutafakari.

"Unadhani atakuwa ameenda kufanya nini huko?" Mfalme akauliza.

"Sijajua," Alphan akabinua mdomo. "Ila chochote atakachokuwa ameenda kukifanya huko, hakitakuwa na nia njema kwetu."

Basi mfalme akaagiza punde tu Rhoda atakapoonekana, atiwe nguvuni na aletwe kwake haraka iwezekanavyo. Alphan akapokea maagizo hayo kwa heshima zote.

"Mbali na hayo, nini shida Alphan? Haupo sawa, kuna jambo lolote?" Mfalme akauliza baada ya kumtazama na kumkagua Alphan vema. Sasa alianza kula na kunywa.

"Hamna shida, mkuu," Alphan akaficha. Macho yake yalikwepa kumtazama mfalme.

"Hapana, kuna shida," mfalme akasisitiza. "Unaonekana dhaifu. Kipi kinakutatiza?"

Alphan akalazimika kueleza kuwa alikabwa usiku wa kuamkia jana yake. Hakumwona mtu aliyefanyia hivyo na kama isingelikuwa askari wake kuwahi kuingia ndani basi angelikufa!

"Mikono yake ilikuwa migumu na mizito kama chuma. Haikujalisha ni kwa namna gani nilipambana, nilikuwa mdhaifu mno niliyeelemewa hata na mikono na miguu yangu!" Akaeleza Alphan.

"Na tangu hapo, sijapata kurejea kwenye hali yangu. Napata shida kuongea, kumeza na hata kugeuza shingo. Najihisi mchovu, na usiku kwangu umekuwa wa kipekee!"

Mfalme akamuuliza kama aliacha mlango wazi na pengine mtu aliyefanya tukio hilo aliacha alama yoyote. Alphan akakanusha yote hayo. Kitu ambacho kilitengeneza kitendawili miongoni.

"Lakini nina mashaka ya dhati na Rhoda," akamalizia Alphan. Mfalme akapaliwa.

***

Jua lilikuwa linaelekea kufutika kwenye uso wa dunia, lilikuwa jekundu zaidi na dhaifu. Njia za kila pande zilikuwa zimetawaliwa na wakulima na wafugaji wakirejea kwenye makazi yao.

Lakini miongoni mwa watu hao, alikuwapo Fanty. Alikuwa anakazana kutembea akihema kama mbwa. Alionekana ametembea kwa muda mrefu na hata anapoenda bado ni parefu. Alirusha mikono na miguu yake kana kwamba yupo kwenye gwaride.

Baada ya kitambo kidogo, alikuwa amewasili mbele ya nyumba ya wakina Roboth. Akapaza sauti kubisha hodi. Punde akatoka mama na kumjulia hali.

"Samahani, naweza nikaonana na dada yangu?" Fanty akaomba. Mama akamwambia Tattiana ametoka kwenda kuteka maji, hivyo amngojee kwa muda kidogo.

Bahati kabla hawajakatisha maongezi hayo, Tattiana akaonekana akiwa anakuja, ndoo ya maji aliiweka kichwani. Basi haraka, Fanty akamuwahi dada yake na kumtua ndoo, kisha wakapata muda wa kuteta wakiwa wenyewe.

"Maisha gani haya umechagua, Tatty? Ona ulivyovaa? Unafanya kazi kama punda?"

Tattiana akaghafirika. Akamtaka kaka yake aondoke kama hicho ndicho kimemleta. Fanty akaomba msamaha na kumweleza dhamira ya ujio wake pale.

"Nimekuja kukuomba urudi nyumbani. Tunakukumbuka sana."

Tattiana akatikisa kichwa akimtazama Fanty ndani ya macho.

"Siwezi, Fanty! Siwezi kwenda kukaa chini ya paa moja na wauaji. Siwezi kabisa..."

"Hapana!" Fanty akamkatisha. "Waliomuua Roboth si baba wala mama. Hawahusiki!"

"Nini unaongea, Fanty?" Tattiana akamkaripia. "Ni wakina nani walikuwa wanamchukia Roboth mbali na mama na baba?"

"Siwezi jua. Ila nakuhakikishia kabisa, si wao waliohusika. Nami nilikuwa kama wewe, nikiamini kwa dhati mikono yao ndiyo imemmaliza Roboth mpaka usiku wa jana niliposikia wakigombana chumbani."

"Wakigombana?"

"Ndio. Jana kulikuwa kuna ugomvi mkubwa sana. Baba alikuwa anamshutumu mama kwamba ni yeye ndiye atakuwa anahusika na mauaji ya Roboth. Yeye alikuwa anataka wamalize haya mambo kidiplomasia kinyume na mama."

"Kwahiyo mama ndiyo kamuua Roboth?"

"Sidhani," Fanty akajibu. "Baba alipoondoka, mama alilia sana. Mpaka muda ninaokuja hapa, mama hajapata kula tangu jana. Amekuwa akilaani na akilaumu. Kama angelikuwa amelitenda hilo, asingelikuwa kwenye hiyo hali."

Kukawa kimya. Tattiana akazama kwa kina kwenye dimbwi la mafikirio.

***

Baadae kwenye majira ya usiku wa saa tatu, endapo tungetumia majira ya sasa, Tattiana akashuka mbele ya geti la hekalu ya mfalme.

Alikuwa amevalia gauni jeusi alilopewa na mama yake Roboth. Halikuwa limemkaa vema, ila angalau lilimsitiri na kupunguza maswali toka kwa walinzi.

"Mwambie mfalme, Tattiana amekuja kumwona," akasema kwa kujiamini kisha akasimama kungoja. Baada ya muda mfupi, akaruhusiwa kuingia ndani akisindikizwa na mwanajeshi mmoja.

Akaelekezwa pa kukaa.

Akiwa amekaa hapo, akatoa kisu nyuma ya mgongo wake. Akakiweka kwenye mkono wake wa kuume na kisha akaufichama chini ya meza.


.
.
.
****


NINI TATTIANA ANATAKA KUFANYA?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom