*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 18*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
"Mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako ... mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako ... mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako."
Sauti hiyo ikakoma kama sekunde nne kisha ikasema tena:
"Wanakumywa damu na kuwaua watu ... wanakunywa damu na kuwaua watu ... wanakunywa damu na kuwaua watu."
Mfalme akasikia vema sana. Lakini sauti ile ikaacha kunong'oneza, ikafoka:
"Amka! Nenda Kawatafute!"
Mfalme akakurupuka toka usingizini. Akiwa ametoa macho akakodoa kutazama kushoto na kulia akihema. Kwa mbali akasikia vishindo vya miguu vikipotelea!
Basi akanyanyuka, akafungua mlango wake na kutupa macho. Hakuona kitu! Akatoka ndani ya chumba na kwenda kutazama. Huku na kule, hakubahatika kuona chochote alichoshuku. Akarudi chumbani na kuketi kitandani.
ENDELEA
Akafikiria sana ila mwishowe akaamua kuachana na mawazo hayo na kulala. Alipoamka akaonana na waziri wake wa ulinzi, bwana Alphan, akampasha habari juu ya ndoto yake.
"La haula!" Alphan akashangaa. Akamshauri mfalme wake kulifanyia kazi hilo jambo na atakuja kumpatia habari karibuni.
"Ulitilie maanani," mfalme akasisitizia. Alphan akanyanyuka aende zake, lakini kabla hajakwenda mfalme akakumbuka na kumuuliza jambo, ni kuhusu yule mwanajeshi wake aliyempatia kazi ya kumfuatilia Tattiana.
"Sijamwona!" Alphan akatahamaki. Hii haikuwa kawaida yake, mfalme akang'aka. Ni nini kimemkumba? Akataka kujua, basi akamuagiza Aplhan akafuatilie hilo jambo kwanza kabla ya mengine.
Alphan akaendaze na kumwacha mfalme. Baada ya muda mfupi akarejea akiwa haehae. Alimkuta mfalme akiwa anakunywa divai kwenye meza yake tukufu.
"Ewe mfalme, kijakazi wako ameishiwa na nguvu. Ametokwa na madonda mwilini na sidhani kama ataliona jua la kesho!"
Mfalme akatahamaki. Haraka akaelekea kumsabahi kijakaziwe. Akamkuta akiwa amejikunyata, dhoofu lihali hajiwezi.
"Ni nini kimekukumba?" Akauliza akijawa na shauku kubwa kujua lakini kijakazi wake hakuwa na hali kujibu. Alikuwa anatetemeka, akipambana na baridi kali alilolisikia peke yake.
Alipojitahidi kufungua kinywa, akashindwa. Mdomo wake ulikuwa umepasuka konani. Na ajabu hakudumu muda mrefu, akafariki!
Mfalme hakuamini macho wala masikio yake. Akachanganyikiwa kwa mawazo. Akauliza watu wa karibu ni nini kilimkumba mtumishi wake huyo, wakamwambia hawajui. Ni alikuja tu akiwa anakohoa damu!
Wakataka kumzika upesi, lakini mfalme akazuia zoezi hilo na kusihi mwili huo upelekwe hospitali na ukaguliwe.
"Nataka kujua nini kimemuua!" Mfalme akasema. Mwili ukapelekwa hospitali na daktari akaomba muda apate kuuchunguza mwili huo na kung'amua nini chanzo.
Mfalme akarejea himayani mwake, akiwa anawaza sana kuhusu lile jambo la mtumishi wake, majira ya jioni kuelekea usiku, akapokea mgeni - Rhoda. Akamkarimu mezani wapate tia chochote kinywani.
"Ni muda umepita sasa hujaja kuniona. Kuna shida yoyote?" Mfalme akauliza. Rhoda akatabasamu na kutikisa kichwa.
"Hapana, mfalme wangu. Ni kazi tu zimenibana."
Mfalme akaguna na kisha akauliza ni kazi gani hiyo kwani amesikia na kuhakikisha kwamba biashara yake imefungwa kwa muda sasa.
Rhoda akatabasamu.
"Ni kweli, mfalme. Tumeifunga ... yani, nimeifunga."
Mfalme akashikwa na butwaa kwani alitegemea Rhoda angeeleza pia na sababu za yeye kufanya hivyo, ila akawa kimya mpaka pale mfalme alipomuuliza nini kimemsibu.
Rhoda hakuwa na majibu ya kueleweka. Mfalmw hakuelewa na kwa kutumia akili zake za kiutu uzima akajua kuna shida iliyofichwa nyuma ya pazia ila hakuhangaika nayo, akanyamaza.
"Kwahiyo nini mpango wako kwa sasa?" Mfalme akauliza akinywa divai. Rhoda akajiumauma, hakuna ambacho mfalme aliambulia. Akawaza sana yule Rhoda wa zamani si huyu wa sasa. Rhoda alikuwa ana hamu ya biashara na mkono wake haukulaza damu kwenye fursa.
Mfalme akajawa na hamu kujua ni nini hicho ambacho kimemleta Rhoda hapo hekaluni.
"Sina mengi sana, mfalme. Kubwa lililonileta hapa ni kutaka kufahamu, huoni sasa ni muda muafaka kwako kuwa kwenye mahusiano? Goshen inahitaji Malkia."
Mfalme akatabasamu. Akamwambia Rhoda kuwa swala hilo halihitaji haraka, analifanyia kazi taratibu.
Rhoda akatabasamu akimtazama kwa macho ya kimahaba. Alitaka kusema jambo, lakini akakatizwa na sauti kali ya Aplhan. Alikuwa anakuja akirusha miguu yake kwa mbali.
"Kuna jambo, mfalme! Kuna jambo!"
Aliposogea karibu akapaza sauti kusema ni kweli kuna walozi ndani ya himaya. Rhoda akamtazama Alphan kwa macho ya kizandiki.
"Una uhakika?" Mfalme akauliza.
"Ndio, mfalme. Nimepata uhakika haswa."
Wakati huo Mfalme ameteta na Alphan, Rhoda akautumia huo mwanya kumtilia mfalme unga mweusi ndani ya kikombe chake cha divai.
Mfalme alipokuja kumtazama, alimtaka awapishe kwani wana maongezi binafsi. Rhoda akanyanyuka na kutoa heshima zake kisha akaondoka akiwa ana mawazo.
Akawaza ni mlozi gani aliyekuwa anamuongelea Alphan. Akawaza kama atakuwa ni yeye na nini mfalme atafanya. Roho yake haikuwa na amani kabisa.
"Unadhani kuna mlozi yupi? Hamna mwingine zaidi yetu!" Alisema kikongwe mmoja punde tu walipofika nyumbani kila mtu akajimega toka kwenye mwili wa Rhoda.
Wakaketi kitandani wakiwa wamejawa mawazo. Tumaini lao likawa lipo kwa Mfalme tu kunywa kile kinywaji walichotia dawa yao.
"Endapo akinywa, tutatoka ndani ya mwili wa Rhoda na kuzama kwenye wake."
Huko kasrini Alphan akamwambia mfalme juu ya yale yote aliyoyasikia huko mitaani na namna habari za walozi zilivyotapakaa. Mfalme akapigwa na bumbuwazi.
"Kwahiyo Alphan, wataka kuniambia ile nyumba ya Rhoda ndiyo imekuwa jumba la walozi?" Mfalme akatahamaki.
"Ndio, mfalme!" Aplhan akasisitiza kwa kutikisa kichwa akiketi chini. Mfalme akanyamaza kimya. Akang'ata kidole chake akiwaza.
Akateka kinywaji chake cha divai akakimiminia kinywani kisha akamtaka Alphan amuitie wanajeshi watano atakaowapa maagizo ya kwenda kutekeleza.
Wanajeshi hao walipokuja, Mfalme akawapa zoezi la kumtazama Rhoda kila aendapo. Kazi yao ni kuamka asubuhi na kwenda kuketi mahali wakimtazama anachofanya asubuhi mpaka jioni.
"Nahitaji mrejesho kila jioni."
***
"Tattiana yupo wapi?" Mama alipaza sauti baada ya kutoka chumbani kwa Tattiana pasipo kuona mtu.
"Sijui!" Akajibu Fanty akipandisha mabega. Mama akamsogelea na kumkunja shati akirudia swali lake. Fanty naye akarejelea kumwambia hajui.
Mama akiwa ameng'ata meno akamwambia Fanty kuwa anajua kinachoendelea, wala asijaribu kumficha. Anafahamu jana Tattiana hakuwa nyumbani, alitoka, na pia hakuwa amekula usiku kama alivyomdanganya.
Fanty akajawa na hofu. Alitamani kusema wapi alipo Tattiana ila hakuwa anajua abadani zaidi ya kuotea pengine atakuwapo kwa Roboth. Tattiana alitoroka, hakuthubutu hata kumwambia.
Mama asitake kuelewa, akafungasha akidhamiria kwenda huko kwa kina Roboth. Jambo lilishamfika kooni, sasa hakuna budi kulivaa.
Akapanda farasi na upesi akafika nyumbani kwa wakina Roboth, kabla hajafanya chochote akapokelewa na sauti ya kilio ya Tattiana. Upesi akashuka na kuzama ndani, akamkuta Tattiana akiwa amekaa pembeni ya mwili mfu wa Roboth.
Roboth alikuwa amefariki, hatamaniki kumtazama. Hata mama akapigwa na ganzi ya bumbuwazi na simanzi.
Tattiana akamuona mama yake, kwa hasira akiwa analia kwa sauti kuu, akapaza sauti kumtusi mama yake na kumuita muuaji asiye na lepe la huruma.
"Amekukosea nini kijana wa watu? Aliwakosea nini!" Akafoka.
******