*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 05*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Zoezi la kumsimika mfalme lilisitishwa maana jua lilikuwa tayari limeshatoka katikati ya anga, na watu pia hawakuwa kwenye munkari wa hilo zoezi tena bali uwoga. Fursa akaghafirishwa mno na hilo. Uso wake ulikuwa mwekundu, kwake kesho ilikuwa mbali mno.
ENDELEA
Kusogezwa kwa zoezi hilo mbele kilikuwa kikombe kigumu sana kukitia mdomoni.
Hakutaka kuongea na mtu yeyote bali kwenda kujifungia ndani ya chumba chake alimojitupia kitandani na kuanza kutafakuri. Aliwaza kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa tukio.
Kwa namna moja ama nyingine alijiona mjinga kwa kutaka kuitawala Goshen nafasi ambayo itamuweka roho yake rehani kutokana na maadui kadha wa kadha, ila baada ya pia kuchambua faida atakazopata akiwa katika hicho kiti, basi akajiona sahihi kuwinda kiti hicho cha kifalme kwa juhudi zote.
“Hakuna atakayenizuia.” Alisema mwenyewe akisaga meno. Macho yake yalikuwa mekundu na mdomo wake aliubinua, ila baada ya muda mfupi akanywea, ni baada ya mawazo juu ya Jayit kumjia kichwani.
Aliwaza na kuwazua namna gani ataweza kumdhibiti mwanaume huyo mdhalimu. Lakini pia aliwaza mwanaume huyo amepanga nini kwa Goshen siku za usoni? Mpaka anachoka, hakuwa amepata jibu lolote.
Aliamua kupuuzia akaugeuza mwili wake upande wa pili wa kitanda. Usingizi ulimjia, ila kabla hajalala akasikia hodi, na kabla hajaitikia, mtu akaingia. Alikurupuka akatazama kwa hasira, ila ghafla uso ukatengeneza tabasamu.
Alimuona mwanamke mrefu mwembamba mwenye shepu ya kuvutia na macho ya kuibia. Alikuwa anatembea kwa madaha, nywele zake ndefu zikiwa zinamghasi. Kifua chake kilikuwa kimejaa. Mdomo wake mwekundu ulikuwa na umbo la kopa.
Anajulikana kwa jina la Rhoda, ama Roy – mwanamke mrembo ndani ya tawala ya Goshen.
Aliendea kitandani akaketi. Na kabla ya kumpa salamu Fursa alimpa kwanza mabusu matatu motomoto kisha akamtazama mwanaume huyo kwa macho ya kulaghai.
“Hata mimi hutaki kuniona?” Aliuliza. Fursa akatabasamu na kumshika kidevu mrembo huyo.
“Nawezaje kukataa kuonana na mwanamke kama wewe, malkia wangu ajaye.”
Rhoda akatabasamu. Kisha akambusu tena mwanaume huyo pasi na kikomo.
***
Ni baada ya masaa matano ya kuwa njiani ndipo Malkia na Zura wakafika ndani ya himaya ya Maam wakiingia upande wa kusini wa tawala hiyo.
Farasi alipunguza mwendo akawa anatembea mpaka wanafika mbele ya nyumba ya babu na bibi wake Malkia Sandarus. Walibisha hodi mara mbili akatoka mwanamke kikongwe ambaye hakuwatambua wageni mpaka pale walipojitambulisha.
“Mjukuu wangu Sandarus!” Bibi alitahamaki. Alimshika mjukuu wake usoni akiwa anatabasamu. Ulikuwa umepita muda mrefu sana hakumuona mjukuu wake kipenzi: miaka kadha wa kadha, alitegemea hata kufa pasipo kumuona. Alimkumbatia mjukuu wake kwanguvu kisha akamwambia:
“Nyumba yangu ni ndogo sana kuruhusu wageni wako.”
Malkia Sandarus akatabasamu.
“Bibi sijaja na watu, nimekuja na mtu mmoja tu.”
Bibi alishangaa lakini pia akapata hofu, iweje malkia atoke umbali wote huo kuja pale akiwa na mtu mmoja? Malkia alimtaka kwanza bibi yake awaruhusu kuingia ndani kisha atamueleza yote.
Wakaingia ndani na kumweleza kila kitu kikongwe huyo mpaka kufikia hapo. Walimwambia wanahitaji kujua mahali mkufu huo umetoka na nini hasa nguvu yake. Bibi akauomba huo mkufu autizame, Malkia akampatia.
Bibi aliupapasa mkufu huo akiutazama na macho yake mabovu. Baada ya dakika kama moja alikunja sura yake akauliza:
“Baba yako alikupa lini huu mkufu?”
“Wakati anakaribia kufariki.”
Bibi akaendelea kuupapasa mkufu huo kwa dakika tena kadhaa. Ni kama vile kuna kitu alikuwa anakisikia na alikuwa anajaribu kuwa mtulivu ilia pate kukisikia vema.
“Bibi, unaujua?”
Bibi hakujibu upesi. Alitulia kwanza alafu akashusha pumzi.
“Huu mkufu baba yako aliutoa mbali sana. Alikuwa ananambia kila siku una nguvu mno, lakini hakupata kunambia vingine zaidi. Hakunambia hata kama alilenga kukupatia huu mkufu. Alikuwa msiri sana.”
“Kwahiyo bibi hujui kabisa wapi mkufu umetoka?”
“Sijui mjukuu wangu.”
Kukawa kimya kwa muda kidogo.
“Ila …” Bibi alidokeza. Malkia na Zura wakamtazama upesi kwa hamu ya kusikia. “Kuna mahali naweza nikawaelekeza. Mahali ambapo ni maarufu kwa kazi za sonara. Huko najua hautoweza kukosa majibu kuhusu huo mkufu. Hata kama watakuwa hawajautengeneza wao, basi watakuwa wanajua wapi ilipo asili yake.”
“Wapi huko?”
“Mnasikika kama watu waliochoka. Acha kwanza niwaandalie chakula, n’tawaambia zaidi.”
Japokuwa macho yake hayakuwa mazima, bibi aliwaandalia wageni wake chakula kitamu. Ilikuwa ni mboga za majani alizoziunga vema kwa ustadi, akazichanganya na nyama ya bata mkubwa aliyemchinja mwenyewe.
Wahenga na washenga wanasema ng’ombe hazeeki maini, hilo likathibitishwa na bibi huyu. Uzee wake haukufanya mkono na ulimi wake kufeli. Aliwapa sababu wageni wake kwanini alikuwa mmojawapo wa wanawake kamili ndani ya tawala ya Maam.
“Ahsante bibi, chakula kitamu,” alisema Malkia akijilamba.
“Ndicho chakula ulichokuwa unakipenda tangu utotoni mwako,” bibi akasema. Alitoa vyombo vyake pasipo kutaka msaada kisha akaketi na kuwaendelezea maneno:
“Taji zote za kifalme hutengenezwa huko, pete pia na mabangili ya kumeremeta na kupendeza. Ni umbali mrefu sana toka hapa, itamgharimu mtu juma zima mpaka kufika huko.
Panaitwa Osheni, ama panajulikana kama tawala ya masonara. Utapita milima mikubwa ya Wawetu na msitu mkubwa wa mianzi kabla hamjafika hapo. Ila mkiwa njiani, kumbukeni mkikutana na yeyote yule msithubutu kumuongelesha. Hata kumsalimia!”
Malkia na Zura walitaka kuondoka upesi ila bibi akawazuia kwani muda ulikuwa umeenda sana. Aliwataka walale pale kisha asubuhi wadamkie safari yao, wakakubali. Walibakia hapo wakapiga soga na bibi huyo mpaka giza lilipoingia. Bibi aliwapikia tena chakula cha usiku wakajipumzikia.
Hakukuwa tena kikubwa kilichojiri mpaka pale baadae mbeleni ambapo Malkia alipata taarifa juu ya yale yaliyojiri huko Goshen, ya kwamba mfalme bado hajapatikana kwasababu ya majira kubadilishwa.
Hiyo ilikuwa taarifa njema kwa Malkia. Ilimpa sababu mojawapo ya kutabasamu ndani ya siku hiyo ngumu.
.
.
.
.
.
.
*** .
.
.
.
.
Mkononi mwa Veda kulikuwa kuna bilauri ya mvinyo. Bilauri hiyo ilikuwa ni ya pili baada ya kumaliza ya kwanza aliyoigida upesi. Pembeni ya kitanda chake kulikuwa kuna meza kubwa na juu ya meza hiyo kulikuwa kuna bilauri kubwa lililobebelea kinywaji cha mvinyo.
Veda alikuwa amechoka kumsubiria Fursa ambaye alipeana naye ahadi ya kukutana majira ya usiku. Yalikuwa sasa yamepita masaa manne toka pale muda wa ahadi ulipokuwa na Fursa hakuonekana wala hakukuwa na dalili yake.
Veda alikuwa amevalia nguo nyepesi iliyoacha viungo vyake moto nje. Macho yake yalikuwa yanarembua na alikuwa anapiga mihayo mara kwa mara. Kama isingelikuwa kinywaji alichokuwa anakinywa, basi angelikuwa amelala.
Ni mvinyo pekee ndio ulikuwa unampa kampani. Hata hamu yake ya kimwili aliyokuwa nayo ikimngojea Fursa kwa bashasha zote, ilianza kupotea. Mwili wake uliokuwa moto kwa hamu za mapenzi ulianza kuwa baridi na kupooza. Na marashi yake aliyokuwa amejipulizia yalikuwa yanaelekea kuisha.
Alimaliza mvinyo wake ndani ya bilauri hiyo ya pili, akachota mvinyo mwingine. Wakati sasa anakunywa huu, ndipo Fursa akatokea. Aliketi kitandani mwa mwanamke huyo, akamtazama kwa sura ya kichovu. Veda alimlaumu Fursa kwanini amechelewa, Fursa akatumia sababu za uongo kumlaghai.
Masikini mwanamke huyo hakuwa anajua ya kwamba Fursa alikuwa ametoka kujimwaya mwaya na mrembo mwingine kwa jina Rhoda, mwanamke ambaye alimkamua mwanaume huyo manii zote akimuacha amechoka hajiwezi.
“Kwahiyo haunipi leo?” Aliuliza Rhoda kwa malalamiko.
“Nimeshakuambia nimechoka. Ntakupaje sasa?” Akajibu Fursa pasipo kumtazama mwanamke huyo.
Veda alijitahidi kuchokonoa hisia za Fursa kwa kumbusubusu mwanaume huyo shingoni, kumpapasa maeneo ya aanjoli, lakini ikawa bure. Mwishowe Fursa alisimamama akamtazama mwanamke huyo. Akawambia hampendi na hana malengo yoyote na yeye. Akamwambia matumizi yake yamekwisha na hamtaki tena!
Kwa Veda hiyo ikawa kama ndoto. Machozi yalimshuka upesi akauliza kana kwamba hakusikia.
“Fursa hunitaki?”
Haikuwa ndoto bali uhalisia, Fursa alikuwa hamtaki tena. Veda alitishia kusema yale maovu aliyofanya na mwanaume huyo lakini Fursa hakuogopa, akamjibu kiulaini:
“Hautopata muda huo.”
Veda hakuelewa nini Fursa anamaanisha. Hakujua kwamba mwanaume huyo alikuwa tayari ameshasuka mipango yake thabiti.
Alipotoka tu ndani ya chumba, aliingia mwanaume mmoja mwenye mwili mkubwa akiwa ameshikilia kiroba cha kahawia. Alichomoa kisu chake kiunoni, akamchoma Veda mara mbili tumboni kisha akamwingiza mwanamke huyo ndani ya kiroba akiwa anavuja damu.
Na kama alivyopewa maelekezo, kuhakikisha maiti hiyo haionekani popote pale ndani ya Goshen, mwanaume huyo alienda kumtupia Veda Tanashe kwa malengo kwamba akawe kitoweo cha wachawi.
Mwanaume huyo alikung’uta mikono yake kwa kumaliza kazi kisha akaondoka.
Baada tu ya muda mfupi, bibi watatu wakafika kwenye mwili huo. Walimkuta Veda akiwa anapumua kwa mbali mno. Walimtwaa upesi na kumpeleka kwenye nyumba yao. Huko walimrepea mwanamke huyo kwa kumtia dawa zao za kichawi, kufumba na kufumbua Veda akawa hai na mwenye nguvu.
Alitaka kuondoka kurejea Goshen akammalize Fursa, ila bibi wale wakamkatalia abadani. Walimpatia kazi aifanye kama malipo ya kumsaidia kuukoa uhai wake. Na kazi hiyo haikuwa nyingine bali kutafuta mkufu wa Malkia kwa hali na mali maana yeye alikuwa na uwezo wa kutoka Tanashe.
“Lakini Sandarus ameshakufa!” Alisema Veda. “Hapana, hajafa.” Akajibiwa na bibi mmoja. “Yu hai huko Maam, na jua likichomoza anaelekea kwenye tawala ya masonara.”
“Usijali.” Akasema bibi mwingine. “Tutakupa njia rahisi ya kumpata.”
“Ila…” Akadakia bibi mwingine. “Kaa ukijua ukitutoroka, tutajua na hautodumu zaidi ya masaa manne kabla hujafa!”
.
.
.
.
Lako jicho! .