SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Shunie kitabu kiingie sokon i will buy it mrembo ur so creative kwa kweli this story inampeleka mtu anakuwa km anaangalia movie
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 16*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

"Tulikuja kuwaokoa," akajibu Fluffy. "Ila pasipo msaada wa hawa Azeth tusingeweza abadani!"

Zura akamkatiza.

"Nadhani ni sahihi ukapumzika, Malkia," akasema akiwa amemuwekea kiganja kwenye paji lake la uso. "Mlidungwa sumu kali na wale watu. Miili yeni imechoshwa sana kwani mlikuwa mkitota sana. Pumzika sasa, tutaongea hapo baadae."

Malkia akataka kunyanyuka. Zura akamrudisha chini.

"Tafadhali. Kama unataka kuishi, fanya ninachokuambia, Malkia. Bado tunakuhitaji."

Malkia akataka kusema jambo, ila kichwa na macho vikamzidi uzito, akapitiwa pasipo ruhusa!

"Unadhani atakuwa sawa?" Akauliza Fluffy.

"Natumai atakuwa sawa. Yeye ni Malkia, hakuna hii safari pasipo yeye."

ENDELEA

***

Yalikuwa ni majira ya mchana wa jua la kando kidogo huko angani. Hali ya hewa haikuwa haba, upepo ulikuwa unapuliza kuashiria ujio wa nyakati za vuli ndani ya himaya ya Goshen. Anga nalo halikuwa kavu bali lililojawa na mawingu kadha wa kadha mashariki kwa magharibi.

Ingawa jua halikuwa mbali sana na utosi, lilikuwa dhaifu. Na mara nyingi likiwa linamezwa na kutemwa na mawingu yale yaliyokuwa yamejazana angani. Mchezo huo ungeweza kukugharimu muda wako kwa kuzubaa kuangaza, ukivutiwa na yale maumbo mbalimbali ya mawingu yalivyokuwa yanapokezana kulidaka jua na kisha kumtupia mwenzake mithili ya mchezo wa mpira wa pete.

Kwa wakati huo, Melkizedek pamoja na mkewe walikuwa wapo hospitalini na nyuso za furaha. Siku hiyo kwao ilikuwa pendwa kwani binti yao aliyekaa hospitalini kwa muda, hatimaye alikuwa anaruhusiwa kurejea nyumbani.

Melkizedek kuhakikisha hakuwa mikono mitupu, akabebelea maua ya uwaridi, mafuta ya mizeituni na marashi ya violeti. Mama naye asiwe nyuma, akabebelea mkufu wa thamani, bangili na kibanio cha nywele chenye vijenzi vya almasi.

"Sasa mnaweza kwenda naye nyumbani," akasema daktari kwa bashasha la tabasamu. "Yupo kheri kabisa. Tumehakikisha hakuna hata tone la sumu lililobakia mwilini!"

"Ahsante sana daktari," Melkizedek akamkabidhi mkono, na kuuliza: "Sasa naweza nikamwona mwanangu kipenzi?"

"Bila shaka!" Daktari akawaelekeza mahali watakampokuta, basi wakaenenda. Wakamveka na kumnyunyuzia mafuta mwana wao na kumbeba kuelekea naye nyumbani kwa rashasha za furaha.

"Hakika umependeza. Kweli wewe wastahili kuwa mke wa mfalme!" Akasema mama akimtazama mwanae, Tattiana. Binti akatabasamu asiseme jambo.

Kichwani kwake hakuwa sawa, bali aliyetingwa na mawazo. Japokuwa kitoroli kile cha farasi cha thamani walichopanda kilikuwa kikiwapeleka kando na kando kwa mwendo, akili yake ilikuwa imetulizana tuli kumfikiria Roboth.

Kwa muda sasa hakuwa amekuja kumwona hospitali. Si kawaida yake. Atakuwa amekumbwa na nini?

Kabla ya kujiuliza kuhusu usalama wa mpenzi wake huyo, Tattiana alikuwa amejawa na wivu kifuani. Akajiuliza, atakuwa amempata mwanamke mwingine wa kumsahaulisha laaziz wake kitandani? Lakini mbona huwa anasema kuwa yeye ndiye mwanamke pekee mwenye nafasi moyoni mwake?

"Nakuapia, Tattiana. Wewe ndiye mwanamke wa maisha yangu. Kama moyo wangu ungalikuwa na sebule na vyumba vitatu, vyote ningekukabidhi wewe mie nikajilaza kibarazani." Sauti ya Roboth ikatembelea masikio yake.

Ikajirudia tena na tena, basi akajikuta anatabasamu mwenyewe macho yake yakiwa mbali milimani. Hakutoka kwenye fikra hizo mpaka alipowasili nyumbani. Akala na kunywa na kisha akajiweka chumbani kwake. Hakutaka kukaa na watu, hata kaka yake Fanty.

"Mpatie muda wa kupumzika, bado hayuko sawa," Mama akahauri. Fanty kishingo upande, akiwa anamtazama dada yake aliyekuwa amejilaza kitandani, akafunga mlango na kwendaze.

Tattiana akaamka na kwenda dirishani, akatazama mandhari ya huko nje na angani. Moyoni akawa anasema na muda. Alikuwa anangoja jua likaribie kulala, afanye jambo.

Alipohakikisha majira yamefika, na hakukuwa na wazazi nyumbani, akatoka chumbani akimuaga na kumpa maagizo kaka yake.

"Chunga mdomo wako, nitarejea hivi punde. Mlango wangu nimeutia ufunguo, watakapotaka kuniona, uwaambie nahitaji kupumzika. Sawa?"

Akakwea na kuruka ukuta aende kwa 'kina Roboth akajua hatma yake. Akatembea na kukimbia kama mwizi. Kabla ya jua kulitelekeza anga akawa amefika, akamkuta Roboth bandani akihudumia mifugo.

"Robo!" Akaita.

Roboth akashtuka kumwona Tattiana. Haraka akatazama nyumbani kwao kisha akamvutia binti huyo bandani.

"Umefikaje hapa? Mama yangu amekuona?"

"Hapana, sijaonana naye. Haukuja kuniona hospitali ... vipi, umeshapata mwanamke mwingine?" Akauliza Tattiana akiwa anamtazama Roboth machoni.

Roboth akatikisa kichwa.

"Hapana, sijapata mwingine. Na sitaweza kupata." Alipomaliza kauli yake hiyo akakohoa. Akataka kuendelea kunena, ila akakohoa tena na tena! Kuanzia hapo hakupata ahueni, akawa anakohoa na kukohoa.

"Roboth, vipi upo sawa?" Tattiana akajawa na mashaka. Hata Roboth akashindwa kujibu kwa kukohoa. Akakohoa mno kiasi cha kukosa pumzi. Mwishowe akadondoka na kuzirai!

Tattiana akatoa macho ya mshangao. Hakujua kipi afanye, akatoka nje ya banda na kuangaza. Kisha akarudi tena akiwa amechanganyikiwa. Akajitahidi, kwa nguvu zote, akambeba Roboth na kumpeleka ndani.

Akamlaza kitandani na kumpepea akitumia nguo yake.

"Roboth! Roboth!" Akaita akimpigapiga Roboth mashavu. "Amka! Amka, Roboth!"

Macho yake yakaanza kuwa mekundu. Punde yakajaa na kuanza kutiririsha machozi!

Akamtazama Roboth aliyekuwa ametulia tuli, akagundua mwanaume huyo alikuwa ametokwa na vipele vidogo vyekundu nyuma ya mikono yake.

Akavutiwa kutazama zaidi. Ni nini kinamsumbua Roboth? Akamtazama shingoni, mgongoni na hata miguuni, kote huko akaona dalili ya vipele hivyo vyekundu kwa mbali.

Akafungua kinywa cha Roboth, ndani ya lips zake akaona uweusi usio wa kawaida. Hapo Tattiana akajua ya kwamba Roboth anaumwa. Hakujua ni ugonjwa gani, ila alikubaliana na moyo yake kuwa si mdogo kabisa.

Akiwa kwenye buwazo hilo, mama yake Roboth akaingia ndani na kustaajabu kumwona.

"Umefuata nini hapa?" Mama akauliza akimtazama kwa macho ya uhasidi. Lakini kabla hajajibiwa, akauliza maswali mfululizo kuhusu hali ya mwanae. Akapiga magoti na kuanza kumuita akimtaka aamke.

"Umemfanya nini mwanangu?"

"Sijafanya kitu, mama. Amedondoka baada ya kukohoa mno," Tattiana akajitetea. "Atakuwa anaumwa sana. Tumpeleke hospitali. Hali yake si nzuri kabisa!"

Mama akajawa na kilio asiseme kitu. Giza lilikuwa linaingia na Tattiana alitakiwa arudi nyumbani. Akavua mkufu wake aliovekwa na mamaye, na kumkabidhi mama yake Roboth.

"Mkufu huu ni wa thamani kubwa. Naomba uuze upate pesa ya kumuwahisha hospitali, na matumizi mengine madogomadogo!"

Aliposema hayo akanyanyua gauni lake na kutoka ndani upesi! Akaanza kukimbia kurudi nyumbani akiomba akute hali shwari huko aendako.

Aliuondoa tu mwili wake nyumbani kwa 'kina Roboth, ila akili na moyo wake aliviacha huko. Aliendelea kuvuja machozi akijiuliza juu ya hali ya mpenzi wake, na hata akijuta kwanini alimshutumu na kumdhania ubaya.

Moyo wake ukawa mzito. Kichwa chake kikawa kinagonga kama saa ya ukutani. Joto la mwili wake likapanda. Usipite muda mrefu, akadondoka chini!

Kwa mbali kichwani kwake akawa anasikia watu wakicheka na kuteta. Hakuwa anawajua watu hawa ni wakina nani. Hakuwa na nguvu ya kunyanyuka kabisa. Na kabla hajapotea kabisa kwenye ulimwengu wa kupoteza fahamu, kwa mbali akasikia sauti ya daktari:

"Hatakiwi kufanya kazi yoyote ngumu, bali apumzike kwa muda mrefu. Mwili wake bado unahitaji muda kurejea katika hali yake ya kawaida."

Na mara akazima asisikie chochote tena.



***
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom