*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II --- 14*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
"Seth, una uhakika na kile ulichokisema?" Malkia akauliza.
"Ndio, kwa asilimia zote. Usijali," Seth akasema kwa kujiamini akitikisa kichwa. Safari ikaanza.
Hakukuwa na maongezi sana huko njiani. Kabla hawajakiacha mbali kijiji cha Azeth, farasi wa Malkia akajiri tokea misituni. Malkia akamkumbatia na kumpanda mnyamawe anayempenda.
Lakini walivyotembea kwa umbali mfupi tu, farasi huyo akaanza kulegea na kukosa nguvu. Ghafla akadondoka chini na kupoteza fahamu. Malkia pamoja na wenziwe wakastaajabu nini kilitokea.
Jitu moja, kati ya wale majitu mawili ya Azeth, likampekua farasi huyo kwa kumnusa na kumkagua mwili, kisha likasema:
"Venerdi kashaka!"
"Anamaanisha nini?" Malkia akawahi kuumuliza Seth.
"Amepewa sumu!" Seth akajibu upesi.
"Waulize kama kuna namna ya kunsaidia, tafadhali!"
Seth akafanya hivyo. Malkia akaona majitu yale yakitikisa kichwa.
"Tafadhali, waombe wamsaidie. Tafadhali!" Malkia akasisitiza.
Seth akawaambia. Wale majitu wakamjibu kuwa farasi huyo atakuwa amekula majani ya sumu, au amepewa sumu.
"Na wakina nani?" Malkia akawahi kuuliza.
ENDELEA
Wale majitu ya Azeth wakatazamana na kuteta kidogo, alafu mmoja akamtazama Seth na kumpatia majibu.
"Wanaasema hapa karibuni kuna binadamu huwa wanakuja kuwinda, huwaua wanyama kwa kutumia sumu na hata huwa wanawadhuru wao kwa kutumia sumu hiyo. Wanadhani hao ndio watakuwa wanahusika."
"Na dawa je?" Akauliza Malkia. Seth akamjibu na dawa pia inapatikana kwa hao watu, lakini ni hatari sana kwenda huko kwani si watu marafiki.
"Malkia, ni bora tukaendelea na safari," Seth akashauri. Malkia akakaa kimya kwanza, wote wakimtazama, mara akanyanyuka na kusema:
"Siwezi nikaondoka, na siwezi kuendelea na safari hii mpaka pale nitakapomtibia farasi wangu."
"Lakini Malkia, ni hatari!" Akasisitizia Fluffy. Malkia akamtazama na kumwambia:
"Huyu farasi si tu mnyama kwangu, bali familia. Tangu nikiwa mtoto amekuwa nami mpaka sasa. Siwezi nikamwacha sasa, afe nami namtazama."
"Sasa utafanyaje? Wataka kwenda hivi?" Akauliza Seth.
"Nitaenda. Hata kama ikinibidi niende mwenyewe," Malkia akajibu kwa kujiamini.
Seth na wenzake wakabaki wakitazamana. Hawakujua cha kufanya. Hawawezi kumwacha Malkia aende peke yake, ila si kutafuta visa huku? Kwenda tena kufanya vita na watu wengine na huku wametokea pona chupu?
"Ni wapi walipo watu hao?" Akauliza Malkia kwa kupaza sauti. Seth akamtazama akitamani kumzuia.
"Fanya upesi, maana muda haupo upande wangu!" Malkia akasihi akimtazama kwa macho yasiyo na utani. Upepo ukavuma kuinamisha miti na kukimbiza ndege.
***
Giza lilikuwa linaingia sasa, taa za makazi ya zamani ya Rhoda bado hazikuwa zimewashwa na chumbani kulikuwa kuna mzozo ukisikika. Mzozo huu haukuwa wa mwingine, bali wa wale bibi walozi toka Tanashe.
Walikuwa wamesimama wima, mwili wa Rhoda ukiwa kitandani, ila hawakuwa watatu, bali wawili, nyuso zao zikiswahibu mambo hayakuwa shwari hata.
Wakinyoosheana vidole vyao virefu, na wakitoleana macho ambayo kila mmoja wao alikuwa analo moja moja! Wakapayuka na kupaza sauti.
"Mpaka lini?" Mmoja akauliza.
"Sasa unadhani tutafanyaje na ndivyo imekuwa vivyo?" Mwingine akajibu kwa kuuliza.
"Tutafanyaje!" Mwenzake akatahamaki. "Tukiendelea hivi, tutafikia wapi? Tumekuja huku kunywa damu za watu ama kushika dola?"
"Natambua hilo. Na si kosa la yeyote yule kati yetu!"
"Vipi kama akikamatwa huko? Vipi ikagundulikana? Itakuwa bahati yetu kama tukarejeshwa Tanashe tukiwa hai. Si tu kwamba tutapoteza uhai, bali lengo lililotuleta huku!"
"Sasa wapaza koromo na mtu angali hayupo? Yasaidiani?"
"Napaza kwakuwa wewe ndiye ulikuwa naye mara ya mwisho kabla hajatokomea tena. Ulishindwa mzuia? Ama amekupa nawe ahadi ya kukuletea pande la nyama ya binadamu?"
"Hakuniaga! Na sikuwa naye tukisongamana kama vifungo. Sijui na wala sihusiki na tukio lake la kwenda huko!"
Kukawa kimya kidogo wakivuta kwanza pumzi na kupunguza msongamano wa pumzi za jazba vifuani mwao. Wakaketi kila mtu akigeukia upande wake. Mwili wa Rhoda ulikuwa katikati yao.
"Tulipanga kwenda kuonana na mfalme, hayajatimia kisa yeye, siku imeisha. Tuliweka mwili wa binadamu yule mlevi ukauke kwa ajili ya kutengenezea dawa, kaumaliza kwa kuutafuna." Akasema kikongwe mmoja akishika tama.
"Hatuwezi kumbadili, tumesema na sasa imeshageuka kuwa matumbuizo masikioni mwake. Amekuwa samaki mkavu, sufuriani hatoshi," akasema mwingine. Wote wakiwa wameshika tama.
"Hakuna namna, inabidi tufanye maamuzi magumu," akasema mwingine.
"Yapi hayo?"
"Kummaliza!"
"Unasema?"
"Ndio, kama ulivyonisikia."
"Huoni kama tutakuwa tumeenda mbali sana?"
"Itabidi twende huko mbali kama njia ya karibu hamna. Unafikiri ni nini tutafanya? Hatuwezi tukamfungia, atatoka. Hatuwezi kumrudisha Tanashe."
Mara wakasikia sauti ya mlango ukisukumwa huko sebuleni. Haraka wakatazama kioo chao cha kilozi na kugundua ni mwenzao.
"Anarejea!"
Mlango ukarejeshewa na mlozi huyu aliyeingia, akapaza sauti akiulizia wenzake kama wapo. Akawasha taa zao za maginga ya moto na kisha akapandisha ngazi kuelekea juu kuwakuta wenziwe.
Akafungua mlango asione kitu. Kitanda kilikuwa kitupu, hawakuwepo wale vikongwe wala mwili wa Rhoda! Akapaza sauti kuita wenzake akijiuliza wapi walipo.
Napo mule chumbani akawasha ginga la moto lililokuwa linaning'inia ukutani. Akaangaza kushoto na kulia, hakuona kitu. Akaguna na kuketi kitandani. Nguo yake ilikuwa ina mabaki ya damu kwa shingoni na kifuani.
Akanyanyuka na kwenda kabatini, akafungua na kuangaza. Ila ghafla akahisi kuna watu nyuma yake, basi akageuka upesi. La haula! Akaona panga likiwa hewani, hajahema, likamkita kichwani na kudondoka chini!
Haikupita muda mrefu, vikongwe wawili wakatoka ndani ya jengo wakiwa wamebebelea kifurushi cheusi. Wakiwa wamejawa na tahadhari wakaelekea nyuma ya nyumba na kuchimba shimo kisha wakazamisha kifurushi kile ndani yake.
"Kazi imekwisha," mmoja akasema akikung'uta mikono yake. Basi wakatoka huko nje na kurudi zao ndani.
"Tutamkumbuka sana."
"Hakika! Hatujawahi kuwa pungufu namna hii, ila sasa tunaweza tukatimiza mipango yetu."
Wakapandisha juu kuelekea chumbani. Ila muda si mrefu, mlango ukagongwa mara tatu. Wakatazamana na kuulizana kabla hawajateka kioo chao na kutazama. Wakamwona askari akiwa amesimama na mwanaume mmoja ambaye hawakumtambua.
"Unahisi nini?" Akauliza mmojawao. Punde wakashuka chini wakiwa tayari wamevalia mwili wa Rhoda.
"Vipi muda huu?" Wakauliza.
"Tafadhali, tumekuja kufanya ukaguzi," akajibu Askari. Na kumbe yule mwanaume aliyekuwa kando yake alikuwa ni yule mlevi ambaye mwenziwe alikufa baada ya kuingia ndani ya jengo la walozi hawa.
"Ukaguzi?" Akatahamaki Rhoda. "Kuna nini?"
"Madam, hamna maelezo ya ziada kwenye hilo. Tunaomba tuongozane wote kwenda ndani," Askari akasema kwa mkazo. Basi wakazama ndani kupekua kama Rhoda yu mwenyewe. Walipomaliza pasipo matunda, wakamtaka waelekee uani.
Rhoda akasita. Akamtazama yule mlevi kwa jicho hasidi, ila mwishowe wakaamua kuelekea huko.
"Fukua!" Akaamuru askari akimkabidhi Rhoda chepeo. Mpaka hapo wale vikongwe wakatambua kuwa watakuwa wameonekana walipokuwa wamemzika mwenzao.
Wafanye nini? Wakaanza kujadiliana ndani ya kifua cha Rhoda.
***