SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 18*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

"Mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako ... mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako ... mfalme, kuna walozi ndani ya himaya yako."

Sauti hiyo ikakoma kama sekunde nne kisha ikasema tena:

"Wanakumywa damu na kuwaua watu ... wanakunywa damu na kuwaua watu ... wanakunywa damu na kuwaua watu."

Mfalme akasikia vema sana. Lakini sauti ile ikaacha kunong'oneza, ikafoka:

"Amka! Nenda Kawatafute!"

Mfalme akakurupuka toka usingizini. Akiwa ametoa macho akakodoa kutazama kushoto na kulia akihema. Kwa mbali akasikia vishindo vya miguu vikipotelea!

Basi akanyanyuka, akafungua mlango wake na kutupa macho. Hakuona kitu! Akatoka ndani ya chumba na kwenda kutazama. Huku na kule, hakubahatika kuona chochote alichoshuku. Akarudi chumbani na kuketi kitandani.

ENDELEA

Akafikiria sana ila mwishowe akaamua kuachana na mawazo hayo na kulala. Alipoamka akaonana na waziri wake wa ulinzi, bwana Alphan, akampasha habari juu ya ndoto yake.

"La haula!" Alphan akashangaa. Akamshauri mfalme wake kulifanyia kazi hilo jambo na atakuja kumpatia habari karibuni.

"Ulitilie maanani," mfalme akasisitizia. Alphan akanyanyuka aende zake, lakini kabla hajakwenda mfalme akakumbuka na kumuuliza jambo, ni kuhusu yule mwanajeshi wake aliyempatia kazi ya kumfuatilia Tattiana.

"Sijamwona!" Alphan akatahamaki. Hii haikuwa kawaida yake, mfalme akang'aka. Ni nini kimemkumba? Akataka kujua, basi akamuagiza Aplhan akafuatilie hilo jambo kwanza kabla ya mengine.

Alphan akaendaze na kumwacha mfalme. Baada ya muda mfupi akarejea akiwa haehae. Alimkuta mfalme akiwa anakunywa divai kwenye meza yake tukufu.

"Ewe mfalme, kijakazi wako ameishiwa na nguvu. Ametokwa na madonda mwilini na sidhani kama ataliona jua la kesho!"

Mfalme akatahamaki. Haraka akaelekea kumsabahi kijakaziwe. Akamkuta akiwa amejikunyata, dhoofu lihali hajiwezi.

"Ni nini kimekukumba?" Akauliza akijawa na shauku kubwa kujua lakini kijakazi wake hakuwa na hali kujibu. Alikuwa anatetemeka, akipambana na baridi kali alilolisikia peke yake.

Alipojitahidi kufungua kinywa, akashindwa. Mdomo wake ulikuwa umepasuka konani. Na ajabu hakudumu muda mrefu, akafariki!

Mfalme hakuamini macho wala masikio yake. Akachanganyikiwa kwa mawazo. Akauliza watu wa karibu ni nini kilimkumba mtumishi wake huyo, wakamwambia hawajui. Ni alikuja tu akiwa anakohoa damu!

Wakataka kumzika upesi, lakini mfalme akazuia zoezi hilo na kusihi mwili huo upelekwe hospitali na ukaguliwe.

"Nataka kujua nini kimemuua!" Mfalme akasema. Mwili ukapelekwa hospitali na daktari akaomba muda apate kuuchunguza mwili huo na kung'amua nini chanzo.

Mfalme akarejea himayani mwake, akiwa anawaza sana kuhusu lile jambo la mtumishi wake, majira ya jioni kuelekea usiku, akapokea mgeni - Rhoda. Akamkarimu mezani wapate tia chochote kinywani.

"Ni muda umepita sasa hujaja kuniona. Kuna shida yoyote?" Mfalme akauliza. Rhoda akatabasamu na kutikisa kichwa.

"Hapana, mfalme wangu. Ni kazi tu zimenibana."

Mfalme akaguna na kisha akauliza ni kazi gani hiyo kwani amesikia na kuhakikisha kwamba biashara yake imefungwa kwa muda sasa.

Rhoda akatabasamu.

"Ni kweli, mfalme. Tumeifunga ... yani, nimeifunga."

Mfalme akashikwa na butwaa kwani alitegemea Rhoda angeeleza pia na sababu za yeye kufanya hivyo, ila akawa kimya mpaka pale mfalme alipomuuliza nini kimemsibu.

Rhoda hakuwa na majibu ya kueleweka. Mfalmw hakuelewa na kwa kutumia akili zake za kiutu uzima akajua kuna shida iliyofichwa nyuma ya pazia ila hakuhangaika nayo, akanyamaza.

"Kwahiyo nini mpango wako kwa sasa?" Mfalme akauliza akinywa divai. Rhoda akajiumauma, hakuna ambacho mfalme aliambulia. Akawaza sana yule Rhoda wa zamani si huyu wa sasa. Rhoda alikuwa ana hamu ya biashara na mkono wake haukulaza damu kwenye fursa.

Mfalme akajawa na hamu kujua ni nini hicho ambacho kimemleta Rhoda hapo hekaluni.

"Sina mengi sana, mfalme. Kubwa lililonileta hapa ni kutaka kufahamu, huoni sasa ni muda muafaka kwako kuwa kwenye mahusiano? Goshen inahitaji Malkia."

Mfalme akatabasamu. Akamwambia Rhoda kuwa swala hilo halihitaji haraka, analifanyia kazi taratibu.

Rhoda akatabasamu akimtazama kwa macho ya kimahaba. Alitaka kusema jambo, lakini akakatizwa na sauti kali ya Aplhan. Alikuwa anakuja akirusha miguu yake kwa mbali.

"Kuna jambo, mfalme! Kuna jambo!"

Aliposogea karibu akapaza sauti kusema ni kweli kuna walozi ndani ya himaya. Rhoda akamtazama Alphan kwa macho ya kizandiki.

"Una uhakika?" Mfalme akauliza.

"Ndio, mfalme. Nimepata uhakika haswa."

Wakati huo Mfalme ameteta na Alphan, Rhoda akautumia huo mwanya kumtilia mfalme unga mweusi ndani ya kikombe chake cha divai.

Mfalme alipokuja kumtazama, alimtaka awapishe kwani wana maongezi binafsi. Rhoda akanyanyuka na kutoa heshima zake kisha akaondoka akiwa ana mawazo.

Akawaza ni mlozi gani aliyekuwa anamuongelea Alphan. Akawaza kama atakuwa ni yeye na nini mfalme atafanya. Roho yake haikuwa na amani kabisa.

"Unadhani kuna mlozi yupi? Hamna mwingine zaidi yetu!" Alisema kikongwe mmoja punde tu walipofika nyumbani kila mtu akajimega toka kwenye mwili wa Rhoda.

Wakaketi kitandani wakiwa wamejawa mawazo. Tumaini lao likawa lipo kwa Mfalme tu kunywa kile kinywaji walichotia dawa yao.

"Endapo akinywa, tutatoka ndani ya mwili wa Rhoda na kuzama kwenye wake."

Huko kasrini Alphan akamwambia mfalme juu ya yale yote aliyoyasikia huko mitaani na namna habari za walozi zilivyotapakaa. Mfalme akapigwa na bumbuwazi.

"Kwahiyo Alphan, wataka kuniambia ile nyumba ya Rhoda ndiyo imekuwa jumba la walozi?" Mfalme akatahamaki.

"Ndio, mfalme!" Aplhan akasisitiza kwa kutikisa kichwa akiketi chini. Mfalme akanyamaza kimya. Akang'ata kidole chake akiwaza.

Akateka kinywaji chake cha divai akakimiminia kinywani kisha akamtaka Alphan amuitie wanajeshi watano atakaowapa maagizo ya kwenda kutekeleza.

Wanajeshi hao walipokuja, Mfalme akawapa zoezi la kumtazama Rhoda kila aendapo. Kazi yao ni kuamka asubuhi na kwenda kuketi mahali wakimtazama anachofanya asubuhi mpaka jioni.

"Nahitaji mrejesho kila jioni."

***

"Tattiana yupo wapi?" Mama alipaza sauti baada ya kutoka chumbani kwa Tattiana pasipo kuona mtu.

"Sijui!" Akajibu Fanty akipandisha mabega. Mama akamsogelea na kumkunja shati akirudia swali lake. Fanty naye akarejelea kumwambia hajui.

Mama akiwa ameng'ata meno akamwambia Fanty kuwa anajua kinachoendelea, wala asijaribu kumficha. Anafahamu jana Tattiana hakuwa nyumbani, alitoka, na pia hakuwa amekula usiku kama alivyomdanganya.

Fanty akajawa na hofu. Alitamani kusema wapi alipo Tattiana ila hakuwa anajua abadani zaidi ya kuotea pengine atakuwapo kwa Roboth. Tattiana alitoroka, hakuthubutu hata kumwambia.

Mama asitake kuelewa, akafungasha akidhamiria kwenda huko kwa kina Roboth. Jambo lilishamfika kooni, sasa hakuna budi kulivaa.

Akapanda farasi na upesi akafika nyumbani kwa wakina Roboth, kabla hajafanya chochote akapokelewa na sauti ya kilio ya Tattiana. Upesi akashuka na kuzama ndani, akamkuta Tattiana akiwa amekaa pembeni ya mwili mfu wa Roboth.

Roboth alikuwa amefariki, hatamaniki kumtazama. Hata mama akapigwa na ganzi ya bumbuwazi na simanzi.

Tattiana akamuona mama yake, kwa hasira akiwa analia kwa sauti kuu, akapaza sauti kumtusi mama yake na kumuita muuaji asiye na lepe la huruma.

"Amekukosea nini kijana wa watu? Aliwakosea nini!" Akafoka.


******
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 19*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Mama asitake kuelewa, akafungasha akidhamiria kwenda huko kwa kina Roboth. Jambo lilishamfika kooni, sasa hakuna budi kulivaa.
Akapanda farasi na upesi akafika nyumbani kwa wakina Roboth, kabla hajafanya chochote akapokelewa na sauti ya kilio ya Tattiana. Upesi akashuka na kuzama ndani, akamkuta Tattiana akiwa amekaa pembeni ya mwili mfu wa Roboth.
Roboth alikuwa amefariki, hatamaniki kumtazama. Hata mama akapigwa na ganzi ya bumbuwazi na simanzi.
Tattiana akamuona mama yake, kwa hasira akiwa analia kwa sauti kuu, akapaza sauti kumtusi mama yake na kumuita muuaji asiye na lepe la huruma.
"Amekukosea nini kijana wa watu? Aliwakosea nini!" Akafoka.
ENDELEA
Mama akapigwa na tahamaki. Hakujua kitu ambacho Tattiana anasema. Hakuwa anamuelewa na hakuwa anajua kitu kinachoendelea pale.
Tattiana akiwa anajiamini kwamba anachokifanya ni sahihi, akamfokea mno mama yake, kama haitoshi akamfukuza hataki kumuona kabisa.
"Mimi si mwanao tena, sitaki kukusikia wala kukuona kabisa!" Akamalizia na kumwambia mama yake akamfikishie hizo habari na baba yake huko nyumbani.
Mama akiwa ameishiwa na nguvu, na anasikia baridi kana kwamba amemwagiwa maji ya mtoni, akarejea zake nyumbani. Hamu yote ilikuwa imemuisha!
Roho ilikuwa inampwita na kichwa chake hakikuacha kumtamka Roboth wa ajabu aliyemuona. Ni nini kile?
Mawazo yake yote hayo yakamkuta na mumewe aliyerejea na kumuuliza nini kimemjiri na mwana wao wa kike yupo wapi. Mama alipomueleza, baba hakuchukua muda, upesi akapanda farasi na kwenda kwa wakina Roboth.
Hakukuta mtu! Loh! Akashangaa akitafuta huku na huko. Akauliza jirani, akaambiwa wametoka kwenda kuzika. Basi haraka akaenda huko na kukuta watu wanne tu! Mama yake Roboth, Tattiana na wanaume wawili waliokuwa wamejifunika manailoni meusi.
Kabla hajafanya kitu akaona wanaume wale wakijifungua nailoni zile nyeusi mikononi mwao na kuanza kumdai fedha mama yake Roboth. Mama akasema hana kitu.
"Mama acha kututania? Tumezika huo mzoga wako alafu unatuambia huna kitu? - unajua ni kwenye hatari gani tumejiweka kufanya kazi hiyo?"
Vijana hao hawakumuelewa huyo mama wakataka hata kuchukua hatua mikononi. Kama si Melkizedek kuingilia hapo upesi basi jambo lingezuka.
"Nitalipa mimi!" Akasema Melkizedek, baba yake Tattiana. Wote wakageuza shingo zao kumtazama.
"Sitaki!" Mama akafoka. Akakataa katakata, hataki mwanaume huyo amlipie chochote kile. Lakini angewapa nini wanaume wale waliotoa jasho lao?
Melkizedek akatoa pesa yake, wanaume hao wakaenda zao wakilaani na wakinenea vibaya ule mwili waliouzika. Wakiusema kuwa unanuka na wala haueleweki.
"Unahitaji nini hapa?" Mama yake Roboth akauliza. Alikuwa anafanana macho na Tattiana. Yalikuwa mekundu yaliyovimba. Na sura zao zikiwa zimelowana huzuni tepe kwa kuondokewa na mpendwa wao.
Melkizedek akamwambia hajafuata lolote lile isipokuwa kumchukua mwanaye, lakini Tattiana akagoma kwenda akimweleza hamtambui kama baba yake.
"Mnataka nami mkaniue kama Roboth?"
"Nani amemuua Roboth?" Melkizedek akashangaa.
"Hujui?" Tattiana akang'aka. Akatoa maneno makali kisha akamtaka mama yake Roboth waende zao. Hakumtaka kumsikiza baba yake kabisa, na akamuonya kumfuata tena.
"Sasa tunafanyaje?" Melkizedek akamuuliza mkewe punde alipoketi kitini baada ya kurejea nyumbani.
Wote walikuwa wamechoshwa na vile walivyoviona, vichwani wakiteswa na maswali kadhaa - haswa nini kimemkumba Roboth? Kwanini Tattiana anaamini wao ndiyo wamemuua?
"Ama ulifanya jambo pasipo kunambia?" Melkizedek akamuuliza mkewe.
"La hasha! Sijui lolote," mama akajibu akikunja sura, kisha akauliza:
"Na ya mfalme je akiyajua haya?"
Wakakosa maneno ya kusema. Walikuwa zaidi ya dimbwini, dimbwi la mawazo.

***

Ndani ya Usiku mzito.

Baada ya siku nzima pevu, ya kupanga na kuhusia wapambanaji wake juu ya walozi wanaotafutwa ndani ya himaya ya Goshen, Alphan sasa akaupata usingizi aliokuwa anautafuta kwa kitambo.
Muda ulikuwa unaenda sasa, na analiona angetakiwa ameshawatia nguvuni walengwa wake lakini haikuwa vivyo. Mambo hayakuwa mepesi!
Lakini si haba, alikuwa amepiga hatua kusogelea malengo yake. Tayari kwa fununu alishajua nyumba ya Rhoda haikuwa tena nyumba ya binadamu wa kawaida.
Habari zimesambaa himayani kuhusu yanayotendeka hapo. Taa haziwashwi ingali kuna watu. Na hata Rhoda kutoonekana tena kama ilivyokuwa hapo awali. Achilia mbali, maneno ya walevi na wale vijakazi wa ndani.
Alphan kuhakikisha hakosi jambo, ameshapandikiza watu wake hapo kutazama na kufuatilia kila nyendo.
Lakini basi, wale walozi walikuwa tayari wameshaling'amua hilo. Walishajua kila ambacho Alphan anakifanya, na hata alichopanga kufanya.
Sasa wamepanga kumuangamiza, kisha wammalize na mfalme! Watajivika mwili wake kama walivyofanya kwa Rhoda, na sasa wakatawale Goshen milele!
Usiku ulivyozidi kutambaa, Alphan akajikuta hayupo peke yake ndani ya chumba.
Akashtuka na kuangaza akiuliza kama kuna yeyote ndani ya chumba asimtambue. Hakukuwa na majibu. Akiwa anahema, akawasha taa yake na kuitupa huku na kule, hakukuwa na jambo!
Basi akadhani ni wenge, akazima taa apate kulala. Loh! Taa kuzima akawaona watu wawili waliosimama kwenye kingo ya kitanda. Mwili ukamtetemeka, akataka kupiga kelele kali la hofu.
Lakini hakuweza abadani!
Kwani kabla hajafanya kitu, alihisi mwili umeishiwa nguvu, sauti haitoki!
Watu wale aliowaona, kwa raha zao, wakaanza kumjongea kumfuata. Wakamkamata koo na kumminyia kitandani. Wakamkaba mpaka pale walipohakikisha amelegea kuukosa uhai.
Kisha wakapotea kama upepo vuuuupp!
Mkono wa Alphan uliokuwa ukipambana kidhaifu ukadondokea kwenye mbao ya kitanda na kutoa sauti, haraka mwanajeshi mmoja huko nje akapaza sauti kuuliza kama kila kitu ni shwari humo ndani.
Alipoona kimya, haraka akaingia ndani na kuangaza. Akamwona mkuu wake akiwa hajielewi, ni mfu kasoro robo tu! Na wala hakukuwa na ishara yoyote kama kuna mtu aliingia ndani.

***

Asubuhi...

Mfalme Phares akiwa anapata kifungua kinywa, haraka anaingia kamanda wa vita na kusimama kando kando yake, akatoa heshima zake na kumwambia mfalme ya kwamba kuna msiba, wa yule kijakazi wake aliyekuwa yu hoi kwa kuumwa!
Mfalme akasikitika sana kwa kupoteza dhana yake muhimu.
Kabla hajasema neno lolote, yule kamanda akaongezea taarifa ya kwamba kila mtu anaogopa kuushika wala kuuzika mwili wa mtumishi huyo.


****
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom