*MKUFU WA MALKIA II -- 25*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Yalikuwa ni majira ya saa kumi ya usiku! Huko nje hakukuonekana na mtu yeyote akirandaranda bali hali ya ukimya mkubwa. Kwa mtu wa kawaida, angeliogopa. Angelitembea kwa kutazama nyuma kila saa.
Walozi hawa, pasipo tembe ya hofu, wakakata safari wakijongea kwenda mpakani mwa Goshen na Tanashe. Japo miili yao bado ilikuwa ndani ya Goshen, akili zao zilishafika Tanashe wakiwaza yatakayojiri huko.
Lakini wakiwa wamekaribia mpakani, wakagundua hawakuwa wenyewe safarini! Kuna watu walikuwa wanawasindikiza. Na watu hawa si wengine bali wanajeshi waliowekwa na yule Afisaa usalama, bwana Alphan baada ya shuku za hapa na pale!
Wanajeshi hawa walikuwa kazini wakitimiza maagizo ya kufuatilia kila jambo alifanyalo Rhoda.
ENDELEA
"Tukimbilie Tanashe!" Kikongwe mmoja akasema ndani ya Rhoda. Lakini mwenzake akapinga hiyo hoja. Endapo wakiwaacha wanajeshi hawa hai, basi habari zao zitasambaa na hata watakaporudi Goshen mbivu na mbichi zitakuwa bayana.
"Kwahiyo inabidi tuwaue. Hatakiwi kubaki hai hata mmoja wao!"
Basi kufumba na kufumbua, vikongwe wakatoka ndani ya mwili wa Rhoda kimiujiza! Haraka wakatapakaa na kuwakamata wanaume watano waliokuwa wamebebelea silaha. Wakawaviringita na kuwanyofoa uhai mara moja, kisha wakaendelea na safari yao kuzama Tanashe.
Baadae jua lilipochomoza, watu wakazingira miili ile ya wanajeshi wakiwa wamestaajabu. Habari zikasambaa ndani ya himaya nzima, muda si mrefu wakafika wanajeshi wengine kuja kuchukua miili ya wenzao.
Kitendawili kikawa ni nani aliyewaua wanajeshi hao? Na kafanya hivyo kwa dhamira gani? Wakapembua mazingira ya tukio, wakagundua hakukuwa na mabaki yoyote kumwonyesha muuaji - si alama za miguu, wala chochote alichoacha.
Muda kidogo, Alphan, mkuu wa jeshi, akawasili eneoni kuja kuhakiki taarifa alizopata.
Alikuwa mchovu na uso wake ukiwa mweusi kwa mbali. Kiafya hakuwa sawa. Alikuwa anakohoa mara kwa mara. Macho yake yalijifinya na shingo yake ilikuwa na alama za mikwaruzo na mgandamizo.
Akatazama miili ya wanajeshi wake kisha akasonya na kutikisa kichwa. Akaamuru itolewe pale ikahifadhiwe kisha, akiwa ameongozana na wanajeshi wanne, akaelekea mpaka nyumbani kwa Rhoda.
Baada ya kugonga kwa muda pasipo majibu, wakachukua hatua ya kuvunja mlango. Wakasaka nyumba nzima, wasifanikiwe kumwona Rhoda popote pale.
Hapo Alphan akatengeneza makisio kichwani. Moja kwa moja akaenda kuonana na mfalme, wakapata chai pamoja mezani.
Akamweleza mfalme juu ya makisio yake.
"Rhoda ameenda Tanashe," akafungua mjadala kwa kauli hiyo. Mfalme akamkabidhi macho na masikio yake apate kusikia.
"Tanashe?"
"Ndio. Ameenda huko ... inaweza kua ajabu lakini ndio ukweli. Askari wangu niliowaweka kumtazama kila nyendo zake, wamekutwa mpakani mwa Tanashe wakiwa wamekufa. Wamefikaje huko? Wakiwa wanamfuatilia Rhoda, pasi na shaka. Na hivi tunavyoongea, Rhoda nyumbani kwake hayupo!"
Maneno hayo yakajenga jumba la ukweli ndani ya kichwa cha mfalme. Aliacha hata kunywa chai akawa anaskiza na kutafakari.
"Unadhani atakuwa ameenda kufanya nini huko?" Mfalme akauliza.
"Sijajua," Alphan akabinua mdomo. "Ila chochote atakachokuwa ameenda kukifanya huko, hakitakuwa na nia njema kwetu."
Basi mfalme akaagiza punde tu Rhoda atakapoonekana, atiwe nguvuni na aletwe kwake haraka iwezekanavyo. Alphan akapokea maagizo hayo kwa heshima zote.
"Mbali na hayo, nini shida Alphan? Haupo sawa, kuna jambo lolote?" Mfalme akauliza baada ya kumtazama na kumkagua Alphan vema. Sasa alianza kula na kunywa.
"Hamna shida, mkuu," Alphan akaficha. Macho yake yalikwepa kumtazama mfalme.
"Hapana, kuna shida," mfalme akasisitiza. "Unaonekana dhaifu. Kipi kinakutatiza?"
Alphan akalazimika kueleza kuwa alikabwa usiku wa kuamkia jana yake. Hakumwona mtu aliyefanyia hivyo na kama isingelikuwa askari wake kuwahi kuingia ndani basi angelikufa!
"Mikono yake ilikuwa migumu na mizito kama chuma. Haikujalisha ni kwa namna gani nilipambana, nilikuwa mdhaifu mno niliyeelemewa hata na mikono na miguu yangu!" Akaeleza Alphan.
"Na tangu hapo, sijapata kurejea kwenye hali yangu. Napata shida kuongea, kumeza na hata kugeuza shingo. Najihisi mchovu, na usiku kwangu umekuwa wa kipekee!"
Mfalme akamuuliza kama aliacha mlango wazi na pengine mtu aliyefanya tukio hilo aliacha alama yoyote. Alphan akakanusha yote hayo. Kitu ambacho kilitengeneza kitendawili miongoni.
"Lakini nina mashaka ya dhati na Rhoda," akamalizia Alphan. Mfalme akapaliwa.
***
Jua lilikuwa linaelekea kufutika kwenye uso wa dunia, lilikuwa jekundu zaidi na dhaifu. Njia za kila pande zilikuwa zimetawaliwa na wakulima na wafugaji wakirejea kwenye makazi yao.
Lakini miongoni mwa watu hao, alikuwapo Fanty. Alikuwa anakazana kutembea akihema kama mbwa. Alionekana ametembea kwa muda mrefu na hata anapoenda bado ni parefu. Alirusha mikono na miguu yake kana kwamba yupo kwenye gwaride.
Baada ya kitambo kidogo, alikuwa amewasili mbele ya nyumba ya wakina Roboth. Akapaza sauti kubisha hodi. Punde akatoka mama na kumjulia hali.
"Samahani, naweza nikaonana na dada yangu?" Fanty akaomba. Mama akamwambia Tattiana ametoka kwenda kuteka maji, hivyo amngojee kwa muda kidogo.
Bahati kabla hawajakatisha maongezi hayo, Tattiana akaonekana akiwa anakuja, ndoo ya maji aliiweka kichwani. Basi haraka, Fanty akamuwahi dada yake na kumtua ndoo, kisha wakapata muda wa kuteta wakiwa wenyewe.
"Maisha gani haya umechagua, Tatty? Ona ulivyovaa? Unafanya kazi kama punda?"
Tattiana akaghafirika. Akamtaka kaka yake aondoke kama hicho ndicho kimemleta. Fanty akaomba msamaha na kumweleza dhamira ya ujio wake pale.
"Nimekuja kukuomba urudi nyumbani. Tunakukumbuka sana."
Tattiana akatikisa kichwa akimtazama Fanty ndani ya macho.
"Siwezi, Fanty! Siwezi kwenda kukaa chini ya paa moja na wauaji. Siwezi kabisa..."
"Hapana!" Fanty akamkatisha. "Waliomuua Roboth si baba wala mama. Hawahusiki!"
"Nini unaongea, Fanty?" Tattiana akamkaripia. "Ni wakina nani walikuwa wanamchukia Roboth mbali na mama na baba?"
"Siwezi jua. Ila nakuhakikishia kabisa, si wao waliohusika. Nami nilikuwa kama wewe, nikiamini kwa dhati mikono yao ndiyo imemmaliza Roboth mpaka usiku wa jana niliposikia wakigombana chumbani."
"Wakigombana?"
"Ndio. Jana kulikuwa kuna ugomvi mkubwa sana. Baba alikuwa anamshutumu mama kwamba ni yeye ndiye atakuwa anahusika na mauaji ya Roboth. Yeye alikuwa anataka wamalize haya mambo kidiplomasia kinyume na mama."
"Kwahiyo mama ndiyo kamuua Roboth?"
"Sidhani," Fanty akajibu. "Baba alipoondoka, mama alilia sana. Mpaka muda ninaokuja hapa, mama hajapata kula tangu jana. Amekuwa akilaani na akilaumu. Kama angelikuwa amelitenda hilo, asingelikuwa kwenye hiyo hali."
Kukawa kimya. Tattiana akazama kwa kina kwenye dimbwi la mafikirio.
***
Baadae kwenye majira ya usiku wa saa tatu, endapo tungetumia majira ya sasa, Tattiana akashuka mbele ya geti la hekalu ya mfalme.
Alikuwa amevalia gauni jeusi alilopewa na mama yake Roboth. Halikuwa limemkaa vema, ila angalau lilimsitiri na kupunguza maswali toka kwa walinzi.
"Mwambie mfalme, Tattiana amekuja kumwona," akasema kwa kujiamini kisha akasimama kungoja. Baada ya muda mfupi, akaruhusiwa kuingia ndani akisindikizwa na mwanajeshi mmoja.
Akaelekezwa pa kukaa.
Akiwa amekaa hapo, akatoa kisu nyuma ya mgongo wake. Akakiweka kwenye mkono wake wa kuume na kisha akaufichama chini ya meza.
.
.
.
****
NINI TATTIANA ANATAKA KUFANYA?